ONGEA NA MUNGU WAKO(2)


INAENDELEA

                  wewe uliniunda tumboni mwa mama yangu;
                       wewe ulinitoa mwangani, mtoto uchi,
        kwa kuwa sheria za umbile letu zinafuata daima amri zako.
                 Wewe uliandaa kwa baraka ya Roho Mtakatifu
                         uumbaji wangu na maisha yangu,
           si kadiri ya matakwa ya mtu wala ya tamaa ya mwili,
                     bali kadiri ya neema yako isiyosemeka.
Uliandaa uzazi wangu kwa matayarisho yanayopita sheria za umbile letu,
                   ulinitoa mwangani kwa kunifanya mwanao,
     uliniandika kati ya wafuasi wa Kanisa lako takatifu lisilo na doa.
  Umenilisha maziwa ya Kiroho, maziwa ya maneno yako ya Kimungu.
      Umenitegemeza kwa chakula kizito cha Mwili wa Yesu Kristo,
                  Mungu wetu, Mwanao pekee mtakatifu sana,
   umenilevya kwa kikombe cha Kimungu cha Damu yake itiayo uzima,
                aliyoimwaga kwa wokovu wa ulimwengu wote…
                      Sasa, Bwana, kwa njia ya kuhani wako
                       umeniita nitumikie wanafunzi wako.
         Sijui kwa mpango gani umefanya hivi; wewe tu unajua…
Unichunge, Bwana, na uchunge mwenyewe pamoja nami watu wengine,
              ili moyo wangu usiniinamishe kulia wala kushoto,
                 bali Roho wako mwema unielekeze njia nyofu
                   ili matendo yangu yafuate matakwa yako,
                        na yayafuate kweli mpaka mwisho.
MT. BONIFAS (675-754)
    Mungu wa milele, kimbilio la wanao wote,
     katika udhaifu wetu ndiwe nguvu yetu,
      katika giza letu ndiwe mwanga wetu,
katika uchungu wetu ndiwe faraja na amani yetu.
MT. SIRILI WA THESALONIKE (827-869)
 Utakase, ulinganishe taifa lako katika imani ya kweli na ungamo sahihi,
             na kuangaza mioyoni neno la mafundisho yako.
    Kwa kuwa ni zawadi yako kutuchagua tuihubiri Injili ya Kristo wako,
     kuchochea ndugu watende mema na kutimiza yanayokupendeza.
                 Wale ulionipa nakurudishia kama wako;
       uwaongoze sasa kwa mkono wako wa kuume wenye nguvu,
                  uwalinde kivulini mwa mabawa yako,
ili wote wasifu na kutukuza jina lako la Baba, Mwana na Roho Mtakatifu.
                                  Amina.
MT. ROMUALDO (952-1027)
Yesu mpenzi, amani ya moyo wangu, hamu isiyosemeka,
20

utamu na unono wa malaika na wa watakatifu!
MT. YOHANE GUALBERTO (999-1073)
Bwana, unihurumie, Kristo unihurumie: niweze kukuamini.
 Bwana, unihurumie, Kristo unihurumie: niweze kukujua,
       niweze kukutumainia, niweze kukupenda,
         na roho yangu iishi ndani yako. Amina.
MT. ANSELMO (1033-1109)
      Bwana, wewe ni Mungu wangu, wewe ni Bwana wangu
                       lakini mimi sijakuona.
Wewe umeniumba na kuniumba upya, umenijalia mema yangu yote,
                     lakini mimi sijakufahamu.
                       Nimeumbwa ili nikuone
     lakini sijafanya hilo ambalo kwa ajili yake nimeumbwa…
      Unifundishe kukutafuta na ujionyeshe ninapokutafuta:
 siwezi kukutafuta usiponifundisha, wala kukuona usipojionyesha.
    Nikutafute kwa kukutamani na nikutamani kwa kukutafuta,
       nikuone kwa kukupenda na nikupende kwa kukuona.
                          Nakuomba, Bwana,
     unijalie nionje kwa upendo yale ninayoyaonja kwa ujuzi;
         unijalie nijue kwa upendo ninayoyajua kwa akili.
        Nakuwia kuliko uhai wangu wote, lakini sina zaidi,
    tena peke yangu siwezi kukurudishia uhai huo kikamilifu.
       Univute kwako, Bwana, katika utimilifu wa upendo.
Mimi mzima ni wako kwa uumbaji; unifanye wako kwa upendo pia.
               Bwana, moyo wangu uko mbele yako.
   Najaribu, lakini peke yangu siwezi kitu; fanya nisichoweza.
     Unikaribishe katika chumba cha ndani cha upendo wako.
                   Naomba, natafuta, napiga hodi.
             Wewe uliyenijalia kuomba, unijalie nipate;
                 uliyenijalia kutafuta, unijalie nione;
              uliyenifundisha kupiga hodi, unifungulie.
M.H. WILIAMU WA SAINT-THIERRY (1085-1148)
                Umetangulia kutupenda ili tukupende;
                  si kwamba ulihitaji upendo wetu,
bali kwa sababu bila ya kukupenda tusingeweza kuwa ulivyotuumbia…
      Kusema kwako kwa njia ya Mwana ni kuweka mwangani tu,
         yaani kuonyesha wazi kadiri na jinsi ulivyotupenda…
               Yale aliyoyatenda, aliyoyasema duniani,
        hata kutukanwa, kutemewa mate na kupigwa makofi,


                   hata kusulubiwa na kuzikwa,
       yalikuwa tu usemi wako kwetu kwa njia ya Mwana:
himizo na uchochezi wa upendo wako kwa upendo wetu kwako.
       Kwa kuwa wewe, Muumba wa roho, ulijua kwamba
   upendo huo hauwezi kulazimishwa kwa roho za binadamu,
                       ila ilibidi uhimizwe tu.
    Ulijua pia kwamba palipo na shuruti hapana uhuru tena;
                 na pasipo uhuru hapana haki pia.
                Basi, ulitaka tukupende sisi ambao
 tusingeweza hata kuokolewa kwa haki kama tusingekupenda,
    tena tusingeweza kukupenda kama tusingejaliwa nawe.
MT. BERNARDO (1090-1153)
    Bwana, mema yangu ni kukaa katika tabu, mradi wewe uwe nami.
    Ni bora kuliko kutawala pasipo wewe, kula karamuni pasipo wewe,
                         kujitukuza pasipo wewe.
         Bwana, mema yangu ni kukukumbatia wewe katika tabu,
           kuwa nawe katika tanuri, kuliko kubaki pasipo wewe,
                      hata kama ingekuwa mbinguni.
                     Kwangu kuna nini zaidi mbinguni,
                nami natamani nini zaidi ya wewe duniani?
      Moto unatakasa dhahabu na jaribio la tabu linatakasa waadilifu.
                Humo, Bwana, u pamoja nao; humo unakaa
kati ya wale waliokusanyika kwa jina lako, kama zamani na vijana watatu.
MMONAKI MWINGEREZA (Karne XII)
       Yesu, tumaini la wanaotubu,
    jinsi ulivyo mpole kwa waombao!
Jinsi ulivyo mwema kwa wanaokutafuta.
  Lakini hasa u nini kwa wanaokupata!
          Ulimi hauwezi kusema,
        wala maandishi kufafanua;
   aliyeng'amua tu anaweza kuamini
          kumpenda Yesu ni nini.
BALDWIN WA CANTERBURY (1120-1190)
              Bwana, uniondolee moyo huu wa jiwe.
Uninyofolee moyo huu ulioganda. Uteketeze moyo huu usiotahiriwa.
          Nipe moyo mpya, moyo wa nyama, moyo safi!
       Wewe, mtakasaji wa mioyo na mpenzi wa mioyo safi,
            utamalaki moyo wangu, ukae ndani yake.
                    Uukumbatie na kuufariji.
              Uwe mrefu kuliko vilele vyangu vyote,


          uwe wa ndani kuliko dhati yangu yenyewe.
 Wewe, kielelezo cha uzuri wowote na asili ya utakatifu wote,
           uchonge moyo wangu kadiri ya sura yako;
uuchonge kwa nyundo ya huruma yako, Mungu wa moyo wangu
   na urithi wangu, Ee Mungu, heri yangu ya milele. Amina.





