| Askofu Josephat Gwajima. | 
Pamoja na hilo, Kibatala aliomba mteja wake huyo kuambiwa kwa maandishi juu ya vitu vinavyotakiwa kuwasilishwa kwa Jeshi hilo.
Barua hiyo ambayo Kibatala ameielekeza kwa Kamanda wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, pia nakala yake ameituma kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, Ernest Mangu na kwa mteja wake huyo.
Barua hiyo ambayo Kibatala ameielekeza kwa Kamanda wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, pia nakala yake ameituma kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, Ernest Mangu na kwa mteja wake huyo.
“Kwa barua hii 
tunaomba Jeshi la Polisi kwa niaba ya mteja wetu kumwandikia rasmi kwa 
maandishi mteja wetu mkiainisha nyaraka mnazohitaji na vifungu vya 
sheria vinavyotumika na Jeshi la Polisi kutaka nyaraka hizo.
“Tutashukuru 
kupata hati hiyo, ambayo bado hatujaipa jina, kwani tunategemea jeshi 
hilo litafahamu jina la kisheria la nyaraka husika inayotumika kutaka 
mteja wetu alete nyaraka tajwa na mara tu mteja wetu akipata maandishi 
tuliyoomba atatimiza wito au kuchukua hatua stahiki za kisheria,” 
ilisomeka sehemu ya barua hiyo.
Juzi wakili 
mwingine wa Gwajima, John Mallya, alilalamikia hatua ya polisi akisema 
mahojiano yalichukua mambo binafsi badala ya kile alichoitiwa na 
kutakiwa kuwasilisha vitu 10.
Wakili huyo 
alitaja mambo yanayotakiwa kuwasilishwa polisi kuwa ni hati ya usajili 
wa kanisa, namba ya usajili, majina ya Baraza la Wadhamini (Baraza la 
Kiroho), idadi ya makanisa (matawi) anayohudumia, nyaraka za helikopta 
ya kanisa na muundo wa uongozi wa kanisa
Vitu vingine ni
 waraka wa maaskofu uliosomwa makanisa yote, nyaraka za nyumba na mali 
za kanisa, nyaraka kuonyesha taarifa za hesabu kutoka kwa Msajili wa 
Vyama vya Hiari na kuambatana na mtu anayepiga picha za video kanisani 
hapo.
Hata hivyo, 
katika barua ya wakili huyo wa Gwajima, Kibatala, ilieleza kwa mshangao 
kwamba Askofu huyo, ambaye anatuhumiwa au anapelelezwa kuhusiana na 
tuhuma za kutoa lugha ya matusi wakati wa mahojiano, hakutaarifiwa kama 
tuhuma hizo ziko chini ya kifungu gani cha sheria.
Gwajima 
alitakiwa kurejea katika Kituo Kikuu cha Polisi Dar es Salaam Aprili 16,
 mwaka huu, akiwa na vitu hivyo 10, hatua ambayo imekuja kinyume na 
matarajio ya wengi kuwa kiongozi huyo angekuwa anahojiwa tu kuhusu 
matamshi yake ya kashfa dhidi ya Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Dar es Salaam,
 Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo.
Kutokana na 
matamshi hayo yaliyosambaa kwa kasi kwenye mitandao ya kijamii kwa njia 
ya video na sauti, Gwajima alitakiwa kuripoti polisi kuhojiwa Machi 27, 
mwaka huu, ambapo kabla ya kukamilika kwa mahojiano aliishiwa nguvu na 
kupelekwa hospitalini alikolazwa kwa siku nne, huku taarifa zikieleza 
kuwa alishtushwa na kuhojiwa taarifa binafsi badala ya tuhuma alizoitiwa
 polisi.
Baada ya kutoka
 hospitalini, Gwajima aliendelea kutembea akiwa kwenye kiti chenye 
magurudumu, alichotumia hadi Aprili 6, alipohubiri katika Ibada ya 
Pasaka ambako alionekana kusimama kutokana na kudai kuombewa na 
wachungaji wageni waliofika kanisani hapo kutoka Japan.
Kamishina Kova hakupatikana kuzungumzia kupokea barua hiyo kutokana na simu yake kuita bila majibu.
Source:Mwananchi
Comments