KUMILIKI HAZINA NA MALI

Na Askofu Dr Josephat Gwajima.

“Maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, jinsi alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake.” 2 Wakorintho 8:9

Mtume Paulo anasema Yesu aliamua awe maskini kwaajili yetu ili kwa njia ya umaskini wake sisi tuwe matajiri. Kama wewe bado ni maskini basi Yesu alaifanyika maskini bure. Yesu kristo alikuja kutoka mbinguni akadhalilishwa kwaajili yetu ili sisi tufanikiwe. Tunakiwa tumiliki na tuwe na mali, utajiri na heshima itokayo kwa Mungu.
Unaposema kumiliki hazina na mali kwa watu wenye imani ya kawaida wanashangaa.
“nami nitakupa hazina za gizani, na mali zilizofichwa za mahali pa siri, upate kujua ya kuwa mimi ni Bwana, nikuitaye kwa jina lako, naam, Mungu wa Israeli.” Isaya 45:3

Ziko hazina na mali lakini zipo gizani zimefichwa na mahala zilipofichwa ni sehemu ya siri, zinapoitwa ni za gizani unatakiwa ujue kuna mfalme wa giza anayezishikilia, lakini yupo pia mfalme wa nuru. Tunatakiwa tuzifuate na tuzichukue tuzimiliki. Haijalishi umesoma au hujasoma Mungu amesema atakupa hazina iliyopo gizani na utafanikiwa kwenye maisha yako.
Chanzo cha historia ya utajiri na mali sio Japan na Marekani wala Uarabuni au ulaya bali ni Mbinguni kwa Baba yetu.
“Na ile milango kumi na miwili ni lulu kumi na mbili; kila mlango ni lulu moja. Na njia ya mji ni dhahabu safi kama kioo kiangavu.” UFUNUO WA YOHANA 21:21

Mbinguni milango yote ni almasi(lulu) safi na barabara za kule ni dhahabu safi, Mungu anatupa ujumbe kwamba mbinguni kuna utajiri mkubwa na historia ya mali na utajiri ni mbinguni tulipotoka.
“Na mmojawapo wa wale wazee akaniambia, Usilie; tazama, Simba aliye wa kabila ya Yuda, Shina la Daudi, yeye ameshinda apate kukifungua kile kitabu, na zile muhuri zake saba. Nikaona katikati ya kile kiti cha enzi na wale wenye uhai wanne, na katikati ya wale wazee, MwanaKondoo amesimama, alikuwa kana kwamba amechinjwa, mwenye pembe saba na macho saba, ambazo ni Roho saba za Mungu zilizotumwa katika dunia yote. Akaja, akakitwaa kile kitabu katika mkono wa kuume wake yeye aliyeketi juu ya kile kiti cha enzi. Hata alipokitwaa kile kitabu, hao wenye uhai wanne na wale wazee ishirini na wanne wakaanguka mbele za MwanaKondoo, kila mmoja wao ana kinubi, na vitasa vya dhahabu vilivyojaa manukato, ambayo ni maombi ya watakatifu. Nao waimba wimbo mpya wakisema, Wastahili wewe kukitwaa hicho kitabu na kuzifungua muhuri zake; kwa kuwa ulichinjwa, ukamnunulia Mungu kwa damu yako watu wa kila kabila na lugha na jamaa na taifa, ukawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu; nao wanamiliki juu ya nchi. Nikaona nikasikia sauti ya malaika wengi pande zote za kile kiti cha enzi, na za wale wenye uhai, na za wale wazee, na hesabu yao ilikuwa elfu kumi mara elfu kumi na elfu mara elfu,wakisema kwa sauti kuu, Astahili MwanaKondoo aliyechinjwa, kuupokea uweza na utajiri na hekima na nguvu na heshima na utukufu na baraka.” Ufunuo wa yohana 5:12

