“16 zaidi ya yote mkiitwaa NGAO YA IMANI, amabayo
kwa hiyo Mtaweza kuizima mishale yote yenye moto ya yule mwovu”
(efe. 6:16)
Bwana Yesu asifiwe!
Ujumbe huu umekufikia kwa kusudi kabisa na ninaamini Mungu atakusaidia na
utatoka hatua moja kwenda nyingine. Hebu chukua nafasi twende tujifunze pamoja
na ni maombi yangu kwamba Mungu akufunulie akili zako ili uelewe kile ambacho
anakwenda kutufundisha!
Kabla ya yote ni
muhimu ufahamu kwanza juu ya imani maana tunachojifunza hapa ni jinsi ya
kuitumia imani kama ngao wakati shetani atakapokutupia mishale yake yenye moto.
Biblia inasema,”1 Basi imani ni kuwa na hakika na
mambo yatarajiwayo, Ni bayana ya mambo yasiyoonekana” (ebr.11:1)
Sikiliza tafsiri
nyingine kutoka katika Kiswahili cha kisasa biblia inasema hivi,“kuwa na imani ni kuwa na hakika ya mambo
tunayoyatumainia Kusadiki kabisa mambo tusiyoyaona”
Kwa hiyo kuwa na IMANI
ni kuwa na HAKIKA ya mambo uanayoyatarajia au unayoyatumainia. Kwa maana hiyo
imani ni sasa hata kama kitu unachotarajia hakipo imani inabaki kuwa sasa,
imani inaleta mambo unayoyatarajia kuwa halisi hata kama hujakiona kile kitu!
Kitu kingine unachopaswa kujua ni chanzo cha imani na unisikilize hapa
nikwambie kitu, kila imani chanzo chake ni kusikia haijalishi ni imani ya
kimungu au la zote chanzo chake ni kusikia! Angalia Biblia yako katika kitabu
cha warumi 10:17, “17 Basi imani
chanzo chake ni kusikia; na kusikia Huja kwa neno la Kristo”
Kwa nini nataka uelewe
chanzo cha imani? Ni kwa sababu watu wengi sana wamekuwa wakiomba kwa Mungu ili
waweze kuwa na imani na wengine wamejaribu hata kufunga wakiomba imani,
sikiliza ndugu yangu! Imani chanzo chake ni kusikia na si kusikia tu bali
kusikia kunakotokana na neno la Kristo, kwa hiyo kama imani chanzo chake ni
kusikia kunakotokana na neno la Kristo basi huwezi kuwa na imani kama huna neno
la Kristo! Nimesema
hivi huwezi kuwa na imani kama hauna neno la kristo! Ndiyo, ni lazima uwe na
neno la Kristo ambalo kwa hilo utaamini kile unachoamini! Imani lazima iwe na
kitu cha kushikilia huwezi ukaamini kitu from no where lazima uwe na kitu
kinachokufanya ushikilie hicho unachoamini na hicho kitu kinaitwa neno la
kristo au neno la Mungu (haleluya!) Ngoja twende kwa mifano utanielewa
tu,angalia rumi 4:17-21 inasema hivi,
“17
Kama ilivyoandikwa,nimekuweka kuwa baba wa mataifa mengi;mbele zake yeye
aliyemwamini, Yaani Mungu, mwenye kuwahuisha wafu,ayatajaye yale
yasiyokuwako kana kwamba yamekuwako.
18
Naye aliamini kwa kutarajia yasiyoweza kutarajiwa,ili apate kuwa baba wa
mataifa mengi,kama ilivyonenwa,ndivyo utakavyokuwa uzao wako.19 Yeye
asiyekuwa dhaifu wa imani,alifikiri hali ya mwili wake uliokuwa
umekwishakufa,(akiwa amekwishakupata umri wa miaka mia),na hali ya kufaya tumbo
lake sara. 20 Lakini akiiona ahadi ya Mungu hakusita kwa
kutokuamini, bali alitiwa nguvu kwaimani,akimtukuza Mungu;21
huku akijua hakika ya kuwa Mungu aweza kufanya yale aliyoahidi”.
