Misri na Historia ya Biblia



Njia Ambayo Waisraeli Walipitia



Kitabu Kinachotegemeka—Sehemu ya 1

Biblia iliandikwa katika kipindi cha miaka 1,600 hivi. Historia na unabii unaopatikana ndani yake unahusiana na serikali saba kuu za ulimwengu: Misri, Ashuru, Babiloni, Umedi na Uajemi, Ugiriki, Roma, na Muungano wa Uingereza na Marekani. Serikali hizo saba zitazungumziwa katika mfululizo wa makala saba. Kusudi la makala hizo ni nini? Kuonyesha kwamba Biblia inategemeka na imeongozwa na roho ya Mungu na kwamba ujumbe wake unatoa tumaini—tumaini la kwamba matatizo yanayosababishwa na utawala mbaya wa wanadamu yatakwisha.
MISRI, inayojulikana sana kwa piramidi zake na Mto Nile, ilikuwa serikali kuu ya kwanza katika historia ya Biblia. Taifa la Israeli lilitokezwa chini ya ulinzi wake. Musa aliyeandika vitabu vitano vya kwanza vya Biblia, alizaliwa na kuelimishwa huko Misri. Je, historia na vitu vya kale vilivyochimbuliwa vinapatana na mambo ambayo Musa aliandika kuhusu nchi hiyo ya kale? Chunguza mifano michache.

Historia Inayotegemeka

Majina ya cheo.

Mara nyingi historia sahihi huonekana kupitia habari zinazotajwa—utamaduni, njia ya kufanya mambo, majina ya maofisa na majina yao ya cheo, na kadhalika. Je, habari inayopatikana katika vile vitabu viwili vya kwanza vya Biblia, Mwanzo na Kutoka, ni sahihi? J. Garrow Duncan anatoa maelezo haya katika kitabu chake New Light on Hebrew Origins kuhusu simulizi la Yosefu mwana wa mzee wa ukoo Yakobo, linalopatikana katika kitabu cha Mwanzo, na pia kuhusu kitabu cha Biblia cha Kutoka: “[Mwandikaji huyo wa Biblia] alifahamu vizuri lugha, utamaduni, imani, maisha katika makao ya mfalme, njia ya kufanya mambo, na jinsi maofisa walivyofanya kazi huko Misri.” Anaongezea hivi: “[Mwandikaji] anatumia majina sahihi ya cheo kama yalivyotumiwa katika kipindi anachozungumzia. . . . Kwa kweli, hakuna kitu kingine kinachothibitisha kwamba waandikaji wa Agano la Kale wana ujuzi wenye kina wa mambo ya Misri na wanategemeka, kuliko utumizi wa neno Farao katika vipindi mbalimbali.” Duncan anaendelea kusema: “Wakati [mwandikaji] anapowaonyesha wahusika wake wakiwa mbele ya Farao, anawaonyesha wakifanya mambo kwa njia inayofaa na wakizungumza kwa njia inayostahili.”


Matofali yaliyotengenezwa kwa nyasi na kukaushwa juani


Bado matofali yaliyotengenezwa kwa nyasi na kukaushwa juani yanatumiwa Misri leo

Kutengeneza matofali.

Wakati wa utumwa wao huko Misri, Waisraeli walitengeneza matofali yaliyochanganywa na nyasi, iliyotumiwa kama kiunganishi. (Kutoka 1:14; 5:6-18) * Miaka fulani iliyopita, kitabu Ancient Egyptian Materials and Industries kilisema hivi: “Ni katika maeneo machache tu ambapo [utengenezaji wa matofali] umefanywa kuliko unavyofanywa huko Misri, ambako tangu zamani matofali yaliyokaushwa kwenye jua ndiyo  yanayotumiwa zaidi katika ujenzi nchini kote.” Kitabu hicho pia kinataja “zoea la Wamisri la kutumia nyasi kutengeneza matofali,” na hivyo kuthibitisha jambo hilo la ziada linalotajwa katika Biblia.


Baadhi ya vifaa vya kunyoa vya Misri


Baadhi ya vifaa vya kunyoa vya Misri—wembe na kioo

Kunyoa ndevu.

