MADHABAHU YA LAANA

Na Askofu mkuu Josephat Gwajima.

Hesabu 22: 1-6
“Kisha wana wa Israeli wakasafiri na kupanga katika nchi tambarare za Moabu ng'ambo ya pili ya Yordani karibu ya Yeriko. Na Balaki mwana wa Sipori akaona mambo yote ambayo Israeli wamewatendea Waamori. Moabu akawaogopa hao watu sana, kwa kuwa walikuwa wengi; Moabu akafadhaika kwa sababu ya wana wa Israeli. Moabu akawaambia wazee wa Midiani, Sasa jeshi hili la watu litaramba vitu vyote vinavyotuzunguka, kama vile ng'ombe arambavyo majani ya mashamba. Na Balaki, mwana wa Sipori, alikuwa mfalme wa Moabu zamani zile. Basi akatuma wajumbe kwa Balaamu mwana wa Beori, hata Pethori, ulio kando ya Mto, mpaka nchi ya wana wa watu wake, kwenda kumwita, akisema, Tazama, kuna watu waliotoka Misri; tazama, wanaufunika uso wa nchi, tena wanakaa kunikabili mimi. Basi, njoo wewe, nakusihi unilaanie watu hawa; maana wana nguvu kunishinda mimi. Labda nitawaweza, tupate kuwapiga, niwafukuze watoke katika nchi yangu, kwa maana najua ya kuwa yeye umbarikiye hubarikiwa, na yeye umlaaniye hulaaniwa.”

Baalam alikuwa mchawi aliyetaka kuwalaani wana wa Israei. Wana wa Israeli walikuwa wameshinda kila walipokuwa wakafika mahali. Wakakutana na mfalme wa moabu ambaye alimkodisha baalam ili awalaani wasije wakamshinda. “Ukilaaniwa hata kama ulikuwa unaelekea kushinda unashindwa.” Baalam alijaribu kuwalaani watu wa Bwana lakini hawakulaanika.
Yoshua 13:22
“ufalme wote wa Ogu uliokuwa katika Bashani, huyo aliyekuwa akitawala katika Ashtarothi na katika Edrei (huyo alisalia katika mabaki ya wale Warefai); kwa kuwa Musa aliwapiga hao na kuwafukuza. Pamoja na hayo wana wa Israeli hawakuwafukuza Wageshuri, wala Wamaaka; lakini Wageshuri na Wamaaka wamekaa kati ya Israeli, hata siku hii ya leo.”

Hesabu 22:7
“Wazee wa Moabu, na wazee wa Midiani, wakaenda, wakichukua ujira wa uganga mikononi mwao; wakamfikilia Balaamu, wakamwambia maneno ya Balaki.”

Kuna ujira wa uganga ambao ni mahitaji ya mchawi anayoyataka ili atimize mambo yake. Huyu baaalam mchawi alichukua ujira ili awalaani wana wa Israeli. Kwenye maisha yetu ya kila siku inawezekana kuna mtu anakuona umefanikiwa sana kwenye ndoa, kazi, biashara akakuonea wivu na kuamua kwenda kwa mganga wa kienyeji na kutoa ujira ili ulaaniwe ushuke chini na kushindwa kuendelea kufanikiwa.
Hesabu 23:1
“Balaamu akamwambia Balaki, Nijengee hapa madhabahu saba, ukaniandalie hapa ng'ombe waume saba, na kondoo waume saba. Balaki akafanya kama Balaamu alivyonena. Balaki na Balaamu wakatoa sadaka, ng'ombe mume mmoja na kondoo mume mmoja juu ya kila madhabahu. Balaamu akamwambia Balaki, Simama karibu na sadaka yako, nami nitakwenda, labda Bwana atakuja kuonana nami; na lo lote atakalonionyesha nitakuambia. Akaenda hata mahali peupe juu ya kilima. Mungu akakutana na Balaamu; naye Balaamu akamwambia, Nimetengeneza madhabahu saba, nami nimetoa sadaka ng'ombe mume mmoja na kondoo mume mmoja juu ya kila madhabahu. Bwana akatia neno katika kinywa chake Balaamu, akasema, Umrudie Balaki; ukaseme maneno haya.”

