AFRIKA YA KUSINI YAMKAMATA NABII ANAYELISHA WAUMINI NYOKA


Nabii Penuel Mnguni akiwa katika moja ya ibada za katikati ya wiki kanisani kwake 


Polisi nchini Afrika ya kusini wanamshikilia nabii anayejizoelea waumini kwa kuwalisha nyoka na nywele aitwaye Penuel Mnguni baada ya shirika linalojihusisha na masuala ya wanyama nchini humo la SPCA kutoa malalamiko yao Polisi dhidi ya nabii huyo wa huduma ya 'The End Times Disciples Ministries". 

Kwa mujibu wa taarifa kutoka kwa msemaji wa polisi huko Pretoria nchini Afrika ya kusini kapteni Rheineth Motlana amesema walianza kumtafuta nabii huyo siku ya ijumaa iliyopita bila mafanikio baada ya shirika hilo dhidi la wanyama kutoa malalamiko yao dhidi ya mchungaji huyo , ambapo Polisi waliweza kumkamata siku ya jumamosi ambapo alishinda kituo cha polisi cha Ga-Rankuwa toka siku hiyo ya jumamosi na hapo jana siku ya jumatatu alitarajiwa kupandishwa mahakamani kujibu mashitaka yake imeandika tovuti ya IOL ya nchini humo.

 Aidha kukamatwa kwa nabii Mnguni lilikuwa pigo kwa waandishi wa habari ambao walipewa mwaliko na nabii huyo kuhudhuria ibada ya jumapili ili wapate kujionea miujiza itakayotendeka. Inspekta Andrew Kekana wa taasisi ya kulinda manyanyaso dhidi ya wanyama (SPCA) amesema baada ya kujilidhisha na upelelezi wao dhidi ya nabii huyo ndipo walipoamua kumfungulia mashitaka. Inspekta Kekana amedai kwamba mashitaka waliyomfungulia nabii huyo ni kuhusiana na matumizi yake juu ya nyoka hao wanaolindwa kuangamizwa. "Tunaamini ni jukumu letu pale tunapoona haki za wanayama zinavunjwa wahusika lazima wawajibishwe kwa vitendo vyao", alisema Kekana. 
 
Kukamatwa kwa nabii Mnguni kunafuatia taarifa za mtume huyo kupamba vichwa vya habari vya magazeti na vinginevyo pamoja na mitandao ya kijamii akiwalisha waumini wake nyoka, nguo, nywele pamoja na kuwafanya wengine farasi kwa kuwapanda katika ibada zake. Ambapo moja ya picha iliyowekwa kwenye ukurasa wa facebook wa huduma ya nabii huyo ulimkariri muumini aliyekuwa anakula nyoka akidai wanaladha ya chocolate.

 Kitendo cha kukamatwa kwa nabii huyo kimepongezwa na taasisi nyingine zinazojihusisha na kutetea haki za wanyama. "Kukamata , kuwauza na kuua nyoka wanaolindwa ni kinyume cha sheria, tungependa kuona anaacha tabia hiyo" alisema Naude anayejihusisha na masuala ya wanyama. "Maisha yetu yote tunayoishi tumekuwa tukijaribu kuwakamata nyoka kutoka makazi ya watu na kuwapeleka katika mazingira watakayokuwa huru. Hebu fikiria itakuwaje kumla nyoka kipande baada ya kipande akiwa bado mzima? aliuliza Naude. Aidha inadaiwa licha ya nabii huyo kutokuwepo ibadani siku ya jumapili kutokana na kushikiliwa na polisi, ibada kanisani kwake iliendelea kama kawaida ingawa wasimamizi wa ibada waliwazuia wanahabari kuingia kanisani hapo. Ambapo mmoja wa wachungaji ambaye alikataa kuzungumza na vyombo vya habari aliwaambia waumini kutoogopa kwa kile kilichotokea kwasababu watu wengine hawajui kazi za Mungu. 

"Hawawezi kusimamisha kazi ya Mungu kwakuja na malalamiko yao dhidi ya kile cha nabii alichokuwa akikifanya kuwa ni ukatili wa wanyama, jibu ni rahisi kwamba tunachofanya ni kazi ya Mungu" alisema mchungaji huyo.

Comments