KUOKOKA NI NINI?



   

Watu wengi wamekua wakijiuliza kuhusu kuokoka ni nini, jamii nyingine wamekua wakipinga jambo la kuokoka hapa duniani kana kwamba wataweza kutenda jambo wakiwa marehemu ambalo litawafanya waokoke.  Lakini kuokoka wanadamu tunaokoka hapa hapa duniani  maana hatuwezi kufanya chochote tukiwa wafu hivyo kwa maamuzi ya leo unaweza kuokoka, kwa matendo yako ya sasa unaweza kuokoka na sio baadae baada ya kufa.


*Kuokoka ni kumwamini YESU KRISTO.Yohana 1:12 -13‘’Bali wote waliompokea aliwapa uwezo wa kufanyika watoto wa MUNGU, ndio wale waliaminio jina lake; waliozaliwa, si kwa damu, wala si kwa mapenzi ya mwili, wala si kwa mapenzi ya mtu, bali kwa MUNGU. ‘’

Kumwamini YESU ni kumkubali YESU na pia kumtegemea kwa kila kitu, na yeye alisema kwamba sisi bila yeye hatuwezi kufanya lolote hata lile lililo dogo kabisa.
Matendo 16:30-31 Biblia inasema ‘’
kisha akawaleta nje akasema, Bwana zangu, yanipasa nifanye nini nipate kuokoka? Wakamwambia, Mwamini BWANA YESU, nawe utaokoka pamoja na nyumba yako. ‘’

*Tukimwamini BWANA YESU tunakuwa na ROHO MTAKATIFU  ambaye hutufanya kuchukia dhambi kwani  bila ROHO MTAKATIFU hakuna awezaye kuacha dhambi.

BIBLIA katika Yohana 3:3 ‘’YESU akajibu, akamwambia, Amin, amin, nakuambia, Mtu asipozaliwa mara ya pili, hawezi kuuona ufalme wa MUNGU. ‘’
 
*Kuzaliwa mara ya pili ni 

1: Kumwamini YESU.
2: Kubatizwa .
3: Kuwa na ROHO MTAKATIFU.

Yohana 3:17-18’’ 
Maana MUNGU hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye. Amwaminiye yeye hahukumiwi; asiyeamini amekwisha kuhukumiwa; kwa sababu hakuliamini jina la Mwana pekee wa MUNGU. ‘’
 
Tunaokoka hapa hapa duniani kwa sababu ‘’ 
Hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya KRISTO amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita tazama! Yamekuwa mapya. ‘’- 2 Korintho 5:17.

 
*Ndugu ukiamua kuokoka usirudi nyuma maana unaweza ukapoteza wokovu wako.Luka 9:61-62''
Mtu mwingine pia akamwambia, BWANA, nitakufuata; lakini, nipe ruhusa kwanza nikawaage watu wa nyumbani mwangu. YESU akamwambia, Mtu aliyetia mkono wake kulima, kisha akaangalia nyuma, hafai kwa ufalme wa MUNGU.'' 


*Watu wengine huogopa kuacha dhambi  eti kwa sababu shetani atawatesa kwa sababu wamewahi kuingia maagano naye ya kishetani huo ni uongo. Maana YESU akikuokoa anakuhamisha kutoka katika kila agano lako na shetani na kuanzia muda hu unakua mtoto wa MUNGU ambaye huwezi kurogwa tena maana mamlaka ya BABA yako wa mbinguni uliyeamua kumpa maisha yako ni kuu sana na hakuna anayeweza kukudhuru tena.na BWANA YESU atakuwa ndiye anayekuchunga Zaburi 23:1’’ BWANA ndiye mchungaji wangu, Sitapungukiwa na kitu. ‘’ .

 
*Ndugu  duniani hapa tunapita tu maana hata kama ukiishi miaka 98 hapa duniani lakini ni bure kabisa kama utapotelea motoni baada ya kufa kwa hiyo bora kumpa YESU maisha yako na utakuwa huru kabisa pia utapata uzima sasa na baadae uzima tele. YESU anasema katika Yohana 10:10b’’
mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele. ‘’.
ndugu dunia hii tuliikuta na tutaiacha hivyo ni heri kwa sasa kuishi maisha ya kumcha MUNGU. Neno la MUNGU linakushauri kwamba ‘’
Msiipende dunia, wala mambo yaliyomo katika dunia. Mtu akiipenda dunia, kumpenda Baba hakumo ndani yake.  Maana kila kilichomo duniani, yaani, tamaa ya mwili, na tamaa ya macho, na kiburi cha uzima, havitokani na Baba, bali vyatokana na dunia.  Na dunia inapita, pamoja na tamaa zake, bali yeye afanyaye mapenzi ya MUNGU adumu hata milele. ‘’-1 Yohana 2:15-17
 Kwa sasa naishia hapo, MUNGU akitupa nafasi tutajifunza tena siku nyingine.na kama hujampokea BWANA YESU muda wa kumpokea ni leo wala sio kesho, amua leo na atakuandika jina lako katika kitabu cha uzima na utaanza kuukulia wokovu kwa mafundisho kanisani. MUNGU ana makusudi kabisa na wewe, hataki upotelee motoni anataka uende uzimani aliko KRISTO BWANA. MUNGU akubariki sana.
Ni mimi ndugu yako
Peter M Mabula
Maisha ya Ushindi Ministry.
+255714252292
mabula1986@gmail.com
MUNGU akubariki sana uliyesoma somo hili.


Comments