Kwenye maisha ya kawaida wachawi nao wana wana madhabahu za kutoa laana ili ziwapate watu waliokusudiwa. Laana ya kichawi hutokea kwenye madhabahu ya kichawi. Baalam alianza kuangalia kwenye ulimwengu wa rohoni ili shetani aje na kuitamka ile laana kwa wana wa Israeli lakini Yehova aliingilia kati na kuizuia laana ile isifanikiwe kutoka kwenye madhabahu ya kishetani ya baali. Baalam alijitahidi ili awalaani wana wa Israeli lakini mdomoni mwake ilitoka Baraka kwasababu Mungu aliingilia madhabahu yake na kumfanya atamke baraka. Hii inamaanisha hata kwenye maisha ya kila siku yeyote anayetaka kukulaani wewe au biashara yako au ndoa yako au kazi yako laana isiyo na sababu haiwezi kukupata kwa jina la Yesu, baalam ahamisha madhabahu ili aweze kuwalaani wana wa Israeli vizuri lakini kila alipokwenda aliishia kuwabariki.
Kila madhabahu iliyo jengwa ina jina lake, jina la madhabahu ndilo linalofanya madhabahu iwe na matokeo Fulani yanayoendana na jina lake. Wana wa Israeli walisafiri kwa miaka 40 kufika kwenye nchi ya ahadi. Ukiangalia kwenye maisha ya kila siku mtu anaweza kuchelewa kuolewa au kufanikiwa kwasababu ya kudharau mambo madogo madogo ambayo ni ya Mungu lakini yanaonekana kama mambo ya kitoto kwenye macho ya wanadamu, jambo lingine mtu anaweza kuchelewa ni kujifanya anajua kila kitu. Mambo ya Mungu ni kama mambo ya kitoto na ukijfanya unayajua sana unaweza ukajikuta unaharibikiwa kabisa. Kwenye maisha ya kila siku Mungu hujidhihirisha kwenye mambo madogo na manyonge ambayo kibinadamu yanadharaulika.
Wana wa Israeli walichelewa kufika kwenye nchi ya ahadi sababu walijifanya wanamjua sana na Mungu ndipo akaamua kuwachelewesha kwa miaka 40 mpaka ule ujuaji wao uishe. Mungu alitaka Misri iwatoke ndani yao kwamaana kama walikuwa wakifanya hivi na hivi waache wafanye hivi. Sababu nyingine Mungu alitaka kuwafundisha vita ndiomaana aliwachelewesha kufika kwenye nchi ya ahadi.

Aina za wokovu
Kuna aina ya wokovu ambao mtu anajisimamia mwenyewe mpaka anasimama imara. Wokovu mwingine ni ule mtu anafuatiliwa mpaka anasimama na kujisimamia mwenyewe, wokovu mwingine ni ule ambao mtu anafuatilia mambo fulani fulani ili ayapate na akishayapata anaondoka na kuendelea na mambo yake. Kuna baadhi ya watu wanawafuatilia watu wa kuwaoa/olewa nao sababu wanajua wakitaka kupata watu wazuri wa kuoana nao wanapatikana kanisani hivyo wanajifanya nao wameokoka wako ndani ya wokovu ili wapate mambo yanayofanana na hayo. Kuna ule wokovu wa asili ambao Mungu anakupa na anakupa ili kukutengeneza uwe mtu wa vita na anakuwa anakucheleweshea baadhi ya vitu usivipate ili akufundishe uwe mtu wa vita na ukija kuvipata unakuwa una uwezo wa kuviongoza na kuvimiliki.
Mungu ni Mungu wa vita sisi pia tunatakiwa tuwe watu wa vita

Waefeso 6: 12
“Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.”
Maana yake tunapopita kuna viumbe wa giza kwenye ulimwengu wa rohoni kwa maana mashetani na mapepo ambayo yanatuzuia tusiende kule tunapotaka kwenda hivyo hiyo ndiyo vita yetu tuliyo nayo. Ule uwezo wako wa kuwaendea na kuwapiga kwenye ulimwengu wa rohoni ndivyo uwezekano wako wa kumili vilevile kama ulivyo shinda baadaye.
Sisi ni vinywa vya Bwana na mabalozi wa Mungu hapa duniani.

