MAMBO MANNE(4) YA KIJANA MTEULE KUZINGATIA.

Na Mtumishi Peter Mabula.

BWANA YESU atukuzwe ndugu yangu.
Karibu tujifunze mambo muhimu ya kuzingatia kwa kijana na kila mpenda uzima wa milele.
Kuna mambo manne nimekuandalia ambayo ukiyazingatia yatakuwa msaada mkubwa kwako.


2 Timotheo 2:21-26 '' Basi ikiwa mtu amejitakasa kwa kujitenga na hao, atakuwa chombo cha kupata heshima, kilichosafishwa, kimfaacho BWANA, kimetengenezwa kwa kila kazi iliyo njema. Lakini zikimbie tamaa za ujanani; ukafuate haki, na imani, na upendo, na amani, pamoja na wale wamwitao BWANA kwa moyo safi. Walakini uyakatae maswali ya upumbavu yasiyo na elimu, ukijua ya kuwa huzaa magomvi.Tena haimpasi mtumwa wa BWANA kuwa mgomvi; bali kuwa mwanana kwa watu wote, awezaye kufundisha, mvumilivu; akiwaonya kwa upole wao washindanao naye, ili kama ikiwezekana, Mungu awape kutubu na kuijua kweli; wapate tena fahamu zao, na kutoka katika mtego wa Ibilisi, ambao hao wametegwa naye, hata kuyafanya mapenzi yake. ''.

Vitu 4 vya kuvizingatia kijana mteule wa MUNGU.

1. Kijana lazima aitafute toba kwa MUNGU kupitia KRISTO YESU na akisha kutakaswa atakuwa chombo safi kifaacho kwa kila kazi njema na tena kitakuwa chombo safi kimfaacho MUNGU.
-Toba hutafutwa maana haiji yenyewe kama hujaamua kuitafuta kwa BWANA YESU kupitia maombi ya kutubu na kuacha dhambi. ukisha kuupata msamaha wa MUNGU unatakiwa uutafute utakatifu. utakatifu hutafutwa tena hutafutwa kwa bidii sana. usipoutafuta utakatifu utabaki mchafu siku zote na hapo hutakuwa chombo safi kimfaacho BWANA. Utakatifu hauji wenyewe bali hutafutwa hivyo kila kijana ni muhimu sana kuutafuta utakatifu.


1 Petro 1:15-16 '' bali kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote; kwa maana imeandikwa, Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu. ''
-Iweni watakatifu maana yake ni jukumu lako kuwa mtakatifu.ni agizo kwako kuutafuta utakatifu ili uuishi.

 
2. Kijana lazima azikimbie tamaa za ujanani.
Tamaa za ujanani ni pamoja na uasherati, kutafuta mali isivyo kihalali, kufanya kila mbinu chafu ili tu uwe kama mtu mwingine, kujiona unao muda mrefu wa kuishi na hivyo kuona kwamba ujana wako ni wakati wa kutenda mabaya ukidhani utatubu uzeeni. hizo ni tamaa za ujanani na Biblia inatuonya kwamba tuzikimbie tamaa za ujanani. Kila kijana lazima ahakikishe anakimbia tamaa za ujanani.
Biblia hapo juu pia imefafanua kwamba tamaa za ujanani zinaweza kuondoa haki, Tamaa za ujanani zinaweza kukuondoa katika imani ya uzima ambayo ni imani katika KRISTO YESU pekee. , Tamaa za ujanani zinaweza kuondoa upendo, Tamaa za ujanani zinaweza kuondoa amani kwako, kwa familia, kwa ukoo na hata kwa taifa.
Kumbe pia Biblia inatushauri vijana kutenda kazi ya MUNGU pamoja na wale wamwitao BWANA kwa moyo safi.
-Kama kijana hatazikimbia tamaa za ujanani ni lazima huyo baadae atakuja kuwaambia watu kwamba '' UJANA NI MAJI YA MOTO''. Ujana umekua maji ya moto kwake kwa sababu hakuzikimbia tamaa za ujanani kama Biblia takatifu inavyoagiza.


1 Yohana 2:15-17 '' Msiipende dunia, wala mambo yaliyomo katika dunia. Mtu akiipenda dunia, kumpenda BABA hakumo ndani yake. Maana kila kilichomo duniani, yaani, tamaa ya mwili, na tamaa ya macho, na kiburi cha uzima, havitokani na BABA, bali vyatokana na dunia. Na dunia inapita, pamoja na tamaa zake, bali yeye afanyaye mapenzi ya MUNGU adumu hata milele. ''


3.Kijana mteule ni muhimu kuyakataa maswali ya kipumbavu ambayo siku zote huibua ugomvi na kumnajisi kijana.
-Maswali ya kipumbavu yasiyo na elimu ni mengi hivyo kijana mwenda mbinguni lazima ajiepushe nayo.
Kama ni maswali ya kipumbavu maana yake yanasemwa na mpumbavu, na maana ya mpumbavu ni mtu yule asiyeamini katika MUNGU aliye hai, maana yake mpumbavu hudhani kwamba hakuna MUNGU au hakuna uzima wa milele au hakuna kuokoka.


