MAOMBI YA TOBA
Na Mtu wa Mungu Nabii Samson,
Utangulizi:
Tunahitaji msaada wa Mungu kwa kila jambo
tunalolifanya katika maisha yetu na
Msaada unapatikana kulingana na Mahusiana yaliyopo baina ya
muombaji na mtoaji, kwa kawaida
unalolitaka kwa kwa mtu ili ulipate mahusiano yanatakiwa yawe mazuri,
Maana
ya Maombi:
Maana ya maombi ni kusema na Mungu au
kuhitaji msaada toka kwa Mungu. Isaya 43:26, Unikumbushe, na tuhojiane; eleza
mambo yako, upate kupewa haki yako. Sehemu pekee ya kueleza mambo yako ni kwa
Mungu,
Unikumbushe – Mungu anaposema tumkumbushe hana maana kuwa amesahau. Hapana.
Ila anataka kuona moyoni umeweka nini. aliwaambia wana wa Israel kuwa “Niliwazungusha
makusudi ili nione mioyoni mwenu mna nini.” Ndiyo maana tunatakiwa
kuliweka Neno la Bwana mioyoni mwetu. Zab 119:10,
Yeremia
1:12
Tuhojiane – Ni jambo la kumshukuru Mungu anayetupatia nafasi ya kueleza
mambo yetu, kero zetu na shida zetu kwake kwa kuhojiana naye ili tupate
kupewa haki zetu.
Haki
zetu:
Katika Biblia ziko haki zetu nyingi
sana ambazo Mungu wetu ametuahidi. Lakini wengi wetu hatuzijuwi. Inatubidi kusoma Biblia kwa bidii
ili Neno lake Kristo likae kwa wingi ndani
Biblia ina mistari 31,173. Hebu jipime uone,
wewe unaijua mingapi? Dan 9:1 – Daniel katika wakati wake alisoma kitabu
alichokuwa ameandika nabii Yeremia akakuta muda ambao walitakiwa watoke
utumwani umepita na bado wako utumwani. Walikuwa huko kwa kutokujua. Kwa hiyo
kusoma Neno la Mungu kuna faida nyingi, muhimu ikiwa ni kufahamu ukweli wa
mambo.
Sababu
za Kuomba:
Ziko sababu mbali mbali za kusema na
Mungu. Na kama tulivyoona hapo juu kuomba ni kusema na Mungu. Hii ina maana
unapotaka kusema na Mungu ni vizuri ujuwe unataka kusema naye kuhusu nini.
Tuchukue
mfano: Unapoenda ofisi ya mtu ye yote, huwezi kuingia ofisini hapo wakati
hujuwi unakwenda kwa sababu gani. Ndiyo maana ukiingia unaambia ‘karibu,
tukusaidie nini?’.
Ni
kawaida kwamba jibu la swali hilo huwa lipo. Lakini watu wengi humwendea Mungu
wakati hawajuwi sababu ya kumwendea. Pia, kwa kuwa Mungu ni baba yetu
hatutakiwi kumwendea wakati wa shida tu, yaani shida ikiisha, basi. Hapana.
kwenye ofisi za watu huenda wakati tunashida
tu, lakini kwa Mungu wetu tunatakiwa kwenda wakati wote. Hii huonyesha ushirika,Mahusiano
yaliyopo kati yetu na Yeye.
Sababu za kusema na Mungu, yaani
sababu za maombi ni nyingi sana. Yako mambo mengi sana ambayo tunatakiwa
kuyabeba wakati wa maombi. Ni vigumu kuyataja yote lakini tutaangalia baadhi,
ambayo yatafanyika kama kielelezo. Lakini kwanza tuangalie maandiko,:
Kolosai
4:2-4 inasema hivi, Dumuni katika kuomba huku na shukurani, mkituombea
na sisi pia, kwamba Mungu atufugulie mlango kwa lile neno lake, tunene siri ya
Kristo, ambayo kwa ajili yake nimefungwa, ili niidhihirishe, kama inipasavyo
kunena.
Hayo mambo
mazito hapo juu ni maagizo ambayo Paulo aliwaandikia Wakolosai. Napenda
tujifunze kutokana na hayo maombi. Mara nyingi watu wa Mungu husema tuko kwenye
maombi, hata wakati mwingine tunakosea maana si jambo la kutangaza. Maandiko
hayo yanatupatia mwelekeo wa sababu za kutupeleka mbele za Mungu kwa maombi.
