Niliingia kwenye Ukristo nilipofikisha miaka 18.
Nilizaliwa kusini mwa Urusi. Nilimpenda sana Yesu, na nikawa na bidii sana
Kanisani, nikabatizwa kwa Roho Mtakatifu na nikawa nawashuhudia watu Injili.
Mungu amenibariki sana.
Mungu aliponibatiza kwa Roho Mtakatifu nilipata
shauku kubwa sana ya kuwashuhudia watu habari za Yesu. Nilikuwa nikiongea
Habari Njema za Yesu karibu kila siku. Nilijihisi niko karibu sana na Mungu.
Nilitumia saa nyingi kuomba na kusoma Biblia.
Wakati fulani nilipatwa na jinamizi. Niliota kuwa
ibilisi ananifukuza. Aliapa kuwa ni lazima atanipata. Nilipozinduka usiku ule,
hofu haikuondoka. Badala yake ilizidi kuongezeka. Hofu iliongezeka sana kiasi
kwamba nikawa nimechanganyikiwa kabisa. Nilijua kuwa niko katikati ya uovu.
Nilikuwa chumbani kwangu, lakini ilionekana kana kwamba niko mahali pengine
kabisa. Nilianza kuhangaika kuomba na kumsifu Mungu. Hili lilikuwa ni jambo
pekee lililonifanya nibakie na akili zangu timamu. Niliomba karibia usiku
kucha. Ile hali ya uovu ilikuja kuondoka asubuhi.
Nilipomsimulia jambo lile mmoja wa wamisionari wa
Kimarekani kanisani kwangu, aliniambia kuwa ibilisi amefungwa na kuwa hana
uwezo wa kumdhuru Mkristo yeyote. Nilikuwa sijawahi kufundishwa chochote
kuhusiana na vita vya kiroho na sikujua kuwa nilitakiwa kufanya kitu ili
kumpinga adui. Nimekuja kujifunza ukweli huo kwa njia ngumu kabisa. Ni miaka
mitatu baadaye ndipo nilipofahamu kuwa ibilisi yu hai na yuko duniani; na
anachukia sana na kushindana na kila mmoja anayeamua kuyatoa maisha yake kwa
Yesu Kristo.
Muda mfupi baada ya kupata ubatizo wa Roho
Mtakatifu, kwa ndani moyoni, nilianza kujiona kuwa mimi nilikuwa mtu maalum sana kwa Mungu kuliko Mkristo mwingine
yeyote au watu wengine. Nilianza kuhisi hivyo kwa sababu ya baraka zote za
kimwili na kiroho alizonipa Mungu. Kazi
yangu ya ukufunzi ilikuwa inakua kule Urusi; nilipokea fedha kwa ajili ya
kusafiri ng’ambo, na zaidi ya hapo, nilipewa skolashipu kamili ya kwenda kusoma
Chuo Kikuu cha Columbia kule New York.
Siku moja wakati nikiomba, Mungu aliniambia kuwa
ninatakiwa kutubu. Mungu alinionya kuhusiana na majivuno yangu na kuniambia
nitubu, vinginevyo NINGEANGUKA. Alisema kuwa mimi sikuwa mtu maalum kuliko mtu
mwingine yeyote. Pia aliniambia niache kuwahukumu wengine. Kwa bahati mbaya,
mimi nilikuwa nimesisimka zaidi kutokana na ukweli kwamba Mungu anasema nami
badala ya ukweli kwamba nilitakiwa kumtii na kufanya kile anachoniambia.
Kuishi katika jiji la New York...
Miaka minne iliyopita, toka tarehe ya kuandikwa kwa
ushuhuda huu, nilienda New York ili kusomea shahada ya pili kwenye Chuo Kikuu
cha Columbia. Nikiwa New York, mambo hayakwenda kama nilivyokuwa nimetarajia.
Nilikuwa na vita vikubwa na sikuelewa kwa nini Mungu aliruhusu nipitie mateso
kiasi hicho. Japokuwa Mungu alinibariki sana kwa skolashipu kamili kwenda
kusomea Columbia, sikumwamini na wala sikumshukuru wakati wa mapito yangu
magumu. Badala yake, nilipachukia New York na Columbia na nikaanza kunung’unika
na kulalamika sana.
