Umoja wa Wakristo wamtaka Waziri Mkuu.Kuuondoa Muswada wa Mahakama ya Kadhi la Sivyo watazunguka Tz nzima kuwashawishi Wakristo kuipigia kura ya hapana Katiba Pendekezwa


Umoja wa Wainjilisti wa Kikisto Tanzania (Uwakita), umemtaka Waziri Mkuu, Mizengo Pinda (pichani) kuuondoa Muswada wa Mabadiliko ya Sheria vinginevyo utazunguka nchi nzima kuwahamasisha waumini wake kuipigia kura ya hapana Katiba Inayopendekezwa.

Wiki hii, Serikali inakusudia kuwasilisha bungeni muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria mbalimbali wa Mwaka 2014 unaopendekeza, pamoja na mambo mengine, kufanya marekebisho kwenye Sheria ya Tamko la Sheria ya Kiislamu, Sura ya 375.
 
Mapema wiki iliyopita, Jukwaa la Wakristo Tanzania lilitoa hoja kutaka Serikali kuondoa muswada wa sheria itakayosimamia kuanzishwa kwa Mahakama ya Kadhi.
 
Hata hivyo, Taasisi ya Masheikh na Wanazuoni wa Kiislamu nchini imesema jukwaa hilo linaingilia madaraka ya Bunge na kutaka Serikali ionekane inasema uongo.
 
Akisoma tamko hilo jana, Mwenyekiti wa Uwakita, Samson Bullegi alisema: “Tunalitaka Bunge la Jamhuri ya Muungano lijiepushe na mijadala ya dini, hususan suala hili la Mahakama ya Kadhi ambalo limekuwa likijirudiarudia kila mwaka pamoja na kwamba lilishahitimishwa na Rais,” alisema.
 
Bullegi alisema Uwakita unamtaka Pinda kuzingatia mambo matatu ambayo ni pamoja na maoni ya Tume ya Kurekebisha Sheria iliyokuwa chini ya Profesa Ibrahim Juma.
Hakuna malumbano kati ya Waislamu na Wakristo hapa wala Waislamu hawana malumbano na Wakristo katika jambo hili naomba tueleweke hivyo.” alisema.
 
Makamu wa Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (Tec), Askofu Severin Niwemugizi alisema anaunga mkono hoja za Uwakita za kushinikiza Serikali kuondoa bungeni muswada wa mabadiliko ya sheria akisema ni nzuri na ndiyo wanayoisimamia tangu awali akisema hakuna msingi wa kuanzishwa kwa Mahakama ya Kadhi kwa sababu jambo hilo halipo pia katika Katiba Inayopendekezwa.
 
Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT), Leonard Mtaita amepinga dhamira ya kuzunguka nchi nzima kwa madai kwamba taasisi yao haifanyi kazi kwa maandamano, bali kuisukuma Serikali kusikiliza hoja zao.
 
Msemaji wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, Sheikh Rajabu Katimba alisema kinachohitajika zaidi ni elimu ili kufahamu uendeshaji wa mahakama hiyo. Alisema Serikali inatumia gharama kubwa kuendesha kesi, lakini baadhi ya mahakimu hawana ujuzi katikakutatua kesi za kidini.

Comments