Zaburi 14:1 '' Mpumbavu amesema moyoni, Hakuna MUNGU; Wameharibu matendo yao na kuyafanya chukizo, Hakuna atendaye mema.''
-Sifa za mpumbavu husema hakuna MUNGU, Hufanya machukizo na matendo yake ni machukizo kwa MUNGU hivyo uijiepushe na maswali ya kipumbavu maana yanaweza hata kukuondoa katika kusudi la MUNGU.

 
4. Kijana uliyempokea YESU hutakiwi kuwa mgomvi bali mwanana na mvumilivu kuku ukiwafundisha watu uhumimu wa kuokoka katika maisha yao.
unao wajibu wa kuvumilia maana wakati mwingine unaweza ukapitia maeneo au mazingira yanayohitaji uvumilivu. Kijana mcha MUNGU lazima ahakikishe anawaonya kwa upole wao washindanao naye, ili kama ikiwezekana, MUNGU awape kutubu na kuijua kweli; wapate tena fahamu zao, na kutoka katika mtego wa Ibilisi, ambao hao wametegwa naye MUNGU, hata kuyafanya mapenzi yake.
Na siku zote ili uweze kuvumilia ni lazima uwe na upendo maana upendo unaweza ukazaa uvumilivu,
-mfano kijana anayempenda MUNGU ni rahisi kwake kuvumilia matukano kutoka kwa wapingakristo.
-Kijana aliye na upendo kwa ndugu zake ni rahisi sana kuvumilia dhihaka zao huku haachi kuwashuhudia habari njema za ufalme wa MUNGU.


1 Kor 13:4 ''Upendo huvumilia, hufadhili; upendo hauhusudu; upendo hautakabari; haujivuni; ''

-Ndugu,Naamini umejifunza na utachukua hatua njema ya kumpokea BWANA YESU kama hujaokoka ili awe BWANA na MWOKOZI wako tangu leo na utaanza kuishi maisha matakatifu

KAMA UNATAKA KUTUBU RUDIA MANENO HAYA KISHA TAFUTA KANISA LA KIROHO UKAJIUNGE NA KUANZA KUISHI MAISHA MATAKATIFU.

''BABA katika jina la YESU KRISTO Niko mbele zako mimi mwenye dhambi, lakini leo nimetambua kosa langu na naomba unisamehe dhambi zangu zote, nisamehe dhambi ninazozikumbuka na pia zile ambazo sizikumbuki. futa jina langu katika kitabu cha hukumu na uliandike jina langu katika kitabu cha uzima. Neno lako katika Warumi sura ya 10 Mstari wa 9 na wa 10 Neno lako linasema ''Kwa sababu, ukimkiri YESU kwa kinywa chako ya kuwa ni BWANA, na kuamini moyoni mwako ya kuwa MUNGU alimfufua katika wafu, utaokoka. Kwa maana kwa moyo mtu huamini hata kupata haki, na kwa kinywa hukiri hata kupata wokovu '' . BWANA YESU mimi nimekuamini leo na hivyo naamini sasa napokea wokovu wako na hakika nimeokoka. Kuanzia leo Naufunga ukurasa wa dhambi na ninaufungua ukurasa wa matendo mema na matakatifu. BWANA nipe ROHO wako Mtakatifu ili aniwezeshe kushinda dhambi na anasa zote za dunia. Kuanzia leo mimi nimeokoka na ni mtoto wa MUNGU mwenye haki zote. ninafuta laana zote na kila roho ya shetani inayonifuatilia naiharibu kwa jina la YESU KRISTO kama neno la MUNGU linavyosema katika Yeremia sura ya kwanza mstari wa 10. BWANA YESU nakushukuru sana kwa kuniokoa. Yote haya kwa imani nimepokea na niko tayari sasa kwa ROHO MTAKATIFU kunitumia. Katika jina la YESU KRISTO nimeomba na kupokea . Amen.'' Kama umetubu toba ya kweli hakika wewe kuanzia sasa ni mshindi na ni shujaa. Kwa sasa naishia hapo, MUNGU akitupa nafasi tutajifunza tena siku nyingine. ulishindwa kumpokea BWANA YESU nafasi yako bado ipo na muda wa kumpokea ni leo wala sio kesho, amua leo na atakuandika jina lako katika kitabu cha uzima na utaanza kuukulia wokovu kwa mafundisho kanisani. MUNGU ana makusudi kabisa na wewe, hataki upotelee motoni anataka uende uzimani aliko KRISTO BWANA.
MUNGU akubariki sana .
Ni mimi ndugu yako Peter M Mabula
+255714252292 mabula1986@gmail.com
MUNGU akubariki sana uliyesoma somo hili

Comments