KWANINI SI RAHISI KUTENDA MEMA?


Kwa Nini Si Rahisi Kutenda Mema?

SAULI alipofanya mabaya, ni nani aliyefurahi?— Ni Shetani Ibilisi. Hata viongozi wa dini ya Wayahudi walifurahi pia. Kisha Sauli alipogeuka na kuwa mwanafunzi wa Mwalimu Mkuu na kuitwa Paulo, viongozi hao wa dini walianza kumchukia. Kwa hiyo unaelewa kwa nini si rahisi mwanafunzi wa Yesu kutenda mema?—

Wakati mmoja kuhani mkuu Anania aliwaambia watu wampige Paulo usoni. Anania hata alijaribu kumfunga Paulo gerezani. Paulo aliteswa sana alipogeuka na kuwa mwanafunzi wa Yesu. Kwa mfano, watu wabaya walijaribu kumwua Paulo kwa kumpiga kwa mawe makubwa.—Matendo 23:1, 2; 2 Wakorintho 11:24, 25.

Watu wengi watajaribu kutufanya tutende mambo yanayomchukiza Mungu. Kwa hiyo swali ni: Unapenda mema kwa kadiri gani? Je, unapenda mema sana hivi kwamba utayatenda hata kama wengine watakuchukia? Unahitaji ujasiri kufanya hivyo, sivyo?—

Lakini labda unajiuliza, ‘Kwa nini watu watuchukie kwa kufanya mema? Je, hawapaswi kufurahi badala yake?’ Inafaa iwe hivyo. Mara nyingi watu walimpenda Yesu kwa sababu ya mambo mazuri aliyoyafanya. Wakati mmoja watu wote mjini walikusanyika mlangoni mwa nyumba ambayo Yesu alikuwa anakaa. Walikuja kwa sababu Yesu aliwaponya wagonjwa.—Marko 1:33.

Lakini wakati mwingine watu hawakupenda mambo ambayo Yesu alifundisha. Ijapokuwa alifundisha yaliyo kweli, watu wengine hawakupenda mafundisho hayo. Wengine hata walimchukia sana kwa sababu ya kusema mambo ya kweli. Ilikuwa hivyo siku moja huko Nazareti, ambako Yesu alilelewa. Aliingia ndani ya sinagogi, mahali ambapo Wayahudi walikuwa wanakutania ili kumwabudu Mungu.

Yesu akatoa hotuba nzuri kutoka kwa Maandiko akiwa huko. Mwanzoni, watu walipenda sana hotuba hiyo. Wakastaajabia maneno mazuri aliyoyasema. Hata hawakuamini kwamba huyo ni yule kijana ambaye amekulia jijini mwao.

Lakini Yesu akasema jambo jingine. Akataja wakati ambapo Mungu aliwapendelea watu ambao hawakuwa Wayahudi. Yesu aliposema hivyo, wale waliokuwa katika sinagogi wakakasirika. Unajua sababu?— Walifikiri kwamba ni wao tu ndio wanaopendelewa na Mungu. Walifikiri kwamba wao ni bora kuliko watu wengine. Kwa hiyo wakamchukia Yesu kwa kusema hivyo. Unajua walijaribu kumfanyia nini?—

Biblia inasema: ‘Walimshika Yesu na kuharakisha kumtoa nje ya jiji. Wakampeleka hadi ukingo wa mlima ili wamwangushe chini na kumwua! Lakini Yesu akapita katikati yao na kwenda zake.’—Luka 4:16-30.

Kama hali hiyo ingekupata, je, ungethubutu kurudi na kuzungumza na watu hao kumhusu Mungu?— Ungehitaji ujasiri kufanya hivyo, sivyo?— Hata hivyo, baada ya mwaka mmoja hivi, Yesu alirudi Nazareti. Biblia inasema: “Akaanza kuwafundisha katika sinagogi lao.” Yesu hakuacha kusema kweli eti kwa sababu ya kuwaogopa wanadamu ambao hawakumpenda Mungu.—Mathayo 13:54.

