VITU MUHIMU AMBAVYO KILA MSHAURI ANATAKIWA KUVIJUA ILI AWE MSHAURI MZURI.

Na Mch Peter Mitimingi
UKARIMU WA MSHAURI!
1. Unapaswa kuwa mkarimu na rafiki kwa mshauriwa wako.
2. Onyesha mazingira ya makaribisho ya urafiki na upendo.
3. Ukarimu ni njia ya kawaida ya kuelezea uelewa na kujali kwako kwa mshauriwa.
4. Ukarimu huwa huonyeshwa kwa vitendo kama vile:
• Ishara zako unavyo zionyesha kwa mshauriwa.
• Mwonekano wa mwili wako ulivyo.
• Kiimbo cha sauti (tone of voice) Ikiwa ya chini sana mshauriwa anaweza kudhani hujafurahia ujio wake. Pia ikiwa ya juu sana mshauriwa anaweza kukuogopa akadhani wewe ni mkali sana.
• Mguso wa mwili (unagusa wapi na unagusaje gusaje, kuna wengine wakisalimia nikama wanakupangusa tu kiganja hawakushiki vizuri ni kama wanakuona una kinyaa. Wengine wanakandamiza mikono ni kama mkono umekanyangwa na tairi ya trekta).
• Mapigo ya moyo yanakwendaje.
• Mwonekano wa uso ukoje. N.k


 MSHAURI ASIONGEZE KIDONDA JUU YA KIDONDA
Mshauri mzuri anapaswa kutumia mbinu bora zinazo kubalika. Anapaswa awe mpole zaidi kwa sababu wengi wa wale ambao wanataka ushauri wana matatizo mengi tayari na kwamba hawatakiwi kuongezea matatizo mengine zaidi kutoka kwa mshauri.
Sentensi kama:
• Naweza kukusaidia?
• Nikusaidie nini?
• Mbona unashangaa shangaa hapo unataka nini?
• Mbona upo hapa unasemaje.
• Umekuja kufanya nini hapa?
Sentesi kama hizo huweza kumfanya mshauriwa akajiona kuwa ameangukia katika mikono isiyo salama.
Usiongeze maumivu kwa mshauriwa hata kabla hujapokea maumivu yaliyo mleta.



AFYA YA MSHAURI

1. Kuna uhusiano mkubwa kati ya ushauri na kuwa na afya njema kimwili kama mshauri.
2. Afya ya mshauri ni ya muhimu sana katika mwonekano wa mshauri hasa kwa mara ya kwanza anapokutana na mshauriwa.
3. Kama afya yako sio nzuri ni vema ukaahirisha ushauri ili ushughulikie matengenezo ya afya yako.
Mfano:
• Kushauri huku unakikoozi kikali inaweza kuwa kizuizi katrika kazi ya ushauri
• Kushauri huku unamafua makali inaweza kuwa kizuizi katrika kazi ya ushauri.
• Kushauri huku una tatizo la kuwashwa sehemu mbalimbali na hususani sehemu za siri na kwingineko inaweza kuwa kizuizi katrika kazi ya ushauri.
• Kushauri huku una homa au mareria kali unatetemeka.
• Kufanya huduam ya ushauri huku unajisikia mdhaifu na usiye na nguvu.

4. Kama mshauri jijengee mazoea ya kufanya mazoezi ya mwili mara kwa mara.
5. Ni hatari kufanya ushauri ukiwa na msongo wa mawazo (stress).
6. Ni hatari kufanya ushauri huku umetoka kuumizwa na mtu umejeruhiwa moyo.
7. Uimara wa afya ya kimwili ya mshauri inaweza kuchangia namna atakavyoongea na mshauriwa wake na namna ambavyo mshauriwa atakavyo muona mshauri.


MSHAURI AZINGATIE LUGHA ZA ISHARA
1. Mikono yako iwe huru:
Usipozingatia lugha za ishara mdomo wako unaweza ukawa unatoa ushauri mzuri lakini baadhi ya vitendo vyako au ishara zako zikawa zinawasilisha ujumbe mbaya tofauti na unachokizungumza.
Usiweke mikono yako kifuani - Ni ishara ya ubosi au ukubwa.
Usiweke mikono yako Kichwani - Ni ishara ya kuchoshwa na mshauriwa.
Usiweke mikono yako Kiunoni - Ni ishara ya Maringo
Usiweke mikono yako Mifukoni - Ni ishara ya Kiburi.
Usichokonoe pua huku unaongea au kula vidole au kula kucha. Ni ishara ya kutojali pia inaleta kinyaa kwa baadhi ya watu.
Usitetemeshe miguu au kuganganisha mapaja wakati unaongea au unamsikiliza mshauriwa - Ni ishara ya (tention) yaani akili yako ndani haijatulia.

