TOFAUTI YA BIBLIA YA VITABU 66 NA ILE YA VITABU 72



BWANA YESU asifiwe.
Karibu tujifunze jambo kuhusu na Biblia Takatifu.
Naandika haya baada ya kuulizwa na rafiki yangu mmoja aliyetaka kujua tofauti ya Biblia ya vitabu 66 na ile Biblia ya vitabu 72. Rafiki yangu alisema hivi ''  Kaka Biblia jumla inavitabu vingapi? Wengne wanasema 72 au 66,naomba msaada wako ndugu yangu''
Karibu tujifunze.

Biblia takatifu imeandikwa kwa miaka 1500 na imeandikwa na waandishi 40 ambao waliongozwa na ROHO MTAKATIFU kuandika, Ndio maana unaweza ukashangaa kwa mfano Musa alindika kuhusu uumbaji wa MUNGU, Musa hakuwepo wakati wa uumbaji lakini ROHO wa MUNGU alikuwepo na ndio maana aliwafunulia wanadamu na wakatambua . 2 Petro 1:21 '' .
Maana unabii haukuletwa po pote kwa mapenzi ya mwanadamu; bali wanadamu walinena yaliyotoka kwa MUNGU, wakiongozwa na ROHO MTAKATIFU. '
' Kitabu cha Ayubu ni moja ya vitabu ambavyo viliandikwa zamani zaidi Mwandishi akiwa Musa lakini Musa hakuwepo wakati wa Ayubu,  ROHO wa MUNGU alimwambia Mwandishi huyo wa kitabu hicho cha Ayubu.

Ndugu zangu ROHO MTAKATIFU ni wa milele na ndiye msimamizi wa waandishi wote wa Vitabu vya Biblia. 2 Timotjeo 3:16 '' Kila andiko, lenye pumzi ya MUNGU, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki  ''

Unaweza ukaona hapa jinsi MUNGU akimwambia mmoja wa waandishi wa Biblia aandike kile anachoelekezwa na yeye mwenyewe MUNGU  Kutoka 17:14-15 '' BWANA akamwambia Musa, Andika habari hii katika kitabu iwe ukumbusho, kisha ihubiri masikioni mwa Yoshua; ya kuwa nitaufuta ukumbusho wa Amaleki kabisa, usiwe tena chini ya mbingu. Musa akajenga madhabahu, akaiita jina lake YEHOVA-nisi; '' 
Biblia imedumu sasa kwa zaidi ya miaka 3500. Ni kitabu sahihi pekee maana vitabu vyote ambayo vilikuja baadae vya dini mbalimbali waandishi wake walikopi tu baadhi ya vitu ambayo viko kwenye Biblia na na kuviweka kwenye maandiko yao kwa kuchanganya na uongo  ili tu kuhakikisha wanadamu hawaendi uzima wa milele. Jina ''Biblia'' linatokana na neno ''Bablos'' ambalo maana yake ni kitabu cha vitabu. 
Biblia sahihi ni ile yenye vitabu 66 Nitatoa ufafanuzi hapo chini.
Agano la kale lina vitabu 39 ambavyo viko katika makundi 5.
1. Vitabu 5 vya Musa au vya sheria.
2.Vitabu 12 Vya Historia.
3. Vitabu 5 Vya Mashairi.
4. Vitabu 4 Vya Manabii wakubwa.
5.Vitabu 12 Vya Manabii wadogo.

Agano jipya lina vitabu 27 ambayo vimepangwa katika makundi 5.
1. Vitabu 4 vya injili.
2. Kitabu 1 Cha Historia.
3.Nyaraka 13 za Mtume Paulo.
4. Nyaraka 8 za Mitume wengine.
5. Kitabu 1 cha Ufunuo.

Wakatoliki ambao hutumia Biblia ya vitabu 72 wameongeza vitabu vifuatavyo
Tobiti, Judithi, Hekima ya Yoshua bin sira,Baruku pamoja na waraka wa Yeremia, 1 Makabayo na 2 Makabayo.

Shabaha ya Biblia ni wanadamu walijue MUNGU muumbaji wao na ili wakombolewe.
 Biblia sahihi ni ile yenye vitabu 66 kwa sababu ya vipimo hivi vichache ambayo kila mtu atajua kwa urahisi zaidi.

