Na Nabii Samson Mboya Kutoka mkoani Geita 0756 809209 |
VIPENGELE VYAKE
( 1 ). KAZI TULIYOPEWA WATU TULIOOKOLEWA
( 2 ). UINJILISTI NI NINI?
( 3 ). NANI ANAHUSIKA NA UINJILISTI?
( 4 ). FURAHA YA MUNGU KWA WATENDAKAZI
( 1 ). KAZI TULIOPEWA WATU TULIOOKOLEWA
Siku chache kabla ya Yesu Kristo kupaa mbinguni, alitukabidhi kazi ya
muhimu sana ya kufanya. Kazi hiyo, ni kuenenda ulimwenguni mwote na
kuhubiri Injili kwa kila kiumbe, na kuwafanya mataifa au watu
wasiookolewa, kuwa wanafunzi wa Yesu, na kuwafundisha kuyashika yote
tuliyoamuriwa, baada ya wanafunzi hao kubatizwa kwa jina la Baba na
Mwana na Roho Mtakatifu. Akasema kwamba, tukishiriki kufanya kazi hii,
atakuwa pamoja nasi siku zote, hata ukamilifu wa dahari hata wakati
atakaporudi tena ( MARKO 16:15; MATHAYO 28:19-20 ). Hili ni Agizo Kuu la
Yesu Kristo kwetu. Wengi wetu tuliookolewa, hatumwoni Yesu Kristo akiwa
pamoja nasi siku zote, kwa sababu hatushiriki kikamilifu kuifanya kazi
aliyotupa Yesu katika Agizo Kuu hili. Kufanya kazi hii, ni kufanya kazi
ya Uinjilisti.. Hili sasa, linatuleta katika kipengele cha pili cha somo
letu.
( 2 ). UINJILISTI NI NINI?
Uinjilisti ni uvuvi wa watu ( MATHAYO 4:19 ). Kwa kuzaliwa na
kutenda, watu wote ni wenye dhambi na hivyo, wamekwisha kuhukumiwa na
kutupwa katika ziwa la moto. Uinjilisti, sasa, ni kuwapelekea watu hawa
habari njema yaani Injili, kwa kuwahubiria kwamba, yeyote kati yao
atakayemwamini Yesu, atasamehewa hukumu aliyokwisha kupata ya moto wa
milele. Tukifanikiwa kuwafanya watu hawa watoke katika ziwa hilo la
moto, kwa kufanya hivyo tumewavua kutoka ziwani, kama kuwavua samaki (
YOHANA 3:18, 36; UFUNUO 21:8; YUDA 1:22-23 )
. Hata hivyo,Uinjilisti hauishii hapo. Kama vile mvuvi wa samaki
asivyowaacha samaki wake aliowavua kwenye ufuo wa bahari au ziwa,
mahali ambapo wataoza, basi huwachukua mara moja na kuwahifadhi vizuri;
au kama mvuvi huyo wa samaki, asivyowaacha samaki wake kwenye ufuo wa
ziwa na wakatembea hapo, mwisho wakarudi ziwani, vivyo hivyo, Uinjilisti
au uvuvi wa watu, unakamilika kwa kuhakikisha wale waliokata shauri
kumwamini Yesu na kuokolewa, wanaendelea Kanisani au nyumbani mwa Bwana,
mahali ambapo watajifunza mafundisho ya mitume na kuukulia wokovu (
LUKA 14:23; YOHANA 15:16; MATENDO 2:41-42; 28:30-31; WAGALATIA 4:9-11,
19-20 ).
( 3 ). NANI ANAHUSIKA NA UINJILISTI?
Watu wengine, kwa kukosa mafundisho, wanafikiri kwamba kazi ya
uinjilisti, inafanywa tu na Wainjilisti, Wachungaji, Walimu au Mitume na
Manabii waliowekwa na Mungu maalum kwa kazi hiyo na kupewa karama
mbalimbali. Hii ni mbinu ya Shetani ya kufanya kazi hii ifanyike kwa
viwango vya chini, ili yeye afurahi kuona wengi wanaangamia.
Wainjilisti, Wachungaji, Walimu, au Mitumne na Manabii; ni Makomanda au
viongozi wa Jeshi, na watu wengine waliookoka ni askari wa jeshi hili la
Kristo Yesu ( 2 TIMOTHEO 2:3 ). Je, ni jeshi gani la nchi yoyote
linaloweza kushinda ikiwa watakaopigana ni makomanda wa jeshi hilo tu na
askari wengine hawashiriki kupigana? Jeshi la namna hiyo, ni lazima
litashindwa vibaya. Askari wa kawaida, ndiyo wengi sana na katika nchi
yetu,
Tanzania, wanaitwa wapiganaji, maana bila wao, makamanda hawawezi
kufanya kazi hiyo wenyewe. Kazi ya makomanda ni kuwa mstari wa mbele wa
mapigano, na kuwaongoza maaskari wengine kuleta ushindi.Hivi ndivyo
walivyofanya Kanisa la kwanza. Uinjilisti, haukuachwa kwa Mitume tu,
pamoja na karama walizokuwa nazo; bali wote, wanaume na wanawake katika
Kanisa la kwanza walishiriki katika kufanya Uinjilisti ( MATENDO 2:17-18
).. Hata pale ambapo mitume walibaki Yerusalemu, wengine wote katika
Kanisa, walitawanyika nakwenda kulihubiri Neno. Ndiyo maana, Kanisa la
Kwanza, liliupindua ulimwengu wa nyakati zao ( MATENDO 8:1, 4 ).
