  | 
| Na Mch. Maximillian Machumu | 
Waamuzi
 15:9-16: Samson alikuwa mnadhiri wa Mungu na aliwekwa kuwaangamiza 
wafilisti, kwasababu ya kuwaangamiza Wafilisti ndugu zake wakaamua 
kumfunga na kumkabidhi kwa wafilisti ili wasije kulipa kisasi kwa wao. 
Katika kumfunga Samsoni, ndugu zake wapatao elfu tatu walitumia kamba 
mbili; kuna mambo mengi ya kujifunza kupitia habari hii 
KWANINI
 NDUGU WALIMFUNGA: kama tulivyosoma katika kitabu cha Waamuzi 15:9-16, 
ndugu zake ndio waliohusika kumfunga Samsoni. Hapa tunajifunza kuwa mara
 nyingi adui (shetani) anapotaka kumfunga mtu hupitia kwa watu wake au 
wanaomjua mtu huyo vizuri. Kifungo kinachotokana na watu wako wa karibu 
ni kibaya zaidi kwasababu wanaujua udhaifu wako; muda gani unaomba na 
muda gani huombi. 
Ndio maana hata Mtume Paulo aliwahi 
kutegeshewa nyoka kwenye kuni (Matendo ya Mitume 28:3). Nyoka ni yule 
mtu wa karibu anayejua siri na mambo unayoyafanya, kwasababu hiyo 
inakuwa rahisi kwa shetani kuwatumia kukuangamiza. Nyoka hakuonekana 
mwanzoni kwa Paulo kwasababu alijifanya kama kuni, na watu wa karibu ni 
vivyohivyo huwezi kuwatambua kwa urahisi. Furaha ni kuwa Mungu 
hakuruhusu yule nyoka kumwangamiza Mtume Paulo.
KWANINI 
WALITUMIA KAMBA MBILI: Ndugu wa Samsoni walikuwa elfu tatu lakini jambo 
la ajabu ni kuwa walibeba kamba mbili tu; Utajiuliza nini siri ya hizi 
kamba mbili?. Yesu mwenyewe aliainisha kamba mbili kuu ambazo shetani 
anazitumia kuwaangamiza na kuwafunga watu duniani. Ukisoma katika Ufunuo
 1:18 “na aliye hai; nami nalikuwa nimekufa, na tazama, ni hai hata 
milele na milele. Nami ninazo funguo za mauti, na za kuzimu.” Kumbe zile
 kamba mbili zina maana ya mauti na kuzimu. Kuzimu inaleta magonjwa na 
matatizo mbalimbali lakini mauti inaleta kifo. Kamba mbili mpya ni mauti
 na kuzimu. Kwa kuzimu na mauti shetani amekuwa akiwaangamiza na 
kuwatesa watu wa Mungu. Inawezekana na wewe ni mmoja wa watu wanaoteseka
 kwasababu ya kamba hizi leo kuna habari njema kuwa Yesu aweza kukata 
kamba hizo.
MATOKEO YA KIFUNGO CHA SAMSONI: baada ya 
kumfunga, ndugu zake wakamkabidhisha kwa wafilisti yaani adui zake. 
Jambo la ajabu likatokea, mara baada ya kukabidhiwa. Imeandikwa, 
“Alipofika Lehi, Wafilisti wakapiga kelele walipokutana naye; ndipo roho
 ya Bwana ikamjia kwa nguvu, na zile kamba zilizokuwa juu ya mikono yake
 zikawa kama kitani iliyoteketezwa kwa moto, na vile vifungo vyake 
vikaanguka mikononi mwake.” Waamuzi 15:14 kupitia kifungo kile Mungu 
akamtumia Samsoni kuwaangamiza wafilisti wote. Kumbe waweza upo katika 
kifungo ambacho Mungu alikiruhusu ili upate ushindi ulio mkamilifu.
MUNGU
 ANAWEZA KUKATA KAMBA ZILIZO KATIKA MAISHA YAKO: Wachawi na waganga 
wanaweza kuwa wajanja mbele ya macho yetu lakini Bwana anawaona, na 
kamba zao zinaonekana mbele ya macho ya BWANA. Hata mfalme Daudi aliwahi
 kuwa katika kamba hizo ukisoma katika Zaburi 119:61 “Kamba za wasio 
haki zimenifunga, Sikuisahau sheria yako.” Upo uwezekano wa mtu 
kufungwa, Mwilini unajiona ni mtu asiye na mafanikio au asiye na 
mwelekeo lakini rohoni unakuwa umefungwa na kamba kabisa. Zaburi 
18:1->…  “…Kamba za mauti zilinizunguka, Mafuriko ya uovu yakanitia 
hofu. Kamba za kuzimu zilinizunguka, Mitego ya mauti ikanikabili. Katika
 shida yangu nalimwita Bwana, Na kumlalamikia Mungu wangu. Akaisikia 
sauti yangu hekaluni mwake, Kilio changu kikaingia masikioni mwake…” 
Mungu anaweza kukutoa katika kamba za matatizo unayopitia. Daudi 
alipokuwa katika kamba hizo aliliitia jina la BWANA.
Yesu
 alipofufuka akatangaza kuwa anazo funguo za mauti na kuzimu, Hata kama 
aliyekufunga awe mtu wa karibu kiasi gani lakini zipo funguo za kufungua
 kamba zilizokufunga. Kama alivyofanya kwa Samsoni; baada ya kukufungua 
kinachofuata ni kipigo kwa wale wote walioshiriki kukufunga. Mungu 
anaweza kukutofautisha; shida na mateso yote unayopitia si kitu mbele za
 Mungu wetu kwasababu yeye anaweza kukuweka huru. Mpokee Yesu upate 
uhuru mkamilifu, kwasababu dunia ya leo haipo salama kama haupo ndani ya
 Yesu. 
 
Comments