KWA NINI TUNASHEREKEA SIKUKUU YA CHRISTMAS ?

Na Mtumishi Gasper Madumla.
Bwana Yesu asifiwe...
Sijiu kama ulishawahi kujiuliza swali kama hilo,au sijui kama ulishawahi kuulizwa swali kama hilo. Au sijui wewe mwenzangu unasherekea sikukuu hii kwa sababu unajisikia kusherekea.
Tunasherekea sikukuu hii kwa sababu nyingi mno,ambazo hata kama nikizieleza mahali hapa,basi hakika hapatatosha kabisa. Lakini nataka nikuambie baadhi ya sababu nne tu za msingi zinazotusukuma sisi sote ulimwenguni kusherekea sikukuu hii ya christmas. Sababu hizo ni kama zifuatazo;
• Tunasherekea sikukuu ya Christmas kwa kukumbuka kuzaliwa mwokozi,masihi wetu yaani Yesu Kristo wa Nazareti.
Kumbukumbu za kuzaliwa kwake Yesu Kristo hazimaanishi kwamba alizaliwa tarehe 25 Disemba exactly. Ikumbukwe kwamba hatusherekei tarehe bali tunasherekea kumbukumbu,
nimesema hivyo maana wako watu waliochanganywa na misongo ya maisha wakidhani tunasherekea siku,au tarehe fulani.

Watu wa namna hii,sikukuu ya christmas imewachanganya hata kutafuta kujua kwamba ni siku gani au terehe gani aliyozaliwa Bwana Yesu. Siku wala tarehe haitusaidii sisi kabisa,tena tarehe kwetu ni ya nini basi?
Tunachotaka kujua ni kuwa na kumbukumbu tu ya ujio wa Bwana na kwa hiyo tunasherekea.

Nabii isaya alitabili kuzaliwa kwa Yesu ( takribani miaka 700 iliyopita kabla ya kuzaliwa kwake Bwana Yesu Kristo ) akisema;
"...bikira atachukua mimba,atazaa mtoto mwanamume,naye atamwita jina lake Imanueli." Isaya 7:14

Tabiri hii ya Nabii Isaya ni hakika na kweli. Zipo tabiri nyingi zilizowahi kutolewa,lakini tabiri ya nabii Isaya imekamilika maana hakika Bwana amezaliwa. Kuzaliwa kwa Bwana Yesu ni muujiza ambao haukuwai kutokea wala haitegemewi kutokea,sababu kuzaliwa kwake kulitokana na UWEZA wa Roho mtakatifu. Tena angali Bwana Yesu amezaliwa alikuwa tayari amekwisha vikwa uwezo,uweza na nguvu ndani yake.
Sasa waweza kufikiria kwamba ni mtoto gani anayezaliwa akiwa na utiisho wa ki-Mungu kama huo,kwa sababu biblia inaanza kumuelezea kwamba alipozaliwa tu aliitwa mtoto mwanamume,yaani si mtoto wa kiume bali ni mwanamume ikionesha tayari alikuwa na nguvu za kipekee tena Yeye ni Imanueli Mungu pamoja nasi ( Mathayo 1:23 )
• Tunasherekea kukumbuka ujio wa wokovu kwa mwanadamu.
Sote twafahamu kwamba mwanadamu alipotea baada ya lile anguko la dhambi ya Adamu na Hawa pale bustani. Mwanadamu alikuwa amehesabiwa kutokuwa na maisha ya raha ya umilele. Lakini kwa kuwa Mungu aliupenda ulimwengu,yaani Bwana Mungu alikupenda wewe na mimi ndipo akamtuma mwanaye wa pekee Yesu Kristo ili kila amuaminie awe na uzima wa milele,tele ( Yoh.3:16 ). Kwa lugha nyepesi ni kwamba tunasherekea siku hii kukumbuka WOKOVU aliouleta Bwana Yesu,maana ndani yake ndimo kuna maisha halisi ya umilele.
• Tunasherekea kwa kukumbuka ushindi wa Mungu ndani ya Yesu Kristo dhidi ya mamlaka mbovu ya shetani chini ya jua hili.
Sikia;
Biblia inasema;
" Hata ulipowadia utimilifu wa wakati,Mungu alimtuma Mwanawe ambaye amezaliwa na mwanamke,amezaliwa chini ya sheria,kusudi awakomboe hao waliokuwa chini ya sheria,ili sisi tupate kupokea hali ya kuwa wana." Wagalatia 4:4-5