Mambo hayo yote yanatoa mawasiliano yasiyo mazuri kwa mshauriwa.
2. Miguu iliyofungwa kwa kuuweka mmoja juu ya mwingine au mokono iliyofngwa huwa inaonesha kuto kushiriki.
3. Kwamba uko katika hali ya kutokuwa huru, au una hofu. Unahitaji mkao ambao unakufanya uwe huru.
4. Mara nyingi mikono yako ikae juu ya mapaja yako baada ya kuonyesha ishara (guestures) mikono iweke kituo juu ya mapaja.
5. Pia ishara zisiwe nyingi kupita kiasi mpaka inakuwa kama sarakasi. Mpaka inakuwa kero kwa mshauriwa na kujihisi kuwa yupo kwenye chumba cha sarakasi au maigizo (comedy) badala ya chumba cha ushauri.



TOFAUTI YA KUSIKIA NA KUSIKILIZA!
Kusikia ni ule uwezo wa ndani ambao mtu huzaliwa nao, wakati kusikiliza ni ujuzi ambao mtu anajifunza na kujiendeleza katika kukomaa ili kuwa msikilizaji mzuri.


 TOFAUTI YA KUSIKIA NA KUSIKILIZA
Kusikiliza inamaanisha ni kuchukua hatua ya kuacha mambo mengine na kuelekeza na kutega akili na masikio ili kupokea kwa kina na ufanisi taarifa fulani.
Kusikiliza ni hatua (listening is a process).
Katika huduma ya Ushauri tunasisitiza zaidi kusikiliza kuliko kusikia.


MACHO YA MSHAURI
1. Macho ya mshauri yasiangalie pembeni au kuangalia chini.
2. Kuangalia bila kuwa unashangaa huwa inaonesha hali ya kujali.
3. Usimuangalie mshauriwa katika hali ya mshangao kwa Mfano:
• He! mbona anavipele namna hii!
• He mbona ana kifua (maziwa) kikubwa namna hii!
• Mbona ni kama hana kifua (maziwa) kabisa sasa huwa ananyonyeshaje?
• He! mbona sasa ni mnene sana au mbona anatumbo sana sasa huwa wanafanyaje huko!
• He! mbona ana makalio makubwa hivi nk.
4. Uwe mwangalifu sana na namna unavyo mwangalia maana macho yanaweza yakaubadilisha ujumbe au yakaleta ujumbe mwingine:
Baadhi huwaza kuonesha kuvutiwa kimapenzi
Baadhi huonesha kuchukizwa
Baadhi huonesha kuchoka kusikiliza
Baadhi huweza kuonyesha macho ya chuki
Macho ya furaha
Macho ya huzuni

Wanawake wengi huwa wanajisikia kutokuwa huru pale wanaume wanapokuwa wanatazama matiti yao, wakati wanaume huwa wanachukizwa na kujisikia kukosa uhuru pale wanawake wanapokuwa wanawatazama katika suruali yake (zipu)
N.B Kwa mshauriwa mwanamke huwa makini sana na mshauri anayemuangalia katika baadhi ya maeneo. Na mshauriwa akisha gundua kuwa mshauri ameelekeza macho yake katika baadhi ya maeneo yake nyeti basi huwa anakasirika na kufunga mlango wa ndani wa mawasiliano kati ya mshauri na mshauriwa.


 MKAO WA MSHAURI WAKATI WA HUDUMA YA USHAURI
• Kuna baadhi ya ishara za mwili ambazo zinaweza kumtishia mshauriwa; kwa mfano:
Kujichezesha chezesha kwenye kiti
Kuegamia nyuma sana
Kuvaa kupita kiasi
Kuvaa chini ya kiwango. nk.
• Hata hivyo, unapaswa kuvaa vizuri kwa hali ambayo inaonesha heshima kwa mtu ambaye unashughulika nae. Uvaaji pia huwa unaleta ujumbe mbali mbali.
• Umbali kutoka ulipo hadi alipo mshauriwa pia huwa inaumuhimu.
• Ni lazima umbali uwe mzuri kusaidia mshauriwa kupata nafasi ya kuwa huru. Epuka kuwa karibu sana au mbali sana.
• Kumshika kwa usahihi ni muhimu. Mshauri anapaswa awe makini anapotumia mbinu hii. Mshauri lazima aweze kuruhusu nafasi ya utaalamu kuwepo. Vilevile utamaduni unapaswa kuzingatiwa.
Aina ya mguso au kushika
Eneo unalogusa au kumshika mshauriwa.
Sababu ya kugusa au kumshika mshauriwa. nk.
• Sentensi fupi za sauti zinaweza kutumika. Mfano samahani, mmh, kweli, ndio, sawa sawa nk. Hii huwa inatoa uhakika kuwa unasikiliza. Hii inapaswa kufanyika kwa usahihi na kwa umbali unaokubalika.
• Kiimbo cha sauti na kasi ya kuongea unayo kuwa nayo inabidi iendane na hali anayojisikia mshauriwa.
Sauti ya juu
Sauti ya kati
Sauti ya chini
Sauti ya huzuni
Sauti ya furaha nk.
• Kutazamana pia ni muhimu. Epuka kuangalia upande wa mbali, inaweza kuonesha kuwa haujafurahishwa na mshauriwa. Mwitikio wa chini unaweza kupeleka ujumbe vile vile.

Comments