Na Pastor Bryson Lema, Ufufuo na uzima  Morogoro.
Utangulizi:
Upo
"mgawo wa kishetani" kwenye maisha ya wanadamu. Katika Kitabu cha MIKA 2:4 imeandikwa hivi:…[Siku hiyo
watatunga mithali juu yenu, na kuomboleza kwa maombolezo ya huzuni nyingi, na
kusema,  Sisi tumeangamizwa kabisa;  Yeye analibadili fungu la watu wangu;  Jinsi anavyoniondolea hilo! Awagawia waasi
mashamba yetu.]…. Jambo la muhimu  katika andiko 
hili  ni kuwa kuna mgawo, tena wa
mashamba. Na kama kuna mgawo, ujue yupo 
mwenye kugawa. Swali la  kujiuliza
hapa ni kuwa,  kwa nini mashamba haya
yagawiwe kwa waasi? Maana yake, mali zangu, 
vitu vyangu vimegawiwa kwa shetani, kwa sababu Biblia inamuonesha
shetani kuwa aliasi kule mbinguni. Na kwa hiyo sasa, huyu  shetani amevikamata vitu vyangu,  akavifanya 
kama vyake.
Ukisoma YEREMIA
1:5 imeandikwa:…[Kabla sijakuumba katika tumbo nalikujua, na kabla
hujatoka tumboni, nalikutakasa; nimekuweka kuwa nabii wa mataifa.]…
maana yake,  kabla ya Yeremia
kuzaliwa,  alishagawiwa mgawo wake
unaomhusu.  Alitakiwa  aende katika mafanikio yake kwa sababu tayari
anao mgawo wake kutoka kwa muumba wake, yaani Mungu (Jehovah).
Shetani alichokifanya ni kutuibia.  Biblia inasema katika YOHANA 10:10 [Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi
nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele.]. Ndani ya
maisha yako,vipo vitu unavyopitia visivyo kuwa vya kwako. Maana yake,  una vitu ambavyo unaviona kama vyako lakini
kumbe ni  “mgawo wa kishetani”. Walipokaa mashetani na mawakala wao,
walikutengenezea ugonjwa,  na ambao
unakaa nao kwa muda mrefu sasa, na hata imefikia wakati umeanza kuuita huo
ugonjwa kuwa ni ‘ugonjwa wangu’. 
Ayubu  vivyo hivyo, alipata magonjwa
na adha mbalimbali, lakini vyote hivi hakugawiwa na Bwana, bali ulikuwa mgawo
wa kishetani. Kosa ambalo wengi wameendelea kulikiri leo hii ni kuungana na
maneno ya Ayubu kusema ‘Bwana ametoa, na Bwana ametwaa”.
Siyo kweli  kwamba Bwana anapokupa
anakuja mara ya pili  kutwaa kile
alichokupatia.  Ingekuwa hivyo basi
Ibrahimu alipoambiwa amtoe sadaka mwanae pekee Isaka,  basi siku ile ile Isaka angechinjwa. Ili
kudhihirisha hili, Bwana hakuruhusu Isaka afe, na badala yake alimuepusha na
kifo kile cha kutolewa sadaka na Ibrahimu baba yake.
Upo mgawo wa kishetani unaong’ang’ania maisha yako. Wakati
mwingine unajikuta kuna mambo unashindwa kuyaacha maishani mwako kwa sababu
tayari huo ni mgawo. Imeandikwa EZEKIELI
23:7…[ Akawagawia mambo yake ya
kikahaba, watu wateule wa Ashuru, wote pia; akajitia unajisi kwa vinyago vyote
vya kila mmoja wa hao aliowapenda.]… Unapoupata mgawo, huo
mgawo unakuwa sehemu ya maisha yako. Ndiyo maana unakuta maisha ya mtu yanakuwa
magumu kwa sababu kuna mgawo wa kishetani ndani ya  maisha yake, na siku ya leo ni maalumu kwa
ajili ya kumrudishia  shetani migawo yake
kwa Jina la Yesu.
