KUOMBA KATIKA ROHO MTAKATIFU.


BWANA YESU atukuzwe ndugu yangu.
Ayubu 33:4 ''ROHO ya MUNGU imeniumba, Na pumzi za Mwenyezi hunipa uhai.''
Baada ya kumpokea YESU KRISTO kama BWANA na MWOKOZI wa maisha yangu Nikiwa Chukwani Zanzibar kwaka 2008, Nilianza kujifunza mambo mengi ya MUNGU. Nilitamani sana kunena kwa lugha,  nilijiona nimepungukiwa kitu muhimu sana katika wokovu wangu. Nilimuuliza mchungaji wangu kwamba  mimi nitanena lini? akaniambia kwamba niendelee kutunza utakatifu na niendelee kutamani kujazwa nguvu za ROHO MTAKATIFU.
Niliyazingatia yote niliyoelezwa na Mchungaji lakini bado sikunena, kuna wakati nilijiapiza kwamba ''Jumapili lazima ninene kwa lugha mpya'' lakini bado haikutokea.
Nilitaka sana kunena kwa Lugha kwa sababu mtumishi mmoja aliniambia kwamba ROHO MTAKATIFU akija kwako hutangulia moto ili kuteketeza kila hila ya shetani, kama ni magonjwa au chochote hata ukimwi. akaniambia kwamba tangu aokoke miaka mingi iliyopita hajawahi kuona mgonjwa wa ukimwi akafanikiwa kunena katika ROHO MTAKATIFU harafu ukimwi wake ukabaki, akaniambia dalili mojawapo za kujua kama huna ukimwi basi upate neema ya kunena kwa Lugha katika ROHO MTAKATIFU  halisi.
Niliamini mimi ni mzima lakini kwa sababu ya michanganyo ya  kipindi sijaokoka  sikujiamini asilimia 100 kwamba ni mzima, hivyo hali hiyo pia iliniongezea hamu ya kutaka kujazwa nguvu za ROHO MTAKATIFU ili moto unaotangulia ukaushe magonjwa yote kama yapo mwilini mwangu japokua nilikuwa mzima kamili ila asiyejiamini.
Siku moja nilikuwa naangalia TV na Mama Diana Mwakasege alikuwa anawaongoza watu katika maombi ya kujazwa nguvu za ROHO MTAKATIFU. Na mimi kwa kutumia TV nilianza kufuata kila walichokuwa wanaelekezwa watu wa kwenye TV. Nilianza kuomba na kuanza kunena lakini mawazo yalianza kunijia na kuanza kuogopa maana nilikua nataka nione ROHO MTAKATIFU ataingiaje ndani yangu. Kumbe nilikuwa nakosea maana kuomba huku unawaza vitu vingine huwezi kujazwa Nguvu za ROHO MTAKATIFU.  baada kama ya mwaka mzima, Siku moja kanisani katika ibada ya jumapili kulikuwa na maombi maalum kwa ajili ya watu kujazwa nguvu za ROHO MTAKATIFU. Niliomba na katika kundi lile walinena wote hadi kikaanza kuwaza au kosa langu ni nini? lakini baadae, baada ya watu wote kunena na mimi ghafla nilianza kunena kwa Lugha mpya . Nilifurahi sana na nilitamani ninene hata mpaka kesho yake watu wanikute. Baadae nilitoka kanisani nina nguvu sana na kiu yangu ni kuwafuata watu wa Zanzibar ili waokoke. Nilikuwa na nguvu kuu, nilikuwa na ujasiri ambao si wa kawaida. Nilipotoka kanisani nikwenda nyumbani na baadae nikaanza kuomba maombi ya kawaida ya kumshukuru MUNGU kwa ajili ya ibada ya siku hiyo.  Nikiwa nyumbani nilipoanza tu kuomba kawaida nikajikuta ulimi wangu umekamatwa na nikaanza kunena tena. Tangu wakati huo nilianza kuwa nanena kwa Lugha hata kama sio kila siku.  Na kuna siku kanisani kwenye maombi ya kufunga siku 5 kavu nilinena huku nimelala hadi nikashangaa.

Mithali 1:23 ''Geukeni kwa ajili ya maonyo yangu; Tazama, nitawamwagia roho yangu, Na kuwajulisheni maneno yangu. ''
 
-ROHO MTAKATIFU ni muhimu sana kwa wateule wa KRISTO.
-ROHO MTAKATIFU ndiye msimamizi wa Wkovu wetu.
-ROHO MTAKATIFU atakaa na sisi wateule wa MUNGU milele.
-ROHO MTAKATIFU ndiye atakayetupeleka pia uzimani.
Katika maombi ROHO MTAKATIFU ni muhimu sana maana kila tunachoomba yeye anakijua hivyo kama tukimpa nafasi atusaidie hakika tutafanikiwa.
Mkristo yeyote ili afanikiwa katika jambo lolote jema ni lazima ahakikishe hawi mbali na ROHO MTAKATIFU. 

