KAZI ZA HUDUMA TANO NDANI YA KANISA.

BWANA YESU atukuzwe ndugu yangu.
Nakukaribisha tujifunze na tupate ufahamu utakaotusaidia katika safari yetu ya uzima wa milele.

Waefeso 4:11-12 '' Naye alitoa wengine kuwa mitume, na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti na wengine kuwa wachungaji na waalimu; kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke, hata mwili wa KRISTO ujengwe; '' 

-BWANA YESU ndiye aliyetoa huduma hizi 5 ukisoma kuanzia Mstari wa 9 wa hiyo waefeso 4 utaona iko hivyo. 
Jambo muhimu kujua ni kwamba Mitume wa kweli wanaletwa na BWANA YESU kwa ajili ya kulitimiza kusudi la injili. Mitume hawa wanaweza wakaitwa mitume na hata wanaweza wasiitwe mitume lakini kazi yao ni utume ambao MUNGU ameuweka ndani yao, hata wasipoitwa mitume bado  ni mitume maana wanafanya kazi ya utume sawasawa na Neno la MUNGU. Mtume yeyote akitenda katika utume wake mambo ambayo yako kinyume na BWANA YESU huyo sio mtume wa MUNGU maana mitume wa MUNGU hutimiza kusudi la MUNGU la injili.
Manabii wana huduma kutoka kwa MUNGU lakini nabii akisema mambo ambayo hayatokani na MUNGU huyo sio nabii wa kweli. Nabii wa kweli sio lazima aitwe Nabii ila kama anatumika sawasawa na kusudi la MUNGU kwa agizo la MUNGU katika unabii wake basi huyo ni Nabii. ila kama nabii yuko tofauti ya Neno la MUNGU na tena yuko tofauti na BWANA YESU huyo sio nabii wa MUNGU.
Uinjilisti ni huduma njema ambayo BWANA YESU ameiachilia kwa watumishi wake kupitia ROHO MTAKATIFU ambaye ndiye msimamizi wa Neno la MUNGU. Mwinjilisti lazima atumike chini ya kuongozwa na Neno la MUNGU.
Wachungaji na waalimu wa Neno la MUNGU ni watu muhimu sana katika kanisa la MUNGU. Wachungaji hawatakiwi kuwa wachungaji wa mishahara bali Wito maalumu kutoka kwa MUNGU. Walimu ni watu muhimu sana katika huduma ila mwalimu kama mfundishaji hatakiwi kufundisha uongo wa aina yeyote.
Mwili wa kanisa ni kanisa  na kanisa sio jengo wala dhehebu bali ni jumuia ya waaminio wote walio katika kweli ya MUNGU kupitia YESU KRISTO.
Kila huduma ina majukumu yake, kila huduma ni muhimu sana kwa kanisa. Shida iliyopo ni kila huduma kujiona ni wakubwa kuliko wengine kwa kigezo tu kwamba Biblia imeanza kuwataja wao badala ya wengine. Kuna watu hudhani kwamba huduma ya Ualimu ni ndogo kuliko unabii, kuna watu hudhani kwamba uchungaji ni huduma ndogo kuliko Uinjilisti. Sasa jiulize kama kanisa fulani mbeba maono ni Mchungaji ndani ya kanisa kuna manabii na wainjilisti inatakiwa wote wawe chini ya Mchungaji lakini watumishi wengine hukataa kuwa chini ya mbeba maono. Biblia haijasema popote kwamba Mwinjilisti ni huduma kubwa au ya maana zaidi kuliko ualimu au uchungaji.

Marko 16:15-18 ''Akawaambia, Enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe. Aaminiye na kubatizwa ataokoka; asiyeamini, atahukumiwa. Na ishara hizi zitafuatana na hao waaminio; kwa jina langu watatoa pepo; watasema kwa lugha mpya; watashika nyoka; hata wakinywa kitu cha kufisha, hakitawadhuru kabisa; wataweka mikono yao juu ya wagonjwa, nao watapata afya.''

