Mch. Mtikila: Serikali ya Tanganyika haiepukiki

Mchungaji Christopher Mtikila

Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba amewasilisha Rasimu ya Pili ya Mabadiliko ya Katiba katika Bunge la Katiba Machi 18, mwaka huu.  Katika hotuba yake, Jaji Warioba alitumia saa matatu, kueleza wazi  kuwa kutokana na maoni ya wananchi na taarifa za uchunguzi na utafiti, muundo wa Serikali tatu ndiyo mwafaka kwa sasa.
Jaji Warioba katika hutuba yake, alianisha malalamiko ya pande zote za Muungano, ambayo kwa zaidi ya miaka 30 yameshindwa kupatiwa ufumbuzi katika Muundo wa Serikali mbili.
Akasema kutopatiwa ufumbuzi kwa malalamiko hayo, sasa kumefanya yafikie hatua ya upande wa Zanzibar kuvunja Katiba ya Muungano kwa kuunda Katiba yake yenyewe. Ilielezwa kwamba Zanzibar ilifanya mabadiliko katika Katiba yake ya mwaka 1984 ambayo sasa inajiita nchi yenye Rais mwenye mamlaka kamili ya kuigawa ardhi ya visiwa hivyo katika maeneo ya utawala.
Jaji Warioba akasema kutokana na mabadiliko hayo ya Katiba sasa Muungano, umetoka kuwa wa nchi moja Serikali mbili, kwenda muungano wa nchi mbili na Serikali mbili. Hivyo ili kuimarisha Muungano kwa mazingira ya sasa tume yake ikapendekeza mfumo wa Serikali tatu, ambazo ni  Serikali ya Tanganyika, Serikali ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri  ya Muungano wa Tanzania.
Mchungaji Christopher Mtikila ni mmoja ya wanasiasa ambao kwa miaka zaidi ya 20 sasa, wamekuwa wakililia kurejea Serikali ya Tanganyika. Katika mahojiano na gazeti hili Mtikila akaeleza kwamba “Serikali ya Tanganyika sasa haiepukiki.”
Swali. Wewe ni Mjumbe wa Bunge la Katiba nini maoni yako baada ya Jaji Joseph Warioba kuwasilisha Rasimu  ya  Pili  ya Katiba Mpya kwenye Bunge la Katiba?
Jibu: Jaji Warioba na tume yake wamefanya kazi nzuri na wameunga mkono harakati zangu za kuidai Tanganyika iliyo huru ambayo ilikuwa  inafichwa na watu wachache.
Swali. Katika taarifa ya Jaji Warioba amebainisha changamoto nyingi ndani ya Serikali mbili je unadhani mfumo wa Serikali tatu sasa ni mwafaka?
Jibu: Muungano ni uhusiano ya hiari na lazima usukumwe na masilahi ya kila upande, hivyo kwa sasa kuendelea na Muungano unaopingwa kila upande ni sawa na  utumwa.
Swali: Baadhi ya Watanzania wamekuwa wakipinga Mfumo wa Serikali tatu ambao, umependekezwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba. Je, wewe maoni yako ni nini?
Jibu: wanaopinga mfumo huu wana matatizo, kwani hakuna taifa la Tanzania ambalo lilikwenda kudai uhuru Umoja wa Mataifa bali waliodai uhuru ni Watanganyika hivyo huwezi kuiua Tanganyika.
Swali: Baadhi ya wanasiasa wamekuwa wakipinga taarifa ya Tume ya Jaji Warioba kuwa watu waliohojiwa na kutoa maoni ya kutaka muundo wa Serikali tatu hawazidi 17,000 ambao  hawafikii hata asilimia tano ya Watanzania wote, nini maoni yako?

Jibu: Mimi ninaamini Maombi ya Serikali tatu ni ya Watanzania wengi hao CCM ambao wanadai, maoni ya Tume ya Warioba ambaye ni CCM mwenzao hawafiki hata milioni 2.5 hata ikipigwa kura ya katiba hatawashinda.
Swali: Kutokana na utata juu ya uhalali wa maoni ya wachache kudai Tanganyika kuna hoja ya sasa kuitishwa kura ya maoni ya Watanzania wote juu ya muundo wa  Muungano nini maoni yako?
JIbu: Hakuna sababu ya kura za maoni kwani suala la kudai utaifa halina wingi au uchache ni muhimu sasa kukubaliana na Muundo wa Serikali tatu, kwani baadaye unaweza kudaiwa kwa njia ya vurugu.
Swali: kwa mujibu wa maelezo ya Jaji Warioba tayari Wazanzibari wamevunja Katiba ya Muungano kwa kuifanya Zanzibar nchi. Je, nini maoni yako?
Jibu: Wazanzibari wanajua haki zao ndiyo sababu wamejivua hilo kongo la Muungano na ninaamini hata Watanganyika ambao walikuwa usingizini, sasa wataamka na kudai Tanganyika yao.
Swali: Kwa  hali ilivyo sasa bado ni vigumu kutabiri kama mfumo wa Serikali tatu utapita. Je, ukiendelea kukwama unadhani kuna njia nyingine za kudai?
Jibu: Binafsi nimeshasema tukishindwa kupata sasa Serikali ya Tanganyika mimi nitakwenda mahakamani tena Mahakama za kimataifa. Najua huku ndiko Watanganyika watapata haki na tayari nina mawakili wanasubiri tukwame.
Swali: Baada ya Rais Kikwete kukuteua kuwa Mjumbe wa Bunge la Katiba, ulitishia kutohudhuria Bunge hili imekuwaje sasa unashiriki?
Jibu: Washauri wangu ambao ni wanasheria ndiyo wamenitaka kushiriki ili tukishindwa kuipata Tanganyika katika Bunge hili ndiyo tuendelee na kesi.
Swali: Nini maoni yako ya jumla kuhusiana na mchakato wa Katiba ambao unaendelea sasa katika Bunge hili?
Jibu: Nina imani watu waliokuwa hawajui matatizo na kero za Muungano wamejua na sasa Tanganyika itapata uhuru wake tena.

                     Chanzo: Mwananchi

Comments