Cecilia; nilikosea kutaka kujiua baada ya kupofuka

Cecilia Ricardo, binti aliyepofuka macho akiwa mdogo, aliyetamani kujiua 


Ilikuwa mwaka 2011 mwezi wa saba katika eneo la Visole Manispaa ya Morogoro, Cecilia Ricardo anasema kuwa wakati huo akiishi kwa dada yake, Theresia Patrick Ricardo alimtuma mtoto wa dada yake, Evodia kwenda dukani kununua sumu ya kuua panya ili anywe kwa lengo la kujiua, maamuzi hayo alichukua kutokana na mateso yaliyotokana na maumivu makali ya macho ambayo baadaye yaliyopoteza kabisa uwezo wa kuona hadi leo.
Zilikuwa siku nne za mateso makali ya maumivu ikiambatana na maumivu ya kichwa mfulululizo na macho kutoka maji, hali ambayo ilimshawishi kumtuma mtoto aende dukani kununua sumu ya panya ili kujiua.
Hata hivyo mtoto huyo alifichua siri hiyo kwa kaka aliyekuwa nje na kunyang’wa fedha na kwa sababu hakuwa na uwezo wa kuona mbinu yake ya kuijua iliishia hapo, anasema Cecilia katika mahojiano na mwandishi wa makala haya eneo la Madizini Kilakala mkoani Morogoro.
Cecilia anaeleza namna mkasa huo ulivyomtokea baada ya kutoka katika mji mdogo wa Turiani Wilaya ya Mvomero mwezi mmoja baada ya kufika kwa dada yake Manispaa ya Morogoro kwa lengo la kujipumzisha huku akiwa amebeba kiasi cha fedha Sh30,000 fedha alizopata kutokana na mradi wa kuuza maji baridi.
Baada ya kuishi Morogoro Mjini kwa muda wa mwezi mmoja aliona upo umuhimu wa kuwasiliana na familia iliyoko Turiani hivyo njia pekee ya kuwasiliana nao ni kununua simu ya kiganjani ndipo alipomwambia dada yake kumpeleka mjini ili akanunue yenye uwezo wa kuweka nyimbo ili kuweza kupata nafasi ya kuweka nyimbo za injili.
“Nilinunua simu dukani na kwenda kusajiliwa lakini nilimwomba dada niwekewe nyimbo za injili ikiwa njia moja wapo ya mimi kuniriwaza pindi ninapokuwa na mawazo juu ya maisha yangu hasa baada ya kupoteza kabisa uwezo wa kuona,” anasema Cecilia huku akiwa mwenye furaha na kuonyesha tabasamu.
Anasema kuwa wakati wamefika eneo la kibanda cha kuweka nyimbo katika simu yake, Cecilia alichagua nyimbo nyingi za kwaya ya Kanisa la Katoliki, jambo hilo lilimpa mshangao mmiliki wa kibanda hicho, Noah Mgeni na kuhoji kwa nini dada huyo amekuwa akitoa masharti ya kutoingiza nyimbo nyingine tofauti na nyimbo za injili tu.
Theresia Patrick Ricardo dada mkubwa wa Cecilia alimwondolea mshangao huo Noah kwa kumweleza kuwa huyo mdogo wake ni mlemavu wa macho (haoni kabisa) na hapo kabla ya kupata ulemavu huo alikuwa mwanakwaya hivyo njia pekee ya kujiliwaza kutokana na ulemavu huo ni kusikiliza nyimbo za kwaya.
Noah aliendelea kuhoji je, anaweza kuimba na kucheza licha ya kuwa mlemavu... Kama anaweza basi mimi nitamuunganisha na mtu ili aweze kutumbuiza katika kumbi za sherehe za harusi, kipaimara na kadhalika.
“Baada ya kugundua Cecilia kuwa ni mlemavu wa macho, nilimwomba namba yake ya simu ili nimuunganishe na yule mtu ambaye niliamini angeweza kumsaidia,” anasema.
Noah anaeleza kuwa baada ya kupata namba ya simu ya Cecilia alimpigia na kufunga safari ya kumtembelea nyumbani kwa dada yake Visole ambako alikuwa anaishi
kwa lengo la kumfahamu zaidi na hilo alilifanya na kumvutiwa naye huyo dada kwa sababu yeye ni msanii na alikuwa anaigiza kucheza muziki wa injili kama mlemavu wa macho.
“Baada ya kuonana naye Cecilia kwa mara ya pili nyumbani kwao, nilimshauri kuwa kutokana na umbo alilokuwa nalo, ni vizuri zaidi kama atakuwa anacheza, naye akakubali,” anasema.
Noah alisema kuwa alianza kumfundisha kucheza, wimbo wa kwanza ni ule wa wasanii wa muziki wa injili kutoka nchini Burundi wa kwaya ya Ambasado kupitia wimbo wa kwetu pazuri na aliweza kumudu vema kucheza kwa hisia jambo ambalo yeye Noah alikuwa analitaka.
“Mimi ni msanii na ninacheza katika sherehe mbalimbali zikiwemo harusi, nacheza nyimbo za injili tu na kuigiza kama mtu nisiyeona na wageni waalikwa hunitunza fedha, lakini nilipogundua Cecilia ni mlemavu wa macho niliona bora nafasi hiyo awe anacheza yeye kwa uhalisia tofauti na mimi hicho ndicho chanzo cha binti huyu kuingia fani ya kucheza muziki”anafafanua Noah.
Cecilia Joseph Ricardo anasema mawazo ya kutaka kujitoa uhai kwa kunywa sumu ya panya kwa sasa hayapo tena katika kichwa chake, ni kutokana na ushawishi wa Noah Mgeni ambaye amembadilisha kwa kumwingiza katika fani ya muziki.
