Unamsaidiaje mtu aweze kusoma Neno/Biblia na kuelewa bila kuchoka.

Na Frank Philip.
SWALI na JIBU

Nimekutana na swali hili, nikaona niliweke hapa kwa maana nimefikiri ni swali ambalo yamkini wapo wengi wanuliza.

Kwa sababu lilikuja kwa njia ya email yangu binafsi, basi nahifadhi jina la aliyeuliza.

SWALI:
Mtumishi Shalom.

Namshukuru Mungu aliyekufanya kuwa mwalimu. Binafsi napata mafundisho vizuri. Kadri siku zinavyoenda najiona niko shallow in the Word of God.

Mwalimu nisaidie haya
1. Unamsaidiaje mtu aweze kusoma Neno/Biblia na kuelewa bila kuchoka.

2. Mtu anajifunza vipi kuomba kwa ku-quote Biblical phrases na kuomba muda mrefu

3. Kukariri mistari ya Biblia na kukumbuka.

JIBU:

Nashukuru kwa maswali yako mazuri.

Kwanza kabisa, namshukuru Mungu aliyeweka ndani yako kiu ya kusoma Neno na kuomba.

Kwa kuanza tu, napenda kukuambia kwamba hakuna kanuni maalumu za kusoma Neno au kuomba zitakazo mwezesha mtu kusoma "sana" Neno au kuomba kwa "muda mrefu".

Shida inayowasumbua wengi ni miili yao kuliko hata pepo. Ndio maana BWANA alisema "roho i radhi ila mwili ni dhaifu". Maneno haya BWANA aliyasema wakati yuko Gestemane akiomba kwa mzigo, ila wanafunzi wake walishindwa kukesha naye hata saa moja tu. BWANA hakusema ni Ibilisi anawazuia, ila miili yao.

Ukiangalia sehemu nyingine utaona tunaambiwa "tusitizame mwili hata kuwasha TAMAA zake" (Rom. 13:13,14). Mwili unataka kulala, kupumzika, hautaki shida, nk. Sasa, jambo la kwanza la MSINGI ni wewe mwenyewe kuutiisha mwili wako kwa kujiwekea utaratibu na KUJILAZIMISHA/KUJITAHIDI kufanya maombi na kusoma Neno bila kuacha. Kwa mfano, unaweza kujiamulia kwamba LAZIMA usome milango 2 asubuhi na 2 kabla ya kulala. Tena usome Kitabu kwa Kitabu kuanzia Injili zote 4 kisha vitabu vingine hadi Ufunuo, then anza Mwanzo na kuendelea. Utagundua kabla mwaka haujaisha utakuwa umemaliza Biblia nzima. Ukianza round ya 2 ya kuanza tena kusoma Kitabu kwa Kitabu, utagundua utaelewa zaidi, na kushika zaidi, na utajikuta unaweza kuunga mistari tofauti tofauti kwenye biblia ili kupata tafsiri fulani ya jambo, au Neno na pia utaweza kuomba vizuri zaidi kwa kutumia Neno kwa maana litakuwa limejaa ndani.

Kumbuka siku zote, uombapo BWANA anasikia. Omba haja zako kwa habari ya kuelewa maandiko na Roho Mtakatifu atakusaidia kwa maana kazi yake ni KUTUKUMBUSHA na KUTUFUNDISHA yote. Sasa, isikusumbue sana kama unahisi kila usomacho unasahu. Hii ni hisia ya watu wote/wengi. Siku ukipita mahali, utashangaa mistari ambayo ulidhani umesahau ikichomoka ndani yako kama ilivyo, kumbe! Mistari usomayo haikai akilini (cramming) ila moyoni, ndio maana DAUDI alisema "moyoni mwangu nimeliweka Neno lako nisikutende dhambi", Daudi hakusema "akilini".

Hali kadhalika, isikusumbue sana habari ya maombi. Lazima uwe na muda na mazoezi ya KUDUMU hapo maombini. Usikae mkao wa kulala. Simama, omba ukitembea-tembea humo chumbani. Ukijisikia kupiga magoti ni sawa, ila jua position ya kuomba sio maombi, ila yale moyo wako uyasemayo kwa dhati mbele za BABA. Kaa mkao ambao uko comfortable. Hapo utaomba kwa muda mrefu. Kadri udumupo kwenye maombi, mwili wako pia utazoea. Usisahau kwamba "Roho mwenyewe hutusaidia KATIKA UDHAIFU WETU kwa maana hatujui kuomba kama itupasavyo", basi uingiapo maombini mwombe Roho Mtakatifu akusaidie.

Summary:
Hatukariri Neno ila tunasoma Neno. Omba msaada wa Roho Mtakatifu ili uweze kuomba IPASAVYO.

Kama unahitaji ufafanuzi karibu kwa maswali zaidi.

Zidi kubarikiwa.

 Frank Philip.

Comments