ASKOFU KAKOBE NA MAFUNDISHO SITA MUHIMU

  (MATHAYO 14:15-36)

Katika mistari hii iliyosalia katika kitabu cha MATHAYO SURA YA 14, tunapata mafundisho sita muhimu, tutayaangalia kwa makini:-
(1)   WAJIBU WETU KATIKA UVUVI WA WATU (MST. 15-21);
(2)   MAOMBI YA YESU YA FARAGHANI (MST. 22-23);
(3)   MADHARA YA WOGA (MST. 24-32);
(4) KUSUJUDIWA KWA YESU (MST. 33);
(5)   MASHAHIDI WALIOMSHUHUDIA YESU KUWA NI MWANA WA MUNGU (MST. 33);
(6)   SIRI YA KUPONYWA MAGONJWA YETU (MST. 34-36).
(1)      WAJIBU WETU KATIKA UVUVI WA WATU   (MST. 15-21)
             Katika mistari hii tunajifunza wajibu wa Kanisa katika uvuvi wa watu.  Ikiwa tunataka matokeo makubwa ya uvuvi wa watu, inatupasa kuchukua mzigo wote wa wale tunaotaka kuwaleta kwa Yesu.  Wanafunzi wa Yesu hapa, walikwepa mzigo na kutaka mataifa waliokuwa wanasikia Injili ya Yesu, watoe fedha zao kujinunulia chakula.  Jibu la Yesu kwa wanafunzi wa Yesu au kwa Kanisa lilikuwa, “WAPENI NINYI KULA“ (Mst. 15-16).
Gharama yote ya maandalizi ya mikutano ya Injili, semina au konferensi za mafundisho ambapo tunawaalika mataifa, ni lazima tuzibebe peke yetu bila kuwahusisha wao; ikiwa tunataka matokeo makubwa ya mikutano yetu.  Ikiwa tutategemea wao wajigharimie, tutawakosa wengi.  Ikiwa tutapanga kurudisha gharama zetu za maandalizi ya mikutano kwa kuwaambia mataifa wachangie gharama hizo, basi tujue kwamba kwa kufanya hivyo tutapunguza mavuno yetu.  Kanisa la Mungu kwa ujumla, linakwepa wajibu huu kama walivyokwepa wanafunzi wa Yesu.  Hatupaswi kuwa hivyo.  Hatuwezi kuliona Kanisa likikua na kuongezeka ikiwa tutakwepa gharama.  Hatupaswi kupokea sadaka yoyote katika mikutano ya namna hii ili tuwapate mataifa.  Ikiwa ni ibada za kawaida za Kanisa hapo ni suala jingine (3 YOHANA 1: 5-7; 2 WAKORINTHO 12:14-16; 1 WAKORINTHO 9:18-19; MATENDO 20:33-35; MATHAYO 10:7-8; MITHALI 23:23; KUMBUKUMBU LA TORATI 23:18).
(2)      MAOMBI YA YESU YA FARAGHANI   (MST. 22-23)
Siri ya upako mkubwa katika huduma ya Yesu na siri ya kuishinda dhambi kabisa na kuushinda ulimwengu, ilikuwa maombi ya faraghani akiwa PEKE YAKE (LUKA 9:18; YOHANA 6:15; MARKO 1:35).  Wengi wetu tunakuwa dhaifu, kwa sababu hatuombi kwa bidii mpaka pale tunapokuwa katika kusanyiko pamoja na wengine.  Maombi katika kusanyiko yana umuhimu wake, hata hivyo, tukiyajumlisha na maombi ya “pekee faraghani”, tutapata matokeo makubwa zaidi.  Hatuna budi kuwalazimisha wengine kuondoka na kutuacha peke yetu na Mungu.
(3)      MADHARA YA WOGA   (MST. 24-32)
             Woga ni dhambi, na waoga hawataurithi ufalme wa Mungu (UFUNUO 21:8).  Kwa sababu woga ni dhambi, woga hutuzuia kupokea miujiza yetu na pia hutuzuia kuitunza miujiza tuliyoipokea.  Ikiwa tunataka kumwona Mungu akitenda kazi, ni lazima tuwe mbali na woga.  Kuruhusu kutawaliwa na woga, ni kumfanya Mungu kuwa na uwezo mdogo kuliko yale yanayotuogopesha.  Ni kumdharau.  Ni kukosa imani.  Hatupaswi kuyaogopa makumi elfu ya watu, waliojipanga juu yetu pande zote (ZABURI 3:6).  Walio upande wetu, ni wengi kuliko walio upande wao               (2 WAFALME 6:15-17).
v  Tusiogope, Bwana atatulisha na watoto wetu             -           MWANZO 50:21;
v  Tusiogope maneno tuliyoyasikia                                  -           ISAYA 37:6;
v  Tusiogope matukano ya watu na dhihaka zao            -           ISAYA 51:7;
v  Tusimwogope Shetani (Mfalme wa Babeli)                 -           YEREMIA 42:11;
v  Tusiogope, bali tufurahi na kushangilia                       -           YOELI 2:21;
v  Tusiwaogope wauuao mwili                                          -           MATHAYO 10:28;
