KIFUNGO CHA AKILI - Na: ADRIANO MAKAZI (RP)


Na RP Adriano  Ufufuo na Uzima Morogoro.
Utangulizi: Somo la leo linaitwa Kifungo cha Akili”. Mungu hata kabla ya kutuumba, alimpa kila mmoja wetu uwezo fulani wa kufanya mambo na kufikia mahali fulani alipokusudia Mungu. Kwa nini tuzungumzie habari za akili? Ni kwa sababu akili ni uwezo aliopewa mtu kufanya mambo yake vizuri na kwa haraka zaidi. Endapo akili ya mtu huyu itakuwa imefungwa au kuibiwa, uwezo wa mtu huyu lazima utapungua.

KUTOKA 35:30-35….[Kisha Musa akawaambia wana wa Israeli, Angalieni, Bwana amemwita kwa jina lake Bezaleli mwana wa Uri, mwana wa Huri, wa kabila ya Yuda; 31 naye amemjaza roho ya Mungu, katika hekima, na akili, na ujuzi, na kazi ya ustadi kila aina; 32 na kuvumbua kazi za werevu, na kufanya kazi ya dhahabu, na fedha, na shaba, 33 na kukata vito vya kutilia, na kuchora miti, atumike katika kazi za werevu kila aina.34 Naye amemtilia moyoni mwake ili apate kufundisha, yeye, na Oholiabu mwana wa Ahisamaki, wa kabila ya Dani. 35 Amewajaza watu hao akili za moyoni, ili watumike katika kazi kila aina, ya mwenye kuchora mawe, na kazi ya werevu, na ya mwenye kutia taraza, katika nyuzi za rangi ya samawi, na za rangi ya zambarau, na nyekundu, na kitani nzuri, na ya mwenye kufuma nguo; ya hao wafanyao kazi yo yote, na ya wenye kuvumbua kazi za werevu.]…. Kama tunavyojua, Mungu alimuandaa Musa kuwatoa wana wa Israeli kutoka Misri walikokuwa wanakaa kwa hali ya utumwa. Wanadamu tumeumbwa ili tumwabudu Bwana. Kazi kubwa kuliko  zote mbinguni ni ya kumwabudu Bwana. Hata shetani naye anataka sana kuabudiwa. Wakati wakiwa njiani jangwani, Mungu alitaka wana wa Israeli wawe wanamuabudu. Hata hivyo Musa hakuwa na ujuzi wa uandisi au ufundi wa ujenzi wa nyumba ya Bwana. Mungu akawa anamwambia Musa kuwa wapo  watu ambao wameshaandaliwa tayari na amewawekea akili ndani yao kwa hiyo kazi.
Kila mtu anatumwa kuja duniani kwa makusudi maalum. Imeandikwa katika YOHANA 1:6-7...[Palitokea mtu, ametumwa kutoka kwa Mungu, jina lake Yohana. 7 Huyo alikuja kwa ushuhuda, ili aishuhudie ile nuru, wote wapate kuamini kwa yeye.]…. Kwa hiyo Yohana tunaona hapa kusudio la kuja kwake duniani. Haipaswi kukaa hapa duniani kama mtalii.

Yamkini umepewa akili  uwe waziri  mkuu siku moja katika taifa hili. Lakini wajanja wachache wameichukua akili yako na leo hii  upo tu mtaani bila chochote cha kufanania na hiyo nafasi. Pengine umepewa akili ufanye biashara lakini leo hii huwezi chochote na wajanja wachache wanatumia akili yako kufanyia biashara zao. Mungu alimpa ‘akili’ Bezaleli mwana wa Uri, mwana wa Huri, wa kabila ya Yuda, ili  kumwezesha kufanya kazi ya werevu kujenga hema ya Bwana (KUTOKA 35:30-35). Kuna namna ya kutenda itokayo kwa Bwana na ambayo inakuwa tofauti na utendaji wa watu wengine. Hata katika uimbaji, siyo wote huvutia kwenye kuimba, bali wale ambao Bwana ameweka kitu cha tofauti ndani  mwao, utendaji wao huwa tofauti kabisa. Kama umepewa kazi na huna akili,  hutaweza kufanya hiyo kazi.

