NDOTO NA MAONO.

Mwl Sospeter Simon S. Ndabagoye
New Elshaddai Ministries NEM-Tanzania.


Kama ilivyoandikwa katika (Matendo ya Mitume 2:17)”Itakuwa siku za mwisho, asema Mungu ,nitawamwagia watu Roho yangu, na wana wenu na binti zenu watatabiri; na vijana wenu wataona maono; na wazee wenu wataota ndoto”. LEO TUTAJIFUNZA JUU YA NDOTO NA MAONO.

Dhana ya Ndoto.
Ni picha zinazoambatana na sauti kama sinema ambazo mtu huziona anapokuwa amesinzia. (Mwanzo 28:10-15).
Maono- ni picha ambazo mtu huziona anapokuwa macho yaani akiwa hajasinzia.
Tofauti iliyopo baina ya hivi vitu viwili ni kuwa, kimoja hutokea usingizini wakati kingine hutokea katika hali ya kawaida pasipo kuwa usingizini.
Sifa kuu ya Ndoto na Maono ni kuwa ni Mafumbo. Hii ina maana kwamba, mawasiliano haya ya kiroho huja kwa namna isiyo ya kawaida, hivyo hayawi na tafsiri ya moja kwa moja. (Hesabu 12 :5-8). Aidha, hakuna kanuni maalumu katika kutafta tafsiri zake (Mwanzo 37 :5-7), japo watu wa Mungu wanaweza kufunuliwa maana ya ndoto, kumbuka Yusufu alivyotafsi ndoto akiwa gerezan. izingatiwe kuwa wakati mwingine, ndoto zaidi ya moja,zinaweza kumaanisha kitu kimoja (Mwanzo 41 :1-7,14-16,25-38)
Mfano: Kornelio aliona maono saa tisa mchana (Matendo 10:1-6)
Petro aliona maono saa sita mchana (Matendo 10:9-16)
Paulo aliona maono alipokuwa njiani kwenda Dameski ilikuwa adhuhuri (Matendo 26:12-16)
Musa alipewa maono alipokuwa akichunga kondoo wa mkwewe Yethro mchana (Kutoka 3:1-3)
Hata hivyo, kuota si kwa watu waliookoka tu, bali hata ambao hawajaokoka wanawezakuota ndoto na kuona maono ya kimungu.
Mfano wa watu ambao hawakuwa wacha Mungu lakini waliweza kuota na kuona maono ya kimungu ni kama ifuatavyo:
Farao (Mwanzo 41:1)
Nebukadreza (Daniel 4:4-5)
Mkewe Pilato Mathayo (27:17-19)
Kornelio (Matendo 10:1-4).
Kutokana na Mifano hiyo hapo juu tunaona kuwa,mtu yeyote anaweza kuota na kuona maono ya kimungu.
Tatizo ni namna ya kupata maarifa ya kupambanua au kutafsiri ndoto hiyo au maono hayo. Hapa inatokana na kuwa ndoto au maono hayana jibu moja, na wala si kila ndoto inatoka kwa Mungu. Na hapa ndipo Hosea anapoliasa kanisa juu ya kuwa na maarifa (Hosea 4:6).
AINA ZA NDOTO.
Aina ya ndoto hutegemea chanzo chake.
VYANZO VYA NDOTO NA MAONO.
Kuna vyanzo vikuu vitatu vya ndoto/maono.
(i) Ndoto au maono yatokanayo na nafsi ya mtu mwenyewe.
Hii hutokana na shughuli alizokuwa akizifanya kutwa nzima,hivyo anapoenda kulala,matukio ya siku nzima hujirudia kutokana na picha zilizohifadhiwa katika ubongo wake. (Mhubiri 5:3)
Kwamaana ndoto huja kwasababu ya shughuli nyingi; na sauti ya mpumbavu kwa njia ya maneno.
Vilevile, mtu anapotafakari kitu kwa muda mrefu. (Isaya 29:8)
Tena itakuwa kama mtu mwenye njaa aotapo, kumbe anakula ; lakini aamkapo,nafsi yake haina kitu…
(ii) Ndoto au maono yanayotoka kwa shetani.
Ndoto hizi,huambatana na vitisho,hutuondolea amani, kuogofya na kutuacha katika hali ya taharuki ya woga. Ndoto hizi huchosha mwili na akili. (Ayubu 7 :14) Biblia inasema « ndipo unitishapo kwa ndoto,na kunitia hofu kwa maono ».
Hizi ndoto hazitoki kwa Mungu kwa kuwa Mungu kamwe hawezi kutupa ndoto za namna hii (2Timotheo 1 :7) « Maana Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi »

MAKUSUDI YAKE NI NINI ?