Lengo la MUNGU kutoa huduma hizi 5 ni;

1.Kuwakamilisha watakatifu.
2.Ili huduma ya injili itendeke vizuri.
3 Ili kanisa la KRISTO duniani lijengwe.

1 Kor 12:4-12 ''  Basi pana tofauti za karama; bali ROHO ni yeye yule. Tena pana tofauti za huduma, na BWANA ni yeye yule. Kisha pana tofauti za kutenda kazi, bali MUNGU ni yeye yule azitendaye kazi zote katika wote. Lakini kila mmoja hupewa ufunuo wa ROHO kwa kufaidiana.  Maana mtu mmoja kwa ROHO apewa neno la hekima; na mwingine neno la maarifa, apendavyo ROHO yeye yule; mwingine imani katika ROHO yeye yule; na mwingine karama za kuponya katika ROHO yule mmoja; na mwingine matendo ya miujiza; na mwingine unabii; na mwingine kupambanua roho; mwingine aina za lugha; na mwingine tafsiri za lugha; lakini kazi hizi zote huzitenda ROHO huyo mmoja, yeye yule, akimgawia kila mtu peke yake kama apendavyo yeye. Maana kama vile mwili ni mmoja, nao una viungo vingi, na viungo vyote vya mwili ule, navyo ni vingi, ni mwili mmoja; vivyo hivyo na KRISTO. ''

Msingi  ulishajengwa na KRISTO, Kazi ya huduma hizi ni kusimamia kama MUNGU atakavyo.
Sio kazi ya huduma hizi kuanzisha  msingi mwingine bali msingi upo tayari na ulitengenezwa na BWANA YESU. Ukiona mtume au nabii kaanzisha msingi mwingine na sio msingi uliowekwa na KRISTO huyo hajatumwa na MUNGU bali adui.
Ukiona Mwinjilisti, Mchungaji au Mwalimu kaanzisha msingi mwingine nje na msingi uliowekwa na BWANA YESU huyo hajatumwa na MUNGU ila shetani.
 Ndugu yangu, hakikisha unatumika vyema katika huduma yako aliyokupa BWANA YESU. Hakikisha huduma yako inakua lakini ukibaki katika kusudi la MUNGU na sio kuhamia kusudi la shetani.
Kuna wakati huduma yako inaweza kupata majaribu lakini nakutia moyo na tambua kwamba Huduma yako kama ndi ndogo na jaribu litakuwa dogo lakini kama huduma yako ni kubwa basi hata jaribu lako litakuwa kubwa. vumilia kama mitume na watumishi wa zamani walivyovumilia. usiondoke katika msingi wa BWANA YESU na kama kuna roho ya kujiinua inakufuatilia ikatae kwa maombi na maamuzi. 
 Huduma yako isiwepo tu kwa sababu ipo bali iwepo kwa sababu YESU KRISTO ndio kiini cha huduma yako.

-Ndugu, linda huduma yako ili isiingiliwe na pando la shetani.
-Usiitupe huduma uliyopewa na MUNGU.
-Ijari huduma yako na kuiombea.
 -Usiwe mtawanyaji na mharibifu wa huduma njema za wengine.
Sote tumeitwa na BWANA mmoja na tunajenga jengo moja kwanini kugombana?
Lengo la kuitwa kwetu ni ili watu wampokee YESU na kuanza kuishi maisha matakatifu, kwanini tusemane vibaya?

1 Kor 3:9 ''  Maana sisi tu wafanya kazi pamoja na MUNGU; ninyi ni shamba la MUNGU, ni jengo la MUNGU.''

-Watumishi wote wa kweli wa MUNGU wanatakiwa watambue jambo hilo.
Wachungaji mkikosana tambueni kwamba anayefaidika ni shetani na sio yeyote.
Mitume mkigeuza mahubiri yenu kuwa mipasho ya kuwasema vibaya wengine, anayefaidika hapo ni shetani na sio vinginevyo.
Kama kuna mmoja wetu amegeuka na sasa sio mtumishi wa MUNGU tena bali mtumishi wa shetani na maandiko yanathibitisha basi huyo na akemewe ili asiendelee kupotosha watu wakati yeye mwenyewe alishamwacha BWANA YESU siku nyingi.