Mafundisho mengine ya Biblia, pia yanaoana na jambo hili. Kila mtu
aliyeokoka, amefanywa kuwa mfalme na kuhani ( UFUNUO 5:9-10; UFUNUO
1:5-6 ).Utukufu wa Mfalme ni wingi wa watu wake, na uchache wa watu wake
ni uharibifu wake ( MITHALI 14:28 ). Mtu ambaye hana hata mtu mmoja
katika milki yake, hawezi kudai kwamba ni mfalme. Mfalme wa nani? Mfalme
wa hewa? Vivyo hivyo, mtu aliyeokoka ambaye hana mtu yeyote katika
milki yake aliyempata kwa uinjilisti, huyu ni mfalme wa hewa.
Kazi ya Kuhani pia, ni kumpatanisha mtu aliyetenda dhambi, na Mungu
wake, kwa kumfanya mtu yule kupata msamaha wa dhambi kutoka kwa Mungu
(MAMBO YA WALAWI 6:1-2, 6-7 ). Kwa misingi hiyohiyo, kila mtu
aliyeokoka, kwa kufanywa Kuhani; amepewa na Yesu Kristo, huduma ya
upatanisho, kuwapatanisha wenye dhambi pamoja na Mungu wao ( 2
WAKORINTHO 5:17-18 ). Kama Kristo alivyotumwa na Baba, anatutuma sisi
pia kufanya huduma ya upatanisho. Tusipofanya uinjilisti kwa wenye
dhambi, tunawafungia katika dhambi. Tukiwa wavuvi wa watu, tunafanya
watu hao waondolewe dhambi, maana watamwitaje Yesu bila kumsikia mtu
akiwahubiri? ( YOHANA 20:21, 23; WARUMI 10:13-14 ). Tukiwafungia watu
katika dhambi kwa kuacha kufanya uinjilisti, tunamuwekea Mungu moshi
machoni pake na kumfanya atoe machozi, na vile vile tunampa siki anywe
na kumfanya apate ganzi kwenye meno. Siyo vema kwetu kumfanyia hivyo
Mungu ikiwa kweli tumeokolewa ( MITHALI 10:26 )
( 4 ). FURAHA YA MUNGU KWA WATENDAKAZI
Hakuna lolote tunaloweza kulifanya kwa Mungu na kumfurahisha,
kama kuwa watenda kazi wanaofanya Uinjilisti, kwa kuwaleta watu kwa
Yesu, na kuwalea katika uchanga wao kiroho, mpaka waukulie wokovu. Kila
mtu aliyeokoka, angependa na kufurahi kuwa Mtendakazi, kama angejua ni
kwa kiasi gani Mungu katika Utatu (Baba, Mwana na Roho Mtakatifu)
anavyomfurahia mtendakazi mmoja anayefanya kazi ya uinjilisti. Ili
tufahamu furaha ya Mungu kwa watendakazi ni muhimu tujifunze Mungu ni
nani kwetu tuliookoka, na sisi ni akina kwake:-
1.
1. Mungu Baba ni Mkulima (YOHANA 15:1)-Mkulima anapopita kwenye
shamba liwe la migomba, mikahawa, michungwa, mipapai, minazi n.,
hufurahia sana kuona tawi linalozaa na kulishughulikia sana. Tawi
lisilozaa, huliondoa na kulitupa motoni (YOHANA 15:2). Mkulima akiona
tawi la migomba lililozaa mkungu na ndizi nzuri, atalitembelea tawi hilo
wakati wote, na kuweka mti ili kulikinga tawi hilo na upepo n.k. Ndivyo
alivyo Mungu kwa mtendakazi wake.
2. Mungu ni Bwana wa Majeshi (YAKOBO 5:4)-Amiri Jeshi Mkuu,
huwafurahia mno askari wapiganaji hodari ambao wanaufanya ufalme wake
kukua na kulindwa. Hawa humpa nguvu na sifa, hivyo huwatunuku medali
maalum za kitaifa. Ndivyo alivyo Mungu kwa watendakazi wake.
3. Mungu ni mwenye mali - Mungu anafananishwa na mtu mwenye
mali aliyesafiri ambaye amewaachia watumwa wake mali ili waifanyie
biashara na kupata faida. Mtu mwenye mali wa namna hii akirudi,
atamfurahia sana mtumwa yule aliyepeta faida kuliko yule aliyeificha tu,
na hakuzalisha chochote (MATHAYO 25:14-30). Ndivyo alivyo Mungu kwa
mtendakazi wake.