Showers of Glory - Bonde la Maono Morogoro wakimwimbia Bwana katika ibada ya  Jumapili iliyopita

Yamkini Mungu amekuwekea akili ya kuleta majibu  kwa mambo yaliyopo katika jamii yako. Katika Biblia,  2 SAMWELI 14:19-20….[Mfalme akasema, Je! Si mkono wa Yoabu ulio pamoja nawe katika haya yote? Mwanamke akajibu, akasema, Kama iishivyo roho yako, bwana wangu, mfalme, hapana mtu awezaye kugeuka kwa kuume, au kwa kushoto, kukana neno lo lote alilolisema bwana wangu mfalme; kwani mtumwa wako Yoabu ndiye aliyeniamuru, na kuyaweka maneno haya yote kinywani mwa mjakazi wako; 20 mtumwa wako Yoabu ameyatenda haya ili kubadili uso wa jambo hili; na bwana wangu anayo akili, kama akili ya malaika wa Mungu, hata ajue mambo yote ya duniani.]…. Yoabu alikuwa anajua siri mbalimbali za ufalme wa Daudi. Yoabu alimtumia huyu mama ili akabadili mawazo ya mfalme ili amwachie Absalomu urithi wa ufalme wake badala ya Sulemani. Mtu mwenye akili hawezi kuletewa mambo mlango wa nyuma naye akayakubali. Shetani huwa anatumia mtindo huu wa kugeuza akili za watu wafanye kinyume na makusudio ya Bwana. Jambo hili la Yoabu la kumjaza maneno huyu mwanamke hata hivyo lilishindikana.


MAOMBI
Kwa Jina la Yesu, Mungu akupe akili ya kuona mambo miaka mitano ijayo kwa Jina la Yesu. Mungu akupe akili ya kufanya mambo makuu kwa Jina la Yesu. Ninaamuru kwa Jina la Yesu, kila aliyekuja kwako amelishwa maneno,  ashindwe kwa Jina la Yesu. Amen



RP Adriano akiombea baadhi ya watu waliookoka kwa
kumpa shetani talaka ya kudumu jumapili iliyopita

Usikubali kuwa kituo cha kupokea kila neno mtaani  mwako. Watu wa aina hii, wenye kuja kwako wakiwa na maneno, usiwape sikio lako ili wasikuharibu. Kama Yesu angesikiliza yale watu wanayoongea juu yake, asingeweza kuhubiri. Ndiyo maana aliwauliza wanafunzi wake kule  nje watu wanasema yeye ni nani. Huko nje, watu walikuwa wanamwita Yesu ni nabii ajaye, wengine Eliya, wengine Yohana Mbatizaji. Lakini wanafunzi wake, wale wa ndani walikuwa wakimuita Yesu kuwa ni “Kristo,  mwana wa Mungu aliye Hai”. Ni vizuri sana uwe na Jina zuri kwa wale wa ndani. Kwa sababu, wale wa ndani wanakuita sawa na Mungu anavyokuita. Wakati wale wa nje wanakuita wewe ‘maskini’, Mungu anakuita tajiri.


MAOMBI
Baba Mungu wa Mbinguni, naomba unipe akili ya kujua jinsi ya kutenda katika Jina la Yesu. Amen



1 NYAKATI 12:32….[Na wa wana wa Isakari, watu wenye akili za kujua nyakati, kuyajua yawapasayo Israeli wayatende; vichwa vyao walikuwa watu mia mbili na ndugu zao wote walikuwa chini ya amri yao.]…. Hawa wana wa Isakari walikuwa na akili ya kujua mambo ya kufanywa kwa nyakati na majira yake na wana wote wa Isreali, na  Israeli  yote iliwategemea sana  hawa ili kufanikiwa.


Sehemu ya umati wa Majeshi ya Bwana waliokuwa wanafuatilia somo la leo 'Kifungo cha Akili' Bonde la Maono-Morogoro
1 NYAKATI 12:33-38…[Wa Zabuloni, watu wawezao kwenda pamoja na jeshi, hodari wa kupanga vita, wenye zana za vita za kila namna, hamsini elfu; askari wastadi wasiokuwa wenye moyo wa kusitasita. 34 Na wa Naftali, maakida elfu, na pamoja nao watu wenye ngao na mkuki thelathini na saba elfu. 35 Na wa Wadani, watu hodari wa kupanga vita, ishirini na nane elfu na mia sita. 36 Na wa Asheri, watu wawezao kwenda pamoja na jeshi, hodari wa kupanga vita, arobaini elfu. 37 Tena, ng'ambo ya pili ya Yordani, wa Wareubeni, na wa Wagadi, na wa nusu kabila ya Manase, wenye zana za vita za kupigania za kila namna, mia na ishirini elfu. 38 Hao wote, watu wa vita, askari wastadi, wakaja Hebroni wenye moyo mkamilifu, ili kumtawaza Daudi awe mfalme juu ya Israeli wote; tena wote waliosalia wa Israeli nao walikuwa na moyo mmoja kwamba wamtawaze Daudi.]… Mungu alipanga hizi idara kwa kazi maalumu iliyohitajika kwa wakati na majira yake. Yehoshafati alitanguliza waimbaji mbele ya jeshi lake, na akashinda vita. Kila mtu  kuna eneo la kufanyia kazi alilopewa na Bwana.