Kumbe kabla ya ujio na kumpokea Bwana Yesu Kristo sisi tulikuwa chini ya sheria. Tukiitumikia miungu ya baba zetu,tulikuwa watu tusiokuwa na mungu duniani. Hivyo basi hatukuweza kufanyika wana wa Mungu,bali ingawa tulikuwa ni watu wa Mungu tu.
Kwa kuliona hili,Bwana Mungu akamtuma mwanaye azaliwe chini ya sheria ili atukomboe sisi sote na tupokee hali ya kuwa wana wa Mungu. Mungu akarejesha ushirika wa Roho wake kwa mwanadamu,ushirika uliokuwa umepotea pale bustanini baada ya dhambi.
•Tunasherekea sikukuu hii kwa kukumbuka ujio wa injili duniani.
Yesu mwenyewe ndio injili
Yeye alipozaliwa,njili ndio ilizaliwa kwa mara ya kwanza chini ya jua.
Maana Yeye ni neno,injili ni habari njema ziletazo wokovu,hivyo ni neno la Mungu liletalo wokovu.Biblia imeeleza vizuri sana jambo hili, inasema;

" Malaika akawaambia,msiogope;kwa kuwa mimi ninawaletea habari njema ya furaha kuu itakayokuwa kwa watu wote;" Luka 2:10
Malaika wa Bwana anatambulisha kuwa ujio wa Yesu Kristo duniani ni ujio wa habari njema ya furaha. Yaani ni ujio wa injili,maana injili ina furaha ndani yake,hivyo siku ya leo tunaposherekea sikukuu hii,tunakumbuka ujio wa habari njema chini ya jua.
Zipo sababu nyingi mno,nyingi sana zinazotufanya tusherekee sikukuu hii kwa furaha tele. Siku ya kuzaliwa Masihi ni siku kubwa sana,maana ni kumbukumbu tosha ya ujio wa ukristo duniani kote.
Na ngoja nikuambie siri hii;
Hivi unajua kwamba hakuna msalaba pasipo kuzaliwa kwake Yesu Kristo wa Nazareti. Msalaba ulimuhitaji Yesu azaliwe kwanza chini ya dhambi ingawa Yeye hakutenda dhambi kabisa ( Waebrania 4:15).

Sasa unisikilize ndugu;
* Sherehe hii haina maana kwako kama Bwana Yesu Kristo hajazaliwa ndani yako. Umaana halisi ni ule wa Yesu kuzaliwa ndani yako. Kuzaliwa Yesu ndani yako ni kumpa maisha yako,ni kuokoka tu. Tazama hatuna njia nyingine ya ushindi isipokuwa njia hiyo tu.

Hivyo basi tunaposherekea kumbukumbu zote hizi ni sawa na kusherekea ushindi dhidi ya kila eneo la maisha yetu ya kiroho hata kimwili pia tunapokuwa ndani yake Bwana Yesu,tumeokoka. Nakuambia hivi,mtu aliyeokoka siku ya leo kwake ni anabubujika machozi ya furaha kwa ujio wa Bwana Yesu,na hawezi kukueleza vyote akamaliza,sababu mambo ya rohoni hayaelezeki yakamalizika.
Ikumbukwe kuwa mambo ya rohoni hutambulikana na mtu wa rohoni, Lakini mtu wa mwilini siku hii ya kumbukumbu ya ujio wa Bwana,kwake ni upuuzi tu tena kwake ni jambo la kawaida kabisa tena ndio siku ya kwake ya kupanga kufanya maasi.
Njoo kwa Bwana Yesu Kristo leo,milango ipo wazi kwa ajili yako.Bwana Yesu anakuhitaji awe Bwana na Mwokozi wa maisha yako. Basi usisite kunipigia simu yangu hii,ili Bwana Yesu mwenyewe akuhudumie siku ya leo. Nipigie sasa;
0655-11 11 49.

Nakutakia sikukuu njema na
UBARIKIWE.

Comments