UKIWAJUA MAADUI WA SIRINI UTASHINDA.



BWANA YESU asifiwe.
Leo tujifunze kwa njia ya shuhuda.
''ombeni bila kukoma;-1 Wathesalonike 5:17''
Neno la MUNGU linatutaka tuombe bila kukoma.
Siku moja katika maombi, niliomba kwa muda mrefu, nilikuwa naombea vitu mbalimbali pamoja na kuwaombea watu mbalimbali, niliomba na kudhani nimegusa kila eneo na hakika nilijua nimeshinda baada ya maombi hayo. Wakati namalizia kuomba ROHO MTAKATIFU akaniambia ''Omba juu ya maadui wa sirini''. Nilijikuta naanza kuombea jambo jipya yaani maadui wa sirini, ni ufunuo muhimu sana maana kuna maadui wengi sana wa sirini ambao adui huwatuma ili kuhakikisha mipango yetu haifainikiwi. ''Kadhalika ROHO naye hutusaidia udhaifu wetu, kwa maana hatujui kuomba jinsi itupasavyo, lakini ROHO mwenyewe hutuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa. Na yeye aichunguzaye mioyo aijua nia ya Roho ilivyo, kwa kuwa huwaombea watakatifu kama apendavyo MUNGU. - Warumi 8:26-27
Ndugu yangu,
yawezekana umeomba mara nyingi sana juu ya jambo furani unalolihitaji maishani mwako. shetani anajua ukilipata hilo hakika hakupati tena, jambo hilo shetani amelishikilia kiasi kwamba huoni pa kutokea. Mfano nyie ni wachumba na mnamuomba MUNGU ili awape pesa muweze kufunga ndoa, shetani anajua kabisa kwamba wewe kijana ukioa/ kuolewa hatakupata tena katika dhambi za uzinzi na uasherati hivyo anahakikisha hufanikiwi na kubaki mtumwa wake siku zote kwa kutamani na kutenda dhambi.
Usiache kuomba lakini Omba katika ROHO MTAKATIFU na pia sio kila jambo umwambie kila mtu.

Siku moja pia tulipokuwa tunaomba usiku alikatisha panya katika lile eneo ambapo katika hali ya kawaida panya hawezi kuwepo eneo hilo, baadae kidogo palijaa nzi kama 6 katika eneo hilo, hatukujali lakini mmoja kati yetu akasema kwamba huyo panya na hao nzi wala sio viumbe vya kawaida ila wachawi wametuma majini na yamejigeuza kuwa nzi na panya ili
-kuchukua kila siri tuliyokuwa tunaiombea.
-kuhakikisha hatuombi katika ROHO,
Tulianza kuharibu na kuteketeza roho hizo za shetani. Wakati tukiomba nilipata ufunuo live kwamba hakika yule panya na wale nzi hawakuwa wa kawaida.

Hata hapo nilijifunza jambo jambo jipya.
''Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa; -Mathayo 7:7''
Ushuhuda mwingine ni kwamba tulikuwa tumefunga siku zaidi ya 20 kwa maombi ya kutwa kila siku, katika maombi hayo mmoja kati yetu akapata ufunuo kwamba ndugu mmoja katika kundi hilo la maombi alikuwa yuko kinyume chetu. Sisi tulikuwa tunafunga kila mpango wa shetani lakini yeye alikuwa anafungua, ni hatari sana na mambo hayo yapo sana katika jumuia zetu. ndugu yangu, sio kila mtu wa kumwambia siri zako, wengine ukiwaambia wakuombea ndio kwanza wataanza kuomba kinyume chako, usipende kuwashirikisha watu kila hitaji lako, angalia waaminifu na mengine omba wewe mwenyewe. Ndio maana BWANA YESU anatushauri kwamba tufungapo tusifunge ili kujionyesha kwa watu kwamba tumefunga,
''Tena mfungapo, msiwe kama wanafiki wenye uso wa kukunjamana; maana hujiumbua nyuso zao, ili waonekane na watu kuwa wanafunga. Amin, nawaambia, wamekwisha kupata thawabu yao. Bali wewe ufungapo, jipake mafuta kichwani, unawe uso; ili usionekane na watu kuwa unafunga, ila na BABA yako aliye sirini; na BABA yako aonaye sirini atakujazi. - Mathayo 6:16-18''