Nitafafanua
vizuri hii habari huko mbele lakini nachotaka uone hapo ni hiki chanzo cha
imani ni kusikia neno na kama ni hivyo chanzo cha imani ni neno la Mungu na
utaona kwenye habari hiyo hapo juu ibrahimu alikuwa na miaka mia na mpaka
anafikisha miaka mia hakuwa na mtoto lakini kama ni msomaji mzuri wa biblia
utakumbuka kuna maneno aliyatamka Mungu kwa ibrahimu huko nyuma kuhusu mtoto na
biblia inasema Ibrahimu alimwamini Mungu na ikahesabiwa kuwa ni haki kwake.
Ilipita miaka mingi na ibrahimu hakuwa na mtoto kwa hiyo kama mwanadamu alianza
kufikiri hali ya mwili wake(uzee alionao maana alishafikisha miaka mia)
akafikiria na hali ya kufa kwa tumbo la mkewe sara maana kibinadamu sara hakuwa
na uwezo wa kubeba mimba tena, lakini akiiona AHADI ya MUNGU, hakusita kwa
kutokuamini bali ALITIWA NGUVU kwa imani……….. sikiliza! hapo anaposema akiiona
ahadi ya Mungu umeshawahi kujiuliza ni ahadi gani hiyo? Na anaposema alitiwa
nguvu umeshajiuliza alitiwa nguvu na kitu gani? Sikia ahadi aliyokuwa akiiona
Ibrahim ilikuwa ni NENO ambalo Mungu alimuahidi huko nyuma na kwa neno hilo
imani ya Ibrahim ilijengwa hapo,(kumbuka nataka uelewe chanzo cha imani ili
uache kufunga na kuomba imani)! Na kwasababu neno hilo ambalo imani ya Ibrahim
ilijengwa hapo ndilo lilikuwa likimpa Ibrahim nguvu ya kuendelea kuamini
japokuwa uzee ulikuwa umemlemea na hali ya kufa kwa tumbo la mkewe Sara ilikuwa
inamzonga lakini akiiona ahadi ya Mungu (neno) hakusita kwa kutokuamini
bali alitiwa nguvu! (haleluya!)
Biblia inasema imani
huja kwa kusikia wala haijasema imani huja kwa kufunga na kuomba na hata
ukiomba upewe imani Mungu atakupeleka kwenye neno lake tu ambalo ndiyo chanzo
cha imani. Angalia mfano huu labda tutamalizia hapa kwa habari ya chanzo cha
imani, luka 17:5,6 inasema hivi,
“5 mitume wakamwambia Bwana, tuongezee imani. 6 Bwana
akasema,kama mngekuwa na imani kiasi cha chembe ya haradali,mngeuambia mkuyu
huu,ng’oka ukapandwe baharini nao ungewatii”.
Unaona kitu ambacho
mitume walikuwa wanaomba! Walikuwa wanaomba waongezewe imani lakini kumbe hata
hiyo imani yenyewe amabayo wao walitaka waongezewe hawakuwa nayo hata kidogo!
Ndo maana unaona Bwana anawaambia kama wangekuwa hata na hiyo imani ya kiasi
cha chembe ya haradali wangeuambia mkuyu ng’oka ukapandwe baharini nao
ungewatii, mi sijui kama unaelewa alichokuwa anamaanisha Bwana lakini kama
unaisoma Biblia kwa kuitafakari mistari yake utagundua alichomaanisha Bwana ni
kwamba imani ina chanzo chake ni kama mwanzo wa mti ambapo kwanza huanza mbegu
ndogo sana lakini unapoipanda inakua na kuwa mti mkubwa sana. Kitu ni kilekile
ukirudi kwenye somo tunalojifunza ni kwamba kama unataka kuwa na imani ni
lazima uwe na mbegu ambayo ukiipanda itaota na kukua nakukufaya uwe na imani
kubwa sana na hiyo mbegu ni neno la Mungu! Angalia kitabu cha luka 8:11
inasema, “11 Na huo mfano,maana yake ni hii
MBEGU
ni NENO la MUNGU”
Hapo
Yesu alikuwa akifafanua mfano wa mpanzi ambapo anafananisha moyo wa mtu na
shamba (udongo) na mbegu anazifananisha na neno lake, kwa hiyo neno la mungu ni
mbegu ambayo kama ukiipanda ndani ya moyo wako itakua na kuzaa matunda sawasawa
na ulivyolipanda, ukipanda mahindi utavuna mahindi ukipanda neno la imani
utavuna imani sawasawa na ulivyoamini! Ni matumaini yangu wewe uliyekuwa
ukifunga na kuomba upewe imani utakuwa umepata kitu cha kukusaidia.