Huu ulikuwa ndio mwanzo wa kuanguka kwangu. Niliingiwa
na huzuni kubwa sana na nikawa katika maumivu na hofu kubwa. Nilifunga,
nikaomba mara kwa mara, nikasoma Biblia, nikaenda kanisani, lakini maumivu na
hofu ile havikuondoka! Hali ile ilikuwa inatia
uchungu moyo wangu kiasi kwamba ikawa ni vigumu kwangu kutembea au kuzungumza.
Kila dakika ilihitaji nguvu sana. Ilikuwa ni kama vile mtu ananivuta chini na
kunizuia kupiga hatua. Muda wote nilikuwa nanyanyaswa na ibilisi ambaye alikuwa
akiniambia kuwa mimi nimeshashindwa kabisa.
Baada ya mwaka mzima wa mateso yangu, Mungu
alinivuta tena kwake kwa muda mfupi. Alizungumza nami na nikaandika maneno yake
kwenye kitabu changu cha kumbukumbu. Ni kwa miaka miwili tu ndio nilielewa kile
alichokuwa ameniambia. Mungu aliniambia kuwa nitapitia majaribu makali sana na
kwamba ningeteseka sana, lakini aliahidi kunivusha katika yote hayo na kuleta
mabadiliko yenye matunda mema ndani yangu.
Wakati nilipokuwa naisikia sauti ya Mungu, nilikuwa
naweza pia kusikia sauti za mapepo. Nilikuwa sijui kabisa kwamba mapepo
yanaweza kuiga sauti ya Mungu ili kuwadanganya Wakristo. Sikujua kuwa natakiwa
kulijaribu kila neno kwa njia ya Biblia. Ndiyo maana, niliposikia kuwa
ningeenda kufanya mafunzo ya vitendo kwenye Benki ya Dunia na kwamba
ningekutana na mume wangu wa baadaye kule D.C, niliamini kuwa hayo yanatoka kwa
Mungu. Kumbe pepo alikuwa anasema na tamaa zangu za kimwili. Niliyapenda maneno
hayo na nikayaamini. Nilikuwa na mashaka, lakini pia nilidhani kwamba Mungu
hawezi kuruhusu pepo anidanganye.
Muda mfupi baada ya hapo, rafiki yangu pekee
Mkristo wa New York aliondoka kwenda kwenye mapumziko ya majira ya joto.
Nilibakia peke yangu. Japokuwa nilikuwa nimeshakaa kwenye jiji hilo kwa mwaka
mzima, bado sikuwa na marafiki wa Kikristo. Nilihudhuria kanisani, lakini
sikuwa namfahamu yeyote pale.
Nilijawa na huzuni zaidi. Nilikuwa peke yangu kabisa
na sikuwa na mtu wa kumshirikisha mashindano yangu. Nilidhani kuwa Mungu
alikuwa hajali na hakunipenda tena kwa kuwa hakujibu maombi yangu ya kupata
kanisa na kuwa na marafiki wa Kikristo. Niliishiwa na nguvu kabisa pale
niliposhindwa kwenye usaili kwenye Benki ya Dunia na kukosa kazi. Sikuelewa kwa
nini Mungu aliruhusu pepo anidanganye. Sikuwa na hamu ya kuishi tena na
nikaanza kuwaza juu ya kujiua! Sikuweza kabisa kustahimili maumivu yangu
yasiyokoma.
Kisha nilitambua kuwa nisingeweza kufa kwa sababu nikijiua
ningeenda jehanamu na kutumbukia kwenye mateso makubwa zaidi, tena ya milele!
Nikajiona kama mtu aliyenaswa. Kuishi sitaki lakini wakati huohuo kujiua nako
siwezi. Nilijihisi kama vile niko jehanamu. Maumivu yalikuwa makali sana kiasi
kwamba nilianza kujikata kwa kisu, maana maumivu ya kimwili yalionekana kwangu
kuwa ni mepesi kuliko mateso ya moyoni mwangu. Uovu ulikuwa wakati wote
umenizunguka, ukipenya ubongo wangu, ukinitesa moyo wangu, wakati wote ukiwa
tayari kusema nami na kuniburuta chini! Kadiri nilivyozidi kuomba na kusoma
Biblia, ndivyo nilivyozidi kuteswa na hizo sauti, na ndivyo maumivu yalivyozidi.
Sikujua cha kufanya na sikuwa na jinsi ya kuzuia!
Ndipo nilifanya jambo ambalo si la kawaida. Sikuwa
na uwezo wa kustahimili maumivu zaidi ya hapo, hivyo nikawa nimeanguka kabisa.
