Askofu Gamanywa awavaa wanamuziki wa Injili wanaowaimbia na kuwasifu wanasiasa


Askofu mkuu wa kanisa la BCIC amewataka wanamuziki na waimbaji wa nyimbo za injili nchini Tanzania kujitathmini na kutathmini huduma zao na kile wanachokifanya kwa sasa katika kipindi hiki kuelekea uchaguzi mkuu wa madiwani,wabunge na Rais unaotarajiwa kuwafanyika mwezi October 2015 

Askofu Gamanywa ametoa kauli hiyo kupitia ukurasa wake wa kijamii katika mtandao wa face book ambapo ameelezea namna ambavyo katika kipindi hiki cha mbio za kuelekea uchaguzi mkuu nchini Tanzania,baadhi ya wanamuziki na waimbaji wa nyimbo za injili kutoa nyimbo zinazowasifia wanasiasa fulani na kuwashawishi wananchi wawapigie kura kwa hoja kwamba ndio chaguo la Mungu hali ambayo imeonekana kuleta utata kwenye jamii,ikizingatiwa kwamba Huduma ya uimbaji tangu mwanzo iliwekwa na Mungu ili kutumika kumsifu Mungu tu.


Blog hii imekuwekea uchambuzi huo aliouandika Askofu Gamanywa kama unavyosomeka hapa

CHANGAMOTO ZA WAIMBAJI WA NYIMBO ZA INJILI KUWAIMBA WANASIASA

Baada ya waimbaji fulani wa nyimbo za injili "kutunga nyimbo maalum za kuwasifia baadhi ya wanasiasa" waliotangaza nia; jamii ya baadhi ya wakristo imekwazika vibaya sana kiasi cha kutoa "maneno ya laana" dhidi yao

Ninatambua kuwepo kwa dhana hii ya:

"mwimbaji wa nyimbo za injili huduma yake ni kwa ajili ya kumwimbia Mungu tu wakati wa ibada au mikutano ya injili au matamasha ya nyimbo za injili"

Mapokeo haya yametujengea mtazamo wa kuwatafsiri "waimbaji binafsi" wa injili kuwa nao ni "watumishi kamili wa madhabahuni" tena kwa majina maarufu kama "walawi" au "wana wa Asafu" "wainjilisiti na wamishenari" kwa kupitia "nyimbo za injili"!

Sasa basi, pamoja na kwamba kitendo walichofanya "hao waimbaji binafsi wa nyimbo za injili" kimepokewa na kutafsiriwa kinyume; nadhani huu ni wakati muafaka wa kufanya upya tathmini kuhusiana na dhana au mtazamo au mapokeo yetu katika kuhakiki usahihi wake na kwa vigezo stahiki

Ili kuvipata vigezo hivi vya kutusaidia tathmini naomba tupate majibu sahihi ya maswali yafuatayo:

1. Je kitendo walichofanya ni "kosa la jinai" kwa mujibu Katiba na sheria halali za nchi? (Tuthibitishe ni vifungu gani vya kisheria vilivyokiukwa)

2. Je kitendo walichofanya ni "dhambi" mbele za Mungu? (Tuthibitishe kwa maandiko)

3. Je! Kitendo walichofanya ni "ukiukwaji wa maadili yenye mamlaka husika? Hivi tunayo mamlaka au taasisi maalum ya Kikristo inayosimamia "maadili ya waimbaji wa nyimbo za injili," na kutambua rasmi "huduma za waimbaji binafsi wa nyimbo za injili" kuwa nazo ni "huduma pekee za madhabahuni"; na hata kufanya tendo la "kuwasimika waimbaji binafsi wa nyimbo za Injili"? (Maana wachungaji na maaskofu wanasimikwa na kupewa vyeti vya utumishi wa madhabahuni! Vipi waimbaji wa nyimbo za injili?)

MAONI YANGU
Kama kitendo kilichofanyika sio "kosa la jinai," au "dhambi", au "sio uvunjifu wa maadili ya mamlaka husika" isipokuwa tu wamevuka "mipaka ya mapokeo/mazoea" na "mitazamo yetu" binafsi; narejea kusema kwa unyenyekevu mbele za Mungu kwamba ni muhimu sasa kutathmini upya uhalali na usahihi wetu kwa "kuwahukumu" kwa vigezo halali na makini.

Vinginevyo shutuma na lawama zetu dhidi yao vitatafsiriwa kuwa ni "sisi ndio tumekiuka na kuvunja haki zao za kikatiba na kisheria" kwa kuwa kitendo walichofanya ni haki yao ya kikatiba, kisheria na kizalendo wakitimiza demokrasia katika nchi yao kama raia huru!

Kwa kusema haya yote naomba nisitafsiriwe kwamba ninakubaliana au kuunga mkono kitendo kilichofanyika. Mimi pia bado nipo kwenye uchunguzi wa kina katika kutafuta vigezo makini vya kufanyia maamuzi

CHANZO CHA TATIZO
Kila tatizo lina chimbuko! Huenda waimbaji wa Injili wamefikia hapo walipo hivi sasa kwa sababu ya mtazamo hasi walionao juu ya uongozi wa kikanisa katika suala zima la ushirikishwaji wao ktk vipaji vyao vya uimbaji.

Yako malalamiko kutoka kwa baadhi ya "Waimbaji binafsi wa Injili" ambao wanadai kutumiwa vibaya na baadhi ya viongozi makanisa kwa mtindo wa kuwaalika ili wavute watu wengi kwenye Ibada na mikutano ya injili; na viongozi hao wanakusanya sadaka na matoleo na kisha wao waliotumia kuleta watu wengi hawapewi mafungu ya kumi au malipo ya sadaka zinazokusanywa kupitia vipaji vya uimbaji wao!?

Eneo jingine linalowachanganya zaidi waimbaji wa nyimbo za injili, hasa hali iliyokitokeza kwa wakuu wa makanisa ambao ni maaskofu na wachungaji walipoamua hadharani kujikita katika itikadi za kisiasa wakiunga mkono upande fulani kundi la kisiasa na kuwa kinyume dhidi ya upande mwingine? Tena maaskofu na wachungaji wengine wamejitokeza hadharani kuwa wapambe wa wagombea!

MSIMAMO WANGU BINAFSI
Mimi binafsi sina mgombea ambaye nampendelea kuliko wengine kwa
kuwa simjui ni yupi atakayechaguliwa kutawala nchi!

Nawatambua na kuwaheshimu na kuwaombea dua sawia wagombea wote wa vyama vyote!

Wakati wote wa kampeni za uchaguzi wajibu wangu ni kuhamasisha na kuelimisha na kuwashauri wagombea wote kuzingatia maadili na kulinda amani ya nchi!

Comments