Zijue Karama Za Roho Mtakatifu – II


na Mwl. Christopher Mwakasege


SEHEMU YA NNE
Karama ya neno la Maarifa
I Wakorintho 12:4,8; ”Basi pana tofauti za karama bali Roho ni yeye yule. Maana mtu mmoja kwa Roho apewa neno la hekima, na mwingine neno la maarifa, apendavyo Roho yeye yule”.
Kama tulivyo jifunza huko nyuma kazi ya karama ni kulijenga kanisa.
Kazi ya karama ya neno la maarifa.
 Kukupa habari ya mambo yaliyopo na/au yaliyopita ili kukurahisishia kufanya maamuzi na kutambua hila zilizojificha ili kukwamisha utumishi wako.
Wakati mwingine karama hii itakupa kujua maswali waliyonayo watu kabla hawajauliza au kujua mahitaji waliyonayo kabla hawajakwambia.
Njia nne ambazo karama ya neno la maarifa inafanya kazi:
i. kwa kutumia mawazo
ii. kwa kutumia ndoto
iii. kwa kutumia maono, maono yamegawanyika katika sehemu zifatazo:
 maono ya ndani
 maono ya wazi
 maono yanayotokea wakati akili zako hazina matunda.(suspended)
iv.  kwa kutumia njia ya kuweka mwilini mwako maumivu au hali aliyo nayo mtu mwenye kuhitaji.

Karama zinafanya kazi kwa kutegemeana/kushirikiana.
Mfano. Unaweza kupewa swali na jibu. Kulijua swali ni neno la maarifa na kujua jibu la swali hilo ni neno la hekima.
i. Njia ya kutumia MAWAZO / WAZO
Hii ndio njia kuu ambayo inatumika mara nyingi zaidi. Marko 2:6-8 inasema ”……. Mara (ghafla) Yesu akafahamu rohoni mwake kwamba wanafikiri hivyo nafsini mwao…..”. Maana yake ghafla wazo tofauti, na lile alilokuwa akiwaza saa hiyo lililetwa na Roho Mtakatifu ndani yake.
Ukisoma Luka 3:15-16; inasema ”……….Yohana alijibu akawaambia wote,…………”. Yaani alijibu swali ambalo lililetwa ndani yake na Roho Mtakatifu; sio kwamba aliulizwa na mtu yeyote yule.
Luka 20:18-26; inasema ”……….wakamvizia-vizia, wakatuma wapelelezi waliojifanya kuwa watu wa haki, ili wamnase katika maneno yake, wapate kumtia katika enzi na mamlaka ya liwali. Wakamwuliza wakisema,………………. Lakini yeye alitambua hila yao akawaambia ……………. Wakastaajabia majibu yake, wakanyamaa”.
Mambo ya kukuwezesha kufanya kazi na njia hii ya mawazo:
a. Jizoeze kukabidhi roho yako, nafsi yako na mwili wako kila siku upya mbele za Mungu.
b. Omba maombi ya vitu vifuatavyo:
 Usikivu (sensitivity)
 Utulivu
 Kufundishwa na Mungu namna ya kutembea katika hiyo karama.
Hii inasaidia kwa mfano, Mungu akisema jenga safina wakati sio msimu wa mvua. Yaani kutii sauti ya Mungu bila kuangalia dalili za nje.
SEHEMU YA TANO
Karama ya neno la hekima
I Wakorintho 12:4,8; inasema ” Basi pana tofauti za karama bali Roho ni yeye yule. Maana mtu mmoja kwa Roho apewa neno la hekima…….”.
I Wakorintho 14:12 ” ……takeni sana mzidi kuwa nazo ili kulijenga kanisa”.
Karama ya neno la maarifa na neno la hekima zinafanya kazi kwa karibu sana.
Kazi ya karama ya neno la hekima na inavyofanya kazi:
1. kukupa jibu la swali unaloulizwa lakini hasa swali lenye hila, mtego, ushindani au mashtaka ndani yake.
Luka 21:12-15 inasema ”lakini, kabla hayo yote hayajatokea watawakamata na kuwaudhi; watawapeleka mbele ya masinagogi…….. basi kusudieni mioyoni mwenu, kutofikiri-fikiri kwanza, mtakavyojibu, kwa sababu mimi nitawapa kinywa na hekima ambayo watesi wenu wote hawataweza kushindana nayo wala kuipinga”.
