MPENDE ADUI YAKO NA MWOMBEE





            "Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako na umchukie adui yako; lakini mimi nawaambia, wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi ...." (Mathayo 5:43, 44)

            Jambo ambalo liko wazi ni kwamba hakuna msamaha wa kweli pasipo upendo,
            "Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu hata akamtuma Mwanae ..." (Yohana 3:16)
     
       Kilichomfanya Baba Mungu kumtuma Yesu Kristo duniani ni Upendo. Alitupenda sisi mno, alitupenda upeo wakati bado tulipokuwa tungali wenye dhambi. Na kuudhihirisha upendo huo, Yesu Kristo alizaliwa duniani na kufa masalabani ili sisi tupone.
             Msamaha wa kweli unadhihirisha upendo ulio ndani ya mtu. Pasipokuwa na upendo, kusameheana hakupo. Palipo na upendo wa kinafiki, pia pana kusameheana kinafiki.
            Kusameheana hakuonekani siku hizi, katika ndoa, kati ya ndugu, kati ya majirani, kati ya watu wa Mungu, KWA SABABU UPENDO WA WENGI UMEKWISHA POA!
            Watu siku hizi wanafanya kile ambacho Yesu Kristo aliwaambia wasifanye. Yesu alisema, " Wapendeni adui zenu." Lakini, unaona katika watu wa Mungu, chuki imejaa, ndoa zinaharibika kwa sababu ya chuki, undugu unakufa kwa sababu ya chuki. Na ni hao wanaosema kuwa wameokoka na Yesu Kristo yumo ndani yao. Usiwachukie wanaokuudhi, wapende.
            Yesu Kristo anakuambia watu wa dunia wanawapenda wanaowapenda na kuwachukia wanaowachukia, lakini wewe si wa dunia hii, wapende hata wale wanaokuchukia na ili kuonyesha kuwa unawapenda kweli, uwaombee!
            Kwa nini Yesu Kristo, alisema "Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi?"
Ni,
            "Ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki Maana mkiwapenda wanaowapenda ninyi, mwapata thawabu gani? Hata watoza ushuru, je! Nao hawafanyi yayo hayo? Tena mkiwaamkia ndugu zenu tu, mnatenda tendo gani la ziada? Hata watu wa mataifa, je? Nao hawafanyi kama hayo?" (Mathayo 5:45- 47).
            Ulipompokea Kristo, ulipokea upendo mpya ndani yako, unaokuwezesha kufanya mambo ambayo mtu wa kale aliyekuwa ndani yako asingeweza kufanya. Mtu mpya ndani yako ana upendo mpya.

Comments