Mtumishi wa MUNGU, Askofu Zacharia Kakobe |
Akizungumza katika mahojiano ofisini kwake
mwishoni mwa wiki iliyopita, NiweMugizi alitaka Serikali kutobeza maoni
ya wananchi wanaotaka Serikali ya Tanganyika kwa kuwa muungano uliopo
unaunganisha nchi mbili.
Kauli hiyo inarandana na ile iliyotolewa na Askofu
Kakobe juzi wakati akitoa mahubiri ya Pasaka, aliposema anaungana na
Watanzania wanaodai Serikali ya Tanganyika na kuahidi kuwapa ari na
shauku ya kuhakikisha inapatikana.
NiweMugizi ambaye pia ni Makamu wa Rais wa Baraza
la Maaskofu Tanzania (TEC), alisema ukosefu wa elimu ya uraia kwa
Watanzania wasomi na wananchi, ndiyo kikwazo cha kutetea uzalendo kwenye
muundo wa Muungano.
Alisema katika miaka 50 ya Muungano wa Tanganyika
na Zanzibar, kumeibuka mambo mengi ya mpasuko wa umoja uliokusudiwa na
waasisi wa kufanya mataifa mawili kuwa moja.
Alisema ili kuhakikisha Tanganyika inapatikana,
lazima Serikali ya Jamhuri ya Muungano ikubali kuwa shirikisho, kwa kila
nchi kupoteza baadhi ya mamlaka na masilahi ya taifa.
Pia, alisema katika kuanzisha Taifa la Tanzania,
mamlaka zilizokuwapo Umoja wa Mataifa (UN), ziliondolewa kwa nchi ya
Tanganyika na Zanzibar na kuunda kiti kimoja cha Tanzania.
“Zanzibar kutangaza kuwa ni nchi ndani ya nchi
nyingine kwa mamlaka kamili ya Serikali na kutaka kujiunga na taasisi za
kimataifa, inaonyesha kuwa Tanzania imemeguka kipande katika Muungano,”
alisema Askofu NiweMugizi.
Alisema Muungano wa sasa una nyufa nyingi zaidi ya zile alizoona Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere na viongozi wengine.
Alisema miongoni mwa mambo yanayosukuma wananchi
kudai Tanganyika ni kupewa elimu ya uraia kufahamu vyema historia ya
Muungano na nyufa zilizopo, hasa baada ya Zanzibar kuwa na mamlaka
kamili ya dola.
Alisema wananchi wanatakiwa kuelimishwa zaidi
manufaa ya Muungano, fursa zinazopatikana na changamoto zake katika
kuutetea na kuulinda.
Askofu NiweMugizi alisema serikali mbili ni maoni
ya viongozi waliopo ndani ya CCM, ambao asilimia kubwa hawawakilishi
Watanzania, ingawa ni sehemu ya Wazanzibari na Watanganyika.
Kuhusu mchakato wa Bunge Maalumu la Katiba, huyo alisema
kupatikana kwa Katiba Mpya lazima kuwepo misingi inayotetea haki za
raia, demokrasia ya kweli na utashi wa watawala bila kuingiliwa na
msimamo kisiasa.
Alionyesha wasiwasi wa kupatikana kwa Katiba Mpya,
kwani wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba wanatetea misimamo ya vyama
vyao na hawapo tayari kumsaliti aliyewateua kwa sababu alitangaza
msimamo wake alipolizindua.
“Rais (Jakaya Kikwete) wakati anazindua Bunge hilo
kwa sababu ana mamlaka kisheria, alivunja taratibu, kwani
asingelihutubia Bunge kwa kushinikiza Jaji (Joseph) Warioba kutangulia
kuwasilisha Rasimu ya Katiba,” alisema Askofu NiweMugizi na kuongeza: “Hotuba ilijikita kutangaza msimamo na mtazamo wa
CCM kutaka serikali mbili, kwa kile tunachokiona ni kukumbatia madaraka
ili viongozi waliopo wasipoteze nafasi, watawale milele, hata
waanzilishi wa Tanganyika wapo hadi leo.”
Alisema mchakato wa kuwapata wajumbe wa Bunge
Maalumu la Katiba ulipata hitilafu baada ya kuingiza wabunge wa Bunge la
Jamhuri ya Muungano na Wawakilishi wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar,
ambao kwa kiwango kikubwa ndiyo wasemaji kuliko wajumbe 201 waliotokana
na taasisi mbalimbali za kiraia.
Chanzo:Mwananchi
Chanzo:Mwananchi
Comments