JUKWAA la 
Wakristo Tanzania (TCF), limeendelea kushikilia msimamo wake wa 
kuwashinikiza waumini kuipigia kura ya hapana Katiba Inayopendekezwa.
![]()  | 
| Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa | 
![]()  | 
| Askofu Dk. Alex Malasusa, Mwenyekiti wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania | 
Limesema Katiba Inayopendekezwa imefika hapo ilipo kwa njia ya ubabe na kukosa uadilifu. 
Tamko la umoja 
huo lililotolewa jana na kusainiwa na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Kikristo 
Tanzania (CCT), Askofu Dk. Alex Malasusa, Mwenyekiti wa Baraza la 
Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa na 
Mwenyekiti wa Baraza la Maaskofu wa Kipentekoste Tanzania (CPCT), Askofu
 Daniel Awet, limesema wao hawana hasira kama ambavyo watu wengine 
wamekuwa wakitafsiri. 
Kauli hiyo 
inaonyesha kujibu kauli ya Rais Jakaya Kikwete aliyoitoa Machi 28, mwaka
 huu alipokutana na viongozi dini wanaounda Kamati ya Amani ya Mkoa wa 
Dar es Salaam. 
Akizungumza na 
viongozi hao, Rais Kikwete alisema msimamo wa TCF wa kuwataka waumini 
wao kuipigia kura ya hapana Katiba Inayopendekezwa ni wa hasira, pia 
usiokuwa na tija kwa maendeleo ya taifa.
Rais Kikwete 
alikuwa akizungumzia tamko la TCF la Machi 12, mwaka huu lililowataka 
waumini wake kujitokeza kwa wingi kujiandikisha katika Daftari la Kudumu
 la Wapigakura na kuipigia kura ya hapana Katiba hiyo. 
Jukwaa hilo 
lilitaja sababu za uamuzi wake huo ni Muswada wa Mahakama ya Kadhi 
kukiuka misingi ya taifa kuwa na Serikali isiyo na dini, na kura ya 
maoni ya Katiba Inayopendekezwa kuweza kusababisha mgawanyiko.
Katika tamko 
lake la jana, maaskofu hao wamesema kwa kuwa utafiti wa Tume ya 
Kurekebisha Sheria ulishaonyesha madhara ya uanzishwaji wa Mahakama ya 
Kadhi ni vema Serikali ikaacha kujadili. 
“Sisi maaskofu 
wa Jukwaa la Wakristo Tanzania tunatamka kwamba matamshi ya Rais Kikwete
 wakati akihutubia watu aliowaita viongozi wa dini Machi 28, kuwa 
Mahakama ya Kadhi ni ya Waislamu wenyewe na Serikali haitajihusisha wala
 kugharamia, yanakinzana na kile kinachoendelea bungeni na nje ya 
Bunge. 
“Hapa 
tunajiuliza, endapo maneno ya rais ni ya kweli, mbona Bunge linaendelea 
kujadili kitu ambacho Serikali yake haitajihusisha wala kukigharimia? 
“Kwa mantiki 
hiyo, tunamtaka rais aagize muswada huu uondolewe bungeni na usijadiliwe
 tena kwa kuwa utafiti wa Tume ya Kurekebisha Sheria ulishaonyesha 
madhara ya uanzishwaji wa Mahakama ya Kadhi, vinginevyo kuendelea 
kujadiliwa kwa muswada huu maana yake ni kwamba Serikali inajihusisha na
 itagharimia. 
“Maaskofu 
tuliokutana hapa hatuna hasira na wala hatuongozwi na mihemko katika 
kufikia maamuzi tunayofanya kama ambavyo wengine wanavyotutafsiri. 
“Tunafikia 
maamuzi yetu baada ya maombi na sala, na tunasukumwa na upendo kwa 
wananchi ili kujenga taifa lenye umoja, amani, utulivu na maelewano,” 
ilisema sehemu ya tamko hilo. 
Maaskofu hao 
wamesema wako mjini Dodoma kufuatilia kwa kina muswada wa marekebisho ya
 sheria mbalimbali ya mwaka 2014 unaopendekeza pamoja na mambo mengine, 
marekebisho ya sheria ya tamko la sheria za Kiislamu la mwaka 1964. 
Wamesema 
muswada huo unaopendekeza kuanzishwa Mahakama ya Kadhi utawasilishwa 
bungeni leo kwa hati ya dharura na hivyo kuufanya umma wa Watanzania 
kutokujua maudhui yaliyomo katika muswada huo, wakati bado hoja zao za 
msingi walizopeleka kwenye Kamati ya Katiba na Sheria ya Bunge na kwa 
Waziri Mkuu hazijajibiwa. 
