KUTOZA PESA KWA AJILI YA HUDUMA ZA KIROHO NI USHIRIKINA, ASKOFU GAMANYWA

Tahadhari imetolewa kwa wale wote wanaoifanyia biashara karama ya Mungu kwa kutoza watu pesa ili waombewe kwa Mungu ili matatizo yao yaishe, kwani huo ni ukengeufu wa imani na maadili. 

Hayo yamesemwa na mwangalizi mkuu wa WAPO Mission International askofu Sylvester Gamanywa wakati akifundisha katika mwendelezo wa operesheni takasika inayoendelea jijini Dar es Salaam katika ukumbi wa BCIC Mbezi beach.

Askofu Gamanywa amewataka watu wanaotozwa pesa na watu hao ili wafanyiwe maombi ni bora wazinduke sasa kwani karama za Mungu yakiwemo maombezi hayauzwi kwa bei yeyote, bali ni bure, na wajue kuwa wanaofanya hivyo ni washirikina. 

"Kila muhubiri yeyote anayetoza fedha katika huduma za rohoni anafanya hivyo kwa roho ya uchawi na ushirikina", anasema askofu Gamanywa na kuongeza;


"hata kama ananukuu maandiko katika Biblia lakini kuifanyia biashara karama ya Mungu ni pale fedha inapotumiwa kama kishawishi kwa mtu ambaye anashida na uponyaji na muujiza kutoka kwa Mungu, pesa inatangulizwa kama kishawishi kwamba akitoa fedha hiyo basi Mungu ataona kile alichotoa ndipo amponye ndipo amtendee muujiza huo ndio ushirikina ninaousema", alimaliza kusema askofu Gamanywa.

Aidha ameendelea kusema kwamba ameyasema yote hayo si kwasababu anataka kumfurahisha mtu bali anasema kutokana na ukengeufu ulioingia katika kanisa na hakuna anayekemea na watu wanafikiri ndivyo ilivyo. Amewaambia vijana kwamba katika yote hayo yanayotokea suluhisho ni kumpokea kutubu na kukubali kuwa Yesu ni Bwana na Mwokozi wao ili Roho Mtakatifu achukue nafasi ya kuwaongoza.

                   chanzo:Gospel Kitaa

Comments