Pamoja na sababu hizo chache, hapo, pia tunaambiwa kuwa tunatakiwa kudumu
katika kuomba, kudumu, ni kutokata tamaa,
kutokuchoka, kutokupunguza, kutoacha,
Katika
maneno hayo MtumePaulo aliwaomba Wakolosai wawaombee pia. Unajua tunafanya
makosa makubwa kama hatutaombea viongozi wetu.
Tutawaombea nini?
Mungu
awafungulie milango, Mungu awape usemi, Mungu awawezeshe katika kunena na
kutenda pia. Je, hayo ndiyo tutaombea kila siku? Hapana. Ni pamoja na hayo.
Tutaona kwa kirefu baadhi ya mambo mengine ambayo tunapaswa kuyaombea, maana
kama ni hayo tu basi nadhani ni muda mfupi tu nasi tutakuwa tumemaliza.
Tuangalie
tena 1Yohana 5:14-15 Na huu ndio ujasiri tulionao kwake, ya kuwa,
tukiomba kitu sawa sawa na mapenzi yake, atusikia. Na kama tukijua kwamba
atusikia, tuombacho chote, twajua kwamba tunazo zile haja tulizomwomba.
Ujasiri wetu unaotupeleka kwenye
maombi ndio huo. Mtu jasiri haogopi, hana mashaka hata kidogo. Kwa hiyo
tunapaswa kuwa majasiri kwa Mungu wetu.
Mahali pengine Biblia inasema mwenye
haki ni jasiri kama simba. Uajua simba ni mnyama wa ajabu sana. Si mwoga.
Hafanani na fisi. Ukiwa karibu na fisi ukamshtua kile anafanya ni kukuharishia:
ishara ya uoga. Lakini ukimshtua simba, yeye hakimbii. Ni kama ndiyo unamwita
kuwa aje mkutane mpambane, yesu Anaitwa
Simba wa Yuda,
Maandiko yanasema pia tuombe sawa
sawa na mapenzi ya Mungu. Ni vizuri tufahamu mapenzi ya Mungu.
Tutayapata wapi? Mapenzi ya Mungu tutayajuaje? Mapenzi ya Mungu yako kwenye
Neno lake. Ebu tuangalie maandiko machache yanayohusu mapenzi ya Mungu. Na haya
tunaweza kuyatumia kama muongozo wa maombi yetu wakati tunapoomba.
1Tim
2:1-4, Basi, kabla ya mambo yote, nataka dua, na sala, na maombezi, na
shukurani zifanyike kwa ajili ya watu wote; kwa ajili ya wafalme na wote wenye
mamlaka, tuishi maisha ya utulivu na amani, katika utauwa wote na ustahivu.
Hili ni zuri, nalo lakubalika mbele za Mungu mwokozi wetu, ambaye hutaka watu
wote waokolewe, na kupata kujua yaliyo kweli.
Hapo
tunaona wajibu wetu. Tunatakiwa kuwaombea watawala wetu, wafalme wetu, ili
tuishi kwa amani. Vinginevyo amani hutoweka. Amani inatakiwa kuendelea kuwepo
kwa ajili ya maombi ya watakatifu. Pia anasema tuombee watu wote. Mpendwa
ukweli Mungu anapenda watu wote, na anapenda wote waokolewe.
Tunachotakiwa
kuendelea kufanya ni kuwaombea. Anzia na wale unaowafahamu, ambao
bado hawajaokoka. Waombee, ukijua kuwa na wewe kuna mtu alikuombea ukapata
wokovu. Kumbuka pengine ulivyokuwa mbishi, hukutaka hata kusikia habari za
wokovu. Pengine uliwafukuza waliokushuhudia habari za wokovu. Je, waweza kujua
kwa nini uliokoka? Jibu: uliombewa na mtu.
Sasa zifuatazo ni baadhi ya
Sababu za maombi,
1.
Isaya 62:7, Wala msimwache akae kiimya, mpaka atakapofanya imara
Yerusalem, na kuufanya kuwa sifa duniani.
Maandiko yanasema tusimwache akae
kimya. Ina maana tuendelee kuomba. Hivyo hayo ni mapenzi ya Mungu kwetu.
2.
Zaburi 122:6, Utakieni Yerusalem(ISRAEL) amani, na wafanikiwe
wakupendao.