4. Yesu ni Mfanyabiashara mwenye vyombo vya uvuvi-
Mfanyabiashara mwenye vyombo vingi vya uvuvi, huajiri wavuvi na kuwapa
vyombo vya uvuvi. Wanaporudi kutoka katika uvuvi, humfurahia sana yule
aliyeleta samaki wengi na kumpenda mno. Asiyeleta samaki, ana hatari ya
kunyang’anywa chombo na asipewe tena. Ndivyo alivyo Yesu kwa mtendakazi
wake aliye mvuvi wa watu (MATHAYO 4:19).
5. Yesu ni Mfugaji mwenye zizi la Kondoo –Baada ya kupotea
Kondoo wengi katika zizi lake, anawatuma watu kuwatafuta. Atamfurahia
mtendakazi atakayerudi na Kondoo wake wengi waliopotea (LIKA 15:3-7)
6. Mungu ni mume wetu (YEREMIA 3;14)- Mume humfurahia sana mke
anayezaa sana na kuwalea vizuri wanae. Asipozaa, upendo kati yao huingia
dosari, na ndoa huingia mashakani ikiwa ni mataifa. Ndivyo alivyo Mungu
kwa mtendakazi wake.
7. Yesu ni Mpanzi wa Mbegu (MARKO 4:3)- Hakuna linalomfurahisha
Mpanzi kama mbegu ile iliyotoa mazao mengi. Baada tu ya kupanda, mpanzi
huanza kuangalia mbegu itakayoota na kutoa mazao mengi. Hiyo huipenda
mno. Ndivyo alivyo Yesu kwa mtendakazi wake.
8. Yesu ni Mwalimu (YOHANA 13:13)- Mwalimu humfurahia sana
mwanafunzi wake anayefanya kama yeye mwenyewe kutokana na jinsi
alivyomfundisha. Ikiwa mwalimu anamfundisha mtu udereva lakini mtu yule
ni mzito wa kufanya kama mwalimu wake, hapendezi kwake. Mtendakazi
anayefanya Uinjilisti kama mwalimu wake Yesu, anamfurahisha mno.
9. Roho Mtakatifu ni Bwana wa mavuno – Anamfurahia sana mtu
yule anayevuna roho za
watu na kuzileta ghalani mwake, kuliko yule anayeacha mavuno yaozee
shambani (MATHAYO 9:38; MATENDO 13:2; YOHANA 4:35-36).
10. Mungu ni Baba kwetu (MATHAYO 6:8-9) –Baba yeyote, hufurahi sana
kuona watoto wa mtoto
wake. Mungu pia hufurahi kuona watoto wa mtendakazi.
Kwa sababu Mungu
anamfurahia mtendakazi:-
( a ). Uwezo wa majibu ya maombi yake huongezeka (YOHANA 15:16)
( b ). Atang’aa kama nyota milel (DANIELI 12:3).
( c ). Watoto wa mtendakazi humuongezea Ushindi juu ya Shetani (ZABURI
127:4-5)
( d ). Watoto hao watakuwa ni taji ya kujionea fahari, furaha na utukufu
wake wakati wa kuja kwa Yesu (1 WATHESALONIKE 2:19-20)
JE UNAPENDA KUINGIA MBINGUNI ?
Ni sifa ipi ya kutuwezesha kuingia mbinguni?
Ni utakatifu (WAEBRANIA
12:14). Ndani yake hakitaingia kamwe chochote kilicho kinyonge (UFUNUO
WA YOHANA 21:27).
Kinyonge ni kipi?
Ni yule anayetenda dhambi. Huyu
ni mtu asiyefaa, ni mnyonge!
Je, wewe ni mtakatifu?
Jibu ni la!
Maisha yako yamejaa dhambi, pamoja na kusema una dini; hivyo wewe pia ni
mnyonge, hufai kuingia mbinguni. Ukitubu leo dhambi zako zote kwa
kumaanisha kuziacha, na kuifuata njia ya Yesu Kristo, ndipo utakapopata
rehema ya kuingia mbinguni (MITHALI 28:13; YOHANA 14:6).
Je, uko
tayari kutubu sasa ili upate rehema hii?
Najua uko tayari. Basi
fuatisha sala hii ya toba kwa dhati kutoka moyoni;
“
Hitimisho:
………………………………………………………………………………………………………………….
Mungu Baba asante kwa ujumbe huu. Hakika mimi ni mnyonge, mwenye
dhambi. Sistahili kuingia mbinguni. Natubu dhambi zangu zote kwa
kumaanisha kuziacha. Kuanzia leo nataka niifuate njia ya Yesu Kristo.
Bwana Yesu niwezeshe. Asante kwa kunisikia katika Jina la Yesu. Amen”.
Mpendwa msomaji umekubaliwa kuingia mbinguni. Ili uzidi kudumu katika
utakatifu mpaka siku ya kuiaga dunia hii, hakikisha unahudhuria
mafundisho katika Kanisa linalohubiri wokovu.
Comments