Hebu
sasa nikumbushe maneno ya Mungu yanayoongoza somo hili ambayo tunayapata katika
efeso 6:16 inasema , “16 Zaidi ya yote mkiitwaa ngao ya
imani,ambayo kwa hiyo Mtaweza kuizima mishale yote yenye moto ya yule
mwovu”.
Hapa
mtume Paul alikuwa anazungumzia silaha za Mungu ambazo wsomaji wengi wa biblia
tumekuwa tukizisoma na tumekuwa tukifundishwa na watumishi wa Mungu lakini
sijui kama umeshawahi kukaa ukatafari hizi silaha mojamoja! Sasa katika silaha
alizotaja mtume paul mojawapo ni hii ngao ya imani na kumbuka kila silaha
zilizotajwa kila moja ina kazi yake na wakati wake wa kuitumia na ndo maana
paul mtume anasema mkiitwaa ngao ya imani ambayo kwa hiyo yaani hiyo ngao ya
imani mtaweza kuizima mishale yote yenye moto ya yule mwovu (shetani). Kwa hiyo
kama mristo unapaswa kuwa na silaha hii muhimu kabisa ili kujikinga na mishale
inayorushwa na adui, hii siyo imani ya kusema namwamini Yesu kristo kama Bwana
na mwokozi hii ni imani inayotumika kama silaha. Ok! wengi tunafahamu ngao ni nini? Ngao ni kifaa
kinachotengenezwa maalum kwa ajili ya kumkinga mtu anayeitumia dhidi ya silaha
zinazotoka kwa adui anaye au anaopigana nao na hii ni silaha ya zamani sana
ambayo ilitengenezwa kwa kutumia miti au ngozi ngumu au shaba laikini vilevile
hata sasa inatumika na baadhi ya makabila machache pamoja na askari wakati
wanapozuia fujo za waandamanaji wanaorusha mawe chupa n.k. mtume paul ametumia
mfano huu wa ngao ili kuwaelewesha watu waweze kumuelewa au kelewa kazi ya
imani inapotumika kama silaha.
Sasa unisikilize!
Ninapozungumzia ngao ya imani ninazungumzia NENO LA IMANI. Usichanganyikiwe!!!
Ndo maana hapo nyuma nimeanza kukufundisha kwanza imani na chanzo chake ili
uweze kuelewa huku tunakokwenda. Sikia! hakuna NENO hakuna IMANI -hakuna
MATENDO hakuna MATOKEO. Ili uweze kushindana na mwovu unahitaji kuvaa silaha za
Mungu,ili uweze kuizima mishale yenye moto ya yule mwovu unahitaji kuwa na
silaha inayoitwa ngao ya imani na labda utajiuliza hii mishale ya mwovu ni ipi
au inakujaje na nitatumia vipi ngao ya imani? Swali zuri, sasa fungua biblia
yako nikupe mifano ambayo itakutoa hatua moja kwenda hatua nyingine na
ninaamini hautakuwa kama ulivyo bali utatoka imani hata imani, amen? Lakini
kabla sijakupa mifano sikiliza maneno haya,
“12 Piga vita vile vizuri vya imani,shika uzima ule wa Milele
ulioitiwa,ukaungama maungamo mazuri mbele ya mashahidi wengi” (1Timotheo 6:12)
Ili uweze kupigana
vita hivi vya kiimani ni lazima uwe na neno au maneno ya imani yatakayokuwa
kwako kama ngao wakati adui atakapourushia mishale yake yenye moto! Angalia
tena 1timotheo 1:18 inasema,
“ 18 Mwanangu Timotheo nakukabidhi agizo hilo
liwe akiba,kwa ajili ya MANENO ya unabii yakiyotangulia juu yako, ili
KATIKA HAYO uvipige vile vita vizuri”.