“Sasa hivi nimepata faraja kubwa kupitia muziki wa nyimbo na nimekuwa nikicheza show katika sherehe za harusi na wasamalia wema wamekuwa wakinitunza fedha ambazo natumia katika kuendesha maisha yangu mwenyewe bila utegemezi wowote kutoka kwa wazazi wangu akiwemo na dada yangu na nina amani sana moyoni na huu upofu ni kama makusudi yake katika mitihani kama binadamu wengine” anasema Cecilia.
Kuna aina nyingi za ulemavu na kukumbwa na changamoto mbalimbali katika jamii inayoizunguka lakini wapo ambao wanaweza kufanya jambo la kuweza kuendesha maisha yao wenyewe bila kuhitaji utegemezi labda kuwezeshwa nyenzo tu na mambo mengine kufanya wenyewe hilo linawezekana endapo kutakuwa na mtu wa kukushika mkono,” anafafanua.
Hali ilivyokuwa awali
Cecilia anasema kuwa yeye kabla ya macho yake kupoteza kabisa nuru ya kuona alikuwa na malengo mengi kama binadamu wengi na kati ya malengo hayo ni kuwa mtawa; enzi za utoto wake alikuwa mwimbaji katika kwaya ngazi ya shule na kanisa Katoliki.
Amekuwa akipenda wasanii wakubwa wa nyimbo za injili wakiwemo Christina Shusho hasa kupitia wimbo wake wa Nipe Macho, Anastazia Mkobwa katika wimbo wa Nishike mkono na Ambasada wimbo wa kwetu pazuri.
Alivyopata ulemavu
Akiwa na umri wa miaka 10 akisoma darasa la tatu shule ya msingi Mtibwa wakicheza mchezo wa kujaza mchanga kwenye chupa ya soda na wenzake saa 7 mchana siku ya jumamosi eneo la kanisa la Anglikana, mtoto Ambe Oden alirusha mpira wakati yeye Cecilia Ricardo akijaza mchanga huku amekaa chini katika chupa, alikwepa mpira huo na uso wake kugonga katika mdomo wa chupa katika jicho lake la kushoto.
Cecilia anasema kuwa baada ya kuinamisha uso wake wakati akikwepa mpira uliorushwa na Ambe Oden na kujibamiza katika jicho la kushoto, aliona nyota nyingi usoni katika macho yote na maumivu makali na mchezo uliishia hapo. Baadaye wenzake walimshika mkono na kumrudisha nyumbani huku macho yakipoteza nuru ya kuona, na maumivu makali.
Baada ya dakika 10 baadaye macho yake yalirejea katika hali yake ya kawaida na kuanza kuona huku yakiwasha na maumivu yalidumu kwa siku mbili na macho yakiwa yamevimba, anafafanua.
Siku ya tatu tangu apate tatizo hilo alipelekwa hospitali ya misheni ya Bwagala Turiani, hiyo ilikuwa mwaka 2000, alipimwa na kugundulika kuwa ana presha ya macho na kutakiwa kufanyiwa operesheni.
Alilazwa kwa siku mbili na siku ya tatu hatimaye alifanyiwa operesheni katika jicho la kulia badala ya kushoto na siku ya saba baada ya kufanyiwa operesheni alirejea nyumbani na kuendelea na masomo ya shule ya msingi huku macho yakiwa katika nuru mzuri ya kuona, ikiwa ni baada ya kufanyiwa oparesheni lile lililoumia.
Anawataja watoto wenzake enzi hizo kwa kutaja timu ya mchezo huo wa kujaza mchanga katika chupa baina ya mtaa wa kanisani na bondeni kwa majina, katika timu yake ya kanisani iliwakilishwa na yeye, Jamhuri Seif, Mwajabu Sufian, Ramadhan Wania, Ruth Elias, Christina Daniel na Christina Anthony.
Wakati timu ya wapinzani wao iliundwa na Amba Oden, Patrick Richard, Mariam Seif, Winfrida Anthony, Halima Abdallah, Anna Anthony, Mwanahamis Sufian, Jesca Pius na Georgina Kulabuku ambao wamefariki dunia.
Hali inajirudia
Akiwa darasa la tatu mwaka 2006 macho yake yalianza kupoteza tena uwezo wa kuona taratibu. Alilazimika kuomba kuomba ahamishiwe kutoka dawati la nyumba ambako alikuwa anakaa na kuhamia mbele ili kuweza kuona kilichoandika ubaoni.
Kabla ya likizo ya mwezi wa sita akiwa kidato cha pili shule ya sekondari ya kata ya Turiani wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro akiwa na umri wa miaka 16, licha kusogezwa dawati la mbele ili kuweza kuona kilichoandikwa ubaoni wakati huo ikiwa ni mwezi wa tano mwaka 2006 dawati lake tena lilisogezwa jirani na ubao ambako maandishi yalikuwa anaona.
Hali imeendelea kuwa mbaya kadri muda ulivyokuwa unaenda mbele, hata baada ya kurudishwa hospitali, hakuweza tena kuwa na uwezo wa kuona.
Mama mzazi wa Cecilia Patrick Ricardo, Evodia Lucas (53) anasema suala hilo anamuachia Mungu.
Evodia anasema baadhi ya madaktari walisema tatizo la mwanaye amerithi kutoka kwa bibi yake lakini jambo hilo yeye anapinga akida hakuna mwenye tatizo hilo ukiachilia mbali kwa mama yake na mtoto wake tu.

                         Source: Mwananchi


Bali wote waliompokea(YESU KRISTO) aliwapa uwezo wa kufanyika watoto wa MUNGU, ndio wale waliaminio jina lake; -Yohana 1:12

Comments