Kutupoteza na kutupeleka mbali na neno la Mungu.

(Zaburi 119 :95,Ufunuo2 :20 1Yohana2 :26)
Kutuonea. (Matendo 10 :38)
Kututesa. (1Petro 5:8-9)
Kutushambulia kwa kutumia sura za kutisha. (Ayubu 16:14).
Kuitichafua miili yetu kupitia ndoto za uasherati na uzinzi na mapepo au watu/mizimu Yuda (1:6-8)
Kututisha na kutupa hofu ili tusiendelee.(Ayubu 7:13-15)

(iii) Ndoto au Maono Yanayotoka Kwa Mungu.(Mwanzo 20:3,Kutoka 3:2)

Tofauti ya zile za Shetani, hizi huambatana na amani ya Mungu!hii ni kwa kuwa Mungu ni wa amani wala si wa machafuko. Hivyo, ndoto yoyote unayoona inaleta machafuko,ujue si ya Mungu.

MAKUSUDI YA NDOTO HIZI NI YAPI ?


Mungu, hutumia njia hii kuwasiliana na watu wake. Mawasiliano haya huwa na shabaha anuwai (Ayubu 33 :14-15) kama ifuatavyo :

Kutupa maelekezo (Mathayo 2:13, Matendo 9 :10-12,Mwanzo 20 :3-7)
Kutuonya/Kututahadharisha juu ua hatari (Matahyo 2:12, Mwanzo 31:24)
Kufanya mawasiliano nasi na kutueleza au kutulewesha mambo mbalimbali Mwanzo 28:10-16,1Wafalme 3:5-15)
Kutuondolea mashaka na wasiwasi juu ya jambo ie kutuongoza palipo sahihi.
(Mathayo 1:20,Matendo 16:6-10)
Kumshughulikia mtu ili kuubadiri mwelekeo wake usio sahihi pengine. (Mathayo 27:19)
Hutuonyesha mambo tusiyoyajua kwaajili ya kanisa au sisi binafsi (Ufunuo 1:1)

Namna ya Kupata tafsiri ya Ndoto au Maono yatokanayo na Mungu.

Kama nilivyotangulia kusema, hakuna kanuni maalum wala taaluma inayohusiana na vitu hivi, hivyo kwa kutumia mawazo yetu au hekima zetu wenyewe si rahisi kupata tafsiri sahihi. Tutajidanganya wenyewe na hapo ndipo tunapopaswa kukumbuka (Mwanzo 40:8) Wakamwambia, tumeota ndoto wala hapana awezaye kufasiri.Yusufu akawaambia, kufasiri ndoto si kazi ya Mungu?Tafadhari mniambie.
HATUA KATIKA KUPATA MAJIBU YA NDOTO/MAONO.
1. Mara tu, baada ya maono au ndoto kuisha, muda ule ule, unapaswa kutulia kimya na kutafakairi kwa muda, na hapo ndipo roho wa Mungu anapoweza kutupa maelezo ya maono/ndoto hiyo (Matendo 10:9-20).izingatiwe kuwa si lazima Mungu afanye hivyo kwa muda huo, hivyo endapo hatafanya hivyo, ni vema sasa ufuate hatua ya pili ambayo ni hii ifuatayo.