Sikiliza tafsiri
nyingine ambayo inatupa ufunuo zaidi, inasema hivi,
“ 18 Mwanangu timotheo, nakukabidhi amri hii kufuatana na maneno
ya unabii Yaliyosemwa zamani juu yako. Yatumie MANENO HAYO yawe
silaha yako katika
Kupigana vita vizuri”.
Bwana asifiwe! Tafsiri
nzuri kabisa na inayoeleweka kwa urahisi kabisa. Hapo juu tumeona jinsi Paul
akimwambia Timotheo kwamba avipige vita vizuri vya imani kisha anendelea
kumkumbusha kuwa kuna maneno ya unabii alipewa na hayo maneno ayatumie kama
silaha ya kupigania vita vya imani. Sijui kama unafahamu kwamba maneno ni silaha
na kama ulikuwa hufahamu kwamba maneo ni silaha sasa ufahamu hilo na maneno
haya yakiwa upande wa mwovu yanakuwa ni kama silaha ambayo kwako ni mishale
yenye moto, lakini kwa kutumia maneno ya Mungu (maneno ya imani) ambayo
yana-act kama ngao utaweza kuizima hiyo mishale ya mwovu. Nadahani sasa unaanza
kuelewa mahali tunakoelekea! Ngoja niseme hivi labda utanielewa. “ ngao ya
imani ni neno au maneno ya imani ambayo yanakusaidia kukukinga wakati adui
anapoleta maneno au mawazo ya kukukatisha tama juu ya kitu unachoamini na
kukitarajia kutoka kwa Mungu ”.
Sasa angalia marko
5:35,36 inasema,
“35 Hata alipokuwa katika kunena, wakaja watu kutoka kwa yule mkuu
wa sinagogi wakisema, binti yako ameshakufa kwani kuzidi kumsumbua mwalimu? 36
Lakini Yesu aliposikia LILE NENO likinenwa,akamwambia mkuu wa sinagogi,USIOGOPE
AMINI TU”.
Nimekwambia hapo juu
kuwa maneno ni silaha sasa hii ni habari inamuhusu mkuu wa sinagogi ambaye
alikwenda kwa Bwana Yesu kuomba uponyaji wa binti yake aliyekuwa akiumwa na
sote tunafahamu kuwa Yesu alikubali kwenda kwa yule mkuu wa sinagogi lakini
wakiwa njiani kuelekea kwa mkuu wa sinagogi wasomaji wa biblia wanakumbuka juu
ya yule mama aliyekuwa akitoka damu jinsi alivyomgusa Yesu akapona ugonjwa
wake. Wakati alipomgusa Bwana aliuliza nani amenigusa? Ule muda walioutumia
katika kuulizana maswali yule mtoto wa mkuu wa sinagogi akafa. Wakatumwa
wajumbe wamebeba ujumbe ambao kwa yule baba ulikuwa ni kama mshale wenye moto,
“binti yako ameshakufa usimsumbue mwalimu”. Biblia inasema Yesu aliposikia lile
neno likinenwa ooh! Akamkinga na ngao ya imani, akamwambia usiogope amini
tu! Lile neno lilikuwa ni mshale wenye moto na Yesu kwa kuwa ndiye
mwenye silaha hizi za kujikinga ambazo tunajifunza hapa alimkinga yule baba kwa
ngao ya imani alimkinga yule baba kwa neno la imani! Haleluyaa!!!
