MGANGA WA KIENYEJI AKABIDHI MKOBA WAKE WA UGANGA KANISANI

Mchungaji kiongozi Morogoro kanisa la Ufufuo na Uzima Dkt. Godson akimuuliza swali Amani kuhusu 'kioo' kilichokuwemo kwenye 'Mkoba' wake wa Uganga huku vitendea kazi vingine vikiendelea kupakuliwa ndani ya Mkoba wake.


UTANGULIZI WA MAISHA YA AMANI
Amani John Mtego, alizaliwa mwaka 1987, alisoma hadi darasa la nne tu na kuacha masomo. Ni kijana lakini pia ni mganga wa kienyeji aliyeianza kazi hii akiwa na miaka 8 tu. Kwake ni kijiji kiitwacho Kife (Gairo, Kilosa). Alipewa hii kazi / ‘mkoba’ huu na babu yake aliyeitwa Boto, (kwa sasa ni marehemu), aliyekuwa ni mganga wa kienyeji enzi hizo. Baba yake Amani ameoa wake watatu, na mama yake mzazi ni mke wa kwanza. Hata hivyo mama mzazi wa Amani hakupenda mwanae awe mganga wa kienyeji, ingawa baba mzazi alimruhusu, pengine kwa sababu mkoba ulitokea kwa babu. Hata hivyo babu huyu humtokea kwa njia ya ndoto na kumsihi Amani asiachane na hii kazi.

NINI KIMEMFANYA AMANI AWEPO HAPO KANISANI?

Ikumbukwe kuwa kwa wiki nzima hili ilikuwepo semina ikiendela hapa Nyumba ya Ufufuo na Uzima Morogoro yenye somo la “Kuzikata kamba ulizofungwa na ndugu zako wa karibu”. Jumapili hii katika kuhitimisha hii semina, Amani amejikuta anaingia hapa kanisani bila kujua akitokea maporini alikokuwa akifanyia uganga wake. Watu walipoitwa kuokoka, Amani alitoka mbele na ndipo nguvu za Mungu zilipomshinda na kujikuta anasalimisha ‘mkoba’ wake mara moja.

NDANI YA MKOBA KULIKUWA NA NINI?

Katika mkoba aliokuja nao Amani, zana / vitendea kazi vyake vya kuzimu vipatavyo 15 na Amani akaelezea kazi ya kimoja hadi kingine, ili ujue UDANGANYIFU WA SHETANI ulivyo, kama mganga huyu kijana alivyohojiwa na Information Ministry, Nyumba ya Ufufuo na Uzima Morogoro:-

1. KIBUYU CHA KWANZA (TUNGULI #1)

Baba (SNP Dr. Godson) akionesha Kibuyu cha kwanza
kilichokuwa kwenye 'mkoba' wa Amani kupata maelezo yake.
Mojawapo ya vitendea kazi alivyopewa na babu yake ni tunguli (kibuyu kilichofungwa kamba). Hiki





Mchungaji Dkt. Godson akionesha Kibuyu cha kwanza
kilichokuwa kwenye 'mkoba' wa Amani kupata maelezo yake.

kilikuwa na kazi ya ‘kuita watu’. Kibuyu hiki hutumiwa kuita watu kwa ‘kupiga miluzi’ ndani yake, na kuagulia watu makaburini. Amani anadai kuwa hawa wanaoitwa ni wale watu wa kawaida waliowahi kupotea kwao naye huwaita wakapatikana tena.

Swali: Je, aliwahi kuwaita na kuwarudisha watu wangapi?
Jibu: Watu waliowahi kurudi ni wawili tu anaokumbuka kwa kipindi chote hicho.

2. KIBUYU CHA PILI (TUNGULI #2)
Kibuyu cha pili kilikuwa maalumu kwa ajili ya mambo ya biashara kwa kuita wateja. Kwa namna gani? Amani alikuwa anatengeneza dawa iitwayo ‘mvuto wa wateja’. Huu ni mchanganyiko wa vitu vitatu: mafuta ya kula, mafuta ya kuku, na nyonyo. Mteja huenda na kuivukiza kwenye moto dawa hii dukani kwake au biasharani mwake nyakati za usiku.

Swali: Je, ipo rangi maalumu ya kuku wa kutengenezea dawa hii?
Jibu: Ndiyo. Mafuta ya kuku yanayofaa ni kuku weupe/ au wekundu. Kuku hawa ni sehemu ya sadaka za kuku ambazo Amani alikuwa akiletewa na wateja wake.

