TATIZO LA KUOA/KUOLEWA NA MPAGANI NI HILI HAPA.

BWANA YESU atukuzwe ndugu zangu.
Karibu ujifunze kitu. 
Mithali 31:10 ''Mke mwema, ni nani awezaye kumwona? Maana kima chake chapita kima cha marijani.''
-Sio kila mwanamke unayemuona mbele yako anafaa kuwa mke mwema.
-Sio kila mwanaume unayemuona anafaa kuwa mme mwema.
Mke na mme mwema hutoka kwa MUNGU,  na anapatikana kwa maombi na amani ya KRISTO kuamua ndani yako.
Huwa kuna madhara ya kiroho kwa mteule kuoa au kuolewa na mpagani. 1 Kor 6:16 '' Au hamjui ya kuwa yeye aliyeungwa na kahaba ni mwili mmoja naye? Maana asema, Wale wawili watakuwa mwili mmoja.   ''
Unaweza ukakosa uzima wa milele kabisa kwa sababu tu ya kuoa au kuolewa na mtu asiye mcha MUNGU maana atakusababishia na wewe utende dhambi.
Unaweza ukawa unafanya machukizo kwa MUNGU kwa sababu tu mkeo au mmeo ni rafiki mtabishaji.
Tatizo La Kuoa Mwanamke Mpagani Au Kuolewa Na Mwanaume Mpagani Ndio Hili. 

Ona Mfano Huu  
1 Wafalme 21:25 " Lakini Hapakuwa Na Mtu Kama Ahabu, Aliyejiuza Atende Maovu Machoni Pa BWANA Ambaye Yezebeli Mkewe Alimchochea". 
- Ahabu Mwanzo Alikuwa Mtu Mzuri Lakini Kumuoa Yezebeli Ilikuwa Mkosi Mkubwa Kuliko Mikosi Yote Maishani Mwake, -Mkewe Alikuwa Mwabudu shetani Na Alipokuja Kwa Mmewe Alikuja Na Sanamu Zake Za Kuziabudu. 
-Yezebeli Kwa Kutumia Nguvu Yake Kama Malkia, Aliwafanya Waisraeli Kuabudu Sanamu Ambayo Ni Machukizo Makuu Kwa MUNGU. 

Upendo Leo Umewatumbukiza Maelfu Ya Watu Kwenye Uasi Mkuu. 
-Umeolewa Na Mlevi Baada Ya Muda Na Wewe Umegeuka Chapombe.
-Umeolewa Na Jambazi Na Wewe Unamtunzia Siri Kitu Ambacho Ni Dhambi.
-Umeolewa Na Mganga Wa Kienyeji Hivyo Lazima Tu Na Wewe Uwe Mfuga Majini. 

Ndugu Zangu, Tuwasikilizeni Sana Wachungaji Wetu, Maana Biblia Inasema Usifungwe Nira Na Asiyeamini.

 Ahabu Mcha MUNGU Alifungwa Nira Na Mwabudu shetani Ikawa Ushetani Nchi Nzima( 1 Wafalme 16:31-33, Ikawa, kama ingalikuwa neno dogo tu kuyaendea makosa ya Yeroboamu mwana wa Nebati, akamwoa Yezebeli binti Ethbaali, mfalme wa Wasidoni, akaenda akamtumikia Baali, akamsujudia. Akamjengea Baali madhabahu katika nyumba ya Baali, aliyoijenga huko Samaria. Ahabu akaifanya Ashera; Ahabu akazidi kumghadhibisha BWANA, MUNGU wa Israeli, kuliko wafalme wote wa Israeli waliomtangulia. ).
-Madhara ya kuoa mpagani yakaleta madhara hadi kwenye taifa.
-Mke wa mfalme akawakosesha hadi taifa zima

Ndugu Uwe Makini Sana.
 2 Kor 6:14-16 ''Msifungiwe nira pamoja na wasioamini, kwa jinsi isivyo sawasawa; kwa maana pana urafiki gani kati ya haki na uasi? Tena pana shirika gani kati ya nuru na giza? Tena pana ulinganifu gani kati ya KRISTO na Beliari? Au yeye aaminiye ana sehemu gani pamoja na yeye asiyeamini? Tena pana mapatano gani kati ya hekalu la MUNGU na sanamu? Kwa maana sisi tu hekalu la MUNGU aliye hai; kama MUNGU alivyosema, ya kwamba, Nitakaa ndani yao, na kati yao nitatembea, nami nitakuwa MUNGU wao, nao watakuwa watu wangu.''