2. Kumwomba Mungu tafsiri moja kwa moja.

Baada ya kutulia kwa muda,kama hujapata tafsiri, tunapaswa kumwomba Mungu mwenyewe atafsiri (Daniel 2:16-19). Na endapo hatujapata majibu bado, tunapaswa kulala na hata kuisahau ndoto hiyo,hapo Mungu huweza kukuletea ndoto ile ile tena huku akiifafanua kwa namna flani. Anaweza kuleta moja au hata zaidi. Tunapaswa kuwa na subira pia (Mwanzo 41:17-23) kwani pengine, anawezaa kukukumbusha juu ya matukio utakayo yaona katika maisha yako siku zitakazofuata. (Waamuzi 7:7-15)
3. Kuuliza Katika Maono au Ndoto.
Hatua hii, hutumika mara unapokuwa unapewa maono moja kwa moja kutoka kwa wale watu au viumbe wanaokuwa wanakupa ujumbe huo. Mara zote, kiumbe yeyote atakaye kuja kwako, atajitambulisha kuwa yeye ni nani na ametumwa na nani kwako, kisha ndiyo atatoa ujumbe aliotumwa kwako. Kama ni malaika wa Mungu, kwanza atakusalimia kwa salamu ya Usiogope na hapa utajisikia amani sana moyoni mwako (Daniel 10 :19, Luka 1 :13, 30) na endapo utaendela kuogopa kemea kwa jina la Yesu, huyo hatakuwa Malaika. Matokeo ya kukemea yatakuthihirishia kuwa huyo ni nani.
Angalizo ; malaika yeyote atakayetumwa kwako atakapojitambulisha, atakachokwambia utapaswa kukipima kulingana na neno la Mungu. Mfano, akikwambia umechanguliwa kuliko wanawake wote duniani kuwa utamzaa masihi wa Bwana.Lazima ujue kuwa hiyo si kweli, kwani masihi alisha kuzaliwa miaka zaidi ya 2000 iliyopita.

Izingatiwe kuwa, Mungu huweza kutuma ujumbe kwako kupitia malaika wake au watu walio hai wala si watu waliokufa kama vile mitume n.k. mfano, ukisikia mtu anajitambulisha kwako akikwambia kuwa yeye ni Paulo,Ayubu,Bikra Mariam n.k. ujue huo ni ujanja wa shetani anataka akutapeli kwa kukudanganya.

Tahadhari : wakati mwingine unaweza ukatokewa na kiumbe atakayejitambulisha kwako kama « Malkia wa Mbingu » huyu kiumbe alikuwepo tangu enzi zile za nabii Yeremia huko Misri (Yeremia 6 :18 )na kwa kuwa hujitambulisha kama mtakatifu, bais amewapoteza watu wengi wa Mungu kwa kutolijua neno hili. (Yeremia 44 :17-19,25).
Kiumbe huyu ndiye aliye watokea watoto wa Fatma yaani Lusia, Franscis na Yasinta akijitambulisha kuwa yeye ni Bikra Maria na kuwafundisha wasali rozali. Izingatiwe kuwa Yesu, alisha tufundisha namna ya kuomba, kuwa ni kupitia jina lake tu, pia akasema kuwa yeye ni mwanzo na mwisho (Ufunuo 22 :13) hivyo, hatutegemei kusikia mtu mwingine atakaekuja kwa lolote badala yake. Lakujihadhari sana ni kuwa, pepo huyu anauwezo wa kufanya miujiza kama ya Yesu, hivyo ni lazima kuwa makini ili asije akaliteka kanisa.

4. Kutosumbuka tusipopata tafsiri ya Ndoto.

Kama Mungu ametuma ndoto kwako, hakika atakupa na tafsiri yake. Endapo utazingatia vigezo vyote hapo juu bado usipate majibu tulia, Mungu mwenyewe atashughulika na tafsiri ya ndoto hiyo.(Luka 12 :25-26). Hii inatokana na kwamba, ndoto hii inaweza ikawa imetokana na nafsi zetu wenyewe, au shetani au pengine ikawa ni ya muda mrefu sana ujao, hivyo tafsiri yake si ya lazima kwasasa. Lamsingi, tunapaswa kutunza kil akitu kwenye kumbukumbu sahihi. (Habakuki 2 :2-3, Daniel 10 :14)
HITIMISHO.
Tunapaswa kuzipinga ndoto na maono ya kufarakanisha kwani hazitoki kwa Mungu hizo. Shetani ni mfitini, hutumia ndoto na maono ili kutugombanisha. Hapendi aone upendo, amani na ushirikiano baina yetu,hivyo huchukua mwanya wa maono na ndoto kuonesha madhaifu ya wenzetu ili tudhoofishane, tusiaminiane. Tuwaone wenzetu watenda maovu kama vile wachawi,wazinzi,n.k. ili kupanda mbegu ya chuki miongoni mwetu. Ndoto kama hizi tunapaswa kuzitupilia mbali kwani ni za baba wa uongo si za Mungu.Kamwe Mungu hawezi kutuonyesha ubaya wa wengine bali hutuonyesha ubaya wetu wenyewe ili tuweze kutubu (Mithali 6 :16, Yakobo 3 :15-17 ;Daniel 5 :1-6).

Mwl Sospeter Simon S. Ndabagoye

New Elshaddai Ministries NEM-Tanzania.

Comments