MT. YOHANE WA DAMASKO (645-750)
Wewe, Bwana, ulinitoa katika viuno vya baba yangu;
19
SALA YA KARNE ZA KATI
  Nakusihi, Bwana, nguvu yenye moto na tamu ya upendo wako
iondoe akili yangu mbali na vitu vyote vilivyopo chini ya mbingu,
                ili nife kwa kupenda upendo wako,
     wewe uliyeona inafaa ufe kwa kupenda upendo wangu.
MT. FRANSISKO WA ASIZI (1181-1226)
                        BABA YETU mtakatifu kabisa:
               muumba, mkombozi, mfariji na mwokozi wetu.
           ULIYE MBINGUNI: katika malaika na katika watakatifu,
  ukiwaangazia wawe na ufahamu, kwa sababu wewe Bwana ni mwanga;
    ukiwawasha wawe na upendo, kwa sababu wewe Bwana ni upendo;
     ukikaa ndani mwao na kuwajaza furaha, kwa sababu wewe Bwana
                  ni wema mkuu kabisa, wema wa milele,
       ambaye kwako hutoka mema yote, na bila yako hakuna jema.
   JINA LAKO LITUKUZWE: ujuzi wetu juu yako uwe wazi zaidi na zaidi,
         tuweze kujua upana wa baraka zako, urefu wa ahadi zako,
                kimo cha ukuu wako, kina cha hukumu zako.
    UFALME WAKO UFIKE: utawale ndani yetu kwa njia ya neema yako
            na kutuwezesha kuingia katika ufalme wako ambapo
              unaonekana kama ulivyo, unapendwa kikamilifu,
       unatia heri ya kukaa nawe, unatia raha ya kukufurahia milele.
   UTAKALO LIFANYIKE DUNIANI KAMA MBINGUNI: tuweze kukupenda
             kwa moyo wetu wote, kwa kukuwaza wewe daima;
             kwa roho yetu yote, kwa kukutamani wewe daima;
           kwa akili yetu yote, kwa kuelekeza nia zetu zote kwako
                 na kwa kutafuta utukufu wako katika yote;
         kwa nguvu zetu zote pia, kwa kutumia uwezo na hisia zote
 za roho na mwili katika kuhudumia upendo wako na si chochote kingine;
        na tuweze kuwapenda majirani wetu kama tunavyojipenda,
      kwa kuwavuta wote kwa nguvu zetu zote kwenye upendo wako,
       tukifurahia mema ya wengine kama tunavyofurahia ya kwetu,
      na tukihuzunika pamoja na wengine kwa mabaya yanayowafikia,
                           bila ya kumuudhi yeyote.
MKATE WETU WA KILA SIKU: Mwanao mpendwa Bwana wetu Yesu Kristo.
             UTUPE LEO: kwa ukumbusho, ufahamu na heshima
                    ya upendo ule aliokuwanao kwetu sisi
na ya mambo yale ambayo alisema na kutenda na kuteseka kwa ajili yetu.

ONGEA NA MUNGU WAKO.

       UTUSAMEHE MAKOSA YETU: kwa huruma yako isiyosemeka,
              kwa nguvu ya mateso ya Mwanao mpendwa,
        pamoja na stahili na maombezi ya Bikira mbarikiwa daima
                         na ya wateule wako wote.
          KAMA TUNAVYOWASAMEHE NA SISI WALIOTUKOSEA:
                     na lolote tusilosamehe kikamilifu,
              wewe Bwana utuwezeshe kulisamehe kabisa,
              tuwapende kweli maadui wetu kwa ajili yako,
na tuwaombee kwa bidii mbele zako, bila ya kumlipa yeyote ovu kwa ovu,
           bali tukijitahidi kumsaidia kila mmoja katika wewe.
      NA USITUTIE KATIKA VISHAWISHI: kilichofichika au cha wazi,
                       cha ghafla au cha muda mrefu.
        LAKINI UTUOPOE MAOVUNI: yaliyopita, ya sasa na yajayo.
           ATUKUZWE BABA NA MWANA NA ROHO MTAKATIFU
             KAMA MWANZO, NA SASA NA MILELE. AMINA.
        Ndiwe Bwana Mungu mtakatifu unayetenda maajabu.
    Wewe una nguvu. Wewe ni mkuu. Wewe ndiwe mkuu kabisa.
                   Wewe ndiwe mfalme mwenyezi.
         Wewe, Baba mtakatifu, mfalme wa mbingu na nchi.
        Wewe ni utatu na umoja, Bwana Mungu wa miungu;
ndiwe wema, wema wote, wema mkuu, Bwana Mungu hai na wa kweli.
  Wewe ni pendo, upendo; wewe ni hekima, wewe ni unyenyekevu,
 wewe ni uvumilivu, wewe ni uzuri, wewe ni upole, wewe ni usalama,
    wewe ni utulivu, wewe ni furaha na heri, wewe ni tumaini letu,
  wewe ni haki, wewe ni kiasi, wewe ni mali yetu yote ya kututosha.
       Wewe ni uzuri, wewe ni upole, wewe ndiwe msimamizi,
 wewe ni mlinzi na mtetezi wetu, wewe ni nguvu, wewe ni burudisho.
  Wewe ni tumaini letu, wewe ni imani yetu, wewe ni upendo wetu,
     wewe ni utamu wetu wote, wewe ni uzima wetu wa milele:
Bwana mkuu na wa ajabu, Mwenyezi Mungu, Mwokozi mwenye huruma.
MT. ELIZABETI WA HUNGARIA (1207-1231)
Bwana, ukitaka kuwa pamoja nami,
 mimi nataka kuwa pamoja nawe,
 nisitake kutengana nawe kamwe.
MT. RICHARD (1197-1253)
Asante kwako, Bwana wangu Yesu Kristo, kwa fadhili zote ulizonistahilia.
      Kwa mateso na matusi yote uliyoyavumilia kwa ajili yangu.
          Mkombozi, rafiki na kaka mwenye huruma nyingi,
  naomba niweze kukufahamu wazi zaidi, kukupenda kwa hisani zaidi,
              kukufuata kwa karibu zaidi, siku kwa siku.