Nilijawa na hasira sana dhidi ya Mungu kiasi kwamba nikamwambia aondoke kwangu
na aachane nami! Nilimwambia kuwa simpendi na sikuwa tayari kuzungumza naye
tena wala kuwa naye. Kwa kuwa nilikuwa ni mtu wa kuzungumza naye kila wakati,
ilibidi nijilazimishe sana kuacha kumfikiria. Niliacha kuomba na kusoma Biblia.
Nikaamua kufuata njia zangu mwenyewe. Sikuwa najua sawasawa madhara ya hatua
yangu hiyo. Sikujua kuwa nilimwacha Mungu na kumfuata ibilisi. Sikutambua kuwa
mtu huwa ama yuko anamtumikia Mungu au anamtumikia shetani – hakuna namna ya
kusema ‘mimi siko kwa Mungu wala kwa shetani.’ Ukiwa kwa Mungu unakuwa hauko
kwa shetani. Ukiwa nje ya Mungu, moja kwa moja unakuwa uko kwa shetani. Hakuna sehemu
ya kati!
Hivi sasa ninatambua kwamba Mungu alikuwa muda wote
ananiangalia licha ya maamuzi yangu yote mabaya.
Katikati ya majira ya joto, nilipata kanisa na kuwa
na marafiki kadhaa. Hatimaye sasa nilikuwa na mtu wa kuzungumza naye na angalau
kutoka naye. New York ni sehemu ngumu sana kwa Wakristo. Pia, hivi sasa
ninatambua kuwa kumbe hata marafiki zangu pale kanisani nao walikuwa wanapitia
magumu mengi vilevile kama mimi! Hata hivyo, kuwa wewe na kuombeana na
kumtazama Yesu yalikuwa ni mambo ambayo tulikuwa hatufanyi. Kutafuta mafanikio
ya kazi lilikuwa ndilo jambo tulilolipa umuhimu zaidi.
Jumapili moja nilikutana na mwanamume mmoja
kanisani. Mara moja nilivutiwa naye. Ninapotafakari sasa ... natambua kuwa mara
nilipoondoa macho yangu kwa Yesu, nilifanyika mtu rahisi sana kushambuliwa na
shetani. Hilo lilimpa nguvu juu yangu na kudhibiti hisia zangu na mawazo yangu.
Na kwa kuwa sikuwa na upendo kwa Mungu moyoni mwangu, nilihitaji kitu mbadala.
Nikawa nimevutika kabisa kwa huyu mwanamume.
Pale nilipokuja kutambua kuwa uhusiano wangu naye
hauwezi kufika mbali, nilianza kumwomba Mungu na kusoma Biblia. Hata hivyo,
bado nikawa sikumwomba Mungu awe Bwana wa maisha yangu tena. Nilitaka tu
anisaidie kwenye matatizo yangu niliyojisababishia mwenyewe. Kwa kule kutoyatoa
maisha yangu yote kwa Mungu, sikuwa na uwezo kabisa wa kuvunja ule uhusiano.
Sikujua wakati ule kwa nini sikuweza kumkatalia yule bwana kunitumia mimi, na
kumwambia ‘hapana’. Nilikuwa nimenaswa kwenye hisia zangu mwenyewe na sikuwa na
uwezo wa kutoka humo. Nilijua kwa moyo wangu wote kuwa nilikuwa namtenda Mungu
dhambi.
Nilibakia nikiwa nimenaswa kwenye uhusiano huu kwa
mwaka mzima. Kwa kuwa huyu bwana hakuwa msomaji wa Biblia na hakupenda
kuzungumza kuhusu Mungu, mimi nami pia niliamua kuacha kuyafanya hayo. Kwa
hiyo, nikawa nimeenda mbali zaidi na Mungu na hatimaye nikawa nimekuwa mwenyewe
tu.
Baada ya mahafali yangu ya chuo, nilifanya kazi New
York katika kipindi cha majira ya joto. Nilipata kazi kwenye benki yenye hadhi
na nilikuwa na uwezo sana kwenye kazi yangu. Bosi wangu aliniambia jinsi
ambavyo alipenda kazi yangu na jinsi nilivyokuwa bora na mwenye akili. Nilijawa
na majivuno na kiburi hata zaidi.