1- Baada ya BWANA YESU kuja na kuanza huduma yake ya injili ya miaka 3 na nusu  muda mwingine alikuwa akisema maandiko ambayo yako Agano la Kale kwamba ''Imeandikwa'' na alisema maneno mengi ambayo yako katika agano la kale. Hata siku moja BWANA YESU hakusema au kutamka andiko ambalo halimo katika vile vitabu 39 vya agano la kale. Hivyo huo ni ushahidi wa kwanza kwamba vitabu 6 vilivyoongezwa na wakatoliki sio neno la MUNGU ila ni maandiko tu ya zamani.

2-  BWANA YESU alithibitisha kwamba Torati, Manabii na Zaburi ni maandiko matakatifu na ni neno hai la MUNGU(Luka 24:44-46, Kisha akawaambia, Hayo ndiyo maneno yangu niliyowaambia nilipokuwa nikali pamoja nanyi, ya kwamba ni lazima yatimizwe yote niliyoandikiwa katika Torati ya Musa, na katika Manabii na Zaburi. Ndipo akawafunulia akili zao wapate kuelewa na maandiko. Akawaambia, Ndivyo ilivyoandikwa, kwamba KRISTO atateswa na kufufuka siku ya tatu; ) Je vitabu hivyo 6 vilivyoongezwa viko kundi gani? Haviko kundi lolote.

3.Vitabu hivyo 6 Wayahudi walikuwa navyo kama vitabu tu vya zamani ila havikuwa katika kundi la Neno la MUNGU. Viliitwa Apokrifa. Kumbuka injili tumeipokea kwa Waebrania hivyo hatuwezi kuongeza vitabu ambayo waebrania hawakuviweka katika orodha yao ya maandiko matakatifu. Hata leo vitabu hivyo 6 waisraeli wanavyo lakini haviko kwenye Biblia yao.

4. Kila  kitabu cha Biblia kina uhusiano na vitabu vingine vya Biblia hakini hivi 6 wala havina uhusiano na maandiko mengine matakatifu.

5.  Vitabu hivyo 6 Wakatoliki waliviongeza kwenye Biblia yao mwaka 1546. Ni wakati ambao wakatoliki  walikuwa na mgogoro mkubwa  huko ulaya kwa sababu ya matengenezo ya akina MartinLuther ambao waliamsha kanisa kutokana na upotovu wa kanisa katoliki. Wakatoliki walikaa baraza kubwa maarufu kwa jina la ''Council of trent'' ambalo husifiwa hata leo,  na walikubaliana kwamba atakayevikataa vitabu hivyo alaaniwe wakitumai kuwalaani waprotestanti.

6. Hata leo wakatoliki wenyewe hawategemei vitabu hivyo 6 kama neno la MUNGU. Hata mimi niliwahi kusali RC lakini sikuwahi kusikia maandiko hayo ya hivyo vitabu 6 yakisomwa. Ukweli ni kwamba maandiko hayo hayana uvuvio.

7. Papa Damasus 1 ndiye aliyeweka kwa kulazimisha vitabu hivi 6 viongezwe kwenye Biblia ya kikatoliki. Ni mbaya sana. Na ndio maana Vitabu vya Ufunuo, Danieli na vingine vilisema juu ya Hayo waliyafanya wakatoliki na utawala wa rumi ni moja ya tawala  ambazo ziko upande wa shetani kwenye Biblia.
Ziko sababu nyingi hata hivyo kwa leo naishia hapo. asante kwa kusoma na kuelewa.
Dhehebu halimpeleki mtu uzima wa milele ila anayepeleka watu uzima wa milele ni BWANA YESU peke yake. 
KUOKOKA NI JAMBO LA LAZIMA KWA KILA MTU.
Ndugu zangu, tupite kupitia Mlango ulio mwembamba. Mathayo 7:13-14 '' Ingieni kwa kupitia mlango ulio mwembamba; maana mlango ni mpana, na njia ni pana iendayo upotevuni, nao ni wengi waingiao kwa mlango huo. Bali mlango ni mwembamba, na njia imesonga iendayo uzimani, nao waionao ni wachache.   ''
  Kwa sasa naishia hapo, MUNGU akitupa nafasi tutajifunza tena siku nyingine.na kama hujampokea BWANA YESU muda wa kumpokea ni leo wala sio kesho, amua leo na atakuandika jina lako katika kitabu cha uzima na utaanza kuukulia wokovu kwa mafundisho kanisani. MUNGU ana makusudi kabisa na wewe, hataki upotelee motoni anataka uende uzimani aliko KRISTO BWANA.
MUNGU akubariki sana .
Ni mimi ndugu yako
Peter M Mabula
Maisha ya Ushindi Ministry.
0714252292
mabula1986@gmail.com
MUNGU akubariki sana uliyesoma somo hili.

Comments