MT. BONAVENTURA (1217-1274)
 Lo, uzuri usiosemeka wa Mungu mkuu,
lo, mng’ao safi kabisa wa nuru ya milele!
    Wewe ni uhai unaohuisha kila uhai,
    mwanga unaoangaza kila mwanga!
      Bwana Yesu Kristo, unichome mpaka kiini cha moyo wangu
        kwa donda lile tamu la kuletea wokovu la upendo wako.
        Unijaze kwa ule upendo motomoto, mnyofu na mtulivu
               uliomfanya mtume wako mtakatifu Paulo
             atamani kutengwa na mwili wake awe nawe.
Roho yangu ikuonee shauku, ikijaa daima hamu ya makao yako ya milele.
MT. THOMA WA AKWINO (1225-1274)
Mungu wa wema wote, utujalie tutamani motomoto, tutafute kwa busara,
  tujue kwa hakika na kutekeleza kikamilifu matakwa yako matakatifu
                      kwa utukufu wa jina lako.
M.H. ANJELA WA FOLIGNO (1248-1309)
                   Mungu wangu, unijalie kujua fumbo kuu
            linalotokana na moto wa upendo wako usiosemeka
                           na wa Nafsi tatu za Utatu,
                  yaani fumbo la umwilisho wako mtakatifu
                      uliotaka kutekeleza kwa ajili yetu.
                        Ndio mwanzo wa wokovu wetu
                 nao unatenda mambo mawili ndani mwetu:
            kutujaza upendo na kutuhakikishia ukombozi wetu.
                Lo, upendo usioweza kueleweka kwa yeyote!
                       Hakuna upendo mkuu kuliko huo:
           Mungu wangu amejifanya mtu anifanye niwe Mungu!
                          Lo, upendo la kupita kiasi:
        umejiharibu ili kunitengeneza wakati ulipotwaa mwili wetu.
      Si kwamba wewe au umungu wako umekuja kupungukiwa kitu,
ila kina cha umwilisho wako kinanitoa midomoni maneno yenye hisia kali!
              Wewe, usiyeeleweka, umejifanya wa kueleweka;
                   wewe usiyeumbwa umejifanya kiumbe;
                   wewe usiyefikirika, umekuja kufikirika;
        wewe Roho tupu umekubali kuguswa na mikono ya watu!...
Ee Mkuu kabisa, uniwezeshe kuelewa zawadi hiyo ipitayo nyingine yoyote:
                 malaika na watakatifu wote heri yao pekee
                   ni kukuona, kukupenda na kukutazama!
                        Ee zawadi ya juu kuliko yoyote,
          kwa kuwa wewe ndiwe zawadi yenyewe, ndiwe Upendo!


Ee Wema mkuu, umekubali kujulikana kama Upendo,
       na unatufanya tuupende Upendo huo.
 Wale wote watakaofika mbele yako watapata raha
      kadiri ya upendo waliokuwanao kwako.
MT. GETRUDA (1256-1301)
 Mungu, unayestahili upendo usio na mipaka,
 sina chochote cha kupimia vema ukuu wako,
   lakini hamu yangu kwako ni hivi kwamba,
kama ningekuwa na yale yote uliyonayo wewe,
    ningekupa yote kwa furaha na shukrani.
            Kwa ajili ya uongofu nakutolea, Baba mpenzi sana,
   mateso yote ya Mwanao mpendwa sana tangu wakati ule ambapo,
       akilazwa horini juu ya nyasi, alianza kulia, halafu akavumilia
       mahitaji ya utoto, mapungufu ya ubalehe, mateso ya ujana,
      hadi alipoinamisha kichwa akafa msalabani kwa mlio mkubwa.
        Vilevile, kwa kufidia makosa yangu ya uzembe, nakutolea,
      Baba mpenzi sana, mwendo wote wa maisha matakatifu sana
             ambayo Mwanao pekee aliyaishi kikamilifu kabisa
                 katika mawazo, maneno na matendo yake
tangu atumwe kutoka ukuu wa kiti chako cha enzi kuja katika dunia yetu,
               hadi alipouonyesha mtazamo wako wa Kibaba
                       utukufu wa mwili wake mshindi.
   Kama shukrani nazama katika kilindi kirefu sana cha unyenyekevu,
                   na pamoja na huruma yako isiyolipika,
                nasifu na kuabudu wema wako mtamu sana.
  Wewe, Baba wa huruma, nilipokuwa ninapoteza maisha yangu hivyo,
             ulikuza kwangu mawazo ya amani, si ya mabaya,
           ukaamua kuniinua kwa wingi na ukuu wa fadhili zako.
 Kati ya mengine, ulitaka kunijalia ujirani usiothaminika wa urafiki wako
kwa kunifungulia kwa namna mbalimbali hazina ile azizi sana ya umungu,
                    ambayo ni moyo wako wa Kimungu,
  na kwa kunitolea kwa wingi mkubwa kila utajiri wa furaha ndani yake.
MT. BIRGITA (1303-1373)
Usifiwe, Bwana wangu Yesu Kristo, kwa kuwahi kutabiri kifo chako,
  kwa kugeuza kwa namna ya ajabu, katika karamu ya mwisho,
           mkate wa kawaida uwe mwili wako mtukufu,
              kwa kuwagawia mitume kwa upendo
          kama ukumbusho wa mateso yako mastahivu,
    kwa kuwaosha miguu kwa mikono yako mitakatifu na azizi,
  ukionyesha hivyo ukuu usio na mipaka wa unyenyekevu wako.
           Heshima kwako, Bwana wangu Yesu Kristo,


        kwa kutoka jasho la damu katika mwili wako usio na kosa
                         kwa hofu ya mateso na kifo,
   na kwa kutekeleza hata hivyo ukombozi wetu uliotamani kuutimiza,
            ukionyesha hivyo wazi upendo wako kwa binadamu.
     Usifiwe, Bwana wangu Yesu Kristo, kwa kupelekwa kwa Kayafa
        na kuruhusu kwa unyenyekevu wako uhukumiwe na Pilato,
                         wewe uliye hakimu wa wote.
Utukufu kwako, Bwana wangu Yesu Kristo, kwa kudhihakiwa pale ambapo,
    kisha kuvikwa nguo ya zambarau, ulitiwa taji la miba mikali sana,
           na kwa kuvumilia kwa subira isiyo na mipaka kwamba
           uso wako mtukufu ujae mate, macho yako yafunikwe,
 mashavu yako yapigwe kwa nguvu na mikono ya kikafiri ya watu waovu.
                   Sifa kwako, Bwana wangu Yesu Kristo,
      kwa kuruhusu kwa uvumilivu mkubwa ufungwe kwenye nguzo,
                           upigwe mijeledi kinyama,
              upelekwe mahakamani kwa Pilato umejaa damu,
 uonekane kama mwanakondoo asiye na kosa anayepelekwa machinjoni.
                 Heshima kwako, Bwana wangu Yesu Kristo,
          kwa kukubali kuhukumiwa katika mwili wako mtakatifu,
                     uliojaa tayari damu, ufe msalabani;
   kwa kubeba kwa uchungu msalaba juu ya mabega yako matakatifu,
       na kwa kutaka kupigiliwa misumari katika mbao za adhabu,
 kisha kuburutwa kikatili hadi mahali pa mateso na kuvuliwa nguo zako.
                     Heshima kwako, Bwana Yesu Kristo,
          kwa kuelekeza kwa unyenyekevu, kati ya mateso hayo,
 macho yako yaliyojaa upendo na wema kwa Mama yako mstahivu sana,
                    ambaye hajawahi kupatwa na dhambi
                    wala kukubali kosa dogo namna gani,
na kwa kumfariji ukimkabidhi kwa ulinzi mwaminifu wa mwanafunzi wako.
                Uhimidiwe milele, Bwana wangu Yesu Kristo,
           kwa kuwapa wakosefu wote, wakati wa kihoro chako,
              tumaini la msamaha ulipomuahidia kwa huruma
                utukufu wa paradiso mhalifu aliyekukimbilia.
              Sifa ya milele kwako, Bwana wangu Yesu Kristo,
       kwa kila saa uliyovumilia msalabani kwa ajili yetu wakosefu
                   machungu na mateso makubwa kabisa;
             kwa kuwa uchungu mkali sana wa majeraha yako
            ulikuwa ukipenya vibaya mno roho yako yenye heri
              na kuchoma kikatili moyo wako mtakatifu sana,
  mpaka pale ambapo, moyo ukishindwa kazi, ulitoa kwa heri roho yako
                         na, kisha kuinamisha kichwa,
     uliikabidhi kwa unyenyekevu wote mikononi mwa Mungu Baba,
                     ukabaki mfu, ukiwa na mwili baridi.
                     Usifiwe, Bwana wangu Yesu Kristo,
             kwa kukomboa roho za watu kwa damu yako azizi
                      na kwa kifo chako kitakatifu sana,


