Mwanafunzi wa kidato cha tatu katika Shule ya Sekondari ya Mwenyeheri Anwarite iliyopo Makoka jijini Dar es Salaam, Naima Nassir akiiweka picha ya Sista Clencesia Kapuli aliyeuawa kwa risasi na majambazi katika eneo la Ubungo Riverside hivi karibuni ikiwa ni maandalizi ya misa ya kumuaga leo |
Sista wa Kanisa Katoliki, Clencensia Kapuli aliyeuawa na majambazi na kuporwa kiasi kikubwa cha fedha ambacho bado hakijafahamika, anatarajiwa kuagwa leo katika Parokia ya Mtakatifu Gaudence Makoka, Dar es Salaam.
Akizungumza jana, Mkuu wa Shule ya Sekondari
Mwenyeheri Anuwarite, Carlos Mgumba alisema ibada ya kuaga mwili wa
marehemu itaanza saa sita mchana shuleni hapo, kabla ya mwili
kusafirishwa kwenda Mbeya kwa maziko.
“Nashindwa kujizuia kila nikifikiria jinsi
walivyomuua kikatili, sista, alikuwa mpole na mnyenyekevu…Wametumia
nguvu kubwa kama shida yao ilikuwa ni fedha wangeweza hata kuchukua bila
kutumia silaha, wametuachia pigo kubwa kwa shule yetu, wamemwonea tu,”
alisema huku akitokwa na machozi. Mgumba alisema katika miaka miwili na
nusu aliyofanya naye kazi, Sista Kapuli alisaidia kwa kiasi kikubwa
maendeleo ya shule kutokana na utendaji kazi wake uliotawaliwa na
uaminifu.
“Nakumbuka siku hiyo tulikuwa pamoja asubuhi kwa
mipango ya malipo ya mishahara ambayo kwa kawaida tunalipa moja kwa moja
kwenye akaunti za walimu, saa sita hivi mchana aliniaga anakwenda benki
kuchukua fedha za (petty cash) matumizi madogo ya shule,” alisema.
Alisema akiwa anaendelea na kazi zake, ndipo
alipopigiwa simu na kujulishwa kuhusu tukio hilo la mauaji lililotokea
eneo la Riverside, Ubungo, Dar es Salaam hukuna dereva Mark Mwarabu
kukatwa kidole gumba kwa risasi.
Rais wa serikali ya wanafunzi wa sekondari hiyo,
James Sweya alisema marehemu alikuwa karibu naye kwa sababu, yeye
anasomea mchepuo wa biashara hivyo alikuwa akimsaidia kumpa mwongozo wa
mambo ya uhasibu.
Mwanafunzi mwingine, Evelyn Kiwenge alisema Sista
Kapuli alikuwa mwenye upendo wa aina yake msaada kwa maisha ya wanafunzi
wengi katika sekondari hiyo.
Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam,
Suleiman Kova alisema juzi kuwa tayari kimeundwa kikosi kazi ili
kufuatilia tukio hilo na akiahidi kwamba atahakikisha wote waliohusika
wanasakwa na kutiwa mbaroni.
Alisema majambazi hayo yaliua na kupora Sh20
milioni lakini hata hivyo, habari zilizopatikana baadaye zilidai kuwa
majambazi hayo yalipora Sh10 milioni.
Sista Kapuli aliuawa akiwa ameongozana na wenzake,
Sista Brigita Mbaga na dereva Mwarabu aliyekuwa akiendesha gari aina ya
Toyota Hilux walikuwa wakitoka Benki ya CRDB, Tawi la Mlimani City
kuchukua fedha.
Baada ya kufika Ubungo kwa lengo la kulipa deni la
chakula katika duka la Thomas Francis, ndipo walitokea majambazi wawili
wakiwa na pikipiki ambayo haikusomeka namba mmoja wao akiwa na bunduki
aina ya SMG na kumpiga risasi ya kidole gumba cha mkono wa kulia Mwarabu
kisha kumgeukia Sista Kapuli na kumuua kisha kuondoka na fedha
zilizokuwa kwenye pochi.
Credit:Mwananchi.
Kama hukusoma habari za kuuawa Sista Clencensia FUNGUA HAPACredit:Mwananchi.
BWANA alitoa na BWANA ametwaa, Jina la BWANA lihimidiwe milele.
Comments