Je Unawezaje kuomba katika ROHO MTAKATIFU?
Mwenye sifa za kuomba katika ROHO MTAKATIFU ni Mkristo Yeyote aliyeokoka.
=ROHO MTAKATIFU ni Roho hivyo kwanza ili tuombe katika Yeye ni lazima tuombe katika Roho, ukiomba kimwili unakuwa hujatimiza sifa muhimu ambayo ni lazima uombe katika Roho.

Yohana 4:24 ''MUNGU ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli.'' 

-Ukiwa mtu wa mwilini ni ngumu sana kumpata ROHO wa MUNGU.

1 Kor 2:14 '' Basi mwanadamu wa tabia ya asili hayapokei mambo ya ROHO wa MUNGU; maana kwake huyo ni upuzi, wala hawezi kuyafahamu, kwa kuwa yatambulikana kwa jinsi ya rohoni. '' 

=ROHO MTAKATIFU ni mtakatifu hivyo sifa ya pili ni lazima uwe mtakatifu wewe unayeomba.

1 Petro 1: 14-16 ''Kama watoto wa kutii msijifananishe na tamaa zenu za kwanza za ujinga wenu; bali kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote; kwa maana imeandikwa, Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu.''

= Ni muhimu sana kujifunza mafundisho kuhusu ROHO MTAKATIFU na kazi zake.
=Ni  muhimu kumtii YESU KRISTO maana ROHO MTAKATIFU humshuhudia YESU hivyo kama huna habari na YESU wewe ROHO MTAKATIFU hakuhusu.

Warumi 8: 8-9 ''Wale waufuatao mwili hawawezi kumpendeza MUNGU. Lakini ikiwa ROHO  wa MUNGU anakaa ndani yenu, ninyi hamwufuati mwili; bali mwaifuata roho. Lakini mtu awaye yote asipokuwa na ROHO wa KRISTO, huyo si wake. ''

=ROHO MTAKATIFU ni MUNGU mwenyewe hivyo kama humtaki MUNGU na neno lake harafu unamtaka ROHO MTAKATIFU hapo sahau kumpata.

 Matendo 2:17-18 '' takuwa siku za mwisho, asema MUNGU, nitawamwagia watu wote ROHO yangu, na wana wenu na binti zenu watatabiri; na vijana wenu wataona maono; na wazee wenu wataota ndoto. Naam, na siku zile nitawamwagia watumishi wangu wanaume na wanawake ROHO yangu, nao watatabiri. ''

Ni Lazima Tuombe Kila Wakati Katika ROHO. 

Yuda 1:20 Biblia Inasema "Bali Ninyi, Wapenzi, Mkijijenga Juu Ya Imani Yenu Iliyotakatifu Sana, Na Kuomba Katika ROHO MTAKATIFU"

Tuko Katika Imani Iliyo Takatifu Sana.
 =Tunatakiwa Tuombe Katika ROHO MTAKATIFU. 

 Waefeso 6:18 ''kwa sala zote na maombi mkisali kila wakati katika ROHO, mkikesha kwa jambo hilo na kudumu katika kuwaombea watakatifu wote; ''

=ROHO MTAKATIFU Katika Moja Ya Kazi Zake Ni Katika Maombi. 
=Nguvu Katika Maombi Huwapata Wanyenyekevu Kwa ROHO MTAKATIFU. 
=MUNGU Hawezi Kumpa ROHO Wake Mtu Yule Asiye Mnyenyekevu. 
=Ni Muhimu Sana Kumsikiliza ROHO MTAKATIFU Katika Maombi Yako. 
Ni Muhimu Kuomba Katika ROHO Na Ni Muhimu Kuishi Kwa Kutii Yale Ya ROHO MTAKATIFU.

 Wagalatia 5:25 "Tukiishi Kwa ROHO, Na Tuenende Kwa ROHO".  

Kumbe Ni Muhimu Sana Kuenenda Kwa ROHO, Hata Katika Maombi Ni Muhimu Tuombe Katika ROHO MTAKATIFU. -Kujitenga Na ROHO MTAKATIFU Ni Kujitenga Na Kusudi La MUNGU.
Nimewahi kuandaa masomo mengi kuhusu ROHO MTAKATIFU ila kuna somo moja wewe ambaye unatamani kujua kazi za ROHO MTAKATIFU basi Nenda blog yangu ya Maisha ya ushindi kishwa kwa juu kwenye Search andika KAZI 12 ZA ROHO MTAKTIFU utajifunza zaidi kuhusu ROHO MTAKATIFU.