na kwa kuzirudisha kwa huruma katika uzima wa milele toka uhamishoni.
                     Usifiwe, Bwana wangu Yesu Kristo,
    kwa kukubali mkuki ukuchome ubavu na moyo kwa wokovu wetu,
                          na kwa damu azizi na maji
          vilivyobubujika kutoka ubavu huo kwa ukombozi wetu.
                 Utukufu kwako, Bwana wangu Yesu Kristo,
      kwa kutaka mwili wako mbarikiwa ushushwe toka msalabani
                       kwa mikono ya marafiki wako,
   ukabidhiwe mikononi mwa Mama mwenye huzuni na kuvikwa naye,
           halafu ufungwe katika kaburi na kulindwa na askari.
           Heshima ya milele kwako, Bwana wangu Yesu Kristo,
                   kwa kufufuka kutoka wafu siku ya tatu
                na kwa kukutana hai na wale uliowachagua;
   kwa kupaa mbinguni, siku arubaini baadaye, ukitazamwa na wengi
na kwa kutawaza huko juu kwa heshima marafiki wako uliowatoa kuzimu.
          Shangwe na sifa ya milele kwako, Bwana Yesu Kristo,
          kwa kumtuma Roho Mtakatifu mioyoni mwa wanafunzi
         na kwa kushirikisha roho zao upendo mkuu wa Kimungu.
      Uhimidiwe, usifiwe na kutukuzwa milele, Bwana wangu Yesu,
     uliyeketi katika kiti che enzi kwenye ufalme wako wa mbinguni,
                        katika utukufu wa enzi yako,
       mwenye mwili hai pamoja na viungo vyako vitakatifu vyote,
                  ulivyovitwaa kutoka mwilini mwa Bikira.
                       Hivyo utakuja siku ya hukumu
               uhukumu roho za wote walio hai na waliokufa:
     wewe unayeishi na kutawala pamoja na Baba na Roho Mtakatifu
                           daima na milele. Amina.
SALA KUTOKA ASSISI (Karne XIV)
     Salamu, Bwana Yesu Kristo, Neno wa Baba, Mwana wa Bikira,
   Mwanakondoo wa Mungu, wokovu wa ulimwengu, Hostia takatifu,
             Neno uliyefanyika mwili, chemchemi ya wema.
  Salamu, Bwana Yesu Kristo, sifa za malaika, utukufu wa watakatifu,
              mandhari ya amani, Mungu mzima, mtu kweli,
                    chipukizi na tunda la Mama Bikira.
    Salamu, Bwana Yesu Kristo, mng’ao wa Baba, mfalme wa amani,
           mlango wa mbingu, utukufu wa ufalme, mkate hai,
               uliyezaliwa na Bikira, chombo cha Umungu.
Salamu, Bwana Yesu Kristo, mwanga wa mbingu, msingi wa ulimwengu,
                     furaha yetu, mkate wa malaika,
           furaha ya moyo, mfalme na bwanaarusi wa ubikira.
   Salamu, Bwana Yesu Kristo, njia tamu, ukweli safi, upendo mkuu,
   tuzo letu, chemchemi ya upendo, amani ya wema, pumziko halisi,
          uzima wa milele, ambapo baada ya unyonge wa sasa
    wewe utujalie kutuburudisha kwa uso wako, Mungu wa miungu,


mfalme wa wafalme, Bwana wa mabwana, daima na milele. Amina.
SALA NYINGINE YA KARNE XIV
       Roho ya Kristo, unitakase.
        Mwili wa Kristo, uniokoe.
       Damu ya Kristo, unilevye.
   Maji ya ubavu wa Kristo, unioshe.
    Mateso ya Kristo, yanitie nguvu.
      Ee Yesu mwema, unisikilize.
     Katika madonda yako unifiche.
       Usikubali nitengane nawe.
       Na adui mwovu unikinge.
      Saa ya kufa kwangu uniite.
         Uniamuru nije kwako,
nikutukuze pamoja na Watakatifu wako,
        milele na milele. Amina.
MT. KATERINA WA SIENA (1347-1380)
                  Mungu wa milele, Utatu wa milele,
umefanya damu ya Kristo iwe azizi kabisa kwa kushiriki umungu wako.
                 Wewe ni fumbo la kina kuliko bahari;
     kadiri ninavyotafuta naona; na kadiri ninavyoona nakutafuta.
Siwezi kamwe kushiba; ninachopokea kitanifanya daima nitamani zaidi.
  Unapojaza roho yangu nazidi kuonea njaa na shauku mwanga wako.
      Hasa natamani kukuona wewe, mwanga halisi, jinsi ulivyo.
    Ndiwe muumba wangu, Utatu wa milele, nami ni kiumbe chako.
          Umenifanya kiumbe kipya katika damu ya Mwanao,
 nami najua unavutwa na uzuri wa kiumbe chako kutokana na upendo.
    Bwana wangu, elekeza jicho la huruma yako juu ya taifa lako
             na juu ya mwili wa fumbo wa Kanisa takatifu.
Wewe utatukuzwa zaidi sana kwa kusamehe na kuwaangazia akili wengi,
     kuliko kwa kupokea heshima toka kwa kiumbe mmoja duni,
              kama nilivyo mimi, ambaye nilikukosea sana
            na kuwa sababu na chombo cha maovu mengi.
Ingenitokea nini kama ningeona mimi ni hai, na watu wako wamekufa?
                   Ingekuwaje kama ningeliona gizani,
          kutokana na dhambi zangu na za viumbe wengine,
    Kanisa lako, Bibiarusi wako mpenzi, lililozaliwa liwe mwanga?
                 Basi, nakuomba huruma kwa taifa lako
        kwa ajili ya ya upendo usioumbwa uliokusukuma wewe
                umuumbe mtu kwa sura na mfano wako.
  Sababu gani ilikufanya umweke mtu katika heshima kubwa hivyo?
           Bila ya shaka ni upendo ule usiothaminika ambao