Mpendwa,
Baraka zingine ni za kuchukua tu, wala hazina gharama sana. Kutamka tu kwamba
tunaitakia amani, tunaiombea amani Yerusalem, hizo ni Baraka za mafanikio;
andiko linasema wafanikiwe wakupendao.
Kuna
watu hawataki kusikia Israel.
Wengine husema wataifuta katika ramani ya
dunia hii! Huwa nacheka kwa kuwa kwa kusema hivyo huwa wanasema:
Watamfuta
Mungu kutoka katika uso wa dunia. Ukweli huwa hawajuwi wanasema nini.
Mungu alimwambia Ibrahimu kuwa yeye atakaye kulaani nitamlaani, yeye
atakayekubariki nitambariki. Ebu tujipatanishe na wateule wa Mungu kama
tunataka kupona. Pia Mungu alisema ‘mpaka mtakapogundua dunia hii inakaa
kwenye nini’,
hapo
ndipo atakapoiacha Israel wasiwe watu wake. Yeremia 31:35-37, Bwana
anasema hivi, awapaye watu jua, ili kuwa nuru wakati wa mchana, na amri za
mwezi na nyota, ili kuwa nuru wakati wa usiku, aichafuaye bahari, hata mawimbi yake
yakavuma, Bwana wa majeshi, ndilo jina lake. Amri hizi zikiondoka, zisiwe mbele
zangu, asema Bwana, ndipo wazao wa Israel nao wataacha kuwa Taifa mbele zangu
milele. Bwana asema hivi, kama mbingu zikiweza kupimwa, na misingi ya dunia
ikiweza kugunduliwa huko chini, ndipo wazao wa Israel pia nitawatupilia mbali,
kwa ajili ya hayo yote waliyoyatenda, asema Bwana.
Mpendwa,
mtu asikudanganye, ukasema vibaya juu ya Israel. Hii pia ni sawa na kusema
vibaya juu ya mcha Mungu ye yote. Wala usithubutu kufungua kinywa kumnena
mabaya. Nikukumbushe kidogo habari ya wale waliofungua vinywa kumnena vibaya
Musa, walikuwa Miriamu na Haruni. Nakuambia Mungu aliingilia kati mwenyewe,
akawaadhibu mara moja. Miriam akapigwa na ukoma. Kwa hiyo tujiepushe kulisema
vibaya Taifa hilo la Mungu. Ni lake. Sikia Mungu anavyosema: ‘kama mtu
atajua dunia imekaa juu ya nini ndipo Taifa hilo liaacha kuwa Taifa lake.’
3.
Luka 6:28, Wabarikini wale ambao wawalaani ninyi, waombeeni wale ambao
wawaonea ninyi.
Mpendwa, safari ya mbinguni imeelekezwa
vizuri namna ya kuisafiri. Hiyo ni njia moja wapo ya kuelekea huko: Kuwaombea
wale wanaowaonea, kuwabariki wale wanaowalaani! Fanya hivyo na Mungu
atakubariki.
4.
Luka 22:40, Alipofika mahali pale aliwaambia, ombeni kwamba msiingie
majaribuni.
Bwana
akawaambia kuwa waombe ili wasiingie majaribuni. Hakusema ‘ombeni kwamba
msijaribiwe’. Aliwaambia waombe kuwa ‘wasiingie’. Maana yake nini? Unaweza
kufika nyumbani kwa mtu, kwa nje, wala usiingie ndani. Waweza kufika Ubungo,
ambapo tunajua ni Dar es salaam. Lakini ukifika Ubungo, bado utakuwa hukuingia
mjini. Ebu tuombe kuwa tusiingie katika majaribu, mpaka yakatumeza na
kutushinda.
5.
2Kor 13:7, Nasi twamwomba Mungu, msifanye lolote lililobaya, si kwamba
sisi tuonekane tumekubaliwa, lakini ninyi mfanye lililojema, tujapokuwa sisi tu
kama waliokataliwa.
Omba kuwa usifanye lolote lililobaya,
yaani usifanye dhambi. Pia ombea watu uwajuao na usiowajua wasifanye dhambi.
Hiyo itawasaidia wengine kujilinda na itafanya watu wengine wawe na breki
katika kutenda maovu.
Omba watu wafanye yaliyo mema, ni
pamoja na wewe mwenyewe, omba kuwa ufanye mema.
