USHAURI KWA VIJANA WANAOTAKA KUOA.


Ujumbe wa Leo: 1WaKorintho7:1-2
“Basi kwa habari ya mambo yale mliyoandika, ni heri mwanamume asimguse mwanamke. Lakini kwa sababu ya ZINAA kila mwanamume na awe na mke wake mwenyewe …..”
[Kwa Vijana na Wazee walio washauri wa Vijana]


1. Ninahitaji kuoa lakini Maisha ni Magumu nifanyeje?
Ushauri: Ugumu wa maisha ni wimbo wa Taifa, unajua ni lini maisha yatakuwa Rahisi. Kuna mithali isemayo Mbuzi hula kulingana na urefu wa kamba yake, ili mradi unafanya kazi, kuna vitu vya msingi kuwa navyo kabla ya Kuoa 

(a) Uwe na chumba chako cha kulala nje ya Wazazi 
(b) Uwe na Kitanda na Godolo hata kama ni futi 3 
(c) Uwe na uwezo wa kupata chakula – sio cha kuhemea
 (d) Uwe na uwezo wa kununua nguo.
 (e) Panga kufunga ndoa Rahisi, Gharama ya Ndoa peke yake bila Sherehe haizidi Sh. 20,000/=. Sherehe ya harusi sio lazima kama huna uwezo. 
(f) Usipende makuu na kushindana na wengine, ishi kulingana na uwezo ulio nao. 
(g) Uwe muwazi kwa mwenzio juu ya hali yako.

2. Sioni Binti wa kuoa nifanyeje, karibu wote hawafai na sio waaminifu?
Ushauri: Mwambie mungu akupatie – Mke mwema mtu hupewa na Bwana, Mithali 19:14. Huoni mke anayekufaa kwa sababu unatumia akili yako. Mbona wengi unawatamkia unawapenda?.
Hata hivyo kuna madai juu ya mabinti yanayotakiwa ushauri:


 (a) Mabinti wanapenda Makuu / Expensive – Mwanaume usiwe muoga ongea nae, huenda ni katika harakati za kuji sop sop ili aonekane, pia mabinti angalieni muwe na kiasi katika kuremba, mnawaogopesha Waoaji. 
(b) Mabinti sio waaminifu - Hili ni tatizo la wote wanaume na wanawake: Kama mwanaume kweli ni mwaminifu basi Tulia, Mungu atakupatia Mke mwema, lakini kama kuna sehemu unajituliza! – Ni kujidanganya kutafuta Binti Mwaminifu, Oa huyo unayejituliza kwake. Dawa ni wote kuwa waminifu (KUTOFANYA ZINAA KABLA YA NDOA).

3. Wanaume wanatudanganya mabinti, wanatuchezea halafu hawaoi, tufanyeje?
Ushauri: 

(a) Usikubali kuchezewa, niliwambia, kati ya wanaume 10 wanaokutamkia wanakupenda, unaweza kubahatisha 1 anayekupenda kweli, wote wanasukumwa na tamaa ya mwili, ndivyo walivyoumbwa. Na kwa sababu mnawaruhusu kukata KIU ndio maana hawaoni haja ya kuoa. 

(b) Kama wewe binti ni Mwaminifu kabisa, tunda lako bado halijawahi kuliwa na wadudu waharibifu – Uwe na Subira, Mungu atakupatia Mwanaume atakayekufaa. Usidanganywe na wachumba FEKI wanaotaka Kuonja kwanza ili kuthibitisha kama kweli unawapenda. Sema kama Yusufu “Nitendeje ubaya huu ni mkosee Mungu?”.
Kwa mabinti wote waliopitia changamoto ya Kuchezewa na kuachwa, msikubali kuchezewa TENA, pamoja na kujiona mnakula STAREHE wote, baada ya hapo mwenye hasara ni Binti. Mpeni Mungu maisha yenu, atawasamehe yote mliyotenda, atawafanya viumbe vipya – Mtaolewa tu, kwa Mungu hakuna lisilowezekana.
Kwa wavulana wenye tabia ya UTAPELI WA MAPENZI, acheni tabia hiyo. Tabia ya kuonja onja, mtakuja kuonja SUMU ambayo mwisho ni Mauti. Kuna vijana ni hodari wa ku “TEST” utafikiri ni mafundi magari wanapima OIL. Toeni maisha yenu kwa Mungu na kuamua kuoa, Neno la Mungu linasema ni “Heri kuoa kuliko mwili kuwaka TAMAA”.

By Charlotte Lyzik

Comments