     ulimuangalia kiumbe chako ndani mwako ukachanganyikiwa naye.
Lakini baadaye kwa dhambi aliyoitenda akapoteza ukuu huo uliomuinulia.
               Ukisukumwa na moto huohuo ambao ulituumba,
          ulipenda kuwatolea binadamu njia ya kupatanishwa nawe.
               Ndiyo sababu umetupatia Neno, Mwanao pekee.
                    Amekuwa mshenga kati yako na sisi,
          amekuwa haki yetu aliyeadhibu ndani mwake maovu yetu.
  Alitii agizo ambalo wewe, Baba wa milele, ulimpa ulipomvika utu wetu.
 Lo, kilindi cha upendo! Moyo upi hautajaa mhemko kwa kuona ukuu huo
       kushukia unyonge mkubwa kama huu, yaani ubinadamu wetu?
                    Sisi ni mfano wako, nawe mfano wetu
         kutokana na muungano uliouanzisha kati yako na binadamu,
                          ukifunika umungu wa milele
               kwa wingu maskini la utu ulioharibika wa Adamu.
                 Kwa sababu gani? Bila ya shaka kwa upendo.
            Kwa upendo huo usiosemeka nakuomba na kukuhimiza
                        uwawie huruma viumbe wako.
JULIANA WA NORWICH (1342-1413)
      Ee Mungu wa wema wako, unipatie wewe mwenyewe,
                  kwa kuwa wewe unanitosha.
    Siwezi kuomba vema chochote kingine ili nikustahili wewe.
Ningeomba chochote kidogo kuliko wewe ningekuwa mhitaji daima,
            kwa sababu ndani mwako tu nina kila kitu.
THOMAS WA KEMPIS (1379-1471)
          Ee Bwana, unangurumisha hukumu zako juu yangu,
         na kutikisa mifupa yangu yote kwa hofu na tetemeko.
                      Roho yangu imeshtuka sana.
Nabaki nimeduwaa na kuzingatia mbingu zenyewe si safi machoni pako.
 Kama uliona kasoro katika malaika usiwaachilie, itakuwaje kwangu?
    Nyota za mbinguni zilianguka, nami, mavumbi, natarajia nini?
          Watu kadhaa walioonekana wenye mwenendo bora
                        walianguka chini kabisa;
                  na mtu aliyekula mkate wa malaika,
         baadaye nikamuona kufurahia vyakula vya nguruwe.
   Basi, hakuna utakatifu wowote, ukiondoa mkono wako, Bwana.
           Hakuna hekima inayofaa, ukiacha kutawala wewe.
            Hakuna nguvu inayosaidia, ukiacha kutegemeza.
                     Tukiachwa, tunazama na kufa.
              Kumbe tukitembelewa, tunainuka na kuishi.
             Hatuna msimamo, lakini wewe unatuimarisha.
                Tunapoa, lakini wewe unatuwasha tena.
 Majivuno yoyote yanamezwa na kilindi cha hukumu zako juu yangu.


                 Mwili wowote ni nini mbele yako?
             Je, udongo utajivuna dhidi ya mfinyanzi?
Anawezaje kupotea katika majivuno mtu ambaye anahisi sana ukweli
                    na kukaa chini ya Mungu?
           Ulimwengu wote hauwezi kumtia kiburi mtu
           anayejiona kutawaliwa na sheria ya ukweli,
        wala midomo ya walaghai wote haitamsogeza mtu
             aliyeweka tumaini lake lote kwa Mungu.
            Wale wenyewe wanaosema si kitu vilevile;
          Watatoweka pamoja na sauti ya maneno yao:
            kumbe, “Uaminifu wa Bwana ni wa milele”.
Bwana Yesu, kadiri maisha yako yalivyodharauliwa na ulimwengu,
                  utujalie tukuige hivi kwamba,
      tukiwa na picha yako daima mbele ya macho yetu,
               hata kama ulimwengu unatudharau,
          tujifunze kwamba watumishi wa msalaba tu
   wanaweza kuona njia ya heri halisi na mwanga wa kweli.
MT. NIKOLA WA FLUE (1417-1487)
Bwana, uniondolee yale yote yanayonizuia nisifike kwako;
     unijalie yale yote yanayoweza kunifikisha kwako;
 ujichukulie nafsi yangu, na kujipatia kabisa mwenyewe.
MT. THOMAS MORE (1478-1535)
Bwana mwema, utujalie neema ya kuyafanyia kazi yale tunayokuomba.
MT. INYASYO WA LOYOLA (1491-1556)
                   Pokea, Bwana, hiari yangu yote.
               Pokea kumbukumbu, akili na utashi wote.
       Vyovyote nilivyonavyo au kuvimiliki nimejaliwa na wewe:
       nakurudishia vyote na kuukabidhi utashi wako uvitawale.
Unijalie tu upendo wako na neema yako, nami nitakuwa tajiri kutosha,
                   nisitamani kitu kingine chochote.
M.H. PETRO FAVRE (1506-1546)
      Ee Yesu Kristo, kifo chako kiwe uhai wangu;
          nijifunze kuona uhai katika kifo chako.
             Uchovu wako uwe pumziko langu,
    udhaifu wako wa kibinadamu uwe nguvu yangu.
Kudhalilishwa kwako kuwe chemchemi ya utukufu wangu,
  mateso yako raha yangu, huzuni yako furaha yangu.


           Kujishusha kwako kuniinue:
kwa ufupi, machungu yako yawe yote nilivyonavyo.
MT. FRANSISKO SAVERI (1506-1552)
                 Ee Mungu wa mataifa yote ya dunia,
               uukumbuke umati wa Wapagani ambao,
                  ingawa waliumbwa kwa sura yako,
hawajakufahamu wewe wala kifo cha Mwanao Yesu Kristo, mwokozi wao.
       Fanya kwamba, kwa sala na kazi za Kanisa lako takatifu,
       wakombolewe kutoka ushirikina wote na utovu wa imani
                    wakaletwe kwenye ibada zako.
   Kwa njia ya yule uliyemtuma awe ufufuo na uzima wa watu wote,
                huyo Mwanao Yesu Kristo, Bwana wetu.
MT. LUDOVIKO BERTRANDO (1526-1581)
Bwana, unichome moto hapa duniani, na kunikausha hapa duniani,
                    ili unihurumie milele.
MT. TERESA WA YESU (1515-1582)
     Bwana wangu, je, hukuweza kujumlisha yote katika neno moja
             na kusema, “Baba, utupe yote tunayoyahitaji”?
    Kwa yule anayejua yote vizuri kabisa, inaonekana haihitajiki zaidi.
     Lo, hekima ya milele! Kwako na kwa Baba yako hiyo ingetosha,
         na kweli ndivyo ulivyosali katika bustani la Getsemane:
ulionyesha matakwa na hofu yako, lakini ukajiachilia kwa matakwa yake.
 Hata hivyo kwa kuwa unajua hatuko tayari kama wewe, Bwana wangu,
     kutii matakwa ya Baba yako, ilikubidi ubainishe vizuri maombi,
              tuweze kuona kama tunayoyaomba yanatufaa,
                   na tujizuie kuomba tukiona haitufai.
     Kwa sababu ndivyo tulivyo kwamba, tusipopewa tunayotamani,
            kwa hiari yetu tunayakataa tunayopewa na Bwana,
                        hata yakiwa mambo bora.
       Kwa kuwa hatujioni matajiri mpaka tushike fedha mikononi.
Bwana wangu, kwa hakika saa niliyoitamani sana hatimaye imefika.
          Kwa hakika wakati wa sisi kuonana umefika.
      Bwana na mwokozi wangu, kwa hakika huu ni wakati
  wa mimi kuchukuliwa kutoka uhamisho huu niwe nawe milele.
             Dhabihu za Mungu ni roho iliyovunjika;
    moyo uliovunjika na kupondeka, Ee Mungu, hutaudharau.
                    Usinitenge na uso wako,
            wala roho yako mtakatifu usiniondolee.
                Ee Mungu, uniumbie moyo safi.


