KUKAMATWA UZAO

Na Mchungaji ADRIANO MAKAZI (RP) UFUFUO NA UZIMA MOROGORO


RP Adriano akifundisha somo la wiki  hii "Kukamatwa Uzao"
katika Nyumba ya Ufufuo na Uzima - Bonde la Maono Morogoro

Utangulizi: Somo la leo linaitwa Kukamatwa Uzao”. Katika kitabu cha  Mwanzo 3:15 imeandkwa [nami nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako na uzao wake; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino.]… Mungu alikuwa anaongea na nyoka.  Ukumbuke kuwa nyoka ni ‘mwerevu kuliko wanyama wote’. Kabla ya tukio hili,  nyoka alikuwa amemdanganya Eva pale bustani  ya Edeni. Ilikuwa ngumu kwa nyoka kumwingia Adamu kwa sababu alijua mwanamke ni mtu rahisi kuelewa kuliko mwanaume.  Kwa kawaida mwanamke yupo karibu zaidi  katika ulimwengu wa roho kuliko mwanaume. Mwanamke ni chombo alichotengeneza Mungu  kuuleta ufalme wake duniani, na ndiyo maana Yesu alizaliwa na mwanamke.

Baadhi ya sehemu  kubwa ya Majeshi ya Bwana waliokuwa wanafuatilia somo la wiki  hii iliyopita

Mungu aliweka uadui kati ya uzao wa nyoka  na uzao  wa mwanamke. Je,ni  nyoka yupi ambaye anazungumziwa hapa? Usije ukafikiri nyoka huyu ni sawa na wale watambaao  ardhini. La hasha!!. Huyu 'nyoka' ni 'shetani',  ambaye hapo kabla alikuwa akiitwa Malaika wa Sifa (Lucifer). Watu walimjaza udhalimu Lucifer na akaamua kuasi, ili naye awe na mbingu yake mwenyewe kama ambavyo Mungu naye ana mbingu yake. Baada ya uasi huu, vita ilitokea mbinguni, na imeandikwa katika Kitabu cha UFUNUO 12:7-9…[Kulikuwa na vita mbinguni; Mikaeli na malaika zake wakapigana na yule joka, yule joka naye akapigana nao pamoja na malaika zake; 8 nao hawakushinda, wala mahali pao hapakuonekana tena mbinguni. 9 Yule joka akatupwa, yule mkubwa, nyoka wa zamani, aitwaye Ibilisi na Shetani, audanganyaye ulimwengu wote; akatupwa hata nchi, na malaika zake wakatupwa pamoja naye.]…. Lucifer baada ya uasi huu,  ndiyo akaingia ndani ya mnyama 'mjanja mjanja na mwerevu',  na ambaye ni 'nyoka'. Akiwa bustani ya Edeni, nyoka huyu kabla ya kuingiwa na roho  ya shetani, alikuwa ni nyoka tu wa kawaida.


YOHANA 4:63…[Roho ndiyo itiayo uzima, mwili haufai kitu; maneno hayo niliyowaambia ni roho, tena ni uzima.]… Maneno ni roho. Eva alifanya kosa la kuongea na Yule nyoka, bila kujua kuwa ndani ya nyoka yalikuwepo maneno ya roho la  shetani. Wakati huo wa mazungumzo, Adamu alikuwa hayupo karibu, kiasi kwamba akili ya Eva ilichukuliwa na roho wa shetani na kumtii shetani zaidi badala ya neno la Mungu.

Showers of Glory wa Bonde la  Maono  Morogoro hawakuachwa nyuma, kwani nao walikuwa na staili ya kumchezea Bwana

Uzao wa mwanamke  mbele za Mungu ni kanisa”. Ndiyo maana Yesu Kristo alipowambwa msalabani, alichomwa mkuki ubavuni, na papo hapo Kanisa likazaliwa. Kumbuka, Mungu alitumia ubavu wa Adamu ndipo ambapo Eva alichukuliwa,na hata kanisa lilizaliwa baada ya ubavu wa Adamu wa pili (Yesu Kristo) ulipochomwa kwa mkuki. Shetani anajua adahabu iliyopo: Kwamba uzao wa mwanamke utamponda kichwa nyoka (shetani). Mbinu  anayoitumia  shetani leo ni kujaribu kuukamata uzao wa mwanamke, yaani kanisa.


Shetani anatumia mbinu na mikakati mbalimbali kudhoofisha uzao wa mwanamke. Ni kanisa pekee lina uwezo  wa kupatanisha hata wale wasioelewana hapa duniani.