Swali: Je mteja angekuletea kuku mweusi ingekuwaje?
Jibu: Endapo akifanya hivyo sadaka yake itakataliwa kwa sababu mchanganyiko wa mafuta ya kuku weusi hutumika kuzuia wezi/ au majambazi wasivamie duka/ au biashara na siyo kuita wateja.

3. KIOO:
Amani alikuwa akitumia kioo maalumu (cha pembe 4) kwa ajili ya kumulika watu / wachawi na kubaini matatizo ya mteja wake hata kabla ya kutajiwa. Amani anasema alikuwa na uwezo wa kuona hata nyumbani kwa huyo mteja mambo yalivyo na kuwa rahisi kuagua. Hata hivyo mteja wake siyo rahisi kuona chochote kwenye hicho kioo hata angekodolea macho yote.


Vitendea kazi vya uganga wa Amani vikiwa vimewekwa chini ili matumizi yake yajulikane kala ya kuviunguza kwa moto.

4. KICHUPA CHENYE MZUNGUSHIO MWEUSI


Kifaa kilichozungushiwa kitu cheusi ubavuni.
Yalikuwemo 'Mafuta ya Binadamu' ndani ya kifaa/kichupa kimojawapo kilichozungushiwa kitu cheusi (hakina jina maalum).
Kazi ya haya mafuta ni kumpatia mteja / mtu mwenye ‘madeni sugu’ na endapo akikutana na wadeni wake hawatomdai tena (Tazama picha kulia).


Amani akifafanua matumizi ya kichupa chenye mzunguko mweusi.

5. CHUPA YA MAJI YA MAITI


Amani akielezea matumizi ya chupa yenye maji ya maiti
Chupa ilikuwa ya kuwekea maji ya maiti, alikuwa analetewa na wachawi ambayo hutumika kupandisha nyota baada ya kumpaka mteja usoni ili kuing’arisha nyota yake.

Kazi ingine ya haya maji ya maiti ni kwenye mahoteli, ambako huchanganywa na vyakula vya mahotelini hasa yale maarufu yanayouza sana vyakula na yenye kujaa wateja wengi sana mijini (Tazama picha kulia kuhusu chupa hii).


Uzi wa kushonea na sindano ikiwa kwa ndani
6. UZI NA SINDANO
Uzi wa sindano na sindano yake ni kwa ajili ya kushonea ‘subala’, ambalo ni hirizi analopewa mteja ili kuvaa kiunoni, kama chachandu kwenye mambo ya mapenzi.

7. USEMBE
Usembe ni kitu mithili ya unga ambayo huchanganywa na mafuta maalumu (mafuta ya kuku na yale ya kula). Huo unga hupewa wateja wakavukize kwenye maduka yao usiku.

8. NGUO YA NDANI YA MWANAMKE
Nguo ya ndani ya mwanamke (asiyefahamika) ilikuwepo kama 'kiwakilishi', ililetwa na mteja ili mke wake aliyeachana naye muda mrefu tu aweze tena kurudiana naye.

Swali: Sasa kama ndivyo kwa nini unabaki na hiyo nguo ya ndani wewe kama mganga?
Jibu: Amani anasema inabidi kufanya hivyo kwa sababu kiwakilishi kama hicho chaweza kutoweka wakati wowote kikiachwa mikononi mwa mteja wako bila huyo mteja kujua kilikoenda.


Nguo ya Ndani ya Mwanamke Iliyokuwemo kwenye Mkoba

9. GANDA LA KONOKONO
Ganda la konokono kazi yake hulitumia hupitisha juu ya kile kioo ili kufanya ‘searching’ ya wapi taarifa ya mteja inapopatikana kwa kutafutwa. Linafanya kazi mithili ya 'kitafutio' cha kwenye computer yaani ‘mouse’.


10. KIFUNIKO CHA TUNGULI
Hiki ni Kijiti kilichochongwa na kuwekewa sura ya binadamu na masikio yake: kazi yake ilikuwa ni kama mfuniko wa tunguli.

11. SUBALA
Subala kanguo kalikoshonwa, kenye pembe nne, na ndani kazi yake ipo kinga kutoka kwenye ule mkoba ili kumsaidia Amani aendelee tu kufanya kazi yake ya uganga.

