RAIS PETER MUTHARIKA AFUNGA NDOA.


Peter Mutharika ni rais wa tatu kuoa baada ya kushika wadhifa wa urais nchini Malawi
Lilongwe. Malawi. Ilikuwa ni nderemo na vifijo katika mji wa Blantyre nchini Malawi baada ya Rais Peter Mutharika wa nchi hiyo kufunga ndoa na Gertrude Maseko.
Harusi hiyo ilifungwa katika Kanisa la Mtakatifu Michael jana mchana .
Muda mwingi Gertrude, alionekana akitabasamu huku akiwa amevaa gauni refu jeupe lililokuwa likiburuza chini.
Harusi hiyo ilishuhudiwa na viongozi mbalimbali wa Serikali ya Malawi, akiwamo Jaji Mkuu, Anastasia Msosa, Spika wa Bunge la Malawi, Richard Msowoya na kiongozi wa upinzani, Lazarus Chakwera.
Watoto wa kiume na wa kike wa rais wa zamani wa Malawi, Bingu wa Mutharika walishuhudia ndoa hiyo ikifungwa na kuhudhuria sherehe iliyofanyika katika mji huo.
Rais Mutharika alianza maisha mapya na mke wake baada ya kutamka: “Nimempokea Gertrude kuwa mke wangu kwa raha na shida.”
Wakati wakila kiapo cha ndoa kanisani, Rais Mutharika alitamka : “Gertrude Maseko ni mke wangu.” Naye Gertrude alitamka maneno hayo, hayo.
Padri Rapson Chikwenzule alitangaza kuwa wawili hao sasa ni mume na mke baada ya kufungisha ndoa hiyo saa 11:45 jana.
“Kuanzia sasa, natangaza Peter na Gertrude wamekuwa mume na mke kwa jina la Baba, Mwana na Roho Mtakatifu. Alichokiunganisha Mungu, mwanadamu hawezi kukitenganisha,” alisema Padri Chikwenzule.
Baada ya kauli ya padri iliyoibua vifijo na vigelegele, wawili hao walisaini hati ya ndoa baada ya Padri Roy Zingani kuibariki tena ndoa hiyo.
Mashahidi wa ndoa hiyo walikuwa ni Arthur Msamba na Rorbert Salama ambao walitia saini hati ya ndoa ya wawili hao.

Baada ya ndoa hiyo kanisani, sherehe za harusi, zitafanyika katika Kijiji cha Ndata, wilayani Thyolo ambako familia ya Rais Mutharika inaishi.
Mume wa Gertrude ambaye amekuwa mbunge tangu mwaka 2009, alifariki dunia mwaka jana na katika uchaguzi wa mwaka huu, alipoteza nafasi ya ubunge, baada Lucius Banda kushinda kiti hicho.
Peter Mutharika ni rais wa tatu kuoa baada ya kushika wadhifa wa urais nchini Malawi.
Rais wa zamani wa nchi hiyo, Bakili Muluzi alifunga ndoa akiwa madarakani baada ya kuachana na mke wake, Anne.
Vilevile rais mwingine wa zamani wa nchi hiyo Bingu wa Mutharika naye alioa kutokana na mke wake wa kwanza, Ethel kufariki dunia.
 
 





Comments