Siku nyingine wakati wa sabato, Yesu alikuwa mahali fulani na pakawa na mtu mwenye mkono uliokuwa umenyauka au kulemaa. Yesu alikuwa na nguvu za Mungu za kumponya mtu huyo. Lakini baadhi ya watu waliokuwapo walijaribu kumfadhaisha Yesu. Mwalimu Mkuu angefanya nini?— Kwanza akauliza: ‘Kama ungekuwa na kondoo mmoja naye aanguke ndani ya shimo siku ya Sabato, je, ungemwondoa shimoni?’

Bila shaka, wangemwondoa kondoo shimoni hata kama ni siku ya Sabato, siku ambayo walipaswa kupumzika. Basi Yesu akasema: ‘Ni bora kumsaidia mtu siku ya Sabato, kwa sababu mtu ni bora kuliko kondoo!’ Ilikuwa wazi kwamba Yesu alihitaji kumsaidia mtu huyo kwa kumponya.

Basi Yesu akamwambia mtu huyo anyoshe mkono wake. Mara tu mkono wake ukaponywa. Mtu huyo alifurahi sana. Lakini namna gani wale watu wengine? Je, walifurahi?— La. Wakamchukia Yesu hata zaidi. Wakatoka nje na kufanya mipango ili wamwue!—Mathayo 12:9-14.

Hivyo ndivyo ilivyo leo. Hata tufanye nini, hatuwezi kuwapendeza watu wote. Kwa hiyo ni lazima tuamue ni nani tunayetaka kumpendeza hasa. Ikiwa ni Yehova Mungu na Mwanaye, Yesu Kristo, basi ni lazima kila wakati tufanye vile wanavyotufundisha. Lakini tukifanya hivyo ni nani atakayetuchukia? Ni nani atakayefanya iwe vigumu kwetu kufanya yaliyo mema?—

Shetani Ibilisi atatuchukia. Lakini ni nani mwingine atakayetuchukia?— Ni wale ambao wamedanganywa na Ibilisi kuamini uwongo. Yesu aliwaambia viongozi wa dini wa siku zake hivi: “Ninyi mmetoka kwa baba yenu Ibilisi, nanyi mnataka kufanya tamaa za baba yenu.”—Yohana 8:44.

Kuna watu wengi wanaopendwa na Ibilisi. Yesu anawaita “ulimwengu.” Unafikiri “ulimwengu” ambao Yesu anazungumzia ni nini?— Hebu tuone Yohana sura ya 15, mstari wa 19. Hapo tunasoma maneno haya ya Yesu: ‘Kama mngekuwa sehemu ya ulimwengu, ulimwengu ungependa sana kilicho chake. Sasa kwa sababu ninyi si sehemu ya ulimwengu, bali nimewachagua ninyi kutoka ulimwenguni, ulimwengu unawachukia ninyi.’

Kwa hiyo, ulimwengu ambao unawachukia wanafunzi wa Yesu unatia ndani wale wote wasiokuwa wanafunzi wake. Kwa nini ulimwengu unawachukia wanafunzi wa Yesu?— Fikiria jambo hilo. Ni nani mtawala wa ulimwengu huu?— Biblia inasema: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” Mwovu huyo ni Shetani Ibilisi.—1 Yohana 5:19.

Unaona sasa ni kwa nini si rahisi sana kutenda mema?— Shetani na ulimwengu wake wanafanya iwe vigumu. Lakini kuna sababu nyingine. Unakumbuka ni sababu gani?— Katika Sura ya 23 ya kitabu hiki, tulijifunza kwamba sote tumerithi dhambi. Je, halitakuwa jambo zuri ajabu wakati dhambi, Ibilisi, na ulimwengu wake hautakuwapo?—

Biblia inaahidi: “Ulimwengu unapitilia mbali.” Hii inamaanisha kwamba wale wote ambao si wanafunzi wa Mwalimu Mkuu hawatakuwapo tena. Hawataruhusiwa kuishi milele. Je, unajua ni nani watakaoishi milele?— Biblia inaendelea kusema: “Yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yohana 2:17) Ndiyo, ni wale tu wanaofanya mema, wanaofanya “mapenzi ya Mungu,” ndio watakaoishi milele katika ulimwengu mpya wa Mungu. Kwa hiyo, hata kama si rahisi, tunataka kufanya mema, sivyo?—

Tusome pamoja maandiko haya yanayoonyesha ni kwa nini si rahisi kufanya yaliyo mema: Mathayo 7:13, 14; Luka 13:23, 24; na Matendo 14:21, 22.

Comments