MTOTO ALIYEPIGWA RISASI YA KICHWA KWENYE SHAMBULIO LA KANISANI AFIKISHWA NAIROBI KWA MATIBABU


Kaka wa Satrin Osinya, Moses Gift akiwa amembeba mdogo wake baada ya kunusurika kifo.

MTOTO Satrin Osinya aliyejeruhiwa na risasi iliyomuua mama yake katika shambulio la kigaidi lililofanywa kwenye kanisa la Joy of Jesus huko Likoni, Mombasa nchini Kenya Jumapili iliyopita, jana amefikishwa jijini Nairobi kwa matibabu.

Mtoto Satrin Osinya wakati akipatiwa matibabu mjini Mombasa baada ya kupigwa risasi.

Osinya mwenye umri wa mwaka mmoja na nusu anatarajiwa kufanyiwa upasuaji wa kichwa katika Hospitali Kuu ya Kitaifa ya Kenyatta ili kuondoa risasi iliyoingia kwenye ubongo wake baada ya kumuua mama yake.

Madaktari wanasema kuwa ubongo wa mtoto huyo umefura na kwamba risasi iko upande wa kulia wa ubongo wenyewe. Upasuaji unatarajiwa kufanywa baada ya wiki mbili ambao utagharamiwa na serikali.


Mtoto Satrin akiwa amebebwa na baba yake mzazi Benson Osinya ndani ya ndege kuelekea jijini Nairobi kwa matibabu.
Mama mzazi wa Satrin aliyekuwa akijaribu kumkinga mwanaye kutoka kwa magaidi waliovamia kanisa la Joy of Jesus siku ya Jumapili, alifariki kanisani humo baada ya kupigwa risasi. Inadaiwa risasi aliyomuingia kichwani Satrin ni risasi iliyomuua mama yake kupitia kifuani na kuishia katika ubongo wa mtoto huyo.
Mamake Satrin, alikuwa miongoni mwa watu sita waliouawa katika shambulizi hilo, baada ya washukiwa watatu wa ugaidi kulivamia kanisa hilo katika mtaa wa Likoni na kuanza kuwafyatulia waumini risasi kiholela.
Siku ya tukio ilikuwa kama ifuatavyo Fungua hapa

Comments