12. SHATI KUU KUU LA MWANAUME / KANIKI

Shati Kuu kuu la Mwanaume, ndani ya Mkoba.
Hii nguo ya kiume (shati kuu kuu liililochanika), maarufu
kwa jina ‘kaniki’ alilipata kutoka kwa mmoja wa marehemu (mtu aliyekufa), na akawa analitumia kwa ajili ya kuwashonea watu wengine 'kinga' hasa wale watu wenye madeni makubwa ili hayo madeni yafutwe.


Amani anasema endapo kipande cha nguo hii kingeshonewa kwenye nguo ya binadamu yeyote wa kawaida, huyo mtu atatembelea ile nyota ya yule marehemu ambako nguo hii ilitokea, na maisha yake yanakuwa ya ‘mtu hai lakini sawa tu na marehemu’ (Tazama picha Kulia)


13. PEMBE YA DIGIDIGI
Pembe ya mnyama digidigi, ilikuwa inatumika wakati wa kutengeneza dawa. Kumbuka dawa zenyewe zilikuwa zikizichimbwa porini. Pembe hii huchomekwa katikati ya hizo dawa ili zifanye kazi iliyokusudiwa. Pembe hutumika kuzuia majambazi na kwenye biashara ya daladala kwa kuzuia ‘mabukula’ wasiweze kuiba pesa. Hii pembe nayo aliachiwa na babu yake.

14. MKIA WA KANUNGU-YEYE


Kanungu-yeye (hedgehog)
Kamkia ka kanungu yeye (hedgehog), kazi yake ni kulindia watu mahindi / au mazao yao mashambani (Picha ya mnyama huyu imewekwa hapa (kushoto) kwa ufafanuzi zaidi).

Ni kwamba baada ya mtu kupanda mahindi yake shambani, kamkia haka atakafukia katikati ya shamba lake. Kwa kitendo hiki mavuno yanakuwa mengi na kama wapo 'bukula' au ‘chuma ulete’ hawataweza kuiba mazao ya shamba hili.

Mkia wa Kanungu-yeye uliokutwa ndani ya Mkoba wa Amani

15. POCHI YA KIKE
Pochi ya kike (Tazama picha Kulia):
Kazi ya pochi hii ya kike ni kuwekea dawa tu na haikuwa na kazi maalumu zaidi ya hiyo.

NGUVU ZA BWANA YESU ZIMEKATA KAMBA ZILIZOMFUNGA AMANI

Amani amekiri kuwa aliwahi kuagulia watu 6 lakini masharti yakamshinda.

Swali: Masharti gani hayo?
Jibu: Zilikuwepo nguvu mbili zinazoshindana na Amani, nguvu ya Mungu itokanayo na maombi ya watu makanisani na nguvu ya ule mkoba. Kitendo cha kupishana / kushindwa nguvu na Mungu kilimfanya aikatae hiyo kazi.

Ndiyo maana Amani alikaa makaburini kwa siku 5 bila kula chakula chochote zaidi ya mizizi ya porini iitwayo ‘mkirika’ na ‘nyonyo’ kwa kipindi chote hiki.


Baada ya siku hizi alisikia sauti iliyokuwa ikimwita aende kanisani akaokoke, na kuachana na uganga. Alitembea kwa miguu kutokea huko kijijini Kife, na kujikuta amewasili hapa kwenye Nyumba ya Ufufuo na Uzima Morogoro na akajisalimisha. Nguo zake zote alizokuwa amezivaa anakiri kuwa zina mabaki na harufu ya 'mafuta ya binadamu'. Amani hajawahi kufika nyumbani kwa wazazi wake kwa zaidi ya mwaka mmoja hadi sasa, kwani uganga ameufanyia maporini tu kipindi chote hiki.


Vitendea kazi vya Mkoba wa uganga wa Aman, vikiwa jalalani muda mfupi kabla ya kuteketezwa kwa moto.

Kama unavyoona, mizigo hii ilimtesa sana kijana huyu Amani. Shetani amewadabgabya na kuwapotosha watu wengi sana. Lakini Yesu amemuokoa Amani leo 12/10/2014, Sifa, heshima na Utukufu Apewe Bwana Yesu aliyezikata kamba za Kuzimu zilizomzunguka Amani na kumweka huru. Imeandikwa "Mtaijua KWELI nayo KWELI itawaweka HURU". Amen

Ushuhuda huu kwa hisani ya blog ya kanisa la Ufufuo na Uzima Morogoro kwa ushirikiano na Gospel Kitaa

Comments