Skip to main content
Rose Muhando atajwa Tamasha la Krismasi
Mwimbaji wa Injili nchini,
Rose Muhando, ni miongoni mwa Watanzania watakaoimba Tamasha la Krismasi
Desemba 25 mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Mwimbaji huyo anayesikika na albamu
zake mbalimbali ikiwemo ya Utamu wa Yesu, pia ataimba Desemba 26 mwaka
huu kwenye Tamasha la Krismasi litakalofanyika Uwanja wa Jamhuri,
Morogoro.
Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya
Tamasha la Krismas, Alex Msama alisema jana kuwa hatua ya kamati yake
kumalizana na Muhando imewapa faraja kubwa, kwani huyo ni miongoni mwa
waimbaji ambao Watanzania wanawapenda.
“Mungu ni mwema, kila tunalolipanga
anatusaidia sana, karibu waimbaji wote ambao mashabiki wanawapenda,
wamekuwa na ushirikiano mkubwa na sisi. Hawana matatizo na si watu wenye
tamaa, bali wanaweka mbele kutoa huduma.
“Tayari hivi sasa waimbaji watatu wa
Tanzania tumeshakubaliana nao ambao ni Upendo Nkone, Upendo Kilahiro na
huyo Rose Muhando, kwa nje tumeshamalizana na Ephraim Sekeleti. Bado
tunaendelea na mazungumzo na wasanii wengine wa ndani ya Tanzania na nje
ya nchi ili wote waje kutumbuiza,” alisema Msama.
Albamu ya Utamu wa Yesu ya Rose
Muhando inabeba nyimbo saba ambazo ni Utamu wa Yesu, Raha Tupu,
Tamalaki, Ndivyo Ulivyo, Woga Wako, Imbeni na Kusifu na Achia.
Mbali na Utamu wa Yesu, Rose Muhando
pia amewahi kuvuma na albamu za Uwe Macho, Nyota ya Ajabu (Zawadi ya
Krismasi) na Jipange Sawasawa.
Pia amepata kung’ara katika wimbo wa Vua
Kiatu, alioshirikiana na Anastazia Mukabwa wa Kenya katika albamu ya
Vua Kiatu, ambayo ilikuwa na nyimbo kama Vua Kiatu, Ee Mungu, Usiwe
Manamba, Nzizilela, Nishike Mkono Bwana, Wanaokudharau na Mfalme.