MAPEPO HAYAWEZI KUSTAHIMILI KUSIKIA NENO LA MUNGU

Mapepo hayawezi kustahimili kusikia Neno la Mungu.
Wakati fulani nilirudi nyumbani kutokea kanisani na nikawa nasoma Maandiko. Niliinua macho na kuyaona mapepo kadhaa. Nikaanza kumwomba Mungu anisaidie. Sikuwa nina hofu lakini nilikuwa tu sijisikii amani kuyaona. Wakati nikiwa namwomba Mungu anisaidie, nilisikia sauti moyoni mwangu ikisema, “Soma Maandiko.”
Nikauliza: “Nini?” Sauti ile ikarudia tena: “Soma Maandiko.”  Nilitii na nikaanza kusoma Maandiko. Lakini baada ya muda kidogo, Mungu akaniambia: “Soma kwa sauti.” Nikawa kama nimechanganyikiwa kidogo, lakini Mungu akarudia tena: “Soma Maandiko kwa sauti.” Nilipoanza kusoma Maandiko kwa sauti niliona kuwa mapepo yale yanafunika masikio yao kwa mikono yao yenye makucha na kuanza kuhangaika kwa mateso makubwa. Hivi ndivyo nilivyojifunza kuwa mapepo hayawezi kustahimili kusikia Neno la Mungu. Neno la Mungu likitumika kwa imani na kweli, ni silaha kubwa dhidi ya nguvu za giza.
Tangu hapo, nimejenga tabia ya kusoma Neno la Mungu kwa sauti. Pia nimepakua kutoka kwenye intaneti Agano Jipya la sauti (lililo katika fomati ya MP3). Nikiwa nyumbani, karibu muda wote huwa nimefungulia Biblia hiyo. Huwa naisikiliza nikiwa nakula, napika, najipamba, nk. Mara kadhaa Mungu amekuwa akielekeza umakini wangu kwenye mistari ya muhimu sana na kunieleza maana yake wakati nikiwa nakula au najiandaa kwenda kazini. Mwenzangu mmoja aliniuliza ni rekodi ya aina gani hii ambayo huwa naisikiliza karibu saa 24 kila siku. Nilimweleza na kumshirikisha sababu zangu za kufanya hivyo, lakini najua kuwa hakunielewa kikamilifu.
Vilevile nilipakua Agano Jipya kwa ajili ya kompyuta yangu ya mfukoni. Kila ninapopata nafasi, huwa najaribu kusikiliza Maandiko niwapo kazini. Mara nyingi ninapopatwa na mashambulizi ya adui nikiwa kazini, huwa naamua kusikiliza Biblia hiyo kama njia yangu mojawapo ya kunisaidi kushinda vita.
Pia nilijifuza kwamba mapepo huteswa sana hasa na Kitabu cha Ufunuo, na hususani sura ya 17, 18, 19, pale ambapo Maandiko yanazungumzia kuhusu hatima yao ya mwisho. Hayawezi kabisa kusikiliza mistari kuhusu Babeli ulioanguka na mistari kuhusu ibilisi na manabii wake wa uongo kutupwa kwenye ziwa la moto.  
Kuna mara kadhaa ambapo niliyatishia mapepo kuyasomea Kitabu cha Ufunuo kama hayakuacha kunisumbua au kuondoka. Ni wazi kuwa sikuyatishia tu, bali nilisoma sehemu hizo. Mbinu hii hata hivyo si kwamba ndiyo jibu la kila kitu. Haikuhakikishii ushindi kwenye kila shambulizi, lakini ni mbinu nzuri ya msaada upande wetu. Mungu mara zote hunisaidia kupata mstari ambao unaweza kunyamazisha kabisa sauti ya adui. Nimeshajifunza kuwa si kila mstari utanyamazisha manyanyaso ya adui bali ni ile mistari ambayo inahusiana moja kwa moja na tatizo lililopo. Ni kama ilivyo kuinua upanga hewani na kupiga kushoto wakati adui yuko kulia. Hiyo haisaidii kumshinda adui. Ni pale tu unapoelekeza mapigo yako kwenye lengo ndipo utashinda mapambano. Hali ni ileile hata kwenye mistari ya Biblia na uongo na unyanyasaji wa adui. Ndiyo maana NI LAZIMA  kujifunza Maandiko kwa bidii na kuweka mistari kwenye kumbukumbu kichwani. 
Katika majaribu ya Yesu ya siku 40 kule jangwani – pale shetani alipomjaribu – je, Yesu alifanya nini? Alimjibu shetani kwa kutumia mistari sahihi kutoka kwenye Neno la Mungu. Alishindana na shetani kwa kutumia upanga wa Roho Mtakatifu, ambao ni Neno la Mungu. Shetani anamnukulia Yesu Neno lakini si kikamilifu; anataja nusu ukweli. Ukweli nusu mara zote huwa ni uongo uliokusudiwa kudanganya wanadamu na kupoteza makusudi ya Mungu kwa ajili ya wanadamu. Yesu alimnukulia shetani Kweli yote kwa  100%  ... na shetani hakuwa na kitu chochote cha kushindana na mbinu ya mapambano ya Yesu. Shetani alishindwa kwa 100% kwenye vita hivyo. Mungu hakuruhusu jambo hili liandikwe kwenye Biblia kwa bahati tu ili kujaza nafasi. Shindana na mashambulizi ya mapepo kwa kutumia kwa usahihi Neno la Mungu.
Lijue Neno ... Liamini Neno ... Fahamu lini pa kulitumia kwa usahihi (usinukuu tu Neno nje ya uhalisia wa hali yako; mapepo watakucheka!); kisha tamka Neno la Mungu kwa sauti, imba nyimbo zinazotokana na Maandiko; omba Neno wakati wa maombi yako na kuyaambia mapepo yanayokuzunguka, (japo huenda hutakaa uyaone) – sikiliza Neno la Mungu linapoongelewa dhidi ya matatizo yanayokukabili, lakini kwa mwongozo wa Roho Mtakatifu.
Mambo yote yanaweza kushindwa lakini haiwezekani kwa Neno la Mungu kushindwa maana Roho Mtakatifu ndiye anayelifanya litende kazi. Mungu hawezi kusema uongo; hivyo Neno la Mungu nalo haliwezi kuongopa. Wanadamu hapa duniani wanaweza wasilielewe Neno la Mungu, hivyo wakalitumia kimakosa katika hali zao, lakini hilo haliwezi kutokea kwa msaada wa Roho Mtakatifu. Hilo kila mara hutokea kwa sababu ya nguvu za kipepo na mawazo ya kimwili ya wanadamu ambao hawana ufunuo kamili wa Neno la Mungu, au huenda wamelipindisha bila wao kujua, na kulifanya liseme kitu ambacho Mungu hajasema. Kama Mungu alivyoandika:   "Mbingu na nchi zitapita; lakini maneno yangu hayatapita kamwe.” (Tazama: Mt. 24:35; Mk 13:31; Lk 21:33).  Mtu anapopokea ufunuo kamili kwamba Yesu Kristo ndiye Neno, haishangazi basi kwamba halitapita kamwe.
BIBLIA TAKATIFU
BIBLIA TAKATIFU NI NENO HAI LA MUNGU

Comments