KIFO CHA YESU NI UPUUZI KWA WANAOPOTEA LAKINI KWETU NI NGUVU YA MUNGU.

BWANA YESU asifiwe ndugu yangu.
Ukitafakari mambo ya rohoni utaona ya rohoni na ukitafakari mambo ya mwilini utaona ya mwilini.
Kujitenga na YESU KRISTO ni kujitenga na uzima wa milele. 

''Kwa hiyo nawaarifu, ya kwamba hakuna mtu anenaye katika ROHO wa MUNGU, kusema, YESU amelaaniwa; wala hawezi mtu kusema, YESU ni BWANA, isipokuwa katika ROHO MTAKATIFU.1 Kor 12:3''
-Andiko hapo juu linaonyesha kwamba wale wanaompinga YESU KRISTO ni kwa sababu tu hawana ROHO wa MUNGU, na kama hawana ROHO wa MUNGU maana yake hawana MUNGU wa kweli. 
-YESU KRISTO ndiye njia pekee ya uzima wa milele.
-BWANA YESU alikubali kufa msalabani ili kutuokoa wanadamu, sio wote wanaompokea, Biblia iko wazi kabisa kuhusu watu hao kwamba '' Kwa sababu neno la msalaba kwao wanaopotea ni upuzi, bali kwetu sisi tunaookolewa ni nguvu ya MUNGU. ''  1 Kor 1:18.
-Kwa wale tu wanaopotea ndio watakataa kuokolewa na BWANA YESU. 
Kifo Cha YESU Msalabani Ni Upuuzi Kwa Wanaopotea Lakini Kwetu Ni Nguvu Kuu Ya MUNGU Kwa Sababu Tunaokolewa Kupitia Kifo Cha YESU KRISTO Msalabani. 
Ndio Maana Ni Marufuku Kwetu Kuionea Haya Injili Kwa Sababu Injili Ni Uwezo Wa MUNGU Pekee Unaoleta Wokovu Kwa Wanadamu Wote(Warumi 1:16, Kwa maana siionei haya Injili; kwa sababu ni uweza wa Mungu uuletao wokovu, kwa kila aaminiye .....).

 Injili Ya YESU Imejificha Tu Kwa Wote Wenye Dini Wanaomkataa YESU,hao Wamepotea Maana Wanaisikia Injili Na Kutaka Kuifananisha Na Vitabu Vyao Vya Kibinadamu Tu, Hakika Injili Imesitirika Kwao  lakini sisi wateule wa MUNGU ni nguvu ya MUNGU ya uzima. Biblia inasema   ''lakini tumekataa mambo ya aibu yaliyositirika, wala hatuenendi kwa hila, wala kulichanganya neno la MUNGU na uongo; bali kwa kuidhihirisha iliyo kweli twajionyesha kuwa na haki, dhamiri za watu zikitushuhudia mbele za MUNGU. Lakini ikiwa injili yetu imesitirika, imesitirika kwa hao wanaopotea; ambao ndani yao mungu wa dunia hii amepofusha fikira zao wasioamini, isiwazukie nuru ya injili ya utukufu wake KRISTO aliye sura yake MUNGU. -2 Kor 4:2-4
 -Wanaokataa wokovu wa BWANA YESU hao shetani amepofusha fikra zao na hawaoni hata kama wana macho.

Injili Ni Habari Njema Za Ufalme Wa MUNGU Unaopatikana Pekee Katika KRISTO YESU, Warumi 10:13 '' kwa kuwa, Kila atakayeliitia Jina la Bwana ataokoka. ''

BWANA YESU Anatushauri Tuiamini Injili Yake(Marko 1:15, akisema, Wakati umetimia, na ufalme wa Mungu umekaribia; tubuni, na kuiamini Injili. )

Ndugu yangu, usije ukamwacha YESU hata siku moja.
Kama Akitokea Mhubiri Au Malaika Akaja Akahubiri Injili Kinyume Na KRISTO Huyo Alaaniwe Maana Huyo Ni Wakala Wa shetani(Wagalatia 1:6-9, Nastaajabu kwa kuwa mnamwacha upesi hivi yeye aliyewaita katika neema ya KRISTO, na kugeukia injili ya namna nyingine. Wala si nyingine; lakini wapo watu wawataabishao na kutaka kuigeuza injili ya KRISTO.  Lakini ijapokuwa sisi au malaika wa mbinguni atawahubiri ninyi injili yo yote isipokuwa hiyo tuliyowahubiri, na alaaniwe. Kama tulivyotangulia kusema, na sasa, nasema tena, mtu awaye yote akiwahubiri ninyi injili yo yote isipokuwa hiyo mliyoipokea, na alaaniwe. ).