Astahiliye kupokea utajiri ni mwanakondoo pekee Yesu kristo ambaye ndiye atupaye utajiri, heshima na utukufu sisi aliotununua kwa damu yake hapa duniani.
“Nchi na vyote viijazavyo ni mali ya Bwana, Dunia na wote wakaao ndani yake.” Zaburi 24:1
Nchi imejazwa na madini, gesi, mimea, milima na viumbe vyote na wanaokaa ndani yake ni mali ya Bwana Yesu.
“Fedha ni mali yangu, na dhahabu ni mali yangu, asema Bwana wa majeshi.“ Hagai 2:8
Shetani amefanikiwa kuwadanganya watu kwamba fedha na dhahabu ni mali yake lakini kiuhalisia fedha na dhanabu ni mali ya Bwana.
“Bali utamkumbuka Bwana, Mungu wako, maana ndiye akupaye nguvu za kupata utajiri; ili alifanye imara agano lake alilowapa baba zako, kama hivi leo.” Kumbukumbu la torati 8:18
Kuna nguvu za kutawala, kufufua na kuna maarifa na akili za kupata utajiri kutoka kwa Mungu na haijalishi uko kwenye hali gani unatakiwa ufahamu utajiri udumuo unatoka kwa Mungu Baba wa mbinguni
2. UTAJIRI NA HESHIMA VINAENDANA.
KUTOKA 19:5
“Sasa basi ikiwa mtaitii sauti yangu kweli kweli, na kulishika agano langu, hapo ndipo mtakapokuwa tunu kwangu kuliko makabila yote ya watu; maana dunia yote pia ni mali yangu, 6 nanyi mtakuwa kwangu ufalme wa makuhani, na taifa takatifu. Hayo ndiyo maneno utakayowaambia wana wa Israeli.”

Utajiri na mali ni haki yetu na historia yake ni mbinguni.
“Bwana atakufanya kuwa kichwa, wala si mkia; nawe utakuwa juu tu, wala huwi chini; utakapoyasikiza maagizo ya Bwana, Mungu wako, nikuagizayo hivi leo, kuyaangalia na kufanya” Kumbukumbu la torati 28:13~17
Mungu anasema kwenye neno lake Bwana atakufanya kuwa kichwa wala si mkia na utakuwa juu tu wala si chini. Tumemiliki tayari kwenye ulimwengu wa roho na sasa tunaenda kumiliki mwilini kwa jinsi ya mwilini. Utajiri unaleta heshima na maskini hatakama ana mawazo mazuri siku zote hathaminiwi na haskilizwi na atakuwa mtumwa wa tajiri na mwenye mali siku zote anatafutwa na kuheshimiwa. Mlokole ni mtu hatari sana akipata utajiri na ndio maana shetani amefanikiwa kumkaba mtu wa Mungu eneo la fedha na watu wengi wamerudi nyuma na kuacha wokovu sababu ya eneo la fedha.
“Utajiri na heshima hutoka kwako wewe, nawe watawala juu ya vyote; na mkononi mwako mna uweza na nguvu; tena mkononi mwako mna kuwatukuza na kuwawezesha wote.” 1 Mambo ya nyakati 29:12
Mwenye kutuwezesha ni Bwana wa majeshi Mungu wetu.
“Ana wingi wa siku katika mkono wake wa kuume, Utajiri na heshima katika mkono wake wa kushoto.” Mithali 3:16
“Nawapenda wale wanipendao, Na wale wanitafutao kwa bidii wataniona. Utajiri na heshima ziko kwangu, Naam, utajiri udumuo, na haki pia.” Mithali 8:17~18
Kuna mali na heshima isiyo dumu ipatikanayo kwa shetani na kuna mali na heshima inayodumu ambayo inapatikana kwa Mungu.
“Thawabu ya unyenyekevu ambao ni kumcha Bwana Ni utajiri, na heshima, nayo ni uzima.” Mithali 22:4
3. BABA ZETU WA IMANI WALIOKUWA MATAJIRI
“Naye Abramu alikuwa ni tajiri sana kwa mifugo, kwa fedha, na kwa dhahabu. Akaendelea kusafiri kutoka kusini mpaka Betheli, mahali pale palipokuwapo hema yake kwanza kati ya Betheli na Ai; napo ndipo palipokuwa na madhabahu aliyofanya hapo kwanza; naye Abramu akaliitia jina la Bwana hapo. Na Lutu aliyesafiri pamoja na Abramu, yeye naye alikuwa na makundi ya ng'ombe na kondoo, na hema. Na ile nchi haikuwatosha, ili wakae pamoja; maana mali zao zilikuwa nyingi, hata wasiweze kukaa pamoja.” Mwanzo 13:2~6
Ibrahimu alikuwa na mali nyingi na alisafiri na kujenga na kuliitia jina la Bwana lakini leo hii watu wanaomba kwa Mungu wa Ibrahimu, Isaka na Yakobo huku wakiwa hawazipati zile Baraka zake alizokuwa nazo, “Mungu ana mpango wa kukupa fedha na mali na utasafiri na kujenga kwajina la Yesu”. Farao alifahamu umuhimu wa mali na alimwambia Musa waondoke bila mali zao lakini Musa alimjibu farao wataondoka na mali zao zote na hawataacha hata kwato.
Abrahamu na Lutu walikuwa na mali nyingi mpaka wakaamua kutengana. Zamani watu walikuwa wakiteka miji walikuwa wakichukua mali na kuwaacha watu bila kuwagusa.
“Wakachukua mali zote za Sodoma na Gomora na vyakula vyao vyote, wakaenda zao. Wakamtwaa Lutu, mwana wa nduguye Abramu, aliyekaa huko Sodoma, na mali yake, wakaenda zao.” Mwanzo 14:11~13
Ibrahimu Baba wa imani alienda kumrudisha Lutu na mali zake zote.
“Naye akarudisha mali zote, akamrudisha na Lutu nduguye na mali zake, na wanawake pia, na watu.” Mwanzo 14:16
Tunatakiwa turudishe mali kwa jina la Yesu siyo watu warudi mikono mitupu na mali iliyofichwa mahali pia inatakiwa irudishwe.
“Hata na taifa lile, watakaowatumikia, nitawahukumu; baadaye watatoka na mali mengi.” Mwanzo 15:14
“Basi Abimeleki akawaamuru watu wote, akisema, Amgusaye mtu huyu au mkewe lazima atauawa. Isaka akapanda mbegu katika nchi ile, akapata mwaka ule vipimo mia kwa kimoja, Bwana akambariki. Na mtu huyu akawa mkuu, akazidi kusitawi, hata akawa mkuu sana. Akawa na mali ya kondoo, na mali ya ng'ombe, na watumwa wengi. Hao Wafilisti wakamhusudu.” MWANZO 26:11~14
ISAKA ALIKUWA NA MALI NYINGI.
Abrahamu alikuwa tajiri na mwanaye naye akawa tajiri, lakini hakuachiwa utajiri na Baba yake.
“Maana mali yako ilikuwa haba kabla sijaja, nayo imezidi kuwa nyingi, Bwana akakubariki kila nilikokwenda. Basi sasa, nitaangalia lini mambo ya nyumba yangu mwenyewe? Mwanzo 30:30
“Yakobo naye alikuwa tajiri. Basi Yakobo akasikia maneno ya wana wa Labani, wakisema, Yakobo amechukua mali yote ya baba yetu; na kwa mali ya baba yetu amepata fahari hii yote. 16 Maana mali yote ambayo Mungu amemnyang'anya baba yetu, mali hiyo ndiyo yetu na ya wana wetu. Basi yo yote Mungu aliyokuambia, uyafanye 18 Akachukua wanyama wake wote, na mali yake yote aliyokuwa ameyapata, na wanyama aliowapata katika Padan-aramu, ili afike kwa Isaka babaye katika nchi ya Kanaani.” Mwanzo 31:1-
Yakobo alikuwa hana kitu sababu alikuwa anamkimbilia kaka yake na alipofika huko akawa tajiri. Alikuwa anafanya biashara.
“Nanyi mtakaa nasi, na nchi hii itakuwa mbele yenu; kaeni, na kufanya biashara humo, mkapate mali humo.” Mwanzo 34:10
Mungu alikuwa anawaruhusu watu wake wafanye biashara wawe matajiri.
MALI YA ESAU
“Esau akawatwaa wakeze, na wanawe, na binti zake, na watu wote wa nyumbani mwake, na ng'ombe zake, na wanyama wake wote, na mali yake yote, aliyoyapata katika nchi ya Kanaani; akaenda mpaka nchi iliyo mbali na Yakobo nduguye. Maana mali yao yalikuwa mengi wasiweze kukaa pamoja, wala haikuweza nchi ya kusafiri kwao kuwachukua, kwa sababu ya wanyama wao.” Mwanzo 36:6 - 7
Baadhi ya Mitume hawakuwa na mali na wengine walikuwa na mali. Mfano Petro na Yohana hawakuwa na mali lakini Paulo alikuwa na mali na ndiomaana Mtume Paulo alitembea nchi nyingi barani Asia na Ulaya kuhubiri injili ya Yesu kristo na ndiye aliyeandika vitabu vingi kwenye agano jipya.
“Baada ya mambo hayo, Paulo akatoka Athene akafika Korintho. Akamwona Myahudi mmoja, jina lake Akila, mzalia wa Ponto; naye amekuja kutoka nchi ya Italia siku za karibu, pamoja na Prisila mkewe, kwa sababu Klaudio amewaamuru Wayahudi wote watoke Rumi, naye akafikilia kwao; na kwa kuwa kazi yao ya ufundi ilikuwa moja, akakaa kwao, wakafanya kazi pamoja, kwa maana walikuwa mafundi wa kushona hema.” Matendo ya mitume 18:1~5
Athene, thesalonike, italia, korintho zote hizo zilikuwa ni ulaya ndiomaana mtume Paulo alikuwa anakwenda kwasababau ya Utajiri wake aliokuwa nao.
Petro na Yohana hawakuwa na mali lakini walikuwa na nguvu za Mungu.
“Na Petro, akimkazia macho, pamoja na Yohana, akasema, Tutazame sisi. Akawaangalia, akitaraji kupata kitu kwao. Lakini Petro akasema, Mimi sina fedha, wala dhahabu, lakini nilicho nacho ndicho nikupacho. Kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, simama uende.” Matendo ya mitume 3:4~6
Wagalatia 3:13
“Kristo alitukomboa katika laana ya torati, kwa kuwa alifanywa laana kwa ajili yetu; maana imeandikwa, Amelaaniwa kila mtu aangikwaye juu ya mti; ili kwamba baraka ya Ibrahimu iwafikilie Mataifa katika Yesu Kristo, tupate kupokea ahadi ya Roho kwa njia ya imani.”

Wayahudi walikwenda katika nchi ya misri wakiwa watumwa baada ya muda wakawa tishio.
“Yusufu akakusanya fedha zote zilizoonekana katika nchi ya Misri na katika nchi ya Kanaani, kwa nafaka waliyoinunua. Yusufu akazileta zile fedha nyumbani mwa Farao. Fedha zote zilipokwisha katika nchi ya Misri na katika nchi ya Kanaani, Wamisri wote walimjia Yusufu, wakisema, Tupe sisi chakula, kwa nini tufe mbele ya macho yako? Maana fedha zetu zimekwisha.” Mwanzo 47:14
Unatakiwa umiliki kila mahali na usiwasikilize wale wanaokuambia bakia ukinena kwa lugha usifuate mali, unatakiwa ukatae na uamue kwenda kumiliki kila mahali na kuwa juu Mungu atengeneze njia ya wewe kumiliki mali kwa jina la Yesu, mapori ya umaskini na kupungukiwa yanafyeka kwa kwa jina la Yesu. Kuna watu wanaenda kanisani na kuabudu kwa furaha hawana hata nauli lakini sisi tumeamua kusimama kwenye wokovu kumiliki na kupata heshima. Tunatakiwa tumiliki mashamba, magari, tusome, tusafiri, tuwe wanasiasa, tuwe madaktari, tuwe na utajiri na heshima tumiliki juu ya nchi kwa jina la Yesu na hili linawezekana sababu Mungu ameweka kitu ndani yetu sababu sisi ni wana wa Mungu watu hatari tunamiliki misingi ya utajiri na heshima kwa jina la Yesu.
Leo watu wanatumiwa makazini na kupewa vitu vizuri kazini kwa kubembelezwa ili uendelee kukaa pale, umekuwa mtumwa na mwenye kampuni yeye anaingiza fedha na kutembea sehemu yeyote atakayo huku wewe ukibaki kutegemea mshahara. Unaweza kuanzisha jambo jipya ambalo halijawahi kufanywa na mtu yeyote Yule na ukafanikiwa kwa jina la Yesu. Sio lazima uajiriwe.
Ukiri:
“Nakataa kutumiwa kwa jina la Yesu”

MHUBIRI 10:5~7
“Liko baa nililoliona chini ya jua, nalo ni kama kosa litokalo kwake yeye atawalaye; ya kuwa upumbavu huwekwa mahali pa juu sana, nao wakwasi hukaa mahali pa chini. Mimi nimeona watumwa wamepanda farasi, na wakuu wakienda kwa miguu juu ya nchi kama watumwa.”

Leo watu wapumbavu wasio na akili hawana Mungu wako juu lakini wewe unayenena kwa lugha na una akili za Mungu umekaa chini na unatembea kwa miguu na wale wanaosema hawana Mungu (wapumbavu) wasiomwamini Mungu wanaendesha na kupanda ndege na kuheshimika kwa mali zako kihalali. Shetani akikuteka anakunyanganya mali, akili na fedha anakuacha uendelee kumwabudu Mungu ukiwa maskini na mwisho unakuwa hauna madhara kwenye ufalme wake.
DANIEL 1:1~2
“Katika mwaka wa tatu wa kumiliki kwake Yehoyakimu, mfalme wa Yuda, Nebukadreza a, mfalme wa Babeli, alikwenda Yerusalemu akauhusuru. Bwana akamtia Yehoyakimu, mfalme wa Yuda, katika mkono wake, pamoja na baadhi ya vyombo vya nyumba ya Mungu; naye akavichukua mpaka nchi ya Shinari, mpaka nyumba ya mungu wake; akaviingiza vile vyombo katika nyumba ya hazina ya mungu wake.”

Mfalme wa babeli alichukua hazina na mali na kwenda kuiweka kwenye hazina ya shetani, pia alichukua wenye akili na wenye uwezo wa kutengeneza mali akawachukua nao na kuwapeleka kujenga ufalme wake wa Babeli, inamaana mfumo wa babeli unachukua wazuri, wenye akili, wazuri wa uso wanawachukua na kuwapeleka kujenga makampuni yao na kuingiza faida na wanafanya hivyo mpaka wazeeke au kuwaacha ikitokea pale wameugua. Shetani anatabia ya kuwachukua vijana wenye akili na kuwatumia kasha kuwatelekeza wanapozeeka kwa posho ambayo haikidhi mahitaji yao, kanisa linatakiwa liwasaidie akili za vijana ili wafaidike kwa akili zao ili wafanye mambo makubwa yenye kuwapa utajiri na mali idumuyo kwa jina la Yesu. Duniani maskini wanakufa haraka lakini matajiri wanaishi muda mrefu sababu ya utajiri wao.
Leo Dunia imewekeza kwa vijana imewapa muziki, mali, utajiri usiodumu lakini kanisa limeshindwa kuwapa vijana chochote lakini leo tunacho cha kuwapa vijana kwa jina la Yesu. Dunia inawachukua vijana na kuwabadilisha majina pamoja na kuwapa vyakula (mafundisho) ya kuwapofusha fikra zao na ndiomaana ukimwambia mtu njoo kwa Yesu anashindwa kuona njia au umuhimu wa kuwa ndani ya Yesu sababu ya kulishwa vyakula vya kuwasahaulisha washindwe kujitambua na kufanya wanachotakiwa kukifanya.
“Tajiri humtawala maskini, Naye akopaye ni mtumwa wake akopeshaye.” Mithali 22:7
“Bwana akawaamsha roho Wafilisti, na Waarabu waliowaelekea Wakushi juu ya Yehoramu, nao wakakwea juu ya nchi ya Yuda, wakaipenya, wakaichukua mali yote iliyoonekama nyumbani mwa mfalme, na wanawe pia, na wakeze; asisaziwe mwana hata mmoja, ila Ahazia, k aliyekuwa mdogo miongoni mwa wanawe.” 2 Mambo ya nyakati 21:16~17
Hii shetani amechukua kwa watu kila kitu kutoka kwa vijana na amewaacha bila kitu chochote. Na akitaka kumteka mtu kwanza anamnyanganya mali na akitaka kuliangusha kanisa analinyanganya mali na ndivyo alivyolifanya kanisa duniani kwamba watu wasiwe na mali ila wawepo watu wanyonge wanyonge wasio na maana huku wenye nguvu na akili ya kumiliki akaondoka nao na kuwatumia kwa ufalme wake.
“Na wana wa Israeli, na makuhani na Walawi, na watu wengine katika hao waliohamishwa, wakaiweka wakfu nyumba ya Mungu kwa furaha. Na katika kuiweka wakfu nyumba ya Mungu, wakatoa sadaka, ng'ombe mia, na kondoo waume mia mbili, na wanakondoo mia nne; tena wakatoa mbuzi waume kumi na wawili, kuwa sadaka ya dhambi kwa ajili ya Israeli wote, kwa hesabu ya kabila za Israeli. Wakawaweka makuhani katika kura zao, wakawaweka na Walawi katika zamu zao, kwa ajili ya huduma ya Mungu, iliyokuwako Yerusalemu; vile vile kama vilivyoandikwa katika chuo cha Musa.” Ezra 6:16~18
“Akawachukua mateka watu wa Yerusalemu wote pia, na wakuu wote, na mashujaa wote, watu elfu kumi; na mafundi wote, na wafua chuma wote; hapana mtu aliyebaki, ila waliokuwa wanyonge wa watu wa nchi. Akamchukua Yekonia mpaka Babeli; na mama yake mfalme, na wake zake mfalme, na maakida wake, na wakuu wa nchi, aliwachukua mateka toka Yerusalemu mpaka Babeli. Na mashujaa wote, watu elfu saba, na mafundi na wafua chuma elfu moja, wote pia wenye nguvu, tayari kwa vita, hao wote mfalme wa Babeli aliwachukua mateka mpaka Babeli.” 2 WAFALME 24:14~16
“Akafa mwenye umri mwema, ameshiba siku, na mali, na heshima; naye Sulemani mwanawe akamiliki badala yake.” 1 Mambo ya nyakati 29:28
“Basi, Yehoshafati alikuwa na mali na heshima tele, tena akafanya ujamaa na Ahabu.” 2 MAMBO YA NYAKATI 18:1
“Nao Yehoshafati na watu wake walipokuja kuchukua nyara zao, wakaona kati yao wingi wa mali, na mavazi, na johari za thamani, walivyojivulia, zaidi kuliko wawezavyo kuchukua; wakawa siku tatu katika kuteka nyara, maana zilikuwa nyingi sana.” 2 Mambo ya nyakati 20:25
Pamoja na ahadi zote hizi tulizozisoma kwamba Mungu anataka watu wote wawe matajini lakini kwanini watu ni maskini?
“ambao ndani yao mungu wa dunia hii amepofusha fikira zao wasioamini, isiwazukie nuru ya injili ya utukufu wake Kristo aliye sura yake Mungu.” 2 Wakorintho 4:4
Shetani jina laki jingine anaitwa mungu wa dunia hii na kazi yake ni kumfanya mtu kuwa kipofu , anamfanya mtu awaze akiolewa tu imetosha, akipata kazi tu imetosha huo ni upofu wa fikra wa shetani, na giza hilo liondolewe kuwako kwa jina la Yesu.
Umaskini na mapepo vina uhusihano, magonjwa na mapepo vina uhusihano, ujinga na mapepo vina uhusihano, shetani anawawekea watu ujinga kwanza kwamba mtu huwezi kumiliki mali sababu mjomba wako anauwezo wa kukusaidia kila siku au kaka yako ana mali hivyo utapata msaada, na kwasababu hiyo unamkuta mtu amepofushwa fikra na shetani kwa stahili hiyo.
Kwenye kufanikiwa kuna kushiba siku, kushiba mali na heshima kutimiza lililokuleta hapa duniani halafu ndio unakufa, ila kushiba maombi, kufunga na kupiga majeshi hapo bado hujafanikiwa. Kwenye ulimwengu wa roho tumemiliki na wachawi na wasomanyota na watumishi wa shetani wanalijua hilo hivyo hawawezi kutugusa.
Tuanze safari ya kutoka kwenye umaskini na kwenda kwenye utele kwa jina la Yesu hata kama ulianguka usiseme huwezi kama hujajaribu mara milioni moja kwa siku. Usiangalie elimu uliyonayo angalia nyota ya vipawa ulivyonavyo na akili ulizopewa na Mungu.
“Kuna umaskini mwingine unatokana na historia za familia sababu ya mapepo ambayo hayaruhusu uwe na mali” tunatakiwa tuvunje historia hiyo kwa jina la Yesu, mfano kwenye ukoo hakuna mbunge hata mmoja au mfanya biashara mkubwa na wewe unapojaribu kufanya hivyo unashindwa na unaona unao uwezo wa kufanya maana yake roho ya umaskini haiwezi kukuwaachia ufanikiwe.
Maombi:
“Kwa mamlaka ya Jina la Yesu kristo ninaiondoa roho ya umasikini kwenye maisha yangu kwa jina la Yesu, roho ya mizimu ya ukoo wa Babu yangu ninaivunja kwa damu ya Yesu, mashetani na majini ya mikataba ya ukoo ninayateketeza kwa jina la Yesu, kuanzia leo ninajitenga na matambiko na mizimu ya ukoo wa Baba yangu na Mama yangu ambayo yamenishikilia nisimiliki utajiri na hazina kwa jina la Yesu, ninamiliki juu ya nchi kwa jina la Yesu ninatawala kwa jina la Yesu, nina tiisha kwa jina la Yesu ninaijaza nchi kwa jina la Yesu Kristo” Amen.

Comments