KWA NINI MAJARIBU YAJE KWANGU?

Ufufuo na uzima Morogoro katika ibada.
 
Na Pastor Bryson Lema.
Utangulizi: Hili ni swali ambalo leo napenda kukuuliza, kwa sababu hata mimi niliwahi kujiuluza swali hili. Hivi kwa nini mimi ninaumwa? Sina shaka kusema majaribu huletwa na adui. Huyu  adui hupenda kuniwekea mazingira ya kunifanya nikate tamaa. Kumbe sasa hiyo shida imesababishwa na mtu mmoja ambaye aliamua kunirushia hii shida. Je, lakini kama ni adui ameniletea hii shida, kwa nini Mungu ambaye ni msaada wangu, kimbilio langu hakuzuia hili jaribu lisinitokee wakati mimi nimeokoka? Kwa nini sasa Mungu amewaachia hawa watu wakakaa vikao vya uharibifu, hata wakafanikiwa kuniletea hili jaribu? 


Wakati mwingine nawaona wale wasiomtii Mungu wanazidi  kufanikiwa na kuinuliwa. Wapo wezi wanaiba, wanafanikiwa na maisha yao yanazidi kunawiri. Wapo wengine wasiomtii Mungu wakikosa kazini hawachukuliwi hatua yoyote, lakini mimi ninayemcha Bwana ikitokea nimekosa kazini hata mara moja nitapewa onyo kali au barua ya kujieleza eti kwa nini nisifukuzwe kazi!!!.
WAAMUZI 3:1-2…[Basi haya ndiyo mataifa ambao Bwana aliwaacha, ili awajaribu Israeli kwa hao, yaani, awajaribu hao wote ambao hawakuvijua vita vyote vya Kanaani; 2 ili kwamba vizazi vya wana wa Israeli wapate kujua ili kuwafundisha vita, hasa wao ambao hawakujua vita kabla ya wakati ule;]… Hili andiko linataja mataifa ambayo Mungu alimwambia Joshua asiwaondoe kabisa,bali awaache. Siyo kwa sababu hawa ni watu wake, au  kwamba wanafaa sana.  La hasha‼!. Wameachwa  kwa sababu ya kazi maalumu.  Hata katika maisha yako, wapo watu walioachwa siyo kwa sababu wewe ufe bali ni kufanya wewe ujue jinsi  ya kupigana vita. Kumbe haja ya Mungu ni kuniona mimi nakuwa mpiganaji wa hii vita.  Hili tatizo ulilo nalo Mungu ameliacha ili ujue jinsi ya kupigana vita. Adui  yako hajaachwa ili kwamba akuangamize, bali kupitia huyo adui amefanyika kama chuo cha  mafunzo ya vita yako. Huyo adui ni kiwanda cha Bwana cha kukutengeneza. Maana bila Penina,hakuna Samweli. Kumbuka Hanna alikuwa akistarehe na mumewe, lakini  alipokuja Penina,  ikamfanya Hanna amtafute Eli. Ndiposa Eli akamwabia Hanna kuwa,”Bwana na akutane na haja ya moyo wako”. Bila  Penina, Hanna asingekubali mwanae Samweli akae hekaluni. Hilo jaribu lako siyo la kukuangamiza, bali la kukufanya uinuliwe. Bwana huruhusu adui aje kwako kwa njia moja lakini humtawanya  kwa njia saba. Uonapo jaribu furahia, kwa sababu lipo kwa ajili ya kukuvusha ng’ambo ya pili.
ZABURI 119:67…[Kabla sijateswa mimi nalipotea, Lakini sasa nimelitii neno lako]… Mateso yalimfanya Daudi ajue jinsi ya kumtafuta Bwana. Hiyo shida yako  si  bure,  ila kuna kitu kimo ndani  yako ambacho maadui wanakiwinda ili  kukipata. Usimchukie  aliyeinuka ili kufanya vita nawe, ila kwa kupitia hilo tatizo alilotengeneza  utakuwa mtu wa tofauti.