Baada ya uhusiano wangu na yule bwana kuvunjika,
nilijihisi kuwa ninataka kugeukia kwenye kitu kingine ili kujaza uwazi
uliotokea. Bado nilikuwa najiona kuwa simhitaji Mungu. Nilikuwa bado nina
hasira naye kutokana na kutonipatia kile nilichohitaji. Ndipo kazi yangu ikawa
ndiyo mungu wangu. Nilimuabudu huyu mungu wangu kwa bidii zote.
Kuishi Moscow…
Nilipoenda Moscow, nilipanga kufanya usaili
na mabenki kumi makubwa ya nje. Cha kushangaza, mambo yaligoma kabisa! Sikuweza
popote kupata kazi niliyoitaka! Najua sasa kuwa, sababu mojawapo ya mimi
kushindwa kwenye kila usaili ilikuwa ni tabia yangu ya majivuno ambayo
ilionekana kunisaidia sana wakati nikiwa New York, lakini hakuna mtu
aliyehitaji kiburi hiki kule Moscow.
Niliishia kupata kazi ambayo niliichukia kabisa. Hata
hivyo, ilibidi niiache baada tu ya miezi mitatu. Niliweza kupata kazi nyingine Moscow.
Nilipoambiwa niache kazi yangu ya pili, kwa vile sikuwa nafaa kabisa kwenye
kazi hiyo, na pale nilipokataliwa kwenye kila usaili niliofanya kule London,
nilitambua kuwa Mungu alikuwa anajaribu kila njia kunifanya nishtuke.
Nilipoteza kazi yangu Aprili (2004). Nilifanya
usaili mara kadhaa, lakini kazi sikupata. Kila jitihada ilikuwa haizai matunda
kwangu! Hatimaye Mungu alifanikiwa kuvuta umakini wangu. Nikaanza kumwomba.
Hata hivyo, nilijihisi kuwa hata nikitubu vipi, siwezi kusamehewa. Nilipakua
Biblia kutoka kwenye intaneti maana nilishatupilia mbali Biblia zangu zote pale
nilipoondoka New York. Nikaanza kusoma Agano Jipya tena.
Siku moja, nilipojua kuwa usaili wangu wote
umekwama, nilimlilia Mungu ili anisaidie. Nilijiona sina tena matumaini kabisa.
Ndipo nilianza tena kusikia sauti ya ibilisi ikiniambia
kuwa Mungu hanipendi na hatanisamehe; na kwamba inabidi nijitupe kupitia
dirishani. Sauti ile ilikuwa ina ushawishi mkubwa na nguvu sana kiasi kwamba
nilidhani kuwa nitakuwa kichaa. Huku nikilia, nilifungua Biblia na kuanza
kusoma kwa sauti japokuwa nilikuwa sielewi hata neno moja. Lakini sauti ile
ikawa imetoweka!
Nilitambua kuwa nilikuwa nimemtenda dhambi Mungu sana
na nilihitaji kujua iwapo angenisamehe. Nikakumbuka hadithi za kwenye Agano la
Kale kuhusu Israeli – wafalme waliomtenda dhambi Mungu, lakini wakatubu.
Nikaanza kusoma hadithi zile. Nikatambua kuwa majivuno yangu na kutotii zilikuwa
ndizo dhambi zangu kubwa mbili.
Katika kipindi cha kurudi kwangu kwa Mungu
nilikutana na tovuti yenye Shuhuda za Thamani. (www.precious-testimonies.com). Nilisoma shuhuda karibu
zote humo! Niliguswa sana na upendo wa Mungu kwenye maisha ya watu mbalimbali.
Niliguswa sana na mateso na maumivu ambayo kila mmoja aliyapitia hadi kuja kumpata
Yesu Kristo. Lengo langu, nilikuwa nataka sana kujua kama Mungu angeweza
kunisamehe dhambi zangu.
Kupitia kwenye Biblia, na shuhuda zile, nilitambua
kuwa sikuwa nimempa Yesu maisha yangu yote
na kwamba nilikuwa bado nimeshikilia mambo yale niliyoyapenda na nilikuwa
naogopa kuyaachia na kumpatia Yesu. Pia nilitambua jinsi ambavyo dhambi zangu
zilimpatia shetani nguvu kubwa ya kuharibu maisha yangu. Nilijifunza jinsi
ilivyo kutembea kwenye njia ya ibilisi. Sitaki ubinafsi tena! Nilitaka kumtumikia Yesu japokuwa isingekuwa rahisi na
wakati mwingine ingekuwa vigumu sana. Lakini Yesu hutoa uzima wa kweli na anajua kile kinachofaa kwa
ajili yetu.