MT. YOHANE WA MSALABA (1542-1591)
Roho yangu ni kavu ndani mwangu kwa sababu imesahau kujilisha wewe.
MT. MARIA MAGDALENA WA PAZZI (1566-1607)
           Neno, wewe ni wa ajabu katika Roho Mtakatifu pia,
               ukimfanya ajimimine katika roho hivi kwamba
  roho inakuja kuungana na Mungu, inamjua Mungu, inamuonja Mungu,
                    haifurahii chochote isipokuwa Mungu.
                      Na Roho Mtakatifu anakuja rohoni
imetiwa daima mhuri azizi ya Damu ya Neno, Mwanakondoo aliyechinjwa;
                    tena damu ndiyo inayomsukuma aje,
                 ingawa mwenyewe anakuja kwa kutaka…
             Roho Mtakatifu, huishii katika Baba asiyebadilika,
                           wala huishii katika Neno;
            ingawa umo daima ndani ya Baba, ndani ya Neno,
         ndani mwako na ndani ya roho zote zenye heri mbinguni
                              na ndani ya viumbe.
    Unahitajiwa na kiumbe kutokana na damu iliyomwagwa na Neno,
                 Mwana pekee, ambaye kwa ari ya upendo
                  amejifanya ahitahiwe na kiumbe chake.
     Unapumzika katika viumbe vilivyojiandaa kupokea ndani mwao,
          kwa kushirikishwa vipaji vyako, mfano wako kwa usafi.
     Unapumzika ndani ya wale wanaopokea tunda la damu ya Neno
                       na kujifanya maskani ya kukufaa.
                             Njoo, Roho Mtakatifu.
                  Uje muungano na Baba, faraja ya Neno.
      Roho wa ukweli, ndiwe tuzo la watakatifu, burudisho la roho,
     mwanga wa giza, utajiri wa mafukara, hazina ya wenye upendo,
                 shibe ya wenye njaa, faraja ya wanaohiji;
                       basi ndiwe mwenye hazina zote.
  Njoo wewe ambaye, kwa kumshukia Maria, ulimfanya Neno awe mwili,
                     fanya tena ndani mwetu kwa neema
            kile ulichomfanyia Maria kwa neema na maumbile.
       Njoo, uliye lishe ya kila wazo safi, chemchemi ya kila wema
                            na fungu la usafi wote.
          Njoo, uteketeze ndani mwetu yale yote yanayotufanya
                      tusiweze kuteketea ndani mwako.
MT. FRANSISKO SOLANO (1549-1610)
             Yesu mwema, mkombozi na rafiki yangu!
Nina kitu gani usichonipa wewe? Najua nini usiyonifundisha wewe?
               Nina thamani gani usipokuwa nami?...

Ndiwe uliyeniumba, tena bila ya kuniuliza. Wewe umeniumba.
    Elekeza macho yako kwangu, Bwana, na unihurumie,
            kwa kuwa mimi ni mkiwa na maskini…
     Kwa nini, Bwana Yesu wangu, wewe umesulubiwa,
             nami nasaidiwa na watumishi wako?
             Kwa nini wewe uchi, nami nina vazi?
   Kwa nini wewe umepigwa makofi na kutiwa taji la miba,
 nami nimepewa vitu vyema na kufarijiwa na fadhili nyingi?...
    Mungu wa roho yangu, utukuzwe kwa yale uliyonijalia!
Bwana wangu, nafurahi kwamba u Mungu; jinsi hilo lilivyo zuri!
MT. ROBERTO BELLARMINO (1542-1621)
          Wewe, Bwana, u mwema, umekuwa tayari kusamehe,
              na mwingi wa fadhili, kwa watu wote wakuitao;
nani hatakutumikia kwa moyo wote baada ya kuanza kuonja walau kidogo
                    utamu wa mamlaka yako ya Kibaba?
                 Unawaagiza nini watumishi wako, Bwana?
             Unasema, Jitieni nira yangu. Na nira yako ikoje?
        Unasema, Nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.
  Nani hatabeba kwa moyo radhi kabisa nira isiyobana bali inapendeza,
                     na mzigo usiolemea, bali unainua?
   Kwa hiyo umeongeza kwa haki, Nanyi mtapata raha nafsini mwenu.
       Na ikoje nira yako hiyo ambayo haichoshi, bali inapumzisha?
                Kwa hakika ndiyo amri ya kwanza tena kuu,
            Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote.
  Nini ni rahisi, nono na tamu kuliko kupenda wema, uzuri na upendo?
             Na hayo yote ndiwe wewe, Bwana Mungu wangu.
 Nawe unafikia hatua ya kuahidi tuzo kwa wale wanaoshika sheria zako,
       ingawa tayari zenyewe ni za thamani kuliko dhahabu nyingi,
                       na tamu kuliko sega la asali?
            Ndiyo, unaahidi kweli tuzo, tena tuzo kubwa mno.
MT. FRANSISKO WA SAL (1567-1622)
                   Ee Mungu wangu, nakutolea siku hii.
                Nakutolea sasa mema yote nitakayotenda
na ninakuahidi nitapokea kwa upendo wako magumu yote yanayonikabili.
          Unisaidie kuenenda siku hii namna inayokupendeza.
      Ee Bwana, mimi ni wako, tena natakiwa kuwa wako tu,
                     si wa mwingine yeyote.
    Roho yangu ni wako, nayo inatakiwa iishi kwa njia yako tu.
  Utashi wangu ni wako, nao unatakiwa kupenda kwa ajili yako tu.
Napaswa kukupenda kama asili yangu kuu, kwa kuwa natoka kwako.
        Napaswa kukupenda kama lengo na pumziko langu,