Sikiliza mfano
mwingine, wengi tunafahamu juu ya habari ya Daudi na Goliati,wakati Israel
ikipigana vita na wafilist alitokea shujaa mapiganaji wa jeshi la wafilist
aliyeitwa Goliati na akayatukana majeshi ya Mungu wa Israel kisha akawaambia
watoe mtu mmoja apigane naye na kama mtu huyo akimshinda itahesabika kuwa jeshi
zima la wafilist limeshindwa lakini pia kama atashindwa muisrael basi
itahesabika jeshi zima la Israel limeshindwa. Sasa unisikilize kwa historia ya
Goliati hapakutokea mtu yeyote kwa upande wa Israel ambaye alithubutu
kujitokeza kupambana naye kwa kuwa kiumbo alikuwa ni mkubwa na kiuzoefu
alimkuwa ni mtu wa vita maisha yake yote! Wakati huo akatokea kijana mmoja
kutoka familia ya Jese jina lake Daudi, akiwa ametumwa kuwapelekea chakula
ndugu zake vitani akasikia jinsi mfilist anavyoyatukana majeshi ya Israel na
jinsi alivyokuwa akitamba. Basi Daudi akajitolea kupigana na mfilist yule
habari zikamfikia mfalme Saul kwamba kuna kijana kutoka nyumba ya Jese
amejitolea kupambana na Goliath, Saul akaamuru aletwe kwake na Daudi alipofika
kwa mfalme, mfalme alimtazama kisha akamwambia maneno haya:-
“34 …Huwezi wewe kumwendea mfilist huyu upigane
naye; maana wewe u kijana tu; Na huyu ni mtu wa vita tangu ujana wake”. (1sam. 17:33)
Nilikwambia hapo nyuma
maneno ni silaha na yakiwa upande wa adui ni kama mishale yenye moto ili
kukukatisha tamaa usiendelee kuamini kile unachoamini na kukitarajia kutoka kwa
Mungu, sasa hapa Daudi anakutana na mishale ya mwovu iliyokuwa ikitaka
kumchoma(kumkatisha tamaa) ili asiendelee kuamini kile alichokuwa anaamini ya
kwamba kupitia yeye Mungu atakwenda kuleta ushindi juu ya taifa la Israel!
Kumbuka maneno mtume Paul alimwambia timotheo akisema:-
“ 18 Mwanangu timotheo, nakukabidhi amri hii kufuatana na maneno
ya unabii Yaliyosemwa zamani juu yako. Yatumie maneno hayo yawe
silaha yako katika Kupigana vita vizuri”.
Katikati ya maneno
(mishale) ya kukatisha tamaa Daudi anakumbuka maneno na matendo ambayo Mungu
alimfanyia huko nyuma na anaamua kuyatumia kama ngao kwake dhidi ya mishale ya
mwovu iliyokuwa inataka kumchoma ili akate tamaa ya kupigana na mfilisti, ooh!
Daudi anasimama mbele ya mfalme Sauli na kumwambia,”34
………Mtumishi wako alikuwa akichunga kondoo za baba yake, na alipokuwa akija
simba au dubu akamkamata mwanakondoo wa lile kundi, 35 mimi hutoka
nikamfuata, nikampiga, nikampokonya kinywani mwake; na akinirukia, humshika
ndevu zake nikampiga nikamwua……….37 Daudi akasema, BWANA aliyeniokoa
na makucha ya simba, na makucha ya dubu ataniokoa na mkono wa mfilisti
huyu…………”. (1sam. 17:34-37)
Kitu ni kilekile hata
kwako wewe unayesoma ujumbe huu wakati mwingine unapita kwenye magumu na
shetani anatupa mshale wake kwako akikwambia hapa hautavuka au hautafanikiwa na
wewe kwa kuwa hauna ngao ya imani (neno la imani) unakata tamaa, lakini leo
ujumbe huu umekufikia kukutoa hapo uliponaswa, hebu changamka kumbuka kitu
ambacho Mungu aliwahi kukufanyia huko nyuma kumbuka neno ambalo Mungu alikupa
huko nyuma na ulitumie katika kupigana vita vizuri vya imani!! Daudi
alipokatishwa tamaa(aliporushiwa mshale na adui) alijikinga kwa neno la imani
na kupitia neno hilo la imani alishinda vita! Haleluya! Nikupe mfano mwingine,
wakati Fulani mtume paul aliingia kwenye mapito Fulani lakini kwa kuwa alikuwa
na ngao ya imani (neno la imani) hakutetereka bali alisimama imara na kusema, “12
Najua kudhiliwa, tena najua kufanikiwa;katika hali yoyote na katika mambo
yoyote,nimefundishwa kushiba na kuona njaa, kuwa na vingi na kupungukiwa. 13
Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu”. (filipi 4:12,13)
Sijui kama unaelewa
nguvu iliyopo katika haya maneno! Yaani paul alikuwa anamaanisha, kwake kuona
njaa au kushiba,kupungukiwa au kuwa na vingi, kudhiliwa au kufanikiwa ni
kawaida kwa sababu ameshafundishwa na Mungu. Kwa hiyo haimpi shida kabisa
anapokutana na hali yoyote haimsumbui, kwa nini? Kwa sababu anayaweza yote
katika yeye amtiaye nguvu. Sasa jiulize wewe mwenyewe kimya kimya unapopita
kwenye magumu anayoyaelezea mtume Paul unafanyaje? Una silaha gani ya kukukinga
na mishale hiyo? Sema nayaweza yote katika yeye anitiaye nguvu!!!
