Kitabu Kinachotegemeka—Sehemu ya 1
Biblia iliandikwa katika kipindi cha 
miaka 1,600 hivi. Historia na unabii unaopatikana ndani yake unahusiana 
na serikali saba kuu za ulimwengu: Misri, Ashuru, Babiloni, Umedi na 
Uajemi, Ugiriki, Roma, na Muungano wa Uingereza na Marekani. Serikali 
hizo saba zitazungumziwa katika mfululizo wa makala saba. Kusudi la 
makala hizo ni nini? Kuonyesha kwamba Biblia inategemeka na imeongozwa 
na roho ya Mungu na kwamba ujumbe wake unatoa tumaini—tumaini la kwamba 
matatizo yanayosababishwa na utawala mbaya wa wanadamu yatakwisha.
MISRI, inayojulikana sana kwa piramidi zake na Mto
 Nile, ilikuwa serikali kuu ya kwanza katika historia ya Biblia. Taifa 
la Israeli lilitokezwa chini ya ulinzi wake. Musa aliyeandika vitabu 
vitano vya kwanza vya Biblia, alizaliwa na kuelimishwa huko Misri. Je, 
historia na vitu vya kale vilivyochimbuliwa vinapatana na mambo ambayo 
Musa aliandika kuhusu nchi hiyo ya kale? Chunguza mifano michache.
Historia Inayotegemeka
Majina ya cheo.
Mara nyingi historia sahihi huonekana kupitia 
habari zinazotajwa—utamaduni, njia ya kufanya mambo, majina ya maofisa 
na majina yao ya cheo, na kadhalika. Je, habari inayopatikana katika 
vile vitabu viwili vya kwanza vya Biblia, Mwanzo na Kutoka, ni sahihi? 
J. Garrow Duncan anatoa maelezo haya katika kitabu chake New Light on Hebrew Origins kuhusu
 simulizi la Yosefu mwana wa mzee wa ukoo Yakobo, linalopatikana katika 
kitabu cha Mwanzo, na pia kuhusu kitabu cha Biblia cha Kutoka: 
“[Mwandikaji huyo wa Biblia] alifahamu vizuri lugha, utamaduni, imani, 
maisha katika makao ya mfalme, njia ya kufanya mambo, na jinsi maofisa 
walivyofanya kazi huko Misri.” Anaongezea hivi: “[Mwandikaji] anatumia 
majina sahihi ya cheo kama yalivyotumiwa katika kipindi anachozungumzia.
 . . . Kwa kweli, hakuna kitu kingine kinachothibitisha kwamba 
waandikaji wa Agano la Kale wana ujuzi wenye kina wa mambo ya Misri na 
wanategemeka, kuliko utumizi wa neno Farao katika vipindi mbalimbali.” 
Duncan anaendelea kusema: “Wakati [mwandikaji] anapowaonyesha wahusika 
wake wakiwa mbele ya Farao, anawaonyesha wakifanya mambo kwa njia 
inayofaa na wakizungumza kwa njia inayostahili.”
Kutengeneza matofali.
Wakati wa utumwa wao huko Misri, Waisraeli walitengeneza matofali yaliyochanganywa na nyasi, iliyotumiwa kama kiunganishi. (Kutoka 1:14; 5:6-18) * Miaka fulani iliyopita, kitabu Ancient Egyptian Materials and Industries kilisema
 hivi: “Ni katika maeneo machache tu ambapo [utengenezaji wa matofali] 
umefanywa kuliko unavyofanywa huko Misri, ambako tangu zamani matofali 
yaliyokaushwa kwenye jua ndiyo  yanayotumiwa
 zaidi katika ujenzi nchini kote.” Kitabu hicho pia kinataja “zoea la 
Wamisri la kutumia nyasi kutengeneza matofali,” na hivyo kuthibitisha 
jambo hilo la ziada linalotajwa katika Biblia.
Kunyoa ndevu.