1 Kor 2:10 '' Lakini MUNGU ametufunulia sisi kwa ROHO. Maana ROHO huchunguza yote, hata mafumbo ya MUNGU
 "
Ngoja nimalizie somo la leo kwa kukueleza  kwamba mtu aliyeokoka atawezeje kuomba katika ROHO MTAKATIFU.
-Maana ya kwanza ya kuomba katika ROHO MATAKTIFU ni kunena kwa lugha, kama unanena kwa lugha halisi basi hapo unaomba katika ROHO.

Matendo 2:1-4 ''Hata ilipotimia siku ya Pentekoste walikuwako wote mahali pamoja. Kukaja ghafula toka mbinguni uvumi kama uvumi wa upepo wa nguvu ukienda kasi, ukaijaza nyumba yote waliyokuwa wameketi. Kukawatokea ndimi zilizogawanyikana, kama ndimi za moto uliowakalia kila mmoja wao. Wote wakajazwa ROHO MTAKATIFU, wakaanza kusema kwa lugha nyingine, kama ROHO alivyowajalia kutamka.'' 

-Maana  ya pili ni pale ambapo ukiwa unaomba utapata msukumo wa kuombea jambo fulani, ukitii utakuwa umefanya vyema maana umemtii ROHO MATAKTIFU.
Imewahi kunitokea mimi katika maombi mara nyingi tu. ngoja nikueleze kwa ufupi 3.
Siku moja niliandaa maombi kwenye karatasi ili kuombea lakini nilipoanza tu kuomba nilianza kuelekezwa na ROHO mambo ya kuombea na kujikuta nikiomba mambo mengi sana huku sikugusa hata moja katika yale niliyoyaandika. Kumtii ROHO MTAKATIFU katika maombi ni muhimu sana maana yeye huona jambo mwisho kabla ya mwanzo. ukimtii ROHO katika maombi hapo unakuwa unaomba katika ROHO.
Kuna ndugu mmoja alikuwa anaumwa sana, tukaanza kumwombea ili apone lakini katikati ya maombi niliambiwa rohoni kwamba ndugu yule atakufa  wala hatarudi hivyo nikabadilisha maombi na kuanza kuomba maombi ya toba na baadae nikamuongoza sala ya toba upya kisha tukaondoka, kesho yake akafariki yule ndugu. Sikumwambia mtu jambo lile maana ni hatari kumwambia mtu kwamba huyu ndugu atakufa wala hatapona, utaonekana una imani ndogo kumbe ROHO anajua kwamba ile ni saa ya ndugu yule kuondoka.
Siku moja katika mkesha kanisani nilikuwa naomba ghafla nikaona ajali mbaya ya pikipiki, nikabadilisha maombi na kuanza kukataa roho ya ajali na huko ndiko kumtii ROHO MTAKATIFU na ndiko kuomba katika ROHO maana ni yeye aliyefunua jambo la mbeleni.
Kuna watu wengi sana wanang'angania kuombea jambo fulani lakini ROHO anawapa mzigo wa kuwaombea watu wengine lakini wanashindwa kutii kumbe kumtii ROHO ndilo jambo muhimu zaidi maana yawezekana umeombea jambo ambalo limefungwa kwenye muda hivyo hilo litakuja tu hivyo ombea mengine ambayo ROHO anayaleta kwako.
Kile anacholeta ROHO MTAKATIFU ndio kitu muhimu zaidi kwako kwa wakati huo hata kama akili yako haitaki.
Nimesema mengi sasa hapa inatosha na naamini umekula na kushiba chakula hiki cha kiroho.
Ukitamani ROHO MTAKATIFU umetamani ushindi katika kila jambo.

Matendo 8:14-17 ''Na mitume waliokuwako Yerusalemu, waliposikia ya kwamba Samaria imelikubali neno la MUNGU, wakawapelekea Petro na Yohana; ambao waliposhuka, wakawaombea wampokee ROHO MTAKATIFU; kwa maana bado hajawashukia hata mmoja wao, ila wamebatizwa tu kwa jina lake BWANA YESU. Ndipo wakaweka mikono yao juu yao, nao wakampokea ROHO MTAKATIFU.''

Ndugu yangu, naamini kuna kitu umejifunza hivyo nakuomba chukua hatua ya kwenda kanisani na kumpokea YESU KRISTO kama BWANA na MWOKOZI wa maisha yako na baada ya hapo hudhuria fundisho kanisani ili uimarike na upate nguvu za kuwasaidia na wengine.
MUNGU akubariki sana.
Ni mimi ndugu yako Peter M Mabula.
mabula1986@gmail.com.
0714252292.

Comments