Wanaume Waebrania wa nyakati za kale walikuwa na ndevu. Hata hivyo, Biblia inatuambia kwamba Yosefu alinyoa ndevu kabla ya kusimama mbele ya Farao. (Mwanzo 41:14) Kwa nini alizinyoa? Ili atende kulingana na utamaduni wa Misri kwani walimwona mtu aliye na nywele usoni kuwa mchafu. “[Wamisri] walijisifu kwa kunyoa ndevu zote,” kinasema kitabu Everyday Life in Ancient Egypt. Kwa kweli, vikasha vya kujipodoa vimepatikana katika makaburi vikiwa na nyembe, vibano, na vioo. Kwa wazi, Musa aliandika mambo kwa usahihi kabisa. Jambo hilohilo linaweza kusemwa kuwahusu waandikaji wengine wa Biblia walioandika matukio kuhusu Misri ya kale.

Biashara.

Yeremia, aliyeandika vitabu viwili vya Wafalme, alitoa habari hususa kuhusu biashara ya farasi na ya magari kati ya Mfalme Sulemani na Wamisri na Wahiti. Gari liligharimu “vipande 600 vya fedha, na farasi . . . vipande 150,” au robo ya gharama ya gari, inasema Biblia.—1 Wafalme 10:29.
Kulingana na kitabu Archaeology and the Religion of Israel, uthibitisho uliotolewa na mwanahistoria Mgiriki Herodoto na uliopatikana katika vitu vilivyochimbuliwa unathibitisha kwamba biashara kubwa ya farasi na magari iliendelezwa wakati wa utawala wa Sulemani. Kwa kweli, “ilikuwa kawaida kubadilisha farasi wanne . . . kwa gari moja la Misri,” kitabu hicho kinasema, na hilo linathibitisha tarakimu zinazoonyeshwa katika Biblia.

Vita.

Yeremia na Ezra wanataja pia kuhusu Farao Shishaki aliyeivamia Yuda, wakitaja kihususa kwamba uvamizi huo ulitukia “katika mwaka wa tano wa Mfalme Rehoboamu [wa Yuda],” au 993 K.W.K. (1 Wafalme 14:25-28; 2 Mambo ya Nyakati 12:1-12) Kwa muda mrefu sana, habari pekee iliyopatikana kuhusu uvamizi huo ilikuwa ile ya Biblia. Kisha mchoro ukapatikana katika ukuta wa hekalu la Karnak (Thebesi ya kale) huko Misri.
Mchoro huo unamwonyesha Shishaki akiwa amesimama mbele ya mungu Amoni, mkono wa Shishaki ukiwa umeinuliwa akiwachinja mateka. Pia majina ya miji ya Israeli iliyoshindwa imeandikwa katika mchoro huo, na mengi ya miji hiyo inahusianishwa na maeneo yanayotajwa katika  Biblia. Zaidi ya hilo, maandishi hayo yanataja “Shamba la Abramu”—na hayo ndiyo maandishi ya kale zaidi ya Misri kumtaja mzee wa ukoo Abrahamu anayetajwa katika Biblia.—Mwanzo 25:7-10.
Ni wazi kwamba waandikaji wa Biblia hawakuandika mambo ya kuwaziwa. Wakitambua kwamba wanawajibika mbele za Mungu wao waliandika ukweli, hata wakati ambapo kufanya hivyo hakukupendeza—kama ilivyokuwa na ushindi wa Shishaki dhidi ya Yuda. Unyoofu huo unatofautiana sana na maandishi ya waandishi wa kale Wamisri ambao walikataa kuandika chochote ambacho kingewashushia heshima watawala au watu wa Misri.

Unabii Unaotegemeka

Ni Yehova Mungu peke yake, Mtungaji wa Biblia, anayeweza kutabiri wakati ujao kwa usahihi. Kwa mfano, ona kile ambacho alimwongoza Yeremia kutabiri kuhusu majiji mawili ya Misri—Memfisi na Thebesi. Wakati mmoja Memfisi, au Nofu lilikuwa kituo maarufu cha kibiashara, kisiasa, na kidini. Lakini Mungu alisema hivi: “Nofu litakuwa kitu cha kushangaza na kwa kweli litawashwa moto, hivi kwamba lisiwe na mkaaji.” (Yeremia 46:19) Na hivyo ndivyo mambo yalivyokuwa. Kitabu In the Steps of Moses the Lawgiver kinasema kwamba “magofu makubwa sana ya Memfisi” yaliporwa na washindi Waarabu, ambao walitumia mawe ya jiji hilo kwa ajili ya ujenzi. Kitabu hicho kinaongezea kwamba leo “hakuna jiwe linaloonekana juu ya udongo mweusi wa jiji hilo la kale na eneo linalozunguka.”