Wakati mwingine
unapita hali ya ugonjwa na hapo adui anakutupia mshale akikwambia utakufa na
kwa sababu huna ngao ya imani unainama unasubiri kufa. Sikiliza! Mwambie “sitakufa
bali nitaishi nami nitayasimulia matendo ya BWANA”. (zaburi 118:18) wakati
neno hili la imani limekukinga imani yako inafanya kazi ndani yako na nguvu za
uponyaji lazima zidhihirike! Ninakwambia utapona tu, hakikisha shetani akitupa
mishale yake inatua kwenye ngao hii ya imani!! Kadiri unavyoendelea kuyasema
maneno ya imani yanafanyika ngome (ngao) ndani yako na unajua kitakachotokea?
Shetani atakimbia! Yakobo 4:8b inasema, “mpingeni shetani naye atawakimbia”.
Na 1Petro 5:9 inasema,
“9 Nanyi mpingeni huyo, mkiwa thabiti katika IMANI……..”.
Tulisoma habari za
Ibrahim hapo nyuma utakumbuka kuwa wakati Ibrahim ameahidiwa mtoto na Mungu
kipindi cha kusubiri adui alimrushia mshale wenye moto kumkatisha tamaa lakini
Bilia inasema akiiona ahadi ya Mungu hakusita kwa kutokuamini! Maana
yake akiliona neno la Mungu ambalo kwake lilikuwa kama ngao iliyomkinga na
mishale yenye moto ya yule mwovu hakusita kwa kutokuamini bali alitiwa nguvu na
akapokea ahadi aliyoahidiwa na Mungu!(unaweza kusema amen!)
Unapita kwenye nini?
Adui amekurushia mshale gani ambao umekupata na kukujeruhi? Mkumbuke Daudi
katika zaburi 23:4 anasema “4 Naam nijapopita kati ya bonde la uvuli wa
mauti,SITAOGOPA Mabaya; kwa maana wewe upo pamoja nami……..”.
Bwana akubariki iko
mifano mingi sana katika biblia lakini hebu hii ikupe hamu ya wewe kuingia
zaidi ili uweze kupata zaidi. Kumbuka kitu hiki ili uweze kuwa na imani kwa kiwango
cha juu unahitajika kulijua neno la Mungu kwa kiwango cha juu pia! Nilikwambia
huko nyuma kwamba neno la Mungu ni MBEGU sasa rejea mfano wa mpanzi pale kwenye
mbegu zilizodondoka kwenye udongo mzuri kuna nyingine zilizaa moja thelathini
nyingine sitini na nyingine mia. Nachotaka kusema hapa ni hiki kiwango cha
uelewa wako juu ya neno la Mungu ndicho kitakachowezesha imani yako kuwa nyingi
au kidogo ndicho kitakachowezesha imani yako kuwa kidogo au nyingi. Biblia
inasema kinywa cha mtu hunena yaujazayo moyo wake, kama umaejaza maneno ya
imani moyoni mwako kinywa chako kitatoa maneno ya imani lakini kama umejaza
maneno ya kuakatisha tamaaa moyoni mwako kinywa chako kitatoa maneno ya
kukatisha tamaaa. Ulichojaza moyoni ndicho utakachokitoa kinywani mwako!!!
BARIKIWA NA BWANA
unapozidi kutafari ujumbe huu BWANA akupe na mengine mengi yaliyofichika katika
ujumbe huu!!!
“50 Hiki ni chakula kishukacho kutoka mbinguni,kwamba mtu akile
asife” (Yohana 6:50)
Mwl. Alfred T.
Katuma.
Comments