          kwa kuwa nipo kwa ajili yako.
      Napaswa kukupenda kuliko nafsi yangu,
       kwa kuwa nafsi yangu inatoka kwako.
    Napaswa kukupenda kuliko mimi mwenyewe,
kwa kuwa mimi mzima ni wako na ndani yako. Amina.
MT. YOHANE WA BREBEUF (1593-1649)
      Ee Mungu wangu, jinsi ninavyosikitika kwamba hujajulikana,
           na kwamba katika makabila haya yasiyostaarabika
               wachache tu wameikumbatia imani yako!
                Dhambi haijatoweka, nawe hujapendwa!
    Naam, Mungu wangu, ikiwa mateso yote ambayo katika nchi hizi
    mateka wanaweza kupatwa nayo, pamoja na ukatili wa adhabu,
                   zitatakiwa kumwagika juu yangu,
niko tayari kwa moyo wote kuyapokea na kuyavumilia hata peke yangu.
SALA ILIYOSAMBAZWA KWA JINA LA KLEMENTI XI
              Nasadiki, Bwana, lakini nisadiki kwa imara zaidi;
                 natumaini, lakini nitumaini kwa hakika zaidi;
                    napenda, lakini nipende kwa ari zaidi;
                  nasikitika, lakini nisikitike kwa nguvu zaidi.
      Nakuabudu kama asili ya vyote; nakutamani kama lengo kuu;
  nakusifu kama mfadhili wa kudumu; nakulilia kama mtetezi wa kufaa.
          Uniongoze kwa hekima yako, unidhibiti kwa haki yako,
            unifariji kwa wema wako, unilinde kwa uwezo wako.
             Bwana, nakutolea ya kuwaza ili yakuelekee wewe,
                          ya kusema yakuhusu wewe,
                          ya kufanya yawe kadiri yako,
                       ya kuvumilia yake kwa ajili yako.
       Nataka chochote unachotaka, nataka kwa sababu unataka,
           nataka jinsi unavyotaka, nataka mpaka utakapotaka.
                Naomba, Bwana: angaza akili, washa utashi,
                           safisha moyo, takasa roho.
        Nilie juu ya maovu yaliyopita, nifukuze vishawishi vijavyo,
       nirekebishe maelekeo mabaya, nistawishe maadili ya kufaa.
          Mungu mwema, unipatie upendo kwako, chuki kwangu,
                    ari kwa jirani, dharau kwa ulimwengu.
            Nijitahidi kutii wakubwa, kusaidia walio chini yangu,
                     nishauri marafiki, nisamehe maadui.
       Nishinde tamaa kwa maisha magumu, uroho kwa ukarimu,
               hasira kwa upole, uvuguvugu kwa umotomoto.
Unifanye niwe na busara katika maamuzi, niwe na msimamo katika hatari,
   niwe mvumilivu katika matatizo, na mnyenyekevu katika mafanikio.
 Ee Bwana, fanya niwe mwangalifu katika sala, niwe na kiasi katika mali,


niwe na bidii katika majukumu, niwe imara katika nia.
  Nijitahidi kuwa na usafi wa ndani, utaratibu wa nje,
     maongezi bora, maisha yanayofuata mipango.
Nikeshe kwa bidii kutawala umbile, kustawisha neema,
             kufuata sheria, kustahili wokovu.
     Nijifunze kwako yalivyo duni mambo ya dunia,
           yalivyo makuu mambo ya Kimungu,
             yalivyo mafupi mambo yapitayo,
               yanavyodumu yale ya milele.
      Unijalie nijiandae kwa kifo, niogope hukumu,
              nikimbie moto, nipate paradiso.
          Kwa njia ya Kristo Bwana wetu. Amina.
M.H. MARIA MAGDALENA MARTINENGO (1687-1737)
            Kwa kweli, Mungu wangu, wewe tu ni mtakatifu!
                  Utufanye wote watakatifu, Bwana,
ukiteketeza kwanza ndani mwetu yale yote yanayopinga utakatifu wako.
MT. LEONARDO WA PORTOMAURIZIO (1676-1751)
                Yesu wangu, kwa haki tu na kwa shukrani
napaswa kujitoa kabisa kwako, baada ya wewe kujitoa kabisa kwangu…
           Wewe umetakasa hisi zangu zote; fanya ziwe zako,
     zisifurahie tena kilicho kinyume cha sheria yako ya Kimungu.
    Umetakasa kumbukumbu yangu; iwe inakukumbuka mfululizo.
               Umetakasa utashi wangu; usigeuke kamwe
                     kupenda chochote kuliko wewe.
              Basi, kutoka dhati ya moyo wangu nakutolea
          kama sadaka kamili ya kudumu, kadiri ninavyoweza,
       mwili wangu na roho yangu, hisi zangu na vipawa vyangu,
                       nilichonacho na jinsi nilivyo.
                      Ee moto wa Kimungu, choma,
             Ee Upendo wa Mwenyezi, choma na kuteketeza
              yale yote yasiyo yako ndani mwangu! Amina.
MT. ALFONSO MARIA WA LIGUORI (1696-1787)
Yesu wangu, nasadiki kuwa umo katika sakramenti takatifu.
  Nakupenda kuliko vyote na kukutamani rohoni mwangu.
   Kwa kuwa sasa siwezi kukupokea katika sakramenti,
          njoo moyoni mwangu walau kiroho.
 Kama umeshafika nakukumbatia na kujiunga nawe kabisa.
           Usiruhusu nitengane nawe kamwe.
MT. YOHANE MARIA VIANNEY(1786-1859)


                      Nakupenda, Bwana,
  na neema pekee ninayokuomba, ni kwamba nikupende milele…
                        Mungu wangu,
ikiwa ulimi wangu hauwezi kukariri kila nukta kwamba nakupenda,
  nataka moyo wangu ukuambie tena na tena kila ninapopumua.
      Yesu wangu, jinsi inavyopendeza kukupenda!
Unijalie niwe kama wanafunzi wako juu ya mlima Tabori,
           nikikuona wewe tu, Mwokozi wangu.
  Tuwe kama marafiki wawili ambao hata mmojawao
     hawezi kukubali kumchukiza mwingine. Amina.
MT. KATERINA LABOURE’ (1806-1876)
Bwana, nipo hapa, nipe chochote unachotaka.
JOHN HENRY NEWMAN (1801-1890)
                        Mungu wangu uliyetuumba,
             ulijua kwamba wewe tu unaweza kutushibisha;
           basi umeamua kujifanya chakula na kinywaji chetu.
       Fumbo abudiwa kuliko yote! Huruma ya ajabu kuliko zote!
       Wewe mwenye utukufu, uzuri, nguvu na utamu kuliko wote
                   ulijua fika kwamba chochote kingine
  kisingeweza kutegemeza umbile letu lisilokoma, mioyo yetu dhaifu;
     kwa hiyo ulitwaa mwili na damu ya kibinadamu, hivi kwamba,
       vikiwa mwili na damu ya Mungu, viweze kuwa uhai wetu…
     Naja kwako, Bwana, sio tu kwa sababu pasipo wewe sina raha,
               sio tu kwa sababu najitambua ninakuhitaji,
                  bali kwa sababu neema yako inanivuta
nikutafute kwa ajili yako mwenyewe, kwa jinsi ulivyo mtukufu na mzuri.
       Naja kwa uchaji mkubwa, lakini kwa upendo mkubwa zaidi.
MT. TERESA WA MTOTO YESU (1873-1897)
                  Ee Mungu wangu! Utatu mtakatifu!
          Natamani tu kukupenda na kukufanya upendwe…
 Ili maisha yangu yaweze kuwa tendo moja tu la upendo kamili:
                          Ninajitoa mhanga
kama kitambiko cha kuteketezwa kabisa na upendo wako rahimu.
                Nakusihi uniteketeze bila ya kukoma,
      ukiyaruhusu yale mawimbi ya upendo wako usiopimika,
        yanayojazana ndani yako, yafurike rohoni mwangu:
hivyo nami niweze kuwa shahidi wa upendo wako, Mungu wangu!
Unijalie kifodini hicho baada ya kunitayarisha kutokea mbele yako,
37

