UMUHIMU WA KWAYA KATIKA KANISA

Kwaya ni kikundi cha watu wanaoimba pamoja(na kupiga vyombo vya muziki). Kwaya ni kiungo muhimu katika Kanisa kinachofanya huduma ya uimbaji. Wapo wanakwaya wenye vipaji vya uimbaji, sauti za kuvutia na uwezo wa kutunga nyimbo  mpya. Kanisa ni mwili wa Kristo wenye viungo vingi; na kila kiungo kina kazi. Kiungo hiki (Kwaya) kikitimiza vizuri wajibu wake, Kanisa litahudumiwa (1 Pet 4:10-11).
Kwaya ni muhimu ndio maana hata katika Agano la Kale walikuwepo watu maalum waliowekwa kufanya huduma ya uimbaji (1Nya 6:31-32). Maneno ya nyimbo yana nguvu kubwa. Yanaweza kubadili hali ya huzuni kuwa ya furaha na moyo mgumu kuwa laini. Mtu mwenye udhaifu anaweza kusikia nguvu na uzima kwa nyimbo. Daudi alipopiga muziki roho mbaya ilimwacha Sauli (1 Sam 16:23).  Tunasoma pia kwamba siku moja Sauli aliingiwa na ghadhabu, chuki na kumwonea Daudi wivu baada ya kusikiliza maneno ya nyimbo (1 Sam 18:6-9).
Nyimbo tunazosikiliza (redioni, katika kanda,  nk) kama hazina maneno yenye maadili mazuri, mioyo yetu inaweza kuchafuliwa na kutufanya twende kinyume na mapenzi ya Mungu.
Nyimbo zinavuta nguvu na uwepo wa Mungu (2 Nya 20:21-22; 2 Fal 3:15-16). Paulo na Sila waliomba na kuimba nyimbo za kumsifu Mungu, hatimaye milango ya gereza ikafunguka (Mdo 16:25-26).
AINA ZA NYIMBO
Nyimbo nyingi zinaangukia katika makundi yafuatayo:
  1. Nyimbo za mafundisho/maonyo (Kol 3:16).
  2. Nyimbo za faraja
  3. Nyimbo za mahubiri (Isa 48:20).
  4. Nyimbo za sifa/shukurani/maombi
  5. Zipo pia nyimbo za upuzi (Amo 6:5). Mungu hapendi nyimbo za upuzi.Biblia inatuagiza kuimba "kwa akili"  yaani tuimbe huku tukiwa na ufahamu wa nyimbo tunazoimba (Zab 47:6-7; 1 Kor 14:15). Kwa sababu hiyo, wanakwaya wanapaswa pia kujua nyimbo wanazoimba zina maana gani au lengo lake ni nini. Zinahubiri au zinafariji? Zinajenga au zinabomoa? Vinginevyo wanaweza kujikuta wanaimba nyimbo za upuzi au zisizokuwa na maana.
    Kama wewe mwenyewe huelewi yale unayoimba, unafikiri wale wanaosikiliza wimbo wako wataelewa? Sio rahisi.









Comments