 Mawakala Wa Kuzimu Watahubiri Kwamba MUNGU Ni Mwenye Huruma Sana Hivyo Hatawaangamiza Wanadamu.
Ndugu Umepotea. 
Wengine Watakataa Wokovu Kabisa Lakini Biblia inatushauri sisi hivi  ''Basi nasema neno hili, tena nashuhudia katika BWANA, tangu sasa msienende kama Mataifa waenendavyo, katika ubatili wa nia zao; ambao; akili zao zimetiwa giza, nao wamefarikishwa na uzima wa MUNGU, kwa sababu ya ujinga uliomo ndani yao, kwa sababu ya ugumu wa mioyo yao; ambao wakiisha kufa ganzi wanajitia katika mambo ya ufisadi wapate kufanyiza kila namna ya uchafu kwa kutamani. Bali ninyi, sivyo mlivyojifunza KRISTO; ikiwa mlimsikia mkafundishwa katika yeye, kama kweli ilivyo katika YESU, mvue kwa habari ya mwenendo wa kwanza utu wa zamani, unaoharibika kwa kuzifuata tamaa zenye kudanganya; na mfanywe wapya katika roho ya nia zenu; mkavae utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya MUNGU katika haki na utakatifu wa kweli.-Waefeso 4:17-24''

Biblia inaendelea kutuambia kwamba ''  Lakini mwenendo wenu na uwe kama inavyoipasa Injili ya KRISTO, ili, nikija na kuwaona ninyi, au nisipokuwapo, niyasikie mambo yenu, kama mnasimama imara katika roho moja, kwa moyo mmoja mkiishindania imani ya Injili; wala hamwaogopi adui zenu, katika neno lo lote; kwao hao ni ishara mathubuti ya kupotea, bali kwenu ninyi ni ishara ya wokovu, huo utokao kwa MUNGU.
Maana mmepewa kwa ajili ya KRISTO., si kumwamini tu, ila na kuteswa kwa ajili yake;
-
wafilipi 1:27-29''  

 Injili ni nzuri sana na hakika Injili Itahubiriwa Kote.

 Natamani MUNGU Asifungue Tu Milango Ya Wokovu Kwa Ndugu Zangu Bali Afungue Gate Kabisa Ili Asiwepo Wa Kusema Kwamba Hawezi Kupita Kwenye Huo Mlango Wa Wokovu Uliofunguliwa. Na Namshukuru MUNGU Maana Amefungua Geti Kabisa Hivyo Ndugu Unaesoma Ujumbe Huu Kama Hutampokea YESU Mwaka Huu Sijui Una Mpango Wa Kuokoka Lini.

Ndugu ambaye hujaokoka, nakusihi okoka leo. BWANA YESU alikuja kwa ajili yako.

''Wakolosai 1:10  ''mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa BWANA, mkimpendeza kabisa; mkizaa matunda kwa kila kazi njema, na kuzidi katika maarifa ya MUNGU;''
Kwa sasa naishia hapo, MUNGU akitupa nafasi tutajifunza tena siku nyingine.na kama hujampokea BWANA YESU muda wa kumpokea ni leo wala sio kesho, amua leo na atakuandika jina lako katika kitabu cha uzima na utaanza kuukulia wokovu kwa mafundisho kanisani. MUNGU ana makusudi kabisa na wewe, hataki upotelee motoni anataka uende uzimani aliko KRISTO BWANA. MUNGU akubariki sana .
Ni mimi ndugu yako Peter M Mabula
Maisha ya Ushindi Ministry.
0714252292
mabula1986@gmail.com
MUNGU akubariki sana uliyesoma somo hili.

Comments