MWANZO 6:1-4….[Ikawa wanadamu walipoanza kuzidi usoni pa nchi na wana wa kike walizaliwa kwao, 2 wana wa Mungu waliwaona hao binti za wanadamu ya kuwa ni wazuri; wakajitwalia wake wo wote waliowachagua. 3 Bwana akasema, Roho yangu haitashindana na mwanadamu milele, kwa kuwa yeye naye ni nyama; basi siku zake zitakuwa miaka mia na ishirini. 4 Nao Wanefili (Wanefili maana yake ni majitu) walikuwako duniani siku zile; tena, baada ya hayo, wana wa Mungu walipoingia kwa binti za wanadamu, wakazaa nao wana; hao ndio waliokuwa watu hodari zamani, watu wenye sifa. 5 Bwana akaona ya kuwa maovu ya mwanadamu ni makubwa duniani na kwamba kila kusudi analowaza moyoni mwake ni baya tu sikuzote. 6 Bwana akaghairi kwa kuwa amemfanya mwanadamu duniani, akahuzunika moyo.]… Kimsingi ‘Wana wa Mungu’ wanaozungumziwa hapa ni ‘malaika’. Kwa hiyo yalikuja kuwepo kwa mahusiano ya ndoa kati  ya wana wa Mungu na binti  za wanadamu, kwamba kingetokea kizazi kisichokubalika kutokana na ukaidi wake. Waliozaliwa hapa wakawa mchanganyiko,”nusu shetani, nusu mwanadamu”.


MAOMBI:
Enyi mashetani wa aina mizimu,majoka,minugu, achia uzao kwa Jina la Yesu, achia uzao wa mwanamke kwa Jina la  Yesu. Amen.


Children Ministry wa Bonde la Maono,wanakiri kuwa Yesus Kristo yupo mioyooni mwao, na hawatamuacha kamwe.


Wana wa Mungu ni malaika.  Ni viumbe wasio na miili, kwa sababu ni roho. Hata hapa Kanisani,malaika wapo,ingawa si rahisi kuwaona kwa macho. Katika Biblia MWANZO 18:1-2 [Bwana akamtokea Ibrahimu karibu na mialoni ya Mamre, alipokuwa ameketi mlangoni pa hema yake mchana wakati wa hari. 2 Akainua macho yake akaona, na tazama, watu watatu wamesimama mbele yake. Naye alipowaona alipiga mbio kuwalaki kutoka mlangoni pa hema, akainama mpaka nchi,]… Mwanzoni, tunaambiwa ni Bwana ndiyo aliyemtokea,lakini katika mstari wa 2,  Biblia inasema watu watatu‼! Hivi inakuwa je Bwana amegeuka kuwa  mtu? 

Kitendo cha Ibrahimu kuwasujudia hawa watu,ni ishara kuwa alijua kati yao yupo Mungu. Katika tamaduni za Wayahudi, si rahisi kumwinamia mtu ovyo ovyo. Ndiyo maana Mordekai akagoma kumwinamia Hamani.  Hatuwezi kuwasujudia malaika. Ukiona katika Biblia, malaika amesujudiwa, ujue huyo siyo malaika,  bali ni Yesu mwenyewe, na hiyo hali ya kusujudu haiombwi, bali ni mawasiliano yaliyopo kati ya roho na roho. Tofauti ni kuwa, shetani hulazimisha watu wamwabudu au kumsujudia.  Katika wale malaika  watatu, mmoja wao alikuwa ni Yesu mwenyewe, na ndiyo maana Ibrahimu alisujudu.


MWANZO 18:3-14 …[akasema, Bwana wangu, kama nimeona fadhili machoni pako nakuomba usinipite sasa mimi mtumwa wako. 4 Na yaletwe basi maji kidogo mkanawe miguu, mkapumzike chini ya mti huu. 5 Nami nitaleta chakula kidogo, mkaburudishe moyo, baadaye mwendelee, iwapo mmemjia mtumwa wenu. Wakasema, Haya, fanya kama ulivyosema. 6 Basi Ibrahimu akaenda hima hemani kwa Sara, akasema, Himiza vipimo vitatu vya unga safi, uukande, ufanye mikate. 7 Ibrahimu akapiga mbio kwenda kundini, akaleta ndama wa ng'ombe aliye laini, mzuri, akampa mtumishi, naye akahimiza kuiandaa. 8 Akatwaa siagi na maziwa, na ndama aliyoiandaa, akawaandikia mbele yao, akasimama karibu nao chini ya mti, nao wakala. 9 Wakamwambia, Yu wapi Sara mkeo? Akasema, Yumo hemani. 10 Akamwambia, Hakika nitakurudia wakati huu huu mwakani, na tazama, Sara mkeo atapata mwana wa kiume. Sara akasikia mlangoni pa hema iliyokuwapo nyuma yake. 11 Basi Ibrahimu na Sara walikuwa wazee, na umri wao mkubwa, na Sara alikuwa amekoma katika desturi ya wanawake. 12 Kwa hiyo Sara akacheka moyoni mwake, akisema, Niwapo mkongwe, nitapata furaha, na bwana wangu mzee? 13 Bwana akamwambia Ibrahimu, Mbona Sara amecheka akisema, Mimi kweli nitazaa mwana, nami ni mzee? 14 Kuna neno gani lililo gumu la kumshinda Bwana? Kwa muhula wake nitakurudia, wakati huu huu mwakani, na Sara atapata mwana wa kiume.]…. Ibrahimu alifikiria anawanawisha miguu watu wa kawaida,  kumbe walikuwa malaika.