6.
Filipi 1:9, Na hii ndio dua yangu, kwamba pendo lenu lizidi kuwa jingi
sana, katika hekima na ufahamu wote.
Omba kuwa upendo wako uzidi kwa watu,
omba kuwa upendo wa watu kwa wenzao uzidi kuwa mwingi sana. Unajua mpendwa Neno
linasema siku za mwisho upendo wa wengi utapoa:
utapoa wao kwa wao, utapoa kwa Mungu.
Sasa omba kuwa watu wapendane. Omba kuwa watu wampende Mungu wao aliye waumba.
Wasimpende adui ambaye hakuwaumba.
7.
1Thes 5:23, Mungu wa amani mwenyewe awatakase kabisa; nanyi nafsi zenu
na roho zenu na miili yenu mhifadhiwe mwe kamili, bila lawama, wakati wa kuja
kwake Bwana wetu Yesu Kristo.
Ndugu mpendwa, haya ni maombi ya
muhimu sana. Kama Biblia isemavyo kuwa Yesu atakuja kama mwivi. Ni wazi kabisa
tunafahamu kuwa mwizi hatoi taarifa ya kuwa anakuja kuiba, labda jambazi.
Jambazi anaweza kutoa taarifa maana huwa anakuja akiwa tayari kwa lolote lile.
Bwana alisema atakuja kama mwivi. Kwa hiyo tunatakiwa kuomba kuwa wakati wa
kuja kwake, tusiwe na kasoro katika miili yetu, nafsi zetu na roho zetu.
8.
Luka 11:13, Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu
vipawa vilivyo vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa Roho
mtakatifu hao wamwombao?
Wapo
watu wengi ambao hukaa muda mrefu kabla hawajajazwa na Roho Mtakatifu, mpaka
wengine wanakata tama na kudhani Roho mtakatifu ni wa watu maalumu. Hapa. Wala
usikate tamaa, endelea kuomba huku ukiamini kuwa Mugu atakupatia Roho
mtakatifu. Pia inawezekana unanena kwa lugha, ambayo wengi wamedhani
kila anayenena kwa lugha ana Roho wa Mungu. Mpendwa, ebu kagua kama kweli
ni Roho wa Mungu. Maana hata waganga wa kienyeji wananena kwa lugha.
Tofauti
iliyopo ni kwamba hawana matunda ya Roho mtakatifu. Usiridhike na lugha tu
isiyo na matunda, maana imeandikwa:Mtawatambua kwa matunda yao. Math
7:16
9.
1Kor 14:13, Kwa sababu hiyo yeye anenaye kwa lugha na aombe apewe kufasiri.
Ziko haki zetu nyingi katika Biblia
ambazo hatujazifahamu. Na kama hatuzifahamu, basi, hatuwezi kuziomba. Lakini
hapa tunaambiwa kuwa mtu anayenena kwa lugha aombe pia apewe kufasiri. Fanya
hivyo na Mungu atakujalia kufasiri.
10.
Zab 37:4, Nawe utajifurahisha kwa BWANA, Naye atakupa haja za moyo wako.
Wakati
mwingine huwa tunayo yale tunayoyawaza mioyoni mwetu, bila mtu mwingine kujua.
Tunapaswa kumuomba Bwana atupatie haja ya mioyo yetu. Ni kweli kuwa Mungu
anajua yote. Lakini anapenda kusikia tukimwambia. Yesu akamuuliza Baltmayo
kipofu kwamba“wataka nikufanyie nini?” Akasema nipewe kuona, akapewa
kuona. Marko 10:51
11.
Zab 71:9, Usinitupe wakati wa uzee, Nguvu zangu zipungukapo
usiniache.
Mpendwa,
hili ni ombi muhimu sana katika maisha yetu. Unajua wako watu wanaishi kama
Wafalme wa zamani. Wafalme wa zamani waliishije? Walikuwa wanasalimiwa ati ‘Uishi
milele ee mfalme’. Hawakuwa wanajiandaa kuwa kwa vyovyote wataondoka katika
utawala. Hawakujua kabisa kuwa siku moja nguvu zao zitakwisha.