Ipo hatari kubwa sana ya kutoijua majira, na kinachoweza kumfanya mtu ayajue majira ni akili. Imeandikwa LUKA 19:40….[Alipofika karibu aliuona mji, akaulilia, 42 akisema, Laiti ungalijua, hata wewe katika siku hii, yapasayo amani! Lakini sasa yamefichwa machoni pako. 43 Kwa kuwa siku zitakuja, adui zako watakapokujengea boma, likuzunguke; watakuzingira na kukuhusuru pande zote; 44 watakuangusha chini wewe na watoto wako ndani yako, wasikuachie jiwe juu ya jiwe, kwa sababu hukutambua majira ya kujiliwa kwako.]….. Yesu Kristo kabla ya kuja duniani  alitabiriwa na manabii mbalimbali, Musa, Eliya, Isaya na hata Yohana Mbatizaji. Ilipaswa watu wazisome alama za nyakati kama ilivyoandikwa katika YOHANA 1:11-12…[Alikuja kwake, wala walio wake hawakumpokea. 12 Bali wote waliompokea aliwapa uwezo wa kufanyika watoto wa Mungu, ndio wale waliaminio jina lake;]… Msaada unaweza kuja lakini kwa kuwa hujui  majira, ukaukataa.  Wokovu unaaweza kuja lakini kama umefungwa akili, hutajua. Watu wengi hupenda kuziona ishara. Maandiko yanasema ‘wana heri wale wanaoamini bila kuona ishara’. Yamkini uliwahi kuwakataa watu kwa macho yako  kukudanganya, na sasa unajutia. Kuna watu leo hii unawaona wanapitia maisha yasiyo yao lakini kumbe Bwana anawatengeneza. Usipende sana kufurahia wale ambao wameshatengenezwa na wengine. Hata kama unayemuona leo hii awe ni kijana au binti hajavaa vizuri kama unavyotaka, bado unayo nafasi ya kuja kumtengeneza mbele ya safari ili apendeze au aonekane kama unavyotaka. Hata 'cake' hupitishwa kwenye 'oven' yenye moto  mkali kwanza na kuokwa kabla ya kuliwa, na ikeshatoka huko hupendwa na watu wote.


Majeshi ya Bwana yakifurahia  kwa shangwe Mafudisho ya Somo la "Kifungo cha Akili" jumapili iliyopita
Katika maisha ya ndoa, watu wenye akili katika ndoa zao wakigombana humalizana wao kwa wao humo ndani bila kuwaona washenga au wachungaji wao. Ukiona wale wanaopeleka mambo ya nyumbani kwao  nje ya nyumba zao ujue 'hao hawana akili'. Biblia inasema katika 1 PETRO 3:7… [‘Kadhalika ninyi waume, kaeni na wake zenu kwa akili; na kumpa mke heshima, kama chombo kisicho na nguvu; na kama warithi pamoja wa neema ya uzima, kusudi kuomba kwenu kusizuiliwe’]. Endapo mambo ya mwanaume hayaendi vizuri nyumbani au kazini kwake,  mume afaa kujua kuwa, mchawi wa kwanza ni mke wake. Maandiko yanaposema "kusudi kuomba kwenu kusizuiliwe" maana yake kama unaomba tenda, hiyo tenda isizuiliwe. Kama uunaomba ubunge, maana yake usizuiliwe. Kama unaomba biashara, maana yake isizuiliwe. Wamama mara nyingi wanakaa na vitu/mizigo mioyoni mwao hata kwa miaka mingi tu wakiishikilia. Matokeo yake uchungu na mambo wanayoweka mioyoni mwao huwaletea shida kiafya.


MAOMBI:
Bwana unirudishie akili yangu. Roho ya uchungu  roho ya kutopenda kusamehe niiachie kwa Jina la Yesu.  Naomba nguvu ya kusamehe kwa Jina la Yesu. Amen



Hakuna jambo gumu sana kama kusamehe. Mara zote, kila unapokumbuka jambo ulilotendewa na mtu fulani ni rahisi sana hali ya uchungu kujirudia. Neno la kuleta msaada kwako ni ‘kuachilia’. Unapomshikilia mtu moyoni mwako huyo  mtu hawezi kufanikiwa. Imeandikwa ‘laana isiyo na sababu haimpati mtu’, lakini kwa kuwa ipo sababu, kile ulichotamka kwa huyo mtu kinampata. Pengine uliwahi kutamka maneno au wewe kutamkiwa maneno na mtu maishani mwako, na matokeo yake hayo yaliyotamkwa yamekuwa yakiyadhuru maisha yako. Leo ni  siku ya maachilio. Lazima uachilie kwanza ili Mungu aweze kukusamehe.