Hiyo ya kufunga bila kujionyesha kwa watu wakati mwingine ni kutusaidia ili tukiombacho tufanikiwe. Yupo dada mmoja kila akianza kufunga alikuwa anawataarifu baadhi ya watu, Kuna kaka mmoja naye alikuwa akifunga kila yule dada akifunga, maombi yake yule kaka yalikuwa ni kuwa kinyume na yule dada kwa sababu tu yule dada alikuwa amemkataa. Ndugu yangu sio kila jambo lazima uwajulishe rafiki zako, wengine ni maadui wa siri na wengine kabisa ni mawakala wa shetani ili kuhakikisha hufanikiwi.
''Kwa sababu hiyo nawaambia, Yo yote myaombayo mkisali, aminini ya kwamba mnayapokea, nayo yatakuwa yenu. - Marko 11:24''
Katika maombi yako nakuomba uwe unaharibu maadui wa sirini wote.

Unaweza kudhani unapambana na shetani kumbe unapambana na mama wa chumba cha pili ambaye wewe kila siku unamsimulia mambo yako.
Ndugu usiache kuomba ila uwe makini sana.
''Na lo lote tuombalo, twalipokea kwake, kwa kuwa twazishika amri zake, na kuyatenda yapendezayo machoni pake. - [1 Yohana 3:22]

-Unaweza kudhani unapambana na jini mahaba kumbe maroho ya ukoo ndio yanakutesa.
-Unaweza ukadhani MUNGU hakupendi kumbe tatizo ni hiyo pete unayovaa maana unaweza kukuta ina pepo la umasikini.
-Unaweza ukadhani unapambana na mfanya kazi mwenzako kumbe nywele bandia zako zina maagano ya kipepo.

''Basi na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji. - Waebrania 4:16''
Ndugu hakikisha una haribu maadui zako wote wa sirini, na Muombe ROHO MTAKATIFU akuonyesjhe adui zako wa sirini, kumbuka vita yetu sisi sio ya damu ya nyama bali ni vita ya kiroho, na huko rohoni hakuna anayeweza kusimama kwako kama tu wewe uko upande wenye nguvu wa YESU KRISTO BWANA wetu. ''Kwa sala zote na maombi mkisali kila wakati katika Roho, mkikesha kwa jambo hilo na kudumu katika kuwaombea watakatifu wote; - Waefeso 6:18''
Najua kuna kitu umejifunza kuhusu maombi.
Omba siku zote maana maombi ni maisiha.
Maombi ni mkono mrefu wa kupokea baraka kutoka kwa MUNGU.
Omba kila siku na mara nyingine funga kabisa.
''Lakini namna hii haitoki ila kwa kusali na kufunga. Mathayo 17:21''
Hapa nilikuwa nazungumza na waombaji waliookoka.

Kwa sasa naishia hapo, MUNGU akitupa nafasi tutajifunza tena siku nyingine.na kama hujampokea BWANA YESU muda wa kumpokea ni leo wala sio kesho, amua leo na atakuandika jina lako katika kitabu cha uzima na utaanza kuukulia wokovu kwa mafundisho kanisani. MUNGU ana makusudi kabisa na wewe, hataki upotelee motoni anataka uende uzimani aliko KRISTO BWANA.
MUNGU akubariki sana .
Ni mimi ndugu yako
Peter M Mabula
Maisha ya Ushindi Ministry.
0714252292
mabula1986@gmail.com
MUNGU akubariki sana uliyesoma somo hili.

Comments