Je tunajua je kuwa hawa walikuwa malaika? Tusome MWANZO 18:16-17 …[Kisha watu hao wakaondoka huko wakaelekeza nyuso zao Sodoma. Ibrahimu akaenda pamoja nao awasindikize. 17 Bwana akanena, Je! Nimfiche Ibrahimu jambo nilifanyalo,]….


MWANZO 19:1…[Basi, wale malaika wawili wakaja Sodoma jioni; na Lutu alikuwa amekaa mlangoni pa Sodoma. Lutu akawaona akaondoka akaenda kuwalaki, akainama kifudifudi.]… Ukumbuke walikuwa watatu,  kati yao,  mmoja ni BWANA na wawili ni malaika. Wanaonekana ni watu, lakini kumbe malaika. Unaweza kuwaona na kuvutiwa nao kwa sababu ya mavazi yao. Siyo kila unayemuona barabarani ni mtu.lazima uwe mjanja kama nyoka na mpole kama njiwa. Ni muhimu  kuzijaribu kila roho kwa Jina la Yesu. lutu alikuwa na maarifa ya rohoni,  na ndiyo maana akaweza kuwabaini hawa watu wawili (malaika) na kwasujudia.


MWANZO 19:4-5..[Hata kabla hawajalala, watu wa mji, wenyeji wa Sodoma, wakaizunguka nyumba, vijana kwa wazee, watu wote waliotoka pande zote. 5 Wakamwita Lutu, wakamwambia, Wa wapi wale watu waliokuja kwako usiku huu? Uwatoe kwetu, tupate kuwajua.]… Watu wa ile nchi walidhani hawa wageni wa Lutu ni watu tu wa kawaida, na si malaika. Kitendo cha wenyeji kutaka ‘kuwajua’ hawa watu  ni kitendo cha kutaka ‘kujamiiana’ nao‼!


MWANZO 19:6-9..[Lutu akawatokea mlangoni, akafunga mlango nyuma yake. 7 Akasema, Basi, nawasihi, ndugu zangu, msitende vibaya hivi. 8 Tazama, ninao binti wawili ambao hawajajua mtu mume, nawasihi nitawatolea kwenu mkawafanyie vilivyo vyema machoni penu, ila watu hawa msiwatende neno, kwa kuwa wamekuja chini ya dari yangu. 9 Wakasema Ondoka hapa! Kisha wakanena, Mtu huyu mmoja amekuja kwetu kuketi hali ya ugeni; naye kumbe, anataka kuhukumu! Basi tutakutenda wewe vibaya kuliko hawa. Wakamsonga sana huyo mtu, huyo Lutu, wakakaribia wauvunje mlango.]… Hiki kizazi kinaonesha jinsi ambavyo kilikuwa jeuri, kwa sababu walitaka kufanya jambo  hili hata kwa Lutu  mwenyewe.


MAOMBI:
Kwa Jina la Yesu, Ninaagiza kuanzia sasa,  maadui zako wapigwe kwa upofu kwa Jina laYesu. Naagiza malaika wa Bwana waawpige upofu wanaoitafuta biashara yako, masomo yako, kazi yako, wakutafute na hata wachoke wasikuone tena kwa  Jina la Yesu.  Amen



Unaona hao ni  malaika lakini wamevaa miili ya wanadamu. Lakini kwa sababu wanadamu na tamaa zao, wakataka kufanya nao mahusiano ya kindoa.


MAOMBI:
Enyi mashetani mliokamata uzao wangu achia kwa Jina la  Yesu. Navunja mikataba yote, navunja makubaliano yote kwa Jina la Yesu. Ninanyausha miti yenu, matunda yenu, kwa Jina la Yesu. Amen.



Hata sasa,  wapo mashetani waliovaa miili ya wanadamu na wewe bila kujua unahisi ni wanandamu wenzako. Wapo watu  wanaosumbuliwa na majini, na wanakuwa na mahusiano ya kukutana kimwili na aina hii ya majini mahaba. Mashetani yanapenda sana kufanya mapenzi na wanadamu, ili  kuweza kuwa level moja na wanadamu. Kawaida, katika  ngazi za kiungu, Yupo MUNGU, halafu WANADAMU waliookoka, halafu MALAIKA, halafu MASHETANI.