'Huwezi Kupigana Ukiwa Umekaa Chini Namna hii',  ni
 maneno ya RP Adriano alipokuwa akifundisha mbinu za
kupigana na Wanaozifunga Akili, jumapili iliyopita
Katika Biblia imeandikwa MALAKI 3:13-17 …[Maneno yenu yamekuwa magumu juu yangu, asema Bwana. Lakini ninyi mwasema, Tumesema maneno juu yako kwa namna gani? 14 Mmesema, Kumtumikia Mungu hakuna faida; na, Tumepata faida gani kwa kuyashika maagizo yake, na kwa kwenda kwa huzuni mbele za Bwana wa majeshi? 15 Na sasa twasema ya kwamba wenye kiburi ndio walio heri; naam, watendao uovu ndio wajengwao; naam, wamjaribuo Mungu ndio waponywao. 16 Ndipo wale waliomcha Bwana waliposemezana wao kwa wao. Naye Bwana akasikiliza, akasikia; na kitabu cha ukumbusho kikaandikwa mbele zake, kwa ajili ya hao waliomcha Bwana, na kulitafakari jina lake. 17 Nao watakuwa wangu, asema Bwana wa majeshi, katika siku ile niifanyayo; naam, watakuwa hazina yangu hasa; nami nitawaachilia, kama vile mtu amwachiliavyo mwanawe mwenyewe amtumikiaye]… Kama Mungu anaweza kuachilia,  wewe ni  nani hata usiachilie? Kitu gani  kinakufanya usiachilie? Ukioa kila unalolifanya halifanikiwi ujue kuna mahali hapajakaa sawa. Kumbe mtu anaweza kumshikilia mwanae au  mke au mume wake‼! Kwa nini amshikilie? Labda watu  wawili waliwahi kugombana, mmojawapo akatamka ‘tutaona kama utafanikiwa’, na mwishowe maneno aliyokutamkia yanakushikilia hadi leo hii. Cha kufanya ni kuyaharibu hayo maneno,  kwa sababu wapo wasimamizi wa maneno ambao ni majini, majoka, mizimu n.k.


WARUMI  10:9….[Kwa sababu, ukimkiri Yesu kwa kinywa chako ya kuwa ni Bwana, na kuamini moyoni mwako ya kuwa Mungu alimfufua katika wafu, utaokoka.]…. Kumbe kinywa cha mtu  chapaswa kifanye ukiri. Kukiri kunaenda na kuamini, na kuamini huendana na kukiri. Huwezi kufayiwa ukiri na mtu mwingine. Lazima imani iendane na matendo. Unapofanya hivyo, wale wenye akili timamu watakucheka. Mfano, unakiri kuwa lazima mwaka huu niolewe, na unaanza kufanya mazoezi ya jinsi ya kutembea na shela yako au jinsi utakavyokuwa siku ya ndoa yako. Unapokiri,  kuna vitu vinaachilia katika ulimwengu wa roho. Waweza kuendesha mfano wa gari hewani  tu, na kuonesha jinsi utakavyoendesha gari lako. Wenye akili wakikuona jinsi unavyoendesha hilo gari hewani ambalo halipo watakucheka, lakini katika ulimwengu wa roho yatakuja kutimia jinsi hiyo hiyo.


MAOMBI
Maneno niliyomtamkia na mtu yeyote leo nayavunja kwa Jina la Yesu. Maneno niliyotamkiwa na mtu yeyote nayo yakanipata, nayavunja maneno hayo  kwa Jina la Yesu. Amen



Wachawi wana uwezo wa kujua akili ya mtu hata kabla mtu huyo hajazaliwa. Kawaida,  mtu anapokuwa amefanikiwaa kisiasa, kiuchumi, kimasomo au kibiashara ujue kuna nguvu nyuma yake inayomfanikisha kuwa hivyo.


KUMBUKUMBU 8:18…[Bali utamkumbuka Bwana, Mungu wako, maana ndiye akupaye nguvu za kupata utajiri; ili alifanye imara agano lake alilowapa baba zako, kama hivi leo.]… Kumbuka Bwana Mungu maana ndiye akupaye nguvu za kupata mume, Bwana Mungu ndiye akupaye nguvu za kupata mke, na Bwana Mungu ndiye akupaye nguvu za kupata ndoa n.k. Shetani hana uwezo  wa kufanya jambo  lolote jipya.

Comments