“Tangu 
tulipokutana Machi 10, mwaka huu tukatoa tamko letu kuhusiana na 
Mahakama ya Kadhi na Katiba Inayopendekezwa, tumekuwa tukiendelea 
kutafakari juu ya yale tuliyokuwa tumesema katika matamko yetu 
mbalimbali na jinsi amani na utulivu wa nchi yetu vinavyoendelea 
kumomonyoka siku zinavyokwenda.
 “Kwanza 
tumeshangazwa na tabia ya viongozi wa Serikali ya kuitisha na kuendesha 
mikutano wanayodai ni ya viongozi wa dini, lakini isiyo rasmi.
 “Machi 3, 
mwaka huu Waziri Mkuu, Mizengo Pinda aliitisha mkutano kupitia mchungaji
 mmoja ambapo hakuna hata kiongozi mmoja wa taasisi au kanisa 
aliyeshiriki. 
“Jambo la 
kushangaza ni kile kilichotokea Machi 28, ambapo rais alishiriki kikao 
cha kikundi ambacho si rasmi, yaani Kamati ya Amani ya Mkoa wa Dar es 
Salaam. “Tunasema kamati hiyo siyo rasmi kwa sababu haina baraka za 
viongozi wa ngazi za juu wa kidini wa mkoa huo na haina mwongozo wa kazi
 zake. 
“Mikutano ya 
jinsi hii, kati ya Serikali na wale ambao imewaona kuwa ndio viongozi wa
 dini si sahihi kwani viongozi wa dini wana taratibu zao za kualikwa au 
kuwakilishwa katika mikutano na viongozi wa Serikali au wa dini au 
madhehebu mengine. 
“Tunawashauri 
wanaohutubia na wanaoshiriki mikutano hii wajue washiriki hawana uwezo 
wa kuamua au kukubaliana na jambo lolote kwa niaba ya viongozi wao wa 
juu, na pia viongozi husika wa Serikali wasifurahi kwamba ujumbe wao 
umewafikia viongozi wa dini, kwani hao washiriki si wawakilishi rasmi na
 hawana uwezo wa kutoa maamuzi au kukubaliana juu ya jambo fulani la 
kitaifa,” imesema sehemu ya tamko hilo. 
Pamoja na mambo
 mengine, tamko hilo linasema kuhusu muswada wa Mahakama ya Kadhi 
imebainika walichokuwa wakikisema awali kitatokea kimeaanza kutokea 
bayana kutokana na yale yaliyotokea kwenye semina kuhusu mahakama hiyo 
ambapo baadhi ya wabunge walitofautiana na kutaka kupigana. 
Hata hivyo, 
maaskofu hao wamesema endapo wabunge wa dini za Kikristo na Kiislamu 
watapigana na kisha baadaye wananchi nao wakafanya hivyo katika maeneo 
yao, Serikali itakuwa ndiyo chanzo cha mapigano hayo. 
Maaskofu hao 
walioweka kambi mjini Dodoma, wamewataka viongozi wa Serikali kuacha 
kutumia vikundi visivyo rasmi kualika mikutano wanayodhani itakubalika 
na waumini wa dini hizo. 
Wamesema mikutano yote ya jinsi hiyo itakayoitishwa ni batili na uamuzi wowote utakaofikiwa hautatambulika kwao.
Muswada 
Mahakama ya Kadhi waota ‘mbawa’ Wakati huohuo, Mwandishi Wetu Fredy 
Azzah anaripoti kutoka Dodoma kuwa muswada wa sheria ya uanzishwaji wa 
Mahakama ya Kadhi iliyotarajiwa kuwasilishwa bungeni leo, imeahirishwa. 
Katibu wa Bunge, Dk. Thomas Kashilila, aliwaambia waandishi wa habari 
mjini Dodoma jana kuwa uwasilishwaji wa sheria hiyo umesitishwa hadi 
itakapopangwa tena.
 “Sheria hii 
haitawasilishwa tena, shughuli nyingine zitaendelea na kuna miswada 
mingi tu imeahirishwa ambayo kutokana na muda haitawasilishwa kwenye 
kikao hiki ikiwamo ya habari,” alisema Dk. Kashilila. Alisema mkutano wa
 20 wa Bunge hilo unaotarajiwa kuanza Mei, ni mahususi kwa bajeti, 
lakini wabunge wakiona inafaa wanaweza kubadili kanuni wakajadili 
miswada watakayoona inafaa.
Chanzo:Mtanzania


Comments