Natumaini unakumbuka jinsi Herode
alipopata taarifa kuwa mfalme mwingine amezaliwa, yeye alipanga namna ya
kumwangamiza. Mfalme aliyezaliwa akiwa kitoto kichanga ingemchukua miaka mingi
kufikia umri wa kutawala kama mfalme. Na inawezekana kabisa hadi afikie umri
huo wa kutawala, yeye Herode tayari angekuwa ameshakufa. Lakini kwa sababu ya
kufikiri ataishi milele kweli, kama ambavyo alikuwa akisalimiwa, yeye akaona
cha kufanya ni kumuangamiza mfalme-mtoto huyo kwa kuwa yeye Herode ataendelea
kutawala milele. Ni ajabu kabisa!
Hebu
tuone maombi hayo ya Daudi katika Zaburi 17:9 yalivyokuja kufanya kazi.
Tunapata habari hiyo katika 2Sam 21: 15-17, Basi kulikuwa na vita tena
kati ya Wafilisti na Israel; Daudi akashuka mpaka Gobu, na watumishi wake
pamoja naye, akapigana na Wafilisti, naye Daudi akaishiwa na nguvu. Naye
Ishi-benobu, aliyekuwa mmojawapo wa Warefai, ambaye uzito wa mkuki wake ulikuwa
shekeli mia tatu za shaba kwa uzani, naye amejifungia upanga mpya, alijaribu
kumwua Daudi. Lakini Abishai, mwana wa Seruya, akamsaidia, akampiga Mfilisti
akamwua. Ndipo watu wa Daudi wakamwapia, wakasema, Wewe hutatoka tena pamoja
nasi kwenda vitani, usije ukaizima taa ya Israel.
Maombi aliyoyaomba Daudi mtumishi wa
Mungu kuwa atakapokuwa mzee, yaani nguvu zake zitakapokwisha asiachwe, siku
ilifika kweli nguvu zake zikaisha. Akakaa chini. Ndugu yangu, mwanaume Daudi
alishindwa hata kukimbia, achilia mbali kupingana. Huyu ni Daudi aliyeua dubu,
aliyeua simba, Daudi aliyeua Goliathi!
Ndugu yangu siku zinakuja, wengine
tayari zimewafikia, hawawezi tena kuomba kama walivyofanya zamani. Hawawezi
tena kuhubiri kama walivyofanya zamani. Nguvu zao zimekwisha. Hata
wanapokabiliana na Ishi-benobu wao, hawawezi tena.
Japo Ish-benobu alikuwa ana upanga
mpya, maana yake mbinu mpya tofauti na ile aliyoizoea enzi zake, lakini kifo
kilikuwa kinamkabili. Daudi aliwahi kuomba zamani na sasa faili lake
likafunguliwa, likakutwa kuna ombi hilo ambalo halikuwa limejibiwa hadi wakati
huo.
Na ndipo ilibidi jibu litumwe. Ndugu
yangu, nikipiga picha jinsi Daudi alivyokuwa amekaa chini, anamwangalia
Ishi-benobu mbele yake, bila shaka alikuwa anamwambia ‘siku zako
zimekwisha…..Wewe ni halali yangu’. Kumbuka vijana wote walikuwa wamekimbia
hivyo Daudi alikuwa amebaki peke yake.
Yawezekana hapo ulipo uko peke yako,
huna mtu wa kulia kwako wala kushoto kwako. Ni vita mbaya sana hiyo. Huna hata
mtu wa kumwambia jambo, kuwa nikifa watazame kitu muhimu nimekiweka mahali.
Kumbuka wakati huo Daudi alikuwa na ramani ya Hekalu, wala asingeweza kumpatia
Ishi-benobu maana haikuwa inamhusu.
Pengine sasa Ishi-benobu yuko mbele
yako, unachokiona ni upanga mpya! Sikia Neno toka kwa Bwana Mungu wako,
hatayaabisha mafuta aliyokupaka, kamwe. Pamoja na maombi yako kuwa asikuache,
lakini nasema Mungu alikupaka mafuta,
Amini tu Mungu hatakuaibisha. Hataaibisha mafuta aliyokupaka. Abishai hayuko mbali. Kaza macho
yako juu, kuna jambo litatokea. Kabla Ishi-benobu hajakufikia, Abishai
atakutokea. Bwana ameshasema na Abishai. Namuona katika ulimwengu wa roho
anakuja mbio. Ole wa Ishi-benobu, mauti imemkaribia sana. Usiogope. Abishai
huyo, anakuja. Hutaaibika. Vita ni vya Bwana! 2Nyakati 20:15
Comments