Wanaume Waebrania wa nyakati za kale walikuwa na 
ndevu. Hata hivyo, Biblia inatuambia kwamba Yosefu alinyoa ndevu kabla 
ya kusimama mbele ya Farao. (Mwanzo 41:14)
 Kwa nini alizinyoa? Ili atende kulingana na utamaduni wa Misri kwani 
walimwona mtu aliye na nywele usoni kuwa mchafu. “[Wamisri] walijisifu 
kwa kunyoa ndevu zote,” kinasema kitabu Everyday Life in Ancient Egypt. Kwa
 kweli, vikasha vya kujipodoa vimepatikana katika makaburi vikiwa na 
nyembe, vibano, na vioo. Kwa wazi, Musa aliandika mambo kwa usahihi 
kabisa. Jambo hilohilo linaweza kusemwa kuwahusu waandikaji wengine wa 
Biblia walioandika matukio kuhusu Misri ya kale.
Biashara.
Yeremia, aliyeandika vitabu viwili vya Wafalme, 
alitoa habari hususa kuhusu biashara ya farasi na ya magari kati ya 
Mfalme Sulemani na Wamisri na Wahiti. Gari liligharimu “vipande 600 vya 
fedha, na farasi . . . vipande 150,” au robo ya gharama ya gari, inasema
 Biblia.—1 Wafalme 10:29.
Kulingana na kitabu Archaeology and the Religion of Israel, uthibitisho
 uliotolewa na mwanahistoria Mgiriki Herodoto na uliopatikana katika 
vitu vilivyochimbuliwa unathibitisha kwamba biashara kubwa ya farasi na 
magari iliendelezwa wakati wa utawala wa Sulemani. Kwa kweli, “ilikuwa 
kawaida kubadilisha farasi wanne . . . kwa gari moja la Misri,” kitabu 
hicho kinasema, na hilo linathibitisha tarakimu zinazoonyeshwa katika 
Biblia.
Vita.
Yeremia na Ezra wanataja pia kuhusu Farao 
Shishaki aliyeivamia Yuda, wakitaja kihususa kwamba uvamizi huo ulitukia
 “katika mwaka wa tano wa Mfalme Rehoboamu [wa Yuda],” au 993 K.W.K. (1 Wafalme 14:25-28; 2 Mambo ya Nyakati 12:1-12)
 Kwa muda mrefu sana, habari pekee iliyopatikana kuhusu uvamizi huo 
ilikuwa ile ya Biblia. Kisha mchoro ukapatikana katika ukuta wa hekalu 
la Karnak (Thebesi ya kale) huko Misri.
Mchoro huo unamwonyesha Shishaki akiwa amesimama
 mbele ya mungu Amoni, mkono wa Shishaki ukiwa umeinuliwa akiwachinja 
mateka. Pia majina ya miji ya Israeli iliyoshindwa imeandikwa katika 
mchoro huo, na mengi ya miji hiyo inahusianishwa na maeneo yanayotajwa 
katika  Biblia. Zaidi ya hilo, 
maandishi hayo yanataja “Shamba la Abramu”—na hayo ndiyo maandishi ya 
kale zaidi ya Misri kumtaja mzee wa ukoo Abrahamu anayetajwa katika 
Biblia.—Mwanzo 25:7-10.
Ni wazi kwamba waandikaji wa Biblia hawakuandika
 mambo ya kuwaziwa. Wakitambua kwamba wanawajibika mbele za Mungu wao 
waliandika ukweli, hata wakati ambapo kufanya hivyo hakukupendeza—kama 
ilivyokuwa na ushindi wa Shishaki dhidi ya Yuda. Unyoofu huo 
unatofautiana sana na maandishi ya waandishi wa kale Wamisri ambao 
walikataa kuandika chochote ambacho kingewashushia heshima watawala au 
watu wa Misri.
Unabii Unaotegemeka
Ni Yehova Mungu peke yake, Mtungaji wa Biblia, 
anayeweza kutabiri wakati ujao kwa usahihi. Kwa mfano, ona kile ambacho 
alimwongoza Yeremia kutabiri kuhusu majiji mawili ya Misri—Memfisi na 
Thebesi. Wakati mmoja Memfisi, au Nofu lilikuwa kituo maarufu cha 
kibiashara, kisiasa, na kidini. Lakini Mungu alisema hivi: “Nofu 
litakuwa kitu cha kushangaza na kwa kweli litawashwa moto, hivi kwamba 
lisiwe na mkaaji.” (Yeremia 46:19) Na hivyo ndivyo mambo yalivyokuwa. Kitabu In the Steps of Moses the Lawgiver kinasema
 kwamba “magofu makubwa sana ya Memfisi” yaliporwa na washindi Waarabu, 
ambao walitumia mawe ya jiji hilo kwa ajili ya ujenzi. Kitabu hicho 
kinaongezea kwamba leo “hakuna jiwe linaloonekana juu ya udongo mweusi 
wa jiji hilo la kale na eneo linalozunguka.”