Kitu cha kuweza kuwaunganisha watu wawilli ni NDOA… Katika kitabu cha MWANZO 2:24…[ 24 Kwa hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja.]… Ndiyo maana Mungu amekataza kitendo cha kufanya ndoa nje ya asiye mume/mke wako.  Maana yake, katika tendo hilo, wengine wanakutana na kufanya ndoa na majini bila kujua,  na kufanyika kuwa mwili mmoja nao!!.


1 KORINTHO 6:15-16…[Je! Hamjui ya kuwa miili yenu ni viungo vya Kristo? Basi nivitwae viungo vya Kristo na kuvifanya viungo vya kahaba? Hasha! 16 Au hamjui ya kuwa yeye aliyeungwa na kahaba ni mwili mmoja naye? Maana asema, Wale wawili watakuwa mwili mmoja.]…. Mashetani yanataka kuwa mwili  mmoja na wanadamu pale wanapooana nao au kufanya nao mapenzi. Hapo ndio mwanzo wa uzao kukamatwa. Mtu anapoota ndoto za yeye  kufanya tendo la ndoa na mtu/watu asiowajua, na kujikuta kweli amejichafua, ni kuwa anakuwa amekwisha unganishwa na huyo mtu/jini katika ulimwengu wa roho. Ujue kuwa mwisho wa yote ni kuzaa watoto katika  ulimwengu wa roho.


1 KORINTHO 7:4…[Mke hana amri juu ya mwili wake, bali mumewe; vivyo hivyo mume hana amri juu ya mwili wake, bali mkewe.].. Mashetani wanajua kuwa, yanapopata fursa ya  kuwa mwili mmoja na mwanadamu, yanaweza kuharibu chochote anachokifanya huyu mwanadamu:  Kuharibu biashara, kuharibu kazi, kuharibu afya, kuharibu masomo na kingine chochote mwanandamu anachokifanya. Kinachofanya haya yatokee ni kwa sababu mashetani yanaitambua hii kanuni  ya kiroho. Jini anapokuwa anammiliki mtu, anataka kuharibu kila alicho nacho huyo mtu.


Baraka za mtu  zipo ndani  ya mtu. Muujiza  wa mtu upo ndani ya mtu.  Inamaanisha kuwa, huwezi kupata maendeleo bila kuhitaji wanadamu wenzako. Ni  kwa Kupitia kwa hao wanadamu, unaweza kuinuliwa au kuangushwa chini. Imeandikwa katika LUKA 2:34….[Simeoni akawabariki, akamwambia Mariamu mama yake, Tazama, huyu amewekwa kwa kuanguka na kuinuka wengi walio katika Israeli, na kuwa ishara itakayonenewa.]….Ni kuwa Yesu aliwekwa kwa ajili ya watu  kuinuka na watu wengine kuangushwa chini. Kwa hiyo, kupitia kwa Yesu,  wengi wanainuliwa na wengi wanaendelea kushushwa   hadi leo.


Ibrahimu alipoenda Misri, alimshawishi mke wake asije kumuita ni mumewe, bali 'mtu  na kaka yake', ili asije kuuawa na Mfalme wa Misri -  aitwae Abimeleki. Mungu alimtokea Abimeleki katika ndoto  na kumzuia asifanye jambo lolote na Sara. Hii ni kuonesha kuwa ndoto ni bayana, na kwamba Mungu  anaweza kuzungumza  na mtu  kwa njia ya ndoto.


MAOMBI:
Enyi mashetani mliokamata uzao wangu, nawatoa nje kwa Jina la Yesu.  Naharibu nguvu zenu kwa Jina la Yesu. Enyi majini  mahaba, naharibu mtandao  wenu kwa Jina la Yesu.  kwa maana imeandikwa 'tokeni katikati yao,  mkajitenge nao', leo  najitenga nanyi kwa Jina la Yesu. Leo nawapiga mashetani wote na kuwaangamiza,  napiga ndoa za kiroho, kwa Damu ya Mwanakondoo, Kwa Jina la Yesu. Amen.


"I surrender to Jesus".... Ndivyo mioyo ya watu  hawa inavyosema,baada ya kumuacha shetani na kuujia msalaba wa Yesu
kwa Maamuzi ya Kuokoka. Picha hii ni sehemu ya watu waliompa Talaka Shetani Jumapili iliyopita

Endapo wewe hujaokoka, ni  vyema kufanya maamuzi hayo kwa sababu huwezi kuangamiza uzao  wa shetani wakati wewe upo mikononi mwake shetani. Maamuzi ya kuokoka ni maamuzi ya kukuweka salama,  ili  uweze kuungamiza uzao  wa  shetani ukiwa mikononi mwa Yesu Kristo.

Comments