KUMSHUKURU MUNGU NI LAZIMA



   




Bwana YESU KRISTO asifiwe rafiki popote ulipo, 


Nakukaribisha tujifunze kuhusu kumshukuru MUNGU na faida zake.

Mfano wewe ni Baba/Mama na una watoto wako ambao mara kwa mara huwa unawaletea zawadi lakini katika hao mmoja hukushukuru kila ukimpa zawadi na mwingine hana habari na kukushukuru na kila mara unawaletea zawadi, je ni yupi kati ya hao watoto wako ambaye utapenda kumletea zawadi kila siku? Ukweli ni kwamba yule anayethamini zawadi yako kwa kukushukuru kila siku ndio utakuwa unatamani kumletea zawadi kila siku. Na kwa MUNGU ni hivyo wale wanaorudisha shukrani huwathamini zaidi kuliko wasio na shukrani. Ndugu kushukuru ni muhimu sana na kama huna utaratibu wa kumshukuru MUNGU anza leo tena kila ukiomba au kupokea toka kwake shukuru ndugu.

-Kwa wateule kumshukuru MUNGU ni jambo la lazima maana kufanya hivyo inaonyesha kwamba ulimtegemea MUNGU  na ulihitaji msaada wake na bado unaamini hata kwa yale unayotarajia au hujapokea, utapokea muda mfupi ujao.

-Kumshukuru MUNGU ni kurudisha shukrani kwake kwa fadhili alizokutendea.

-Kumshukuru MUNGU ni kuthibitisha kwamba MUNGU anaweza kukutendea muujiza hata kwa yale ambayo bado hujapokea yaani kwa imani unaamini utapokea na kwa kweli tendo hili ni tendo la imani sana yaani unakuwa na uhakika kwamba utapokea tu hata iweje.


-Kumshukuru MUNGU ni kumwonyesha shetani na adui zako wote kwamba MUNGU ndiye msaada wako na atakushindia.

-Kumshukuru MUNGU ni kuonyesha kwamba kiwango chako cha imani  kwa YESU KRISTO ni kikubwa sana maana una uhakika kwamba amekutendea tayari na bado atakutendea tena na tena. Ni tendo la imani kwamba jambo hilo uliloomba kwa MUNGU tayari limetendeka kwenye ulimwengu wa roho na sasa bado kidogo tu litatimia kwenye ulimwengu wa mwili.


-Kumshukuru MUNGU ni kuonyesha kwamba shetani ameshindwa kwako.


-Kumshukuru MUNGU ni kumwaibisha shetani na malaika zake.

MUNGU akupe ufahamu wa kumshukuru siku zote katika jina la YESU KRISTO.

Katika Zaburi 9:1-2 inasema ‘’Nitamshukuru BWANA kwa moyo wangu wote; Nitayasimulia matendo yake yote ya ajabu. Nitafurahi na kukushangilia wewe; Nitaliimba jina lako wewe uliye juu” Mtumishi wa MUNGU hapa anasema atamshukuru MUNGU siku zote yaani siku zote za mwaka na haya ndiyo yanatakiwa yafanywe na wewe ndugu yangu  unayesoma ujumbe huu, na mimi naamini kila mtu ana sababu ya kumshukuru MUNGU siku zote maana pumzi na uzima aliokupa MUNGU ni zawadi ambayo lazima umshukuru MUNGU kila siku maadamu uko hai maana ni kwa neema yake,  

Ndugu uwe katika imani na matendo ambayo yanasema ‘’MUNGU ananionaje  na sio kwamba watu wananionaje’’.

Ukimwangalia MUNGU utamshukuru kila saa lakini ukiwaangalia wanadamu  utashindwa kumpa MUNGU utukufu wake kwa kumshukuru. Liko tatizo kwa watu wengi na hata tatizo hili lipo hadi kwa baadhi ya wahubiri mfano wakati wa ibada ya maombi kipindi ambacho kanisa linatakiwa liombe rehema kwa MUNGU na kumshukuru MUNGU ndio wakati wa mchungaji au Nabii au Mtume kuomba bila kutumia Mic au kuomba kwa sauti ya chini chini kwa sababu ya kuwatazama wanadamu badala ya kumtazama MUNGU. Mtumishi mwenzangu katika KRISTO naomba tumpe MUNGU utukufu wote sio tunaomba kwa sauti wakati tu tunaomba MUNGU atuinue kihuduma lakini wakati wa kutubu na kumshukuru MUNGU tunazima mic na kuomba kwa sauti ya chini sana.