Thebesi, ambalo zamani lilijulikana kama 
No-amoni au No, lilipatwa na msiba kama huo, pamoja na miungu yake 
isiyojiweza. Yehova alisema hivi kuhusu mji huo ambao wakati mmoja 
ulikuwa mji mkuu wa Misri na kituo cha ibada ya mungu Amoni: “Tazama, 
ninakaza fikira zangu juu ya Amoni . . . na juu ya Farao na juu ya Misri
 na juu ya miungu yake . . . Nami nitawatia . . . mkononi mwa 
Nebukadreza mfalme wa Babiloni.” (Yeremia 46:25, 26)
 Kama ilivyotabiriwa, mtawala wa Babiloni alishinda Misri na jiji hilo 
maarufu lililoitwa No-amoni. Kisha, baada ya mtawala wa Uajemi 
Cambyses wa Pili kulishinda jiji hilo kwa mara nyingine katika mwaka wa 
525 K.W.K., lilipoteza umaarufu wake upesi na mwishowe likaharibiwa 
kabisa na Waroma. Naam, unabii sahihi unafanya Biblia iwe kitabu 
kisichoweza kulinganishwa na kitabu kingine, na hivyo kufanya tuwe na 
uhakika kuhusu mambo inayosema juu ya wakati wetu ujao.
Tumaini Lenye Kutegemeka
Unabii wa kwanza katika Biblia uliandikwa na Musa wakati wa utawala wa serikali kuu ya  ulimwengu ya Misri. * Unabii huo unaopatikana katika Mwanzo 3:15,
 unasema kwamba Mungu angetokeza “uzao,” ambao ungemponda Shetani na 
“uzao” wake, yaani, wale wanaotenda kulingana na njia za Shetani zenye 
uovu. (Yohana 8:44; 1 Yohana 3:8) Sehemu ya msingi ya “uzao” wa Mungu ilikuja kuwa Masihi, Yesu Kristo.—Luka 2:9-14.
Kristo ataitawala dunia yote naye ataondoa uovu 
na ukandamizaji wote unaoletwa na serikali za wanadamu. Mwanadamu 
hataendelea ‘kumtawala mwanadamu kwa kumuumiza.’ (Mhubiri 8:9)
 Zaidi ya hilo, kama Yoshua wa kale ambaye aliwaongoza Waisraeli kwenye 
Nchi ya Ahadi, Yesu ataongoza “umati mkubwa” wa wanadamu wanaomwogopa 
Mungu waingie katika ‘Nchi kubwa zaidi ya Ahadi’—dunia iliyosafishwa na 
kufanywa kuwa paradiso.—Ufunuo 7:9, 10, 14, 17; Luka 23:43.
Tumaini hilo lenye thamani linatukumbusha unabii mwingine ulioandikwa katika nyakati za Misri ya kale. Katika Ayubu 33:24, 25,
 unabii huo unasema kwamba Mungu atawakomboa wanadamu kutoka “shimoni,” 
au kaburini, kupitia ufufuo. Naam, mbali na wale watakaookoka uharibifu 
unaokuja wa waovu, mamilioni ya wengine waliokufa watafufuliwa wawe hai 
wakiwa na taraja la kuishi milele katika Paradiso duniani. (Matendo 24:15) “Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu,” inasema Ufunuo 21:3, 4. “Atafuta
 kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala 
maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.”
Historia na unabii wenye kutegemeka—mambo hayo 
yataendelea kuzungumziwa katika makala ifuatayo ya mfululizo huu, ambayo
 itakazia fikira Ashuru ya kale, serikali kuu ya ulimwengu iliyofuata 
baada ya Misri.
Comments