Ndugu ambaye uko kwenye ndoa ambayo ina matatizo hakika unamuomba MUNGU ili ndoa yako ipone.
Zipo ndoa shetani ameziweka kwenye jeneza, wanandoa hao wanahitaji kumwita BWANA YESU ili aifufue tena ndoa hiyo.
Ndugu kama ndoa yako ina tatizo hakika sema hivi
''NAMTAKA YESU ILI NIPONE'' unataabika bure kwa waganga,na hayo mazindiko sio chochote ila kumbuka tu kuwa UNAMTAKA YESU KRISTO ILI UPONE.
BWANA YESU anasema 'Nanyi mkiomba lo lote kwa jina langu, hilo nitalifanya, ili BABA atukuzwe ndani ya Mwana. Mkiniomba neno lo lote kwa jina langu, nitalifanya. Mkinipenda, mtazishika amri zangu.-Yohana 14:13-15''

 Ndoa Ya Wazazi Ndio Shule Ya Ndoa Ya Watoto. Kama Wazazi Ndoa Yao Imejaa Matukano Na Mapigani kila siku, Hiyo Ndio Maana Ya Ndoa Watakayoielewa Watoto Wao.
Wengi wametokea kwenye ndoa ambazo kila siku ilikuwa mapigano, kama watoto wamejifunza maana ya ndoa kutoka kwa wazazi.
 Ni muhimu sana kuwa na umakini katika kuchagua mwenzi wa maisha, kama kijana huyo anataka mfanye mapenzi kabla ya ndoa huyo sio muoaji bali mharibifu, kataa na usikubali kumtenda MUNGU dhambi.
Samsoni alinasa kwa Delila, akina Delila wa leo ni wengi sana, Biblia inasema Samsoni hakuusikiza ushauri wa wazazi wake kwenye suala la mke. Waamuzi 14:1-3 ''Samsoni akatelemkia Timna, akaona mwanamke huko Timna, mmojawapo wa binti za Wafilisti.  Kisha akapanda, akawaambia baba yake na mama yake, akasema, Nimemwona mwanamke huko Timna, mmojawapo wa binti za Wafilisti; basi mnipatie, nimwoe. Ndipo baba yake na mama yake wakamwambia, Je! Hapana mwanamke hata mmoja katika ndugu zako, au katika jamaa zangu zote, hata uende kumwoa mwanamke kwa hawa Wafilisti wasiotahiriwa? Samsoni akamwambia baba yake; Mnipatie huyo, kwa maana ananipendeza sana.''
-Hata leo kuna vijana wengi wa kiume au vijana wa kike ambao wakati wa kumpata mwenzi hawapendi ushauri kutoka kwa wazazi wao wa kiroho au hata wa kimwili walio wacha MUNGU.
-Samsoni aling'olewa macho kwa chuki ya mke wake Delila '' Wafilisti wakamkamata, wakamng'oa macho; wakatelemka naye mpaka Gaza, wakamfunga kwa vifungo vya shaba; naye alikuwa akisaga ngano katika gereza.-Waamuzi 16:21''

 Ndugu Kijana, Unatakiwa Upange Mipango Na Malengo Yako Huku Ukimtegemea ROHO MTAKATIFU.
 Usipokuwa Na Mipango Wala Msimamo shetani anaweza kukupangia mipango ya kuhakikisha Unalia Kila Siku. 
Maombi ili kumpata mwenzi wako wa maisha ni jambo muhimu sana kuoa/kuolewa na mtu ambaye hana hofu ya MUNGU inaweza ikakughalimu sana. Sio kila mtu anafaa, amani ya KRISTO iamue ndani ya wateule wa MUNGU.
Ukioa au ukiolewa basi huyo ndio wako siku zote, heri uwe makini kabla ya kuingia kwenye ndoa, BWANA YESU anasema '' Akawaambia, Kila mtu atakayemwacha mkewe na kuoa mwingine azini juu yake; na mke, akimwacha mumewe na kuolewa na mtu mwingine, azini.-Marko 10:11-12'' 
Kuzini ni dhambi hivyo hakuna kuachana kwa wanandoa.