Mungu alikuwa na rehema na neema sana kwangu na
Roho Mtakatifu wake aliniongoza kwenye toba. Alihukumu majivuno yangu na kukosa
kwangu utii na uzinzi wangu. Tarehe 12
Juni, 2004, nilimpokea Yesu kama Bwana na Mwokozi wa maisha yangu yote – si kwa sehemu yake tu! Nilimwambia achukue ndoto na mapenzi yangu
yote ya ubinafsi na aweke ndani yangu
ndoto na mapenzi yake.
Nilimkabidhi hofu zangu zote. Nilimwambia kuwa sikutaka tena kumtumikia shetani
bali nataka kumtumikia Yeye – Yesu. Maamuzi yangu yote ya nyuma yalinipeleka
kwenye kushindwa kabisa. Nilitaka sasa Yesu atawale maisha yangu na kuyabadili
apendavyo, na si vile ninavyotaka mimi.
Baada ya kufanya hivyo, nilijisikia faraja kubwa
sana! Kwa mara ya kwanza katika miaka mitatu, nilikuwa natembea barabarani huku
nikitabasamu na kupumua kwa uhuru tena. Nilijisikia mwepesi na huru kabisa.
Nilikuwa nimeishi Moscow kwa karibu mwaka mzima,
lakini nilikuwa sina rafiki Mkristo hata mmoja. Kabla ya toba yangu,
nilihudhuria kanisa jingine lakini bado nilikuwa simfahamu hata mtu mmoja.
Kutokana na tabia yangu ya New York ya kutojiweka wazi, nilikuta ni vigumu sana
kuweka wazi mambo yangu ya moyoni kwa watu wengine. Hii ndiyo sababu hakuna
aliyejua kile nilichokuwa napitia; na pia ndiyo sababu sikuwa na mtu wa
kumweleza kuhusu mapito yangu.
Baada ya uamuzi wangu huo, nilidhani kuwa ningeweza
kurudi kwa Mungu kwa nguvu za maombi yangu, toba na kusoma Biblia mwenyewe. Lakini siku chache baada ya kuamua
kumrudia Mungu, nilihisi kama kuzimu yote imesimama kinyume nami! Nilianza
kuona kiumbe mwenye manywele mengi. Taswira hii ilikuwa mbele za macho yangu
muda wote kwa wiki kadhaa. Nilikuwa ninaomba na kuomba na kusoma Biblia.
Nilifunga pia. Nilikiri damu ya Yesu juu yangu. Taswira hii mbaya wala
haikuondoka! Nilihisi kuwa ninachanganyikiwa. Usiku haikuwa rahisi kulala.
Sauti ilianza kuniambia tena kuwa Mungu hatanisamehe kwa kuwa nimemkufuru Roho
Mtakatifu na kutenda dhambi ambayo Yesu hawezi kusamehe.
Siku moja niliamka nikiwa na uchungu na hasira.
Nilihisi ule mzigo na uzito tena. Nikaanza kumwomba Mungu anisamehe na
kumshukuru Yesu kwa kunifia. Lakini mashindano yangu yakaendelea kuwa magumu
zaidi na zaidi. Siku ile nilitambua kuwa siwezi kushindana na ibilisi peke
yangu. Nilihitaji msaada. Nilihitaji sana mtu wa kuniombea.
Kweli imeshafunuliwa …

Ulimwengu wa roho…
Nilipokuwa ninakandamizwa na adui mara baada ya
kutubu kwangu, Mungu alinifungua macho ili niweze kuona ulimwengu wa roho. Kama
nilivyosema, nilidhani kuwa ninachanganyikiwa pale nilipoona kiumbe mwenye
manywele mengi. Baada ya kutuma mahitaji yangu ya maombi, nilijisikia amani
kubwa. Nilijua kuwa kuna mtu ameanza kuniombea.
Hata hivyo, niliendelea kuyaona mapepo
yakinizunguka. Nilipoamka siku iliyofuata, si tu kwamba niliweza kuyaona
mapepo, bali pia nilimwona malaika wangu. Taswira zilikuwa kama kioo. Nilikuwa
sina hofu hata kidogo. Niliweza kuona kwenye ulimwengu wa roho kwa wiki kadhaa.
Mungu alinifundisha masomo muhimu sana katika kipindi hicho. Hadi sana namtumikia na nimempa BWANA YESU maisha yangu kwani hakuna uzima kwingine zaidi ya kwake.
Comments