Huduma au kazi yako utalipwa. kama ni kazi mbaya utalipwa na kama ni kazi nzuri wewe una heri.

1 Kor 3:11-14 ''Maana msingi mwingine hakuna mtu awezaye kuuweka, isipokuwa ni ule uliokwisha kuwekwa, yaani, YESU KRISTO. Lakini kama mtu akijenga juu ya msingi huo, dhahabu au fedha au mawe ya thamani, au miti au majani au manyasi, kazi ya kila mtu itakuwa dhahiri. Maana siku ile itaidhihirisha, kwa kuwa yafunuliwa katika moto; na ule moto wenyewe utaijaribu kazi ya kila mtu, ni ya namna gani. Kazi ya mtu aliyoijenga juu yake ikikaa, atapata thawabu. '' 

-Ndugu,Naamini umejifunza na utachukua hatua njema ya kumpokea BWANA YESU kama hujaokoka  ili awe BWANA na MWOKOZI wako tangu leo na utaanza kuishi maisha matakatifu
KAMA UNATAKA KUTUBU RUDIA MANENO HAYA KISHA TAFUTA KANISA LA KIROHO UKAJIUNGE NA KUANZA KUISHI MAISHA MATAKATIFU.
''BABA katika jina la YESU KRISTO Niko mbele zako mimi mwenye dhambi, lakini leo nimetambua kosa langu na naomba unisamehe dhambi zangu zote, nisamehe dhambi ninazozikumbuka na pia zile ambazo sizikumbuki. futa jina langu katika kitabu cha hukumu na uliandike jina langu katika kitabu cha uzima. Neno lako katika Warumi sura ya 10 Mstari wa 9 na wa 10 Neno lako linasema ''Kwa sababu, ukimkiri YESU kwa kinywa chako ya kuwa ni BWANA, na kuamini moyoni mwako ya kuwa MUNGU alimfufua katika wafu, utaokoka. Kwa maana kwa moyo mtu huamini hata kupata haki, na kwa kinywa hukiri hata kupata wokovu '' . BWANA YESU mimi nimekuamini leo na hivyo naamini sasa napokea wokovu wako na hakika nimeokoka. Kuanzia leo Naufunga ukurasa wa dhambi na ninaufungua ukurasa wa matendo mema na matakatifu. BWANA nipe ROHO wako Mtakatifu ili aniwezeshe kushinda dhambi na anasa zote za dunia. Kuanzia leo mimi nimeokoka na ni mtoto wa MUNGU mwenye haki zote. ninafuta laana zote na kila roho ya shetani inayonifuatilia naiharibu kwa jina la YESU KRISTO kama neno la MUNGU linavyosema katika Yeremia sura ya kwanza mstari wa 10. BWANA YESU nakushukuru sana kwa kuniokoa. Yote haya kwa imani nimepokea na niko tayari sasa kwa ROHO MTAKATIFU kunitumia. Katika jina la YESU KRISTO nimeomba na kupokea Amen.
Kama umetubu toba ya kweli hakika wewe kuanzia sasa ni mshindi na ni shujaa. Kwa sasa naishia hapo, MUNGU akitupa nafasi tutajifunza tena siku nyingine. ulishindwa kumpokea BWANA YESU nafasi yako bado ipo na muda wa kumpokea ni leo wala sio kesho, amua leo na atakuandika jina lako katika kitabu cha uzima na utaanza kuukulia wokovu kwa mafundisho kanisani. MUNGU ana makusudi kabisa na wewe, hataki upotelee motoni anataka uende uzimani aliko KRISTO BWANA. MUNGU akubariki sana .
Ni mimi ndugu yako Peter M Mabula
+255714252292
mabula1986@gmail.com
MUNGU akubariki sana uliyesoma somo hili.

Comments