A statue from ancient Egypt


Sanamu hii kubwa iliyopatikana karibu na Memfisi ikiwa imeanguka ilikuwa na kimo cha mita 12 hivi
Thebesi, ambalo zamani lilijulikana kama No-amoni au No, lilipatwa na msiba kama huo, pamoja na miungu yake isiyojiweza. Yehova alisema hivi kuhusu mji huo ambao wakati mmoja ulikuwa mji mkuu wa Misri na kituo cha ibada ya mungu Amoni: “Tazama, ninakaza fikira zangu juu ya Amoni . . . na juu ya Farao na juu ya Misri na juu ya miungu yake . . . Nami nitawatia . . . mkononi mwa Nebukadreza mfalme wa Babiloni.” (Yeremia 46:25, 26) Kama ilivyotabiriwa, mtawala wa Babiloni alishinda Misri na jiji hilo maarufu lililoitwa No-amoni. Kisha, baada ya mtawala wa Uajemi Cambyses wa Pili kulishinda jiji hilo kwa mara nyingine katika mwaka wa 525 K.W.K., lilipoteza umaarufu wake upesi na mwishowe likaharibiwa kabisa na Waroma. Naam, unabii sahihi unafanya Biblia iwe kitabu kisichoweza kulinganishwa na kitabu kingine, na hivyo kufanya tuwe na uhakika kuhusu mambo inayosema juu ya wakati wetu ujao.

Tumaini Lenye Kutegemeka

Unabii wa kwanza katika Biblia uliandikwa na Musa wakati wa utawala wa serikali kuu ya  ulimwengu ya Misri. * Unabii huo unaopatikana katika Mwanzo 3:15, unasema kwamba Mungu angetokeza “uzao,” ambao ungemponda Shetani na “uzao” wake, yaani, wale wanaotenda kulingana na njia za Shetani zenye uovu. (Yohana 8:44; 1 Yohana 3:8) Sehemu ya msingi ya “uzao” wa Mungu ilikuja kuwa Masihi, Yesu Kristo.—Luka 2:9-14.
Kristo ataitawala dunia yote naye ataondoa uovu na ukandamizaji wote unaoletwa na serikali za wanadamu. Mwanadamu hataendelea ‘kumtawala mwanadamu kwa kumuumiza.’ (Mhubiri 8:9) Zaidi ya hilo, kama Yoshua wa kale ambaye aliwaongoza Waisraeli kwenye Nchi ya Ahadi, Yesu ataongoza “umati mkubwa” wa wanadamu wanaomwogopa Mungu waingie katika ‘Nchi kubwa zaidi ya Ahadi’—dunia iliyosafishwa na kufanywa kuwa paradiso.—Ufunuo 7:9, 10, 14, 17; Luka 23:43.
Tumaini hilo lenye thamani linatukumbusha unabii mwingine ulioandikwa katika nyakati za Misri ya kale. Katika Ayubu 33:24, 25, unabii huo unasema kwamba Mungu atawakomboa wanadamu kutoka “shimoni,” au kaburini, kupitia ufufuo. Naam, mbali na wale watakaookoka uharibifu unaokuja wa waovu, mamilioni ya wengine waliokufa watafufuliwa wawe hai wakiwa na taraja la kuishi milele katika Paradiso duniani. (Matendo 24:15) “Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu,” inasema Ufunuo 21:3, 4. “Atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.”
Historia na unabii wenye kutegemeka—mambo hayo yataendelea kuzungumziwa katika makala ifuatayo ya mfululizo huu, ambayo itakazia fikira Ashuru ya kale, serikali kuu ya ulimwengu iliyofuata baada ya Misri.
 
 
                         Na  Injili Forever

Comments