TAHADHARI KUTOKA JESHI LA POLISI KATIKA KUSHEREHEKEA PASAKA


Tunapoelekea kipindi hiki cha sikukuu ya Pasaka, Jeshi la Polisi nchini, linatoa tahadhari kwa
wananchi kuwa makini katika suala la usalama wa maisha na mali zao.

Uzoefu unaonyesha kwamba, katika kipindi kama hiki cha sikukuu kuna baadhi ya watu hupenda kutumia fursa hiyo kufanya vitendo vya uhalifu. Hata hivyo, Jeshi la Polisi katika mikoa yote limejipanga vizuri kwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama kuhakikisha kwamba hakuna vitendo vyovyote vya uhalifu vitakavyojitokeza na endapo vitajitokeza viweze kudhibitiwa kwa haraka.

Aidha, ulinzi umeimarishwa kwenye maeneo yote, yakiwemo maeneo ya kuabudia, fukwe za bahari, sehemu za starehe na maeneo mengine ambayo yatakuwa na mikusanyiko mikubwa ya watu.

Vilevile, Jeshi la Polisi linawataka madereva na watu wote watakaokuwa wakitumia barabara, kuwa makini na kuzingatia sheria za usalama barabarani, kuepuka kwenda mwendo kasi, kujaza abiria kupita kiasi na

kutumia vilevi wawapo kazini.

Wamiliki wa kumbi za starehe wazingatie uhalali na matumizi ya kumbi zao katika uingizaji wa watu kulingana na
uwezo wa kumbi hizo, badala ya kuendekeza tamaa ya fedha kwa kujaza watu kupita kiasi.

Aidha, wazazi wawe makini na watoto wao, kutokuwaacha watembee peke yao ama kwenda disko toto bila kuwa chini ya uangalizi wa watu wazima ili kuepusha ajali na matukio mengine yanayoweza kusababisha madhara juu yao.

Wananchi wakumbuke kutokuacha makazi yao bila uangalizi na endapo italazimu kufanya hivyo watoe taarifa kwa majirani zao, na pale wanapowatilia mashaka watu wasiowafahamu wasikae kimya, watoe taarifa haraka kwenye vituo vya polisi vilivyo karibu yao, ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa haraka.

Mwisho, Jeshi la Polisi linapenda kuwashukuru wale wote ambao tayari wamefunga kamera za CCTV katika maeneo yao ya biashara hususani yale yanayokuwa na mikusanyiko mikubwa ya watu, yakiwemo maduka, mahoteli na maeneo ya benki.

Jeshi la Polisi linaendelea kuwasisitiza ambao bado hawajaweka kamera hizo, kuweka ili ziweze kusaidia kubaini wahalifu na hata kurahisisha ukamataji wa wahalifu hao endapo uhalifu unatokea.

Tunawatakia Watanzania wote Pasaka njema.


Imetolewa na:-
Advera Senso-SSP

Msemaji wa Jeshi la Polisi.

Comments