Mwaka 2012 Kuna Dada Mmoja Alijikuta Akiniambia Kwenye Simu Kwamba, Ananipenda Sana Kisha Nilipomuuliza Zaidi Nikaona Kama Ulimi Wake Umeshikwa Na Kitu Fulani, Baadae Akasema Ametumwa Na shetani Ili Aniondoe Kwenye Kusudi La MUNGU, Nilihuzunika Sana Kisha Baadae Akaniambia Alikuwa Ananitania Ila Ukweli Hakuwa Anatania Maana Baada Ya Kusema Alijilaumu Sana, Sikumuona Tena. 
Ndugu yangu, omba sana katika hili, sio kila kijana anayekuambia kwamba ameonyesha na wewe unamkubali, sio kila anayekuambia kwamba amefunga siku 7 kwa ajili yako ukadhani huyo ndiye anayefaa. Omba ndugu. 
 ''Nyumba na mali ni urithi apatao mtu kwa babaye; Bali mke mwenye busara, mtu hupewa na BWANA.-Mithali 19:14''
Mke au mme mwema hutolewa na MUNGU baada ya wewe kuomba. Na haiwezekani wewe mtenda dhambi harafu utake mke mwaminifu.
Haiwezekani wewe kahaba uombe kupewa mme mcha MUNGU.

Ndugu Yangu Unayetaka Au Kutarajia Mchumba Sahihi Tambua Kwamba.
-Sio Kila Vinavyoonekana Vinafaa.
-Na Sio Kila Anayekuvutia Ni Wa kwako.
-Sio Kila Anayekuchekea Anakutakia Mema.
 Ndugu yangu, usijidanganye kwamba uoe au kuolewa na mpagani ukitumaini kwamba atabadilika baadae, Biblia inasema hili kuhusu hilo '' Kwa maana wajuaje, wewe mwanamke, kama utamwokoa mumeo? Au wajuaje, wewe mwanamume, kama utamwokoa mkeo? - 1 Kor 7:16  ''
Omba Ndugu Maana shetani anajua kwamba muda wako wa kutafuta mchumba umefika hivyo anaweza kutegeshea magari(watu) yake ili ukijifanya una haraka udandie gari hilo kumbe ni la shetani.  1 Kor 7:10-11 ''  Lakini wale waliokwisha kuoana nawaagiza; wala hapo si mimi, ila BWANA; mke asiachane na mumewe; lakini, ikiwa ameachana naye, na akae asiolewe, au apatane na mumewe; tena mume asimwache mkewe. ''
Ndugu Omba Na Sikiliza Ushauri Wa Wachungaji Au Watumishi Waaminifu Wa Kanisani Kwenu. Omba Sana
Waebrania 13:4 '' Ndoa na iheshimiwe na watu wote, na malazi yawe safi; kwa maana waasherati na wazinzi MUNGU atawahukumia adhabu. ''
 Kwa sasa naishia hapo, MUNGU akitupa nafasi tutajifunza tena siku nyingine.na kama hujampokea BWANA YESU muda wa kumpokea ni leo wala sio kesho, amua leo na atakuandika jina lako katika kitabu cha uzima na utaanza kuukulia wokovu kwa mafundisho kanisani. MUNGU ana makusudi kabisa na wewe, hataki upotelee motoni anataka uende uzimani aliko KRISTO BWANA. MUNGU akubariki sana .
Ni mimi ndugu yako Peter M Mabula
Maisha ya Ushindi Ministry.
0714252292
mabula1986@gmail.com
MUNGU akubariki sana uliyesoma somo hili.

Comments