v  Tusiogope kuhubiri habari za Wokovu                        -           MATENDO 18:9;
v  Tusiogope mambo yatakayotupata                              -           UFUNUO 2:10.
Tunapomlilia Mungu wakati wote anasema “TUSIOGOPE” (MAOMBOLEZO 3:55, 57) MAANA TUMEKOMBOLEWA (ISAYA 43:1).  Bwana ni ngome ya uzima wetu tumwogope nani?  (ZABURI 27:1).
(4)      KUSUJUDIWA KWA YESU  (MST. 33)
            Yesu mwenyewe alisema kwamba wa kusujudiwa na kuabudiwa ni Mungu peke yake (MATHAYO 4:10).  Malaika hawakubali kusujudiwa na wanaeleza kwamba wa kusujudiwa ni Mungu tu (UFUNUO 22:8-9).  Mitume hawakubali kuabudiwa (MATENDO 14:8-18).  Hata hivyo Yesu alikubali kusujudiwa na kuabudiwa mara nyingi (MATHAYO 14:33; 15:25; 18:26; 28:9; 2:2, 11; 8:2; 9:18; MARKO 5:6; LUKA 24:52; YOHANA 9:35-38).  Huu ni uthibitisho dhahiri kwamba Yesu ni zaidi ya mtume na malaika.  YESU NI MUNGU.
(5)      MASHAHIDI WALIOMSHUHUDIA YESU KUWA NI MWANA WA MUNGU  (MST. 33)
            Biblia inasema, kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu, kila neno lithibitike.  Mashahidi wafuatao walimshuhudia Yesu kwamba ni Mwana wa Mungu.
  1. Mungu Baba                    (MATHAYO 3:16-17; 17:5);
  2. Wanadamu                     (MATHAYO 14:33; 16:16; 27:54; YOHANA 1:49);
  3. Shetani                             (MATHAYO 8:29; MARKO 5:7-9);
  4. Malaika                             (LUKA 1:35);
  5. Yesu mwenyewe             (YOHANA 9:35-37).
(6)      SIRI YA KUPONYWA MAGONJWA YETU  (MST. 34-36)
            Siri ya kuponywa magonjwa yetu ni kumtambua Yesu ni nani.  “Watu wa mahali pale WALIPOMTAMBUA………….wakaponywa kabisa.”  Inatupasa kumtambua Yesu kuwa ni:-
  1. Mwenye huruma kwetu (MATHAYO 14:14; LUKA 7:13; ZABURI 103:13);
  2. Mwenye uwezo wa kuponya (LUKA 5:17; 4:18);
  3. Mwenye kupenda kuchukua mizigo yetu (MATHAYO 11:28);
  4. Mwenye kuja ili tuwe na uzima, kisha tuwe nao tele (YOHANA 10:10);
  5. Mwenye kudhihirishwa ili azivunje kazi za Ibilisi (1 YOHANA 3:8);
  6. Mwenye jina lipitalo majina yote na jina lake lina uwezo wa kututia nguvu ya uponyaji (WAFILIPI 2:9-11; MATENDO 3:16);
  7. Mkuu wa Uzima (MATENDO 3:15).
HERI MASIKIO YAKO KWA KUWA YANASIKIA (MATHAYO 13:16)
. . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . . Ni sifa ipi ya kutuwezesha kuingia mbinguni?  Ni utakatifu (WAEBRANIA 12:14).  Ndani yake hakitaingia kamwe chochote kilicho kinyonge (UFUNUO WA YOHANA 21:27).  Kinyonge ni kipi?  Ni yule anayetenda dhambi.  Huyu ni mtu asiyefaa, ni mnyonge!  Je, wewe ni mtakatifu?  Jibu ni la!  Maisha yako yamejaa dhambi, pamoja na kusema una dini; hivyo wewe pia ni mnyonge, hufai kuingia mbinguni. Ukitubu leo dhambi zako zote kwa kumaanisha kuziacha, na kuifuata njia ya Yesu Kristo, ndipo utakapopata rehema ya kuingia mbinguni (MITHALI 28:13;  YOHANA 14:6).  Je, uko tayari kutubu sasa ili upate rehema hii?  Najua uko tayari.  Basi fuatisha sala hii ya toba kwa dhati kutoka moyoni;  Mungu Baba asante kwa ujumbe huu.  Hakika mimi ni mnyonge, mwenye dhambi.  Sistahili kuingia mbinguni. Natubu dhambi zangu zote kwa kumaanisha kuziacha.  Kuanzia leo nataka niifuate njia ya Yesu Kristo.  Bwana Yesu niwezeshe.  Asante kwa kunisikia katika Jina la Yesu.  Amen.  Mpendwa msomaji umekubaliwa kuingia mbinguni.  Ili uzidi kudumu katika utakatifu mpaka siku ya kuiaga dunia hii, hakikisha unahudhuria mafundisho katika Kanisa linalohubiri wokovu.  MUNGU AKUBARIKI !!!. . . . .

   Neno la Uzima kutoka kwa  Askofu Zachary Kakobe     tembelea sehemu zifuatazo katika inernet  
Tovuti       : www.bishopzacharykakobe.org
Facebook : www.facebook.com/bishopkakobeministries
Youtube   : www.youtube.com/user/bishopkakobe

Comments