                      hatimaye unisababishe kufa:
 na roho yangu iruke moja kwa moja, bila ya kuchelewa popote pale,
         ifikie kukumbatiana milele na upendo wako rahimu.
  Ee mpenzi wangu, mimi napenda, katika kila pigo la moyo wangu,
               kurudia upya, mara nyingi zisizohesabika,
                   hili tendo langu la kujitoa kwako.
                  Mpaka hapo vivuli vitakapotoweka,
nami nikaweza kukuambia milele, uso kwa uso, jinsi ninavyokupenda.
Ee Yesu, upendo wangu, hatimaye nimegundua wito wangu.
                  Wito wangu ni kupenda!
       Ndiyo, nimeona nafasi yangu ndani ya Kanisa,
      na nafasi hiyo umenipatia wewe, Mungu wangu.
 Katika moyo wa Kanisa, mama yangu, nitakuwa upendo:
       hivyo nitakuwa yote na hamu yangu itatimia.
 Ee Bwana Yesu, mimi si tai, ila nina macho na moyo wake.
Ingawa ni mdogo, nathubutu kulikazia macho jua la upendo,
              na kutamani kurukia kwake.
M.H. ELIZABETI WA UTATU (1880-1906)
Ee Mungu wangu, Utatu, ninayekuabudu, unisaidie nijisahau kabisa
           ili nikukazie wewe bila ya kubadilika na kwa utulivu,
   kama kwamba roho yangu ingekuwa tayari katika uzima wa milele.
               Kisiwepo chochote cha kuvuruga amani yangu
      wala cha kunitoa nje yako, wewe usiyebadilika, uliye wangu;
        bali kila nukta nizidi kuzama katika vilindi vya fumbo lako!
                Tuliza roho yangu; uifanye iwe uwingu wako,
      makao yako unayoyapenda zaidi na mahali pa pumziko lako.
        Humo nisikuache kamwe peke yako; bali niwemo mzima,
               mwenye kukesha na kutenda kwa imani yangu,
                      mwenye kuzama katika kuabudu,
        mwenye kujiachilia kikamilifu kwa utendaji wako Muumba.
          Ee Kristo mpendwa wangu, uliyesulubiwa kwa upendo,
                    nataka kuwa bibiarusi wa moyo wako,
                          nataka kukujaza utukufu,
                  nataka kukupenda hadi kufa kwa upendo!
  Lakini nahisi unyonge wangu wote: hivyo nakuomba uwe vazi langu,
     ulinganishe matendo yote ya roho yangu na yale ya roho yako,
               unizamishe ndani mwako, uenee ndani yangu,
  ushike nafasi yangu, ili maisha yangu yake kioo cha maisha yako tu.
                Njoo ndani mwangu ili uabudu, ufidie, uokoe.
                 Ee Neno wa milele, Neno wa Mungu wangu,
                 nataka kutumia maisha yangu kukusikiliza,
            nataka kuwa msikivu kabisa kwa mafundisho yako,


                       nijifunze yote kwako,
  halafu katika usiku wa roho, katika utupu, katika unyonge
                 nataka kukukazia macho daima
             na kubaki chini ya uangavu wako mkuu.
                  Ee nyota yangu ninayoiabudu,
  unichanganye hata nisiweze tena kukwepa mng’ao wako.
Ee moto unaoteketeza, Roho wa upendo, ushuke ndani yangu
   ili katika roho yangu itokee aina ya umwilisho wa Neno!
          Niwe kwake mwendelezo wa ubinadamu wake
           ambapo aweze kutekeleza upya fumbo lake.
       Nawe Baba uniinamie mimi kiumbe chako maskini,
 unifunike kwa kivuli chako, usione ndani yangu kitu kingine
       isipokuwa mpenzi wako uliyependezwa naye sana.
           Enyi watatu wangu, yote yangu, heri yangu,
 upweke usio na mipaka, upana ambao napotea ndani yake,
                 najiachilia kwenu kama mateka.
      Mzame ndani mwangu ili nami nizame ndani mwenu,
  wakati ninapongojea kuja kutazama katika mwanga wenu
                      kilindi cha ukuu wenu.
M.H. CHARLES DE FOUCALD (1858-1916)
 Baba yangu, najiaminisha kwako; unifanyie unavyopenda wewe;
        kwa chochote utakachonitendea, nakushukuru tu.
            Niko tayari kwa lolote; nakubali yoyote,
          mradi matakwa yako yatimizwe ndani yangu
                  na katika viumbe vyako vyote.
              Sitamani kitu kingine, Mungu wangu.
Naweka roho yangu mikononi mwako; naitoa kwako, Mungu wangu,
    kwa upendo wote wa moyo wangu, kwa kuwa nakupenda.
           Basi, kwangu ni sharti la upendo kujitolea,
            kujitia mikononi mwako, pasipo kipimo,
                 ila kwa tumaini lisilo na mipaka,
             kwa sababu wewe ndiwe Baba yangu.
MT. MASIMILIANO MARIA KOLBE (1894-1941)
       Wewe umenipenda milele, tangu u Mungu;
       hivyo umenipenda na utanipenda milele!...
 Upendo wako kwangu ulikuwepo hata kabla sijakuwepo,
na ni kwa sababu ya kunipenda, Mungu mwema, kwamba
    umeniita kutoka utovu wa vyote nianze kuwepo!
M.H. TERESA WA KOLKATA (1910-1997)
Baba yetu, mwanao nipo hapa, tayari kwako


 unitumie ili kuendelea kupenda ulimwengu kwa kuupatia Yesu
na, kwa njia yangu, kumtoa kwa kila mmoja na kwa ulimwengu.
     Ee Bwana, utufanye tustahili kutumikia watu wenzetu
ambao ulimwenguni kote wanaishi na kufa kwa ufukara na njaa.
     Kwa mikono yetu uwape leo mkate wao wa kila siku;
 na kwa upendo wetu wenye kuelewa uwape amani na furaha.
   Ee Bwana wangu, nakupenda,
       Mungu wangu, najuta,
     Mungu wangu, nakuamini,
    Mungu wangu, nakutumainia.
Utusaidie kupendana unavyotupenda.
          Bwana Yesu, wewe ambaye uliumba kwa upendo,
ulizaliwa kwa upendo, ulitumikia kwa upendo, ulitenda kwa upendo,
          uliheshimiwa kwa upendo, uliteseka kwa upendo,
               ulikufa kwa upendo, ulifufuka kwa upendo,
 nakushukuru kwa upendo wako kwangu na kwa ulimwengu wote,
        na kila siku nakuomba: unifundishe mimi pia kupenda!
                                Amina.
YOHANE PAULO II (1920-2005)
          Ee Kristo, kichwa na mwokozi pekee,
            uvute kwako viungo vyako vyote.
   Uwaunganishe na kuwageuza katika upendo wako,
    ili Kanisa ling’ae kwa ule uzuri upitao maumbile
unaodhihirishwa katika watakatifu wa kila wakati na taifa,
        katika wafiadini, waungamadini, mabikira
          na mashahidi wasiohesabika wa Injili!
             Ee Yesu mtamu, Yesu mwema,
                  Yesu, mwana wa Maria!
                          Amina!

ITAENDELEA...............

Comments