Ukiri
“Katika jina la Yesu laana ya wachawi inayotokea kwenye madhabahu haitanipata mimi kwa jina la yesu.”
Kuna baadhi ya koo zimejengewa madhabahu za kumilikiwa ambapo familia zinakuwa zinamilikiwa na balaa, ajali, magonjwa, zingine zinakuwa za kuzuia mafanikio na vitu mbalimbali na unapofanikiwa kuzibomoa madhabahu hizo ndipo unapenya kwenye maisha yako. Kuna madhabahu ambazo zimeshikilia roho za watu ambapo unaweza kumwona mtu mjanja kweli lakini ukimwangalia kwenye mambo ya kufanikiwa hana kitu. Kuna baadhi ya mambo huwezi kuyachangamkia sababu umelazwa kwenye madhabahu.
Matendo 17:23
“Kwa sababu nilipokuwa nikipita huko na huko na kuyaona mambo ya ibada yenu, naliona madhabahu iliyoandikwa maneno haya, KWA MUNGU ASIYEJULIKANA. Basi mimi nawahubirini habari zake yeye ambaye ninyi mnamwabudu bila kumjua.”
Kwenye madhabahu hii inategemea kuhani anasema nini sababu Mungu wake hajulikani.

Maombi
“Katika jina la Yesu ninaamuru kila madhabahu iliyonilaza na aliyenilaza ninaivunja kwa jina la Yesu, ninawaponda na kuwaangamiza makuhani wa madhabahu kwa jina la Yesu, ninazinyamazisha kafara za madhabahu kwa damu ya mwanakondoo katika jina la Yesu. Amen”

Mwanzo 33:20
“Akajenga huko madhabahu, akaiita, El-elohe-Israeli (El-elohe-Israeli maana yake ni Mungu, Mungu wa Israeli).”
Neno Israeli maana yake ni “aliyeshindana akashinda”, Unaweza kuona shetani alipotaka kuiteka nchi alibomoa madhabahu kwanza. Duniani wachawi wanajua kuna watu ukiwasonga’songa uhusihano wa watu wengi na Mungu utaharibika
Warumi11:3 “Bwana, wamewaua manabii wako, wamezibomoa madhabahu zako, nami nimesalia peke yangu, nao wananitafuta roho yangu. Lakini ile jawabu ya Mungu yamwambiaje? Nimejisazia watu elfu saba wasiopiga goti mbele ya Baali. Basi ni vivi hivi wakati huu wa sasa, yako mabaki waliochaguliwa kwa neema.”

Kuna madhabahu ya usalama ambayo mtu anaitengeneza ili awe salama, biashara yake iwe salama, familia yake iwe salama na unaweza kuona kuna baadhi ya familia ambazo watu wanaishi ndani yake na wamejiwekea ulinzi kutoka kwenye madhabahu hizi ili kujilinda. Ufalme wa shetani unafanya kazi na baadaye unakuumbua, shetani haukuachi hivihivi unakuwa unatoa kafara kwenye madhabahu hizo mpaka unaishiwa unafariki wewe mwenyewe.
Kutoka 17:15 “Musa akajenga madhabahu, akaiita jina lake Yehova-nisi (Yehova-nisi maana yake ni Bwana ni bendera yangu); akasema, Bwana ameapa; Bwana atakuwa na vita na Amaleki kizazi baada ya kizazi.”
Amaleki ni kabila ambalo kipindi wana wa Israeli wakiongozwa na Musa walipita kwenye nchi yao ambapo wana wa Israeli waliwaomba wapiti kwa Amani bila kushika chochote chao wala maji yao wala udongo wao ni kupita tu lakini amaleki walikataa na kujaribu kuwazuia wasipite na ikumbukw Bwana aliwalaani amaleki kizazi hadi kizazi na leo hii Mungu anafanya vita na amaleki wa Tanzania anayewatesa watu na ndoa zao, anayewatesa watu na ajira zao, anayewatesa watu na uchumi wao, Mungu ameapa kufanya nao vita na wameshapigwa kwa jina la Yesu. Musa alipeleka barua ya kuwaomba kupita katika njia kuu kwenda kwenye nchi ya ahadi hivyo watulie bila kuogopa jinsi walivyokuwa wanaonekana lakini walipokataa Mungu aliwatia wana waIsraeli nguvu wakawashinda amaleki na kusonga mbele kwenye nchi ya ahadi.

“Biblia imetufundisha mambo matatu la kwanza tunatakiwa tutambue yale tunayotakiwa kuyafanya “iweni watakatifu kama mimi nilivyo mtakatifu”, “hamkosi kuzitambua hila zake adui”, pili Biblia imetufundisha kutoka kwa wenzetu ambao walifanya makosa walipokuwa ndani ya wokovu ili kupitia yale makosa yao sisi tujifunze na Tatu Biblia imetufundisha yale ambayo hayakutimia kwa mikono ya akina Petro, Yohana na manabii wengine sisi tuyatende kama Askari wa Mbinguni, Mabalozi wa mbinguni hapa duniani”

Comments