![]()  | 
| Rais Jakaya Kikwete | 
RAIS Jakaya Kikwete leo anatarajiwa kushiriki maziko ya Askofu Mkuu 
wa Kanisa la EAGT, Moses Kulola (86), aliyefariki Agosti 29, jijini Dar 
es Salaam. Maziko hayo yatafanyika katika Kanisa la EAGT Bugando, ambapo
 ibada ya maziko, inatarajiwa kuanza kati ya saa 3 na 4 asubuhi na 
maziko yatakuwa kati saa 4 na 7.30 mchana.
Akizungumza na waandishi wa habari, Mkuu wa Mkoa Mwanza, Evarist 
Ndikilo, alisema Rais Kikwete anatarajiwa kuwasili leo, ambapo 
atashiriki maziko ya Askofu huyo na baada ya hapo, atakuwa na ziara ya 
wiki moja mkoani Mwanza.
“Atafanya ziara katika wilaya zote saba za mkoa wa Mwanza na atakagua
 shughuli mbalimbali za maendeleo zinazofanyika katika wilaya hizo,” 
alisema Ndikilo.
Alisema baadhi ya shughuli anazotarajiwa kuzifanya ni kuzindua miradi
 ya nishati, ukiwemo mradi wa MCC unaofadhiliwa na Wamarekani katika 
wilaya za Sengerema, Ilemela, Misungwi, Nyamagana na Magu.
Alisema wilayani Sengerema kuna maeneo 30 ya mradi huo, Misungwi 
maeneo mawili, Ilemela mawili, Nyamagana mawili na Magu eneo moja la 
mradi, ambapo mradi huo utazinduliwa katika eneo la Bukokwa wilayani 
Sengerema. Pia katika ziara hiyo, Rais atazindua mradi wa kufua umeme wa
 megawati 60 katika eneo la Nyakato jijini Mwanza.
Kwa upande wa biashara, Rais ataweka jiwe la msingi katika jengo la 
kitega uchumi cha biashara lililopo eneo la Ghana na kufungua hoteli ya 
Gold Crest. Ndikilo alisema kwa maeneo ya afya, atazindua zahanati ya 
Rugeye, maabara ya hospitali ya wilaya ya Ukerewe na mashine ya X- ray 
katika hospitali ya Misungwi, ambayo ni ahadi yake ya muda mrefu, 
itakayowasaidia wananchi wa wilaya.
Kwa upande wa elimu, atafungua shule ya msingi Itulya iliyojengwa kwa
 msaada wa shirika la Marekani yenye madarasa saba na kuweka jiwe la 
msingi katika jengo la ghorofa tatu kwa ajili ya ofisi ya Mkuu wa wilaya
 ya Magu. Aliwaomba wananchi kujitokeza kwa wingi wakati Rais 
atakapokuwa kwenye ziara katika maeneo yao.
- Habari Leo - 

Comments