Luka 20:19-26; ”…lakini yeye alitambua hila yao …..”
Marko 3:1-6; inasema ”……….akamwambia yule mtu mwenye mkono uliopooza simama katikati ……….nyosha mkono wako. Naye akaunyosha mkono wake ukawa mzima tena”.
Hapa tunaona neno la maarifa (kutambua hila ya wale waliotaka kumkamata) ilianza kufanya kazi, neno la hekima pia likafanya kazi baadaye pale Yesu alipomwambia yule mwenye kupooza ”simama katikati” na tunasoma akaanza kuzungumza na wale watu.
2. inakupa uwezo wa kutatua tatizo lililoko mbele yako.
Mathayo sura ya 1 na ya 2: Habari ya Yusufu na Mariamu. Katika sura hizi karama ya neno la maarifa na la hekima ilifanya kazi kwa kutumia ndoto. Si ndoto zote zinatoka kwa Mungu lakini kama ukiwa na neno la Mungu utatambua ndoto ya Mungu na isiyo ya Mungu.
3. kukupa uhuru wa kushirikiana na watu usiowajua kwa kazi ya Mungu.
Matendo ya mitume 10:1-20; Habari za Petro na Kornelio. Habari hii inaeleza jinsi Petro alivyoona maono wakati amezimia roho (akili zake zilikuwa hazina matunda).
Maono ya aina nyingine, kama tulivyokwishaona hapo nyuma ni ya wazi, ambapo akili zako zinaona na zinaelewa na bado unaweza kuona katika ulimwengu wa roho.
Aina nyingine ni maono ya ndani kwa mfano: unapoomba halafu ghafla ndani yako inakuja picha.
Sasa karama ya neno la maarifa na la hekima itakusaidia kukuwezesha kushirikiana na watu usiowajua.
4. inakurahisishia kuamua kwa haki katika nafasi ya uongozi Mungu aliyokupa au mahali unapohitajika kutoa maamuzi
I Wafalme 3:4-28; habari za mfalme Sulemani, jinsi alivyoomba hekima kwa Mungu na akapewa. Vilevile tunaona jinsi ambavyo aliweza kutoa uamuzi wa haki juu ya kesi ya wanawake wawili waliokuwa wakigombea mtoto. Uamuzi wa haki unahitaji msaada wa Mungu.
SEHEMU YA SITA
Karama ya unabii
I Wakorintho 12:4,10 ”Basi pana tofauti za karama bali Roho ni yeye yule. na mwingine matendo ya miujiza; na mwingine unabii, na mwingine kupambanua roho; mwingine aina za lugha; na mwingine tafsiri za lugha.
I Wakorintho 14:12; inasema ”…….takeni kwamba mzidi sana kuwa nazo ili kulijenga kanisa”.
Mambo ya msingi kuhusu huduma ya Nabii na karama ya unabii:-
1. kuna tofauti kati ya huduma ya nabii na karama ya unabii.
Efeso 4:11 ”Naye alitoa wengine kuwa Mitume; na wengine kuwa manabii….”. Hapa anazungumza habari ya nabii (ofisi) ya nabii. Huduma ni ofisi na karama ni vitendea kazi katika ofisi.
Kazi za nabii (kama huduma)
kufundisha mafundisho ya msingi / ya kuweka msingi wa kiroho ndani yako. Efeso 2:19-20 inasema, ”Basi tangu sasa ninyi si wageni wala wapitaji, ……..mmejengwa juu ya msingi wa mitume na manabii, naye Kristo Yesu mwenyewe ni jiwe kuu la pembeni”. Hii haimaanishi kwamba kila nabii amepewa kufundisha.
 Nabii pia anaweza kupewa kufanya kazi ya kubomoa na kuharibu kazi za shetani na kupanda pando la Mungu ndani ya mioyo ya watu, kama kuna mahali panahitajika kufanya hivyo. Tunaweza kusoma haya katika kitabu cha Yeremia 1:4,5,10; inasema ” …..kabla sijakuumba katika tumbo nalikujua, na kabla hujatoka tumboni, nalikutakasa; nimekuweka kuwa nabii wa mataifa …………. Ili kung’oa na kubomoa na kuharibu na kuangamiza; ili kujenga na kupanda”.