Ndugu yangu kushukuru MUNGU  ni jambo ambalo hata BWANA YESU alitufundisha mfano angalia Mathayo 5:11-12(Heri ninyi watakaowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo kwa ajili yangu. Furahini na kushangilia kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa ndivyo walivyowaudhi manabii waliokuwa kabla yenu’’ Ndugu ni vizuri kusema ‘’Asante BABA wa mbinguni’’  hata kama unapitia kwenye hali ngumu ila weka imani kwamba MUNGU yuko pamoja na wewe na muujiza wako uko karibu sana.


BWANA YESU anatutaka tushukuru kwa kushangalia na kufurahi.

Hana aliomba maombi ya shukrani baada ya kupata mtoto Samweli na MUNGU baada ya maombi hayo ya kushukuru ya Hana alimpa watoto wengine watano(5) hii iko 1 Samweli 2:1,2,10,21.(Naye Hana akaomba, akasema, Moyo wangu wamshangilia BWANA, Pembe yangu imetukuka katika BWANA, Kinywa changu kimepanuka juu ya adui zangu; Kwa kuwa naufurahia wokovu wako;  Hakuna aliye mtakatifu kama BWANA; Kwa maana hakuna ye yote ila wewe, Wala hakuna mwamba kama MUNGU wetu....... Washindanao na BWANA watapondwa kabisa; Toka mbinguni yeye atawapigia radi; BWANA ataihukumu miisho ya dunia......Naye BWANA akamwangalia Hana, naye akachukua mimba, akazaa watoto, wa kiume watatu na wa kike wawili. Naye huyo mtoto Samweli akakua mbele za BWANA. )
-Ndugu mshukuru MUNGU kwa hicho kimoja alichokupa ili azione shukrani zako na kukupa vingine 5 kama alivyofanya kwa Hana. Lakini kama tukiwa hatuna shukrani kwa MUNGU tunaweza hata kunyang’anywa hata hicho kimoja tulichonacho.
Katika 2 Nyakati 20:21(
Naye alipokwisha kufanya shauri na watu, akawaweka wale watakaomwimbia BWANA, na kumsifu katika uzuri wa utakatifu, wakitoka mbele ya jeshi, na kusema, Mshukuruni BWANA; kwa maana fadhili zake ni za milele. ) ni mambo ya kumshukuru MUNGU pia katika Zaburi 107:1(Mshukuruni Bwana kwa kuwa ni mwema, Kwa maana fadhili zake ni za milele.), Zaburi 118:21 pia katika Isaya 12:4.
BWANA YESU alishukuru hata kabla ya kupokea kutoka kwa BABA yake iko Mathayo 26:27.

Katika Warumi 14:9 pia katika 1 Kor 15:57 Hii inaonyesha kumshukuru MUNGU ni jambo la lazima kwa wateule wake KRISTO.

-Ndugu shukuru hata kwa ajili ya wengine, shukuru kwa ajili ya mmeo/mkeo ambaye MUNGU amekupa, shukuru kwa ajili ya Watoto wako ambao MUNGU amekupa, shukuru kwa ajili ya mchungaji wako, Mama yako ,Baba yako, kiongozi wako na hata kazi yako ambayo MUNGU amekupa.

Waefeso 1:16 inatufundisha kumshukuru sana MUNGU maana kwa kuonyesha shukrani ndio kuendelea kupokea zaidi.

Tunatakiwa kumshukuru MUNGU bila kukoma 1 Thesalonike 2:13 pia 1 Thesalonike 5:16:22. Na wakolosai 1:3.

Tudumu katika kuomba huku tukimshukuru MUNGU kila iitwapo leo. Wakolosai 4:2.

Maombi

Asante BABA wa mbinguni kwa somo hili linalonijurisha kwamba nimepokea kutoka kwako na pia nitapokea zaidi kutoka kwako baada ya mimi kuwa mtu wa kukushukuru . Asante BWANA kwa uzima wa milele ulionipa kupitia Mwanao YESU KRISTO, Hakika unastahili kushukuriwa MUNGU siku zote na miaka yote, unayenilinda ushukuriwe milele katika jina la YESU KRISTO. Amen.

MUNGU akubariki sana .
By Mwl Peter Mabula.
Mtenda kazi katika shamba la Bwana YESU KRISTO Mwokozi 
+255714252292(Whatsapp)

Comments