JE UNAKOSA USINGIZI? TAHADHARI


Je unakosa usingizi? tahadhari!


Maradhi ya Alzheimer
Tatizo la kukosa usingizi huenda likawa ishara ya kutambua mapema maradhi ya kusahau au ''Alzheimer'' kwa mujibu wa utafiti uliofanywa kwa kutumia panya ambaye ana maumbile yanayofananishwa na binadamu.
Vipande vya protini, kwa lugha ya kitaalamu (plaques) au uchafu kwenye ubongo yanadhaniwa kuwa sehemu nyeti inayosababisha maradhi haya.
Utafiti uliofanywa na kuchapishwa katika jarida la tafsiri ya matukio ya Sayansi, umeonyesha kuwa punde chembe chembe za uchafu ule ulipoanza kukua kwenye ubongo wa panya, usingizi ukaanza kuwa tatizo kwa viumbe hao.
Taasisi inayosimamia utafiti wa maradhi hayo, (Alzheimer's Research UK) imehimiza kuwa ikiwa uhusiano huo unaweza kuthibitishwa huenda ikawa muhimu kwa Madaktari.
Utafiti wa kutaka kugundua mapema kama mtu anaelekea kukumbwa na maradhi ya Alzheimer inadhaniwa kuwa muhimu katika kutibu maradhi hayo.
Wagonjwa hawaonyeshi dalili kupitia hisia au kumbukumbu zao hadi baada ya mda mrefu wa maradhi kumkumba mgonjwa. Yanapofikia hapa sehemu za ubongo huwa zimeharibika kiasi kwamba tiba inakua vigumu kupatikana au hata kushindwa kupatikana.
Ndiyo sababu wataalamu wanafanya juhudi za kuanza mapema kugundua kama mtu atapata maradhi haya, miaka kadhaa kabla ya dalili hizo kujitokeza.
Viwango vya protini ijulikanayo kama Beta Amyloid kimaumbile hupanda na kushuka miongoni mwa binadamu na pia panya katika kipindi cha saa 24. Hata hivyo ni ile protini ambayo hujenga uchafu usiofutika kwenye ubongo na maradhi ya Alzheimer.
Majaribio yaliyofanywa katika Chuo Kikuu cha Washington yameonyesha kuwa panya wanaotoka usiku kwa kawaida hulala kwa dakika 40 kwa kila saa mchana. Lakini ubongo ulipoanza kupatwa na uchafu panya hawa wakaanza kusinzia kwa dakika 30 pekee.

Ugonjwa wa sahau
Mmojapo wa wataalamu, Prof David Holtzman, alisema: "endapo mapungufu katika usingizi huanza mapema kiasi hiki katika ugonjwa wa Alzheimer, mabadiliko hayo yanaweza kutupa ishara ya wepesi wa kuweza kuyatambua maradhi haya."
"ikiwa matatizo haya ya usingizi yapo, hatuelewi hasa yanachukua mfumo gani, kupungua kwa usingizi kikamilifu au ni tatizo la kushindwa kabisa kulala au ni kitu tofauti kabisa."
Hata hivyo, utafiti unaofanyika kwa kutumia panya mara nyingi hayafai kutumika kwa binadamu kwa sababu nyingi zinazosababisha kutatizika na usingizi.
Dr Marie Janson, kutoka shirika la kujitolea Alzheimer's Research UK, ametaka utafiti zaidi ufanywe kwa kuwapima binadamu kuona kama kuna uhusiano baina ya matatizo ya kukosa usingizi na ugonjwa wa Alzheimer.
Aliongezea kuwa: "tayari umekuwepo utafiti unaounganisha mabadiliko katika usingizi huchangia katika matumizi ya ubongo kwa fikra, lakini matokeo haya yanaonyesha kuwa kuna uwezekano wa kuwa mapungufu katika usingizi pia inaweza kuwa ishara na onyo la maradhi ya kusahau au Alzheimer.

Comments