Kazi nyingine ni kuonya. Tunaweza kuona haya katika kitabu cha Ezekieli 2:3-5; ”akaniambia mwanadamu, nakutuma kwa wana wa Israel, kwa mataifa wanaoasi, walioniasi mimi wao na baba zao wamekosa juu yangu…..”
Kazi nyingine ni mwonaji. I Samweli 9:9 ”(Hapo zamani katika Israel, mtu alipokwenda kuuliza neno kwa Mungu, husema hivi, Haya! Twende kwa mwonaji; maana mtu aitwaye sasa Nabii hapo zamani aliitwa mwonaji)”.
 Kutabiri (kusema mambo yajayo). Yeremia 23:21; inasema ”mimi sikuwatuma manabii hao, lakini walikwenda mbio; sikusema nao, lakini walitabiri.
Kazi ya karama ya unabii. (kama kitendea kazi):
Ni kujenga, kufariji, kutia moyo na kujirunza, pia huthibitisha kile ambacho Mungu amekwisha kusema na wewe. Katika kitabu cha I Wakorintho 14:3,4,24,25,31; tunasoma ”Bali yeye ahutubuye, asema na watu maneno ya kuwajenga, na kuwafariji, na kuwatia moyo. Yeye anenaye kwa lugha hujijenga nafsi yake; bali ahutubuye hulijenga kanisa. Lakini wote wakihutubu, kisha akaingia mtu asiyeamini, au mjinga, abainishwa na wote, ahukumiwa na wote; siri za moyo wake huwa wazi, na hivyo atamwabudu Mungu, akianguka kifudi-fudi, na kukiri ya kuwa Mungu yu kati yenu bila shaka. Kwa maana ninyi nyote mwaweza kuhutubu mmoja mmoja, ili wote wapate kujifunza, na wote wafarijiwe”.
2. manabii wapo hata leo ila nafasi zao ni tofauti na za wale wa agano la kale.
Efeso 4:11,14; ”naye alitoa wengine kuwa mitume na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti na wengine kuwa wachungaji na waalimu; kwa kusudi la kuwakamisisha watakatifu; hata kazi ya huduma itendeke hata mwili wa Kristo ujengwe; hata na sisi sote tutakapoufikia umoja wa Imani na kumfahamu sana mwana wa Mungu, hata kuwa mtu mkamilifu…………. Ili tusiwe tena watoto wachanga, tukitupwa huku na huku na kuchukuliwa na kila upepo wa elimu, kwa hila ya watu, kwa ujanja tukizifuata njia za udanganyifu”.
Pia katika kitabu cha Matendo ya Mitume 13:1; tunasoma ”……. Palikuwako manabii na waalimu …..”. hii inaonyesha kuwa manabii wapo hata leo.
Tofauti iko hivi: kwamba manabii hapo zamani (katika agano la kale) walikuwa viongozi wakiongoza watu, yaani walipewa kuongoza watu, lakini katika agano jipya huduma ya nabii ipo ndani ya Kanisa na nabii hakupewa kuongoza kanisa- kila mmoja wakati huu amepewa Roho Mtakatifu ambaye anamwongoza. Hivyo nabii anayesema kwa mausia ya Mungu ni yule anayesema sawasawa na neno la Mungu.
Kanisa linajengwa juu ya misingi miwili ambayo ni:
a. Yesu Kristo
b. Mafundisho ya mitume na manabii ambao wanafundisha mafundisho ya msingi ambayo yanamfanya mtu awe mkristo. (foundation series). Ukisoma kitabu cha Waebrania 6:1; inasema ”kwa sababu hiyo, tukiacha kuyanena mafundishao ya kwanza ya Kristo; tukaze mwendo ili tuufikilie utimilifu; tusiweke msingi tena wa kuzitubia kazi zisizo na uhai, na wa kuwa na Imani kwa Mungu na wa mafundisho ya mabatizo, na kuwekea mikono, na kufufuliwa wafu na hukumu ya milele”.
Manabii wa sasa wanatofauti na akina Paulo na akina Petro ambapo hao wa zamani walipewa mafundisho ya msingi na hawa wa sasa wanapewa wito (hekima au special revelation) wanaposoma Biblia wanafungua siri za mafundisho ya msingi, ambayo akina Paulo walifundisha, na kutufunulia sisi.

Comments