ZABURI 119:71…[Ilikuwa vema kwangu kuwa naliteswa, Nipate kujifunza amri zako.]….  Wakati mwingine unaweza kudhani Mungu hakupendi,  ila  ujue kuwa Mungu anataka ujue Yeye ni nani. Mungu hupenda kutufundisha,na huyo  adui yako yupo  ili  ujifunze jinsi ya kukaa kwake. Nyuma ya kila jaribu kuna ushindi. Yule aliyeshikilia vitu vyako  kukuzuia wewe usipate Baraka zako, lazima umfyeke kwanza ili uweze kuvuka ng’ambo ya pili. Kabla ya tatizo, nilikuwa mtu wa kawaida, lakini  baada ya  tatizo nimehitimu chuo cha vita. Sikuzuii kunipinga ila ninaachojua ni kuwa  nitakusagasaga, kwa sababu imeandikwa “mimi ni rungu la Bwana na silaha za Bwana za vita”.
Kila kizazi kina mfalme na nabii wake. Mungu huangalia, pale anapoinuka Ahabu na Eliya lazima ainuke.  Ahabu haogopi  machozi ya akina Yeremia. Anapaswa kuinuka Eliya ili  aizuie mvua kwa miaka  mitatu  na nusu. Eliya hana majadiliano.  Hata kwa sasa lazima liwepo  kanisa ambalo halina majadiliano, Kanisa ambalo linalosema ,  "kabla ya kuzika huyu mtu, ‘maombi kwanza". Sisi hatusemi ‘Bwana ametoa na Bwana ametwaa  hapana‼! Kwa sababu hata wanadamu wapo wanaotwaa‼! Shetani hapaswi kubembelezwa. Siyo muda wa kukaa na kusema ‘tumshukuru Bwana kwa kila jambo’ siyo muda wa kufarijiwa kwa maneno matupu. Shetani  ni  wa kupigwa siyo wa kuombolezewa. Biblia inasema MATHAYO 2:18…“Sauti ilisikiwa Rama, Kilio, na maombolezo mengi, Raheli akiwalilia watoto wake, Asikubali kufarijiwa, kwa kuwa hawako.”. Inakuwa je wewe unakubali kirahisi tu kusimama na kumsubiri Bwana, badala ya kudai kilicho chako? Ili hilo tatizo lako liondoke, pigana‼

Usikatishwe tamaa na tatizo lililopo maishani  mwako, kwa sababu upo mlango  wa kutoka kwa hilo tatizo. Limekuwepo ili  wewe ujue jinsi ya kupigana. Biblia inasema ”Kila pando asilolipanda Baba litang’olewa”. Pando la magonjwa, pando la umaskini, pando  la kukosa kazi n.k lazima yang’oke kwa Jina la Yesu.  Cha muhimu kwako ni kupigana. Waliokueweka gerezani  ili usage ngano kama Samsoni, wajue kwamba hiyo ni njia ya kufanya misuli yako iongezeke. Na pale nywele za kichwa chako zitakapoota tena kama za Samsoni, wale utakaowaua baada ya kusaga ngano gerezani watakuwa ni wengi zaidi ya wale ulioua kabla  ya tatizo lako. Tatizo la kanisa la leo ni kuwa watu wamezoea kufarijiwa. Huyu shetani tuliye naye amezoea kuona unafarijiwa. Zipo aina mbili za sura ya  mdai anapokwenda kwa mdaiwa wake. Sura ya kwanza ya anayedai ni ile ambayo  humwendea mdaiwa huku akitabasamu, na kwa upande wa mdaiwa huwa haogopi chochote jinsi ya kulipa hilo deni la mtu kama huyu. Lakini mdai anapokuja na sura ya ghadhabu, mdaiwa hufanya juhudi  zote ili  kulipa salio lote la hilo deni husika. Leo ni  siku ya kudai kilicho chetu,  kwa kuvaa sura ya ukali kwa wale waliotuonea.
Bila kuwa na Yesu maishani mwetu si rahisi kudai kilicho chetu kutoka kwa shetani.  Wewe ambaye hujaokoka ni wasaa wako sasa kuamini na kumpa Yesu  Krsito maisha yako kwa kuokoka.

                          © Information Ministry (Ufufuo Na Uzima - Morogoro)

Mtaa wa Nguvu Kazi, (Minara Mitatu), Mkundi-Morogoro.

 /or

Contact our Senior Pastor:

 Dr. Godson Issa Zacharia

 (Ufufuo Na Uzima – Morogoro)

Cellphone: (+255) 757 550878 / +255 719798778

Comments