Mwanadamu mara 
zote anakuwa na Tabia ya kukataa mambo mapya.  Hata hivyo, baada ya mambo mapya kuanza na
kuyazoea, mwanadamu husahau kuwa mwanzoni 
hakuwa anafurahia hali hiyo. Mfano ni pale ambapo mtoto wakati wa
kuzaliwa, hulia kwa sababu alishazoea maisha ya kukaa kwenye tumbo la mama
yake,  na hivyo kukaa duniani nje ya hilo
tumbo  hataki. Hata hivyo, baada ya mtoto
huyu  kuzaliwa na kuzoea dunia, hapendi
tena kutoka humu duniani (kufa),  kwa sababu
ameshazoea maisha ya kuwa humu duniani. Ndivyo ilivyo hata kwa baadhi ya watu
wanapopata matatizo. Mwanzoni mtu huyakataa matatizo/magonjwa/ au mateso fulani, na
huwa tayari kuyakemea, lakini  matatizo haya
yakiendelea kukaa kwa miaka miwili  na
kuendelea, mtu huyazoea matatizo hayo na kuyafanya kuwa sehemu ya maisha ya
huyo mtu.
Yesu Kristo alipokuwa anakutana na mgonjwa,
kabla  ya kumponya alikuwa  akimuuliza “Je, unaamini?”. Lengo la
swali kama hili ni kutaka kufahamu, je mtu huyu anao utayari kwa kupokea
uponyaji? Inabidi awepo mtu  aliye tayari
kubadilika. Kwa Yesu 'hakuna kujaribu’ bali kuna kudhamiria kupokea sawa sawa
na imani  yako kwake. Kama unataka
kumiliki ujiandae kuua visivyotakiwa kuwepo. Kwenye  Baraka
zako, yupo Goliath anayekuzuia. Daudi alipomuoana Goliath, alisema “huyu  ni nani anayetukana majeshi ya Mungu aliye
hai?”  Wakati umewadia
ambapo Lazima kizazi cha Daudi kiamke katika taifa letu kwa Jina la Yesu.  Huu siyo 
wakati  tena wa kuongozwa  na viongozi wanaotumia nguvu za giza. Siyo
wakati tena wa kuongozwa na viongozi wanaoenda kwa waganga wa kienyeji ili kupata
nguvu au uongozi. Je, hayupo Mungu 
katika taifa hili hata watu hawa wazitegemee nguvu za giza?
Wapo waliokuibia urithi wako wakakugawia mateso na
magonjwa,  na leo hii ni wakati wako wa
kupambana ili  kurudia kilicho chako. Mtu
anayeomba na asiyeomba ni watu wawili tofauti. Anayeacha maombi, humpa nafasi
shetani kukaa ndani ya moyo wake. Ndiyo maana migawo ya kishetani inaendelea
kuwepo kwa sababu mtu  apewaye  huo mgawo hana nguvu ya kuikaataa.
Imeandikwa 2NYAKATI
32:8…[kwake
upo mkono wa mwili; ila kwetu yupo Bwana, Mungu wetu, kutusaidia, na
kutupigania mapigano yetu. Na watu wakayategemea maneno ya Hezekia, mfalme wa
Yuda.]…. Mgawo wa kishetani una mkono wa mwili, mkono wa
kibinadamu. Leo kataa kuwa chini ya mgawo wa kishetani  ambao adui amekugawia kwa Jina la Bwana.
Upo  mkono wa Bwana kukusaidia ili
kuangamiza kila  mgawo  wa kishetani maishani  mwako. 
Kumbuka kuwa ndani mwako kuna mkono wa Bwana wa kukusaidia, kama
Hezekiah alivyosema, kwa Jina la Yesu.
Kila "mgawo wa kishetani" utaweza tu kuuangamiza endapo
umempokwa Yesu Kristo  maishani  mwako. Endapo mtu hujaokoka, chukua hatua ya
kumpokea Yesu Kristo  maishani mwako, ili
uweze kuiangamiza migawo yote ya kishetani 
maishani mwako.
UKIRI 
Kila  mgawo
  wa kishetani  uteketee kwa Jina la
  Yesu.  Leo naenda kinyume na kila mgawo
  wa kishetani maishani mwangu. Kila 
  uzao wa giza leo ninauteketeza kwa Jina la Yesu. Ninaikataa migawo
  yote ya mashetani. Leo ninakataa kupatana na wachawi. Achieni maisha